Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee III

Mamlaka ya Mungu (II) (Sehemu ya Tano)

Kifo: Awamu ya Sita

Baada ya mahangaiko mengi na masikitiko mengi, na kuvunjwa moyo kwingi, baada ya furaha nyingi na huzuni nyingi na baada ya misukosuko ya maisha, baada ya miaka mingi sana isiyosahaulika, baada ya kutazama misimu ikipita na kujirudia, mtu hupita kwenye kiungo muhimu sana cha maisha bila ya arifa, na kwa ghafla tu mtu anajipata kwenye miaka yake ya kufifia. Alama za muda zimejichora kotekote kwenye mwili wa mtu: Mtu hawezi tena kusimama wima, kichwa cha nywele nyeusi kinageuka na kuwa cha nywele nyeupe, macho maangavu na mazuri yanabadilika na kuanza kufifiliza na kuwa na wingu mbele yao, nayo ngozi laini, yenye unyumbufu inageuka na kuwa na makunyanzi na madoadoa. Kusikia kwa mtu kunaanza kufifia, meno yake kulegea na kuanza kujiangukia, mwitikio wa mtu unaanza kuchelewachelewa, kutembea kunakuwa ni kwa kujikokota…. Wakati huu mtu ameaga kwaheri kabisa miaka yake ya nguvu ya ujana wake na kuingia katika maisha yake ya kwaheri: umri wa uzee. Kisha, mtu atakabiliana na kifo, awamu ya mwisho ya maisha ya binadamu.

1. Muumba Pekee Ndiye Anayeshikilia Nguvu za Maisha na Kifo juu ya Binadamu

Kama kuzaliwa kwa mtu kulipangiwa na maisha ya awali ya mtu, basi kifo cha mtu kinaadhimisha mwisho wa hatima hiyo. Kama kuzaliwa kwa mtu ndiyo mwanzo wa kazi maalum ya mtu ya maisha, basi kifo cha mtu kinaadhimisha mwisho wa kazi hiyo maalum. Kwa sababu Muumba amepangilia mseto maalum wa hali mbalimbali za kuzaliwa kwa mtu, ni wazi na dhahiri shahiri kwamba amepangilia pia mseto wa hali zisizobadilika kwa minajili ya kifo cha mtu. Kwa maneno mengine, hakuna anayezaliwa kwa bahati na hakuna kifo cha mtu ambacho hakitarajiwi, na si kuzaliwa, si kufa vyote vina uhusiano na maisha ya mtu ya awali na ya sasa. Hali za kuzaliwa na kifo cha mtu, vyote viliamuliwa kabla na Muumba; hii ni kudura ya mtu, hatima ya mtu. Kama vile tu mengi yanaweza kuzungumzwa kuhusu kuzaliwa kwa mtu, hata kifo cha kila mtu kitafanyika katika mseto tofauti katika hali maalum, hivyo basi urefu wa maisha tofauti miongoni mwa watu na njia tofauti pamoja na nyakati tofauti zinaandama vifo vyao. Baadhi ya watu wana nguvu na afya na ilhali wanakufa mapema; wengine ni wanyonge na wanauguaugua ilhali wanaishi hadi umri wa uzee, na wanaaga dunia kwa amani. Baadhi wanafarakana na dunia kutokana na sababu zisizokuwa za kawaida, wengine kutokana na sababu za kawaida. Baadhi wanakata roho wakiwa mbali na nyumbani, wengine wanayafumba macho yao wakiwa na wapendwa wao kando yao. Baadhi ya watu hufia hewani, wengine wakafia chini ya nchi. Wengine huzama chini ya maji, wengine nao kwenye majanga. Baadhi hufa asubuhi, wengine hufa usiku. … Kila mtu hutaka kuzaliwa kwa heshima, maisha mazuri, na kifo kitukufu, hakuna mtu anayeweza kuendeleza hatima yake mwenyewe, hakuna mtu anayeweza kukwepa ukuu wa Muumba. Hii ni hatima ya binadamu. Binadamu anaweza kufanya aina zote za mipango ya siku zote za usoni, lakini hakuna mtu anayeweza kupanga njia na muda wa kuzaliwa kwake na kuondoka kwake ulimwenguni. Ingawaje watu hufanya kila wawezalo kuepuka na kuzuia kuja kwa kifo chao, ilhali, bila wao kujua, kifo huwa kinakaribia polepole. Hakuna anayejua ni lini atakapofarakana na dunia au ni vipi atakavyofanya hivyo, isitoshe hata pale hayo yote yatakapofanyikia. Bila shaka, si binadamu wanaoshikilia nguvu za maisha na kifo, wala si kiumbe fulani kwenye ulimwengu wa kimaumbile, lakini ni Muumba, ambaye mamlaka yake ni ya kipekee. Maisha na kifo cha binadamu si zao la sheria fulani ya ulimwengu wa kimaumbile, lakini athari ya ukuu wa mamlaka ya Muumba.

2. Yule Asiyejua Ukuu wa Muumba Atahangaika kwa Woga wa Kifo

Wakati mtu anapoingia kwenye umri wa uzee, changamoto anazokabiliana nazo si kutosheleza mahitaji ya familia au kuanzisha maono makubwa katika maisha yake, lakini namna ya kuyaaga maisha yake, namna ya kukutana na mwisho wa maisha yake, namna ya kuweka kikomo kwenye mwisho wa uwepo wake binafsi. Ingawaje juujuu inaonekana kwamba watu hutilia makini kidogo kwa kifo, hakuna anayeweza kuepuka kuchunguza suala hili, kwani hakuna anayejua ikiwa ulimwengu mwingine uko kule upande mwingine wa kifo, ulimwengu ambao binadamu hawawezi kung’amua au kuhisi, ulimwengu wasiojua chochote kuuhusu. Hali hii huwafanya watu kuwa na wasiwasi kukabiliana na kifo moja kwa moja, wasiwasi wa kukabiliana nacho kama inavyostahili, na badala yake wanafanya kadri ya uwezo wao kuepuka mada hii. Na kwa hivyo mada hii humfanya kila mmoja kutishika kuhusu kifo, huongezea uzito kwenye fumbo hili kuhusiana na hoja hii isiyokwepeka ya maisha, huweka kivuli kisichoisha juu ya moyo wa kila mmoja.

Wakati mtu anapohisi mwili wake unaanza kudhoofika, wakati mtu anapohisi kwamba kifo chake chakaribia, mtu huhisi tishio, woga usioelezeka. Woga wa kifo humfanya mtu kuhisi kuwa mpweke zaidi na asiyejiweza, na kwa wakati huu mtu hujiuliza: Nilitoka wapi? Ninaenda wapi? Je, hivi ndivyo nitakavyokufa, huku maisha yangu yakinipita kwa haraka hivi? Je, huu ndio wakati unaoadhimisha mwisho wa maisha yangu? Ni nini, hatimaye, maana ya maisha? Maisha yana thamani gani, kwa kweli? Je, yanahusu umaarufu na utajiri? Je, yanahusu kulea familia? … Haijalishi kama mtu amewahi kufikiria maswali haya mahususi, haijalishi ni vipi mtu ana woga wa kifo, katika kina cha moyo wa kila mmoja siku zote kuna tamanio la kutaka kuchunguza zaidi mafumbo, hisia zisizoeleweka kuhusu maisha, pamoja na haya yote, ni uhusiano wa karibu na ulimwengu wenyewe, na kutotaka kuuacha. Pengine hakuna anayeweza kufafanua zaidi ni nini ambacho binadamu huogopa, ni nini ambacho binadamu hutaka kuchunguza zaidi, na nini kile ambacho ana uhusiano wa karibu nacho na kinachomfanya kutotaka kuondoka au kukiacha nyuma …

Kwa sababu wanaogopa kifo, watu huwa na wasiwasi mno; kwa vile wanaogopa kifo, vipo vitu vingi ambavyo hawawezi kuachilia. Wakati wako karibu kufa, baadhi ya watu huhangaika kuhusu hiki au kile; wanakuwa na wasiwasi kuhusu watoto wao, wapendwa wao, utajiri wao, ni kana kwamba kwa kuwa na wasiwasi hivyo wanaweza kuondoa mateso na hofu ambayo kifo huleta, ni kana kwamba kwa kuendeleza aina fulani ya urafiki wa karibu na wale wanaoishi wanaweza kukwepa ile hali ya kutoweza kujisaidia na upweke unaoandamana na kifo. Katika kina cha moyo wa binadamu kunao woga usiokamilika, woga wa kuachwa na wapendwa, woga wa kutowahi kutuliza macho yako kwenye mbingu za samawati, woga wa kutowahi tena kuangalia ulimwengu huu yakinifu. Nafsi pweke, iliyozoeana na wapendwa wake, husita kuachilia mshiko wa maisha na kuondoka, ikiwa pekee, kuelekea kwenye ulimwengu usiojulikana, usiozoeleka.

3. Maisha ya Kuishi Ukitafuta Umaarufu na Utajiri Yatamwacha Mtu Akiwa na Hasara Akikabiliana na Kifo

Kwa sababu ya ukuu na kuamuliwa kabla kwa Muumba, nafsi pweke iliyoanza bila chochote kwa jina lake huweza kupata wazazi na familia, fursa ya kuwa mwanachama wa kizazi cha binadamu, fursa ya kupitia maisha ya binadamu na kuona ulimwengu; na pia inafaidi fursa ya kupitia ukuu wa Muumba, kujua uzuri wa uumbaji wa Muumba, na zaidi kuliko vyote, kujua na kutii mamlaka ya Muumba. Lakini watu wengi zaidi huwa hawatumii vizuri fursa hii nadra na ya kipekee. Mtu hutumia nguvu zake zote maishani akipigana dhidi ya hatima yake, akatumia muda wake wote akihangaika na akijaribu kulisha familia yake na akisafiri huku na kule kati ya kutafuta utajiri na hadhi katika jamii. Mambo ambayo watu huthamini ni familia, pesa, na umaarufu; wanaona mambo haya kuwa mambo yenye thamani zaidi katika maisha. Kila mtu hulalamikia hatima yake, ilhali bado wanazisukuma hatima hizi nyuma ya akili zao na wanabaki na maswali ambayo ni lazima zaidi kuchunguza na kuelewa: kwa nini binadamu yuko hai, namna ambavyo binadamu anafaa kuishi, ni nini maana na thamani ya maisha. Katika maisha yao yote, hata hivyo iwe miaka mingapi, wanakimbilia tu kuhusu kutafuta umaarufu na utajiri, mpaka ujana wao ukawaacha, mpaka wakawa na nywele za kijivu na makunyanzi kwenye uso wao; mpaka wakagundua utajiri na umaarufu ni vitu visivyoweza kusitisha mtu kuelekea katika udhaifu unaotokana na uzee, kwamba pesa haiwezi kujaza utupu wa moyo: mpaka wanapoelewa kwamba hakuna mtu ambaye anaachwa nje kutoka kwenye sheria ya kuzaliwa, kuwa mzee, magonjwa, na kifo, kwamba hakuna mtu anayeweza kutoroka hatima ile inayomsubiri. Mpaka tu pale ambapo anapolazimishwa kukabiliana na awamu ya mwisho maishani ndipo anapong’amua kwa kweli kwamba hata kama mtu anamiliki mamilioni ya mali, hata kama mtu anayo heshima na cheo kikubwa, hakuna anayeweza kutoroka kifo, kwamba kila mtu atarudi kwenye sehemu yake asilia: nafsi pweke, bila chochote kwa jina lake. Wakati mtu anapokuwa na wazazi, mtu husadiki kwamba wazazi wa mtu ni kila kitu; wakati mtu anapokuwa na mali, mtu hufikiri kwamba pesa ndio kitu cha muhimu, kwamba ni rasilimali za mtu maishani; wakati watu wanapokuwa na hadhi katika jamii, wanaishikilia na hata wanaweza kuhatarisha maisha yao kwa ajili ya hadhi hiyo. Ni pale tu ambapo watu wanakaribia kuondoka ulimwenguni ndipo wanapotambua kwamba mambo yale waliyoishi katika maisha yao wakifuatilia si chochote bali mawingu yanayopita, hakuna chochote kati ya vitu hivi ambacho wanaweza kushikilia, hakuna hata chochote wanachoweza kwenda nacho, hakuna hata chochote kinachoweza kuwaondolea kifo, hakuna kile kinachoweza kuwapa ushirika au tulizo wakati nafsi yao inapokuwa pweke ikielekea kufa; na hata, hakuna kati ya hivyo vyote vinavyoweza kumpa mtu wokovu, na kuwaruhusu kushinda kifo. Umaarufu na utajiri ambao mtu hupata kwenye ulimwengu yakinifu humpa mtu kutosheka kwa muda, anasa ya kupita, hisia ya uwongo ya utulivu, na kumfanya mtu kupoteza njia. Na kwa hivyo watu, wanapong’ang’ana kila pahali kwenye bahari pana ya binadamu, wakitafuta amani, tulizo na utulivu wa moyo, wanafunikwa zaidi na zaidi na mawimbi. Wakati ambapo watu hawajapata maswali ambayo ni muhimu zaidi kuelewa—ni wapi wametoka, ni kwa nini wako hai, ni wapi wanakoenda na kadhalika—wanashawishiwa na umaarufu na utajiri, wanapotoshwa, wanadhibitiwa na vitu hivyo, na wanaishia kupotea bila kujua njia. Muda huyoyoma; miaka hupita kama kupepeswa kwa jicho; kabla ya mtu kutambua, mtu huaga kwaheri miaka yake bora zaidi ya maisha yake. Wakati mtu anakaribia kuondoka ulimwenguni, mtu anafika katika utambuzi wa taratibu kwamba kila kitu ulimwenguni kinamwacha polepole, kwamba mtu hawezi kushikilia tena vitu alivyomiliki; kisha mtu anahisi kwa kweli kwamba hamiliki chochote kamwe, kama mtoto mchanga anayelia ambaye ndio mwanzo amezaliwa na kubisha mlango ulimwenguni. Wakati huu, mtu anashawishiwa kutafakari kile ambacho amefanya maishani, thamani ya kuwa hai, ni nini maana yake, kwa nini mtu alikuja ulimwenguni; na wakati huu, mtu anaendelea kutaka kujua kama kweli kunayo maisha baada ya kifo, kama Mbinguni kweli ipo, kama kweli kunayo adhabu…. Kwa kadri mtu anavyokaribia kifo, ndipo anavyotaka zaidi kuelewa maisha yanahusu nini haswa; kwa kadri mtu anavyokaribia kifo, ndipo moyo wake unapoonekana kuwa mtupu; kwa kadri mtu anavyokaribia kifo, ndipo anapohisi kuwa hawezi kusaidika; na kwa hivyo woga wa mtu kuhusu kifo unazidi kuwa mwingi siku baada ya siku. Kunazo sababu mbili zinazoelezea kwa nini watu huwa hivi wanapokaribia kifo: Kwanza, wako karibu kupoteza umaarufu na utajiri ambao maisha yao yalitegemea, wako karibu kuacha nyuma kila kitu kinachoonekana ulimwenguni; na pili, wako karibu kukabiliana, wakiwa peke yao, na ulimwengu usiojulikana, wenye mafumbo, himaya isiyojulikana ambapo wana woga wa kukanyaga guu lao kule, kule wasikokuwa na wapendwa na mbinu zozote za kupata msaada. Kwa hizo sababu mbili, kila mmoja anayekabiliana na kifo huhisi vibaya, hupitia hali ya wasiwasi na hujipata katika hali ya kutoweza kusaidika ambayo hawajawahi kupitia awali. Kwa hakika punde watu wanapofikia wakati huu ndipo wanapotambua kwamba kitu cha kwanza ambacho mtu lazima aelewe, anapokanyaga guu lake hapa duniani, ni wapi binadamu hutoka, kwa nini watu wako hai, nani anayeamuru hatima ya binadamu, ni nani anayekidhi mahitaji ya binadamu, na Aliye na ukuu juu ya uwepo wa binadamu. Hizi ndizo rasilimali za kweli za maisha, msingi muhimu kwa kuwepo kwa binadamu, kutojifunza namna ya kutosheleza familia ya mtu au namna ya kutimiza umaarufu na utajiri, kutojifunza namna ya kujitokeza katika umati au namna ya kuishi maisha mazuri zaidi, bila kutaja namna ya kutia fora na kushindana kwa ufanisi dhidi ya wengine. Ingawaje mbinu mbalimbali za kuishi ambazo watu huishi wakijaribu kumiliki zinaweza kumpa wingi wa tulizo la mali, hazijawahi kumpa mtu amani ya kweli moyoni na tulizo, lakini badala yake hufanya watu kila wakati kupoteza mwelekeo wao, kuwa na wakati mgumu kujidhibiti, kukosa kila fursa ya kujifunza maana ya maisha; na kuunda mawimbi fiche ya matatizo kuhusu namna ya kukabiliana kikamilifu na kifo. Kwa njia hii, maisha ya watu yanaharibika. Muumba hushugulikia kila mmoja bila mapendeleo, huku akipatia kila mmoja wetu fursa ya kutosha maisha yote ili kuweza kupitia na kujua ukuu Wake, ilhali ni mpaka tu kifo kinapokaribia, wakati kivuli cha kifo kinaponing’inia karibu na mtu, ndipo mtu huyu huanza kuona nuru—na kisha muda huwa umeyoyoma mno.

Watu huishi maisha yao wakitafuta pesa na umaarufu; wanashikilia nyuzi hizi, wakifikiri kwamba ndizo mbinu zao pekee za msaada, ni kana kwamba wakiwa nazo wangendeelea kuishi, wangejitoa kwenye hesabu ya wale watakaokufa. Lakini pale tu wanapokuwa karibu kufa ndipo wanapotambua namna ambavyo vitu hivi vilivyo mbali na wao, namna walivyo wanyonge mbele ya kifo, namna wanavyosambaratika kwa urahisi, namna walivyo wapweke na wasivyoweza kusaidika, na hawana popote pa kugeukia. Wanatambua kwamba maisha hayawezi kununuliwa kwa pesa au umaarufu, kwamba haijalishi mtu ni tajiri vipi, haijalishi cheo chake kilivyo cha hadhi, watu wote ni maskini kwa njia sawa na wanaofanya mambo bila mpango mbele ya kifo. Wanatambua kwamba pesa haiwezi kununua maisha, kwamba umaarufu hauwezi kufuta kifo, kwamba si pesa wala umaarufu vinaweza kurefusha maisha ya mtu kwa hata dakika moja, hata sekunde moja. Watu wanapohisi hivi zaidi, ndipo wanapotamani zaidi kuishi; watu wanapohisi hivi zaidi, ndipo wanapohofia kukaribia kwa kifo. Ni katika wakati huu tu ndipo wanapotambua kwa kweli kwamba maisha yao si yao, si yao kudhibiti, na kwamba mtu hana usemi kuhusu iwapo ataishi au atakufa, kwamba haya mambo yote yanapatikana nje ya udhibiti wa mtu.

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp