Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee III

Mamlaka ya Mungu (II) (Sehemu ya Pili)

Awamu Sita katika Maisha ya Binadamu

Katika mkondo wa maisha ya mtu, kila mtu hufikia kwenye misururu ya awamu muhimu. Hizi ni hatua za kimsingi zaidi, na muhimu zaidi, zinazoamua hatima ya maisha ya mtu. Kile kinachofuata ni ufafanuzi mfupi kuhusu mafanikio haya ambayo kila mtu lazima apitie kwenye mkondo wa maisha yake.

Kuzaliwa: Awamu ya Kwanza

Mahali ambapo mtu amezaliwa, amezaliwa katika familia ya aina gani, jinsia ya mtu, umbo la mtu, na wakati wa kuzaliwa: haya ndiyo maelezo ya awamu ya kwanza ya maisha ya binadamu.

Hakuna yeyote aliye na chaguo kuhusu sehemu hizi za awamu hii; zote ziliamuliwa kabla, mapema kabisa na Muumba. Haziathiriwi na mazingira ya nje kwa vyovyote vile, na hakuna masuala yanayosababishwa na binadamu yanaweza kubadilisha hoja hizi ambazo Muumba aliamua kabla. Kwa mtu kuweza kuzaliwa inamaanisha kwamba Muumba tayari ametimiza hatua ya kwanza ya hatima ambayo Amempangilia mtu huyo. Kwa sababu Aliamua kabla maelezo haya yote tena mapema mno, hakuna aliye na nguvu za kubadilisha maelezo yoyote yale. Licha ya hatima ya baadaye ya mtu, hali za kuzaliwa kwa mtu ziliamuliwa kabla, na zinabakia kama zilivyo; haziathiriwi kwa njia yoyote ile na hatima ya mtu katika maisha, wala haziathiri kwa vyovyote vile ukuu wa Muumba juu yazo.

1. Maisha Mapya Yanazaliwa Kulingana na Mipango ya Muumba

Ni maelezo yapi ya awamu ya kwanza—mahali mtu anapozaliwa, familia ya mtu, jinsia ya mtu, umbo la mwili wa mtu, muda wa kuzaliwa kwa mtu—ambayo mtu anaweza kuchagua? Bila shaka, kuzaliwa kwa mtu ni tukio asiloweza kuchagua: Mtu anazaliwa bila hiari yake, katika mahali fulani, muda fulani, kwenye familia fulani, akiwa na umbo fulani la kimwili; mtu anakuwa mmojawapo wa familia fulani bila hiari, anarithi kizazi fulani cha familia. Mtu hana chaguo kwenye awamu hii ya kwanza ya maisha, lakini anazaliwa kwenye mazingira yanayochaguliwa kulingana na mipango ya Muumba, kwenye familia mahususi, na jinsia na umbo mahususi, kwenye wakati mahususi ambao unaunganishwa kwa undani na mkondo wa maisha ya mtu huyu. Mtu anaweza kufanya nini katika awamu hii muhimu? Yote yakisemwa, kwa kweli mtu hana chaguo kuhusu maelezo yoyote yale yanayohusu kuzaliwa kwake. Kama isingekuwa kuamua kabla kwa Muumba na mwongozo Wake, mtu aliyezaliwa upya kwenye ulimwengu huu asingejua ni wapi atakapoenda au ni wapi atakapoishi, asingekuwa na mahusiano yoyote, asingekuwa na popote na asingekuwa na maskani yoyote halisi. Lakini kwa sababu ya mipangilio makinifu ya Muumba, anaanza safari ya maisha yake akiwa na mahali pa kuishi, wazazi, na mahali anapoita nyumbani na watu wa ukoo. Kotekote kwenye mchakato huu, mwanzo wa maisha haya mapya unaamuliwa na mipango ya Muumba, na kila kitu ambacho mtu huyu atakuja kumiliki ataweza kukabidhiwa na Muumba. Kutoka kwenye kiumbe kinachoelea kisichokuwa na jina lolote hadi kinapoanza kuwa na nyama na damu polepole, kinachoweza kuonekana, na hatimaye kuwa binadamu anayeweza kushikika, mojawapo ya viumbe vya Mungu, anayefikiria, anayepumua, anayehisi joto na baridi, anayeshiriki katika shughuli za kawaida za kiumbe kilichoumbwa kwenye ulimwengu yakinifu na ambaye atapitia mambo haya yote ambayo kiumbe kilichoumbwa lazima kipitie maishani. Kule Kuamuliwa kabla kwa kuzaliwa kwa mtu na Muumba kunamaanisha kwamba ataweza kumpa mtu huyu mambo yote yanayohitajika kwa kuishi kwake; na kwamba mtu anazaliwa vilevile inamaanisha kwamba yeye atapokea mambo yote yanayohitajika kutoka kwa Muumba, kwamba kuanzia wakati ule kwenda mbele yeye ataishi katika umbo jingine, linalotolewa na Muumba na linalotii ukuu wa Muumba.

2. Kwa Nini Binadamu Tofauti Wanazaliwa Katika Hali Tofauti

Mara nyingi watu wanapenda kufikiria kwamba, kama wangezaliwa tena, wangezaliwa kwenye familia maarufu; kama wangekuwa wanawake, wangefanana na Binti wa Kifalme Anayependeza na wangependwa na kila mtu, na wangezaliwa wanaume, wangekuwa Kaka Mwenye Mvuto na Haiba, wasikose mahitaji yoyote, huku ulimwengu mzima ukiwaitikia mara moja kila unapoitwa na wao. Mara nyingi kuna wale walio na picha nyingi kuhusu kuzaliwa kwao na huwa hawajatosheka kabisa na huko kuzaliwa kwao, wanachukia familia zao, umbo lao, jinsia yao, na hata wakati wa kuzaliwa kwao. Ilhali watu hawajawahi kuelewa ni kwa nini wamezaliwa katika familia fulani au kwa nini wanafanana jinsi fulani. Hawajui kwamba, licha ya ni wapi wamezaliwa au ni vipi wanavyoonekana, wanafaa kuendeleza wajibu mbalimbali na kutimiza kazi maalum tofautitofauti katika usimamizi wa Muumba—kusudi hili halitawahi kubadilika. Ingawa katika macho ya Muumba, mahali anapozaliwa mtu, jinsia ya mtu, umbo la mwili wa mtu hivi vyote ni vitu vya muda. Ni misururu ya mambo madogomadogo katika kila awamu ya usimamizi Wake wa mwanadamu kwa ujumla. Na hatima halisi ya mtu na mwisho wake vyote haviamuliwi kutokana na wapi ambapo yeye amezaliwa katika awamu yoyote ile, lakini vinaamuliwa na kazi maalum ambayo yeye atatekeleza katika kila maisha, kwa hukumu ya Muumba kwao wakati ambapo usimamizi Wake wa mpango vitakamilika.

Inasemekana kwamba kunayo sababu katika kila athari, na kwamba hakuna athari ambayo haina sababu. Na kwa hivyo kuzaliwa kwa mtu kumefungamanishwa haswa na maisha yake ya sasa na yale ya awali. Kama kifo cha mtu kinasitisha awamu yake ya sasa ya maisha, basi kuzaliwa kwa mtu ndio mwanzo wa mzunguko mpya; kama mzunguko wa kale unawakilisha maisha ya awali ya mtu, basi mzunguko huo mpya kwa kawaida ndio maisha yao ya sasa. Kwa sababu kuzaliwa kwa mtu kunaunganishwa na maisha ya kale ya mtu huyu pamoja na maisha ya sasa ya mtu huyu, mahali anapoishi, familia yake, jinsia, umbo na mambo mengine kama hayo, ambayo yanahusiana na kuzaliwa kwa mtu, vyote vinahusiana na mambo yote. Hii inamaanisha kwamba, mambo yanayoathiri kuzaliwa kwa mtu hayaathiriwi tu na maisha ya awali ya mtu, lakini yanaamuliwa na hatima ya mtu katika maisha ya sasa. Hii inaelezea mseto wa hali tofauti ambazo watu wanazaliwa: Baadhi wanazaliwa katika familia fukara, wengine katika familia tajiri. Baadhi wanazaliwa katika kundi la watu wa kawaida, wengine wanazaliwa katika ukoo wa kipekee. Baadhi wanazaliwa kusini, wengine wanazaliwa kaskazini. Baadhi wanazaliwa jangwani na wengine wanazaliwa katika ardhi zenye rotuba. Kuzaliwa kwa baadhi ya watu kunaandamana na vifijo, vicheko, na sherehe, wengine wanaleta machozi, janga, na matatizo. Baadhi wanazaliwa ili wathaminiwe, wengine wawekwe pembeni kama magugu. Baadhi wanazaliwa wakiwa na heshima na staha na wengine wanazaliwa wakiwa na mikosi na mikasa. Baadhi wanapendeza kuwatazama, na wengine wanatisha kuwatazama. Baadhi wanazaliwa usiku wa manane, wengine wanazaliwa chini ya jua kali la utosi. … Kuzaliwa kwa watu wa kila aina kunaamuliwa na hatima ambazo Muumba ameweka kwa ajili yao; kuzaliwa kwao kunaamua hatima zao katika maisha ya sasa pamoja na wajibu ambao wataendeleza na kazi maalum watakazotimiza. Yote haya yanategemea ukuu wa Muumba, ulioamuliwa kabla na Yeye; hakuna anayeweza kukimbia kundi hili lao lililoamuliwa kabla, hakuna anayeweza kubadilisha hali za[a] kuzaliwa kwao, na hakuna anayeweza kuchagua hatima yake binafsi.

Kukua: Awamu ya Pili

Kutegemea na aina gani ya familia ambayo wamezaliwa ndani, watu hukua katika mazingira tofauti ya nyumbani na wakajifunza mafunzo tofauti kutoka kwa wazazi wao. Hii huamua masharti ambayo mtu anafikisha umri wa kubaleghe na kukua[b] inawakilisha awamu ya pili muhimu ya maisha ya mtu. Inajulikana kwamba, watu hawana chaguo katika awamu hii, vilevile. Hii pia imepangwa, ilipangwa kabla.

1. Hali Ambazo Mtu Hukulia Ndani Zimepangwa na Muumba

Mtu hawezi kuchagua watu au mambo ambayo yataweza kumhimiza na kumwathiri anapokua. Mtu hawezi kuchagua ni maarifa au mbinu gani atapata, ni mazoea gani ataishia kuwa nayo. Mtu hana kauli kuhusiana na wazazi na watu wake wa ukoo, aina ya mazingira ambayo atakulia ndani; mahusiano yake na watu, matukio, na mambo yaliyo katika mazingira yake na namna yanavyoathiri maendeleo yake, vyote ni zaidi ya udhibiti wake. Ni nani anayeamua mambo haya, basi? Ni nani anayeyapangilia? Kwa sababu watu hawana chaguo katika suala hili, kwa vile hawawezi kuamua mambo haya wao wenyewe, na kwa sababu bila shaka hayajipangi yenyewe kwa kawaida, ni wazi kabisa kwamba kuundwa kwa haya yote kunategemea mikono ya Muumba. Kama vile tu Muumba anavyopanga hali fulani za kuzaliwa kwa kila mtu, Yeye hupangilia pia hali mahususi ambazo mtu hukulia, bila shaka. Kama kuzaliwa kwa mtu kutaleta mabadiliko kwa watu, kwa matukio, na mambo yanayomzunguka yeye, basi kukua na maendeleo ya mtu huyo vyote vitaweza kuwaathiri vilevile. Kwa mfano, baadhi ya watu wanazaliwa katika familia fukara, lakini wanalelewa wakiwa wemezungukwa na utajiri; wengine wanazaliwa katika familia tajiri lakini husababisha utajiri wa familia zao kupungua, kiasi cha kwamba wanalelewa katika mazingira ya kimaskini. Hakuna kuzaliwa kwa yeyote kunatawaliwa na kanuni isiyobadilika, na hakuna anayelelewa katika hali zisizozuilika, na zisizobadilika. Haya si mambo ambayo binadamu anaweza kufikiria au kudhibiti; mambo haya yote ni mazao ya hatima ya mtu, na yanaamuliwa na hatima ya mtu. Bila shaka, kimsingi ni kwamba yote haya yaliamuliwa kabla katika hatima ya mtu na Muumba, yanaamuliwa na ukuu wa Muumba juu ya, na mipango Yake ya, hatima ya mtu huyu.

2. Hali Mbalimbali Ambazo Watu Hukulia Ndani Husababisha Wajibu Tofauti

Hali za kuzaliwa kwa mtu huanzisha katika kiwango cha kimsingi mazingira na hali ambazo hukulia ndani, na hali ambazo mtu hukulia ndani vilevile ni zao la hali za kuzaliwa kwake. Kwenye wakati huu mtu anaanza kujifunza lugha, na akili za mtu zinaanza kukumbana na kuchanganua mambo mengi mapya, na katika mchakato huu mtu anakua bila kusita. Mambo ambayo mtu anasikia kwa masikio yake, anaona kwa macho yake, na anang’amua kwa akili zake huboresha na kuhuisha kwa utaratibu ulimwengu wa ndani wa mtu. Watu, matukio, na mambo ambayo mtu anakumbana nayo, maarifa ya kawaida, maarifa, na mbinu anazojifunza, na njia za kufikiria ambazo mtu anaathiriwa nazo, anaambiwa au kufunzwa, vyote vitamwongoza na kuathiri hatima ya maisha yake. Lugha anayojifunza mtu anapokua na njia yake ya kufikiria haviwezi kutenganishwa kutoka kwenye mazingira ambayo yeye analelewa katika ujana wake, na hayo mazingira yana wazazi, ndugu zake, na watu wengine, matukio, na mambo yanayomzunguka. Kwa hivyo mkondo wa maendeleo ya mtu unaamuliwa na mazingira ambayo yeye anakulia ndani, na pia unategemea watu, matukio, na mambo ambayo mtu anakumbana nayo kwenye kipindi hiki cha muda. Kwa sababu masharti ambayo mtu hukulia ndani yaliamuliwa kabla na tena mapema mno, mazingira anayoishi kwenye mchakato huu pia, kwa kawaida, yaliamuliwa kabla. Hayaamuliwi na chaguo na mapendeleo ya mtu, lakini yanaamuliwa kulingana na mipango ya Muumba, yanaamuliwa na mipangilio makinifu ya Muumba, na ukuu wa Muumba juu ya hatima ya mtu huyo katika maisha. Kwa hivyo watu ambao mtu yeyote hukumbana nao katika mkondo wa kukua, na mambo ambayo mtu hukutana nayo, vyote vimeunganishwa bila kuzuilika kwa mipango na mipangilio ya Muumba. Watu hawawezi kutabiri aina hizi za mahusiano mapevu, wala hawawezi kuyadhibiti au kuweza kuyaelewa. Mambo mengi tofauti na watu wengi tofauti wanao mwelekeo wa mazingira ambayo mtu hukulia, na hakuna binadamu anaweza kupangilia na kupanga mtandao mpana kama huo wa maunganisho. Hakuna mtu au kitu isipokuwa Muumba anaweza kudhibiti kujitokeza, kuwepo, na kutoweka kwa watu mbalimbali, matukio na mambo, na ni mtandao mpana ajabu wa maunganisho unaounda maendeleo ya mtu kama ilivyoamuliwa kabla na Muumba, na kuunda mazingira tofauti ambayo watu wanakulia ndani, na kuunda wajibu mbalimbali unaohitajika kwa minajili ya kazi ya Muumba ya usimamizi, kuweka misingi thabiti, yenye nguvu ili watu waweze kukamilisha kwa ufanisi kazi yao maalum.

Tanbihi:

a. Maandishi asilia yameacha kauli “zile hali za.”

b. Maandishi asilia yanasoma “hii.”

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp