Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee X

Mungu ni Chanzo cha Uhai kwa Vitu Vyote (IV) (Sehemu ya Nne)

Mahitaji ya Mungu kwa Wanadamu

1. Utambulisho na Hadhi ya Mungu Mwenyewe

Tumefikia mwisho wa mada ya “Mungu ni chanzo cha uhai kwa vitu vyote,” vilevile na ile ya “Mungu ni wa kipekee Mungu Mwenyewe.” Baada ya kufanya hivyo, tunahitaji kufanya muhtasari. Muhtasari wa aina gani? Unaomhusu Mungu Mwenyewe. Kwa kuwa ni kumhusu Mungu Mwenyewe, basi lazima ugusie kila kipengele cha Mungu, vilevile aina ya imani ya watu kwa Mungu. Na kwa hiyo, kwanza lazima Niwaulize: Baada ya kusikia mahubiri, Mungu ni nani katika jicho la mawazo yako? (Muumbaji.) Mungu katika jicho la mawazo yako ndiye Muumbaji. Kuna kitu kingine chochote? Mungu ni Bwana wa vitu vyote. Maneno haya yanafaa? (Yanafaa.) Mungu ndiye mtawala wa vitu vyote, na anayeendesha vitu vyote. Aliumba vitu vyote, Anaendesha vitu vyote, na pia Anatawala vitu vyote na kukimu vitu vyote. Hii ndiyo hadhi ya Mungu, na utambulisho wa Mungu. Kwa vitu vyote na vyote vilivyopo, utambulisho wa kweli wa Mungu ni Muumbaji, na Mtawala wa vitu vyote. Huo ni utambulisho unaomilikiwa na Mungu, na ni wa kipekee miongoni mwa vitu vyote. Hakuna Kati ya viumbe wa Mungu—wawe miongoni mwa wanadamu, au katika ulimwengu wa kiroho—ambao wanaweza kutumia namna yoyote au kisingizio kuiga au kuchukua nafasi ya utambulisho wa Mungu na hadhi Yake, kwa kuwa kuna mmoja tu kati ya vitu vyote anayemiliki huu utambulisho, nguvu, mamlaka, na uwezo wa kutawala vitu vyote: Mungu wetu wa kipekee Mwenyewe. Anaishi na kutembea miongoni mwa vitu vyote; Anaweza kufikia palipo mbali zaidi, juu ya vitu vyote; Anaweza kunyenyekea kwa kuwa mwanadamu, kuwa mmoja wa wenye mwili na damu, kuonana ana kwa ana na watu na kushiriki na wao dhiki na faraja; wakati huo huo, Anaamuru vitu vyote, na Huamua hatima ya vitu vyote, na njia itakayofuata, zaidi na hayo, Anaongoza hatima za wanadamu wote, na njia za wanadamu. Mungu kama huyu anastahili kuabudiwa, kuheshimiwa, na kujulikana na viumbe wote. Na hivyo, pasipo kujali uko katika kundi na aina gani ya wanadamu, kumwamini Mungu, kumfuata Mungu, kumheshimu Mungu sana, kukubali utawala wa Mungu, na kukubali mipango ya Mungu katika hatima yako ndio uamuzi wa pekee, na uamuzi unaofaa, kwa mtu yeyote, kwa kiumbe chochote kinachoishi. Katika upekee wa Mungu, watu huona kwamba mamlaka Yake, tabia Yake ya haki, kiini Chake, na namna ambazo Anakirimia vitu vyote ni za kipekee; upekee Wake unabainisha utambulisho wa kweli wa Mungu Mwenyewe, na unabaini hadhi Yake. Na kwa hivyo, miongoni mwa viumbe vyote, kama kuna kiumbe anayeishi katika ulimwengu wa kiroho au miongoni mwa wanadamu angetamani kusimama badala ya Mungu, haingewezekana, sawa na kujaribu kumuiga Mungu. Huu ni ukweli. Ni mahitaji yapi kwa mwanadamu aliyonayo Muumbaji na Mtawala kama huyu, ambaye Aliye na utambulisho, nguvu, na hadhi ya Mungu Mwenyewe? Hili linapaswa kuwa wazi kwa kila mtu, na linapaswa kukumbukwa nanyi, na ni muhimu sana kwa Mungu na mwanadamu!

2. Mielekeo Mbalimbali ya Wanadamu kwa Mungu

Jinsi watu wamtendeavyo Mungu huamua hatima yao, na huamua jinsi Mungu anavyowatendea na kuwashughulikia. Kufikia sasa nitawapa mifano kadhaa ya jinsi watu wanavyotenda mbele za Mungu. Hebu tusikie kitu kuhusu ama mienendo na tabia ambazo kwazo wanamtendea Mungu ni sahihi au la. Hebu tuangalie mwenendo wa aina saba za watu wafuatao:

1) Kuna aina moja ya watu ambao mwelekeo wao kwa Mungu haswa ni wa kipuuzi. Wanafikiria kuwa Mungu ni kama Bodhisattva au kiumbe takatifu wa masimulizi ya kibinadamu, na kuwataka watu kusujudu mara tatu wanapokutana na kuchoma ubani baada ya kula. Kwa hivyo, katika mioyo yao, wanapomshukuru Mungu kwa neema Yake, na kuwa wenye shukrani kwa Mungu, mara nyingi wana msukumo kama huo. Hivyo wanatamani Mungu wanaomwamini leo, kama kiumbe takatifu wanayemtamania ndani ya mioyo yao, anaweza kukubali mienendo yao Kwake ambapo wanasujudu mara tatu wanapokutana, na kuchoma ubani baada ya kula.

2) Watu wengine wanamwona Mungu kama Budha anayeishi, mwenye uwezo wa kutoa wanaoishi wote kutoka kwenye mateso, na kuwaokoa; wanaona Mungu kama Budha anayeishi mwenye uwezo wa kuwatoa kwenye mateso mengi. Imani ya watu hawa kwa Mungu ni kumwabudu Mungu kama Buddha. Ijapokuwa hawachomi ubani, kusujudu, au kutoa sadaka, katika nyoyo zao Mungu ni kama tu Buddha, na huwataka tu wawe wema na wenye huruma, kuwa wasiue chochote kilicho hai, wasiwaapie wengine, waishi maisha yanayoonekana kuwa manyoofu, na wasifanye chochote kibaya—vitu hivi tu. Huyu ndiye Mungu mioyoni mwao.

3) Watu wengine humwabudu Mungu kama mtu mkubwa au maarufu. Kwa mfano, kwa namna yoyote mtu huyu mkubwa hupenda kuongea, kwa kiimbo chochote huongea, maneno na msamiati anaotumia, kiimbo chake, ishara zake za mikono, maoni na matendo yake, ukali wake—wanaiga yote, na hivi ndivyo vitu ambavyo ni lazima watavisababisha katika mwendo wa imani yao kwa Mungu.

4) Watu wengine wanamwona Mungu kama mfalme, wanahisi kuwa Yuko juu ya vitu vyote vingine, na hakuna anayejaribu kumkosea—na wakifanya hivyo, wataadhibiwa. Wanaabudu mfalme kama huyo kwa sababu wafalme huwa wanashikilia sehemu fulani kwenye mioyo yao. Mawazo, tabia, mamlaka, na asili ya wafalme—hata na maslahi na maisha yao ya kibinafsi—yote huwa kitu ambacho watu hawa lazima waelewe, masuala na mambo ambayo wanashughulika nayo, na hivyo wanamwabudu Mungu kama mfalme. Imani ya namna hiyo inachekesha.

5) Watu wengine wana imani fulani katika uwepo wa Mungu, ambayo ni kubwa na isiyotingishika. Kwa sababu ufahamu wa Mungu kwao ni wa juujuu mno na hawana mazoea ya maneno ya Mungu, wanamwabudu kama sanamu. Sanamu hii ni Mungu aliye ndani ya mioyo yao, ni kitu ambacho wanafaa kuogopa na kusujudia, na ambayo wanalazimika kufuata na kuiga. Wanamwona Mungu kama sanamu, ambayo wanafaa kufuata maisha yao yote. Wanaiga sauti ambayo kwayo Mungu huzungumza, na kwa nje wanaiga wale ambao Mungu anapenda. Aghalabu wanafanya mambo ambayo yanaonekana kuwa manyoofu, safi, na ya kweli, na wanafuata hii sanamu kama mwenzao au mwandani wao ambaye wanaweza kushirikiana. Hiyo ndiyo aina ya imani yao.

6) Kuna watu ambao, kando na kusoma maneno mengi ya Mungu na kuwa wameyasikia mahubiri mengi, wanahisi ndani ya nyoyo zao kuwa msimamo tu wa mienendo yao kwa Mungu ni kuwa kila wakati wanafaa wawe watiifu na kujipendekeza, la sivyo wanafaa kumsifu Mungu na kumwabudu kwa njia isiyo halisi. Wanaamini kuwa Mungu ni Mungu anayewahitaji kutenda hivyo, na wanaamini kuwa wasipofanya hivyo, basi wakati wowote wanaweza kuchochea hasira Yake au kumtenda dhambi, na kwamba kwa sababu ya kutenda dhambi Mungu atawaadhibu. Huyo ndiye Mungu mioyoni mwao.

7) Kisha kuna watu wengi, wanaotafuta riziki ya kiroho katika Mungu. Kwa sababu wanaishi katika ulimwengu huu, hawana amani au furaha, na hakuna wanapopata faraja. Baada ya kumpata Mungu, wanapokuwa wameona na kusikia maneno Yake, ndani ya mioyo yao wanafurahi na kusisimka kisiri. Na kwa nini hivyo? Wanaamini kuwa tayari wamepata mahali ambapo patawapa furaha, kwamba hatimaye wamepata Mungu ambaye atawapa riziki ya kiroho. Hii ni kwa sababu, baada ya kukubali Mungu na kuanza kumfuata, wanakuwa wenye furaha, maisha yao yanakamilishwa, hawako kama wengine wasioamini tena, wanaotembea usingizini maishani mwao kama wanyama, na wanahisi kuwa kuna kitu cha kutamania katika maisha. Kwa hivyo, wanafikiri kuwa huyu Mungu anaweza kuwatimizia mahitaji yao ya kiroho na kuleta furaha kubwa katika mawazo na Roho. Bila ya kujua, wanakuwa hawawezi kumwacha huyu Mungu anayewapa riziki ya kiroho, Anayeleta furaha katika Roho na familia zao. Wanaamini kuwa imani katika Mungu haihitaji zaidi ya kuwapa riziki ya kiroho.

Je, mielekeo kumwelekea Mungu ya watu hawa wa aina mbalimbali waliotajwa hapo juu ipo miongoni mwenu? (Ipo.) Kama, katika imani yao katika Mungu, moyo wa mtu una mwelekeo wowote kati ya hii, je, kweli wanaweza kuja mbele za Mungu? Kama watu wana mwelekeo wowote kati ya hii katika mioyo yao, je, wanamwamini Mungu? Je, wanamwamini Mungu Mwenyewe yule wa kipekee? (La.) Kwa kuwa humwamini Mungu wa kipekee Mwenyewe, unamwamini nani? Kama unachoamini si Mungu Mwenyewe wa kipekee, kuna uwezekano unaamini katika sanamu, mtu maarufu, au Bodhisattva, kuwa unamwabudu Budha moyoni mwako. Zaidi ya hayo, kuna uwezekano unaamini katika mtu wa kawaida. Kwa muhtasari, kwa sababu ya aina tofautitofauti za imani za watu na mielekeo kwa Mungu, watu humweka Mungu wa utambuzi wao wenyewe katika nyoyo zao, wanamlazimishia Mungu fikira zao, wanaweka fikira na mielekeo yao kuhusu Mungu sambamba na Mungu Mwenyewe wa kipekee, na kisha wanayanyanyua juu kuyashangilia. Ina maana gani watu wakiwa na mielekeo hiyo isiyofaa kwa Mungu? Ina maana kuwa wamemkataa Mungu wa kweli Mwenyewe na kuabudu Mungu bandia, na ina maana kuwa wakati uleule wanapomwamini Mungu, wanamkataa Mungu, wanampinga, na kuwa wanakana uwepo wa Mungu wa kweli. Kama watu watazidi kushikilia imani za aina hiyo, matokeo yao yatakuwa gani? Kwa aina hiyo ya imani, je, wanaweza kufikia karibu na kutimiza matakwa ya Mungu? (La, hawawezi.) Kinyume cha hayo, kwa sababu ya dhana na fikira zao, watu watazidi kuwa mbali na njia ya Mungu, kwa kuwa njia wanayoifuata ni kinyume cha njia ambayo Mungu anawahitaji waifuate. Umekwisha kusikia hadithi ya “kwenda kusini kwa kuendesha gari la farasi kuelekea kaskazini”? Hii yaweza kuwa ni mfano wa kwenda kusini kwa kuendesha gari la farasi kuelekea kaskazini. Watu wakimwamini Mungu kwa njia hii ya kipumbavu, basi kadiri unavyojaribu kwa nguvu, ndivyo utakavyokuwa mbali zaidi na Mungu. Na kwa hiyo nakuonya hivi: Kabla ya kufunga safari, ni lazima kwanza ujue kama unaenda njia iliyo sawa. Lenga katika juhudi zako, kuwa na uhakika na kujiuliza, “Je, Mungu ninayemwamini ni Mtawala wa vitu vyote? Je, huyu Mungu ninayemwamini ni mtu tu wa kunipa riziki ya kiroho? Ni sanamu yangu? Je, huyu Mungu ninayemwamini anataka nini kutoka kwangu? Mungu huwa anakubali chochote ninachokifanya? Je, kila kitu ninachokifanya na kutafuta kinalingana na kazi ya kumjua Mungu? Je, kinalingana na mahitaji ya Mungu kwangu? Je, njia ninayoifuata inajulikana na kukubaliwa na Mungu? Je, Mungu anaridhishwa na imani yangu?” Aghalabu na mara kwa mara unafaa ujiulize haya maswali. Kama ungetaka kuutafuta ufahamu wa Mungu, basi lazima uwe na dhamiri safi na malengo wazi ndipo uweze kumridhisha Mungu.

Inawezekana kuwa, kutokana na ustahimilivu Wake, Mungu anaweza kukubali mielekeo hii hasi ambayo Nimeizungumzia shingo upande? Mungu anaweza kuipongeza mielekeo ya watu hawa? Ni mahitaji yapi ya Mungu kwa wanadamu na wale ambao wanamfuata? Je, mnajua ni mwelekeo gani anaouhitaji kwa watu? Leo, nimezungumza mengi, nimezungumzia mengi kuhusu mada ya Mungu Mwenyewe, pamoja na matendo ya Mungu na kile Anacho na alicho. Sasa unajua ni kitu gani Mungu anatamani kupata kutoka kwa watu? Unajua ni kitu gani Mungu anataka kutoka kwako? Zungumzeni. Kama bado ufahamu wako kutokana na mazoea na matendo yako unakosa au ni wa juujuu sana, unaweza kusema kitu kuhusu ufahamu wako juu ya maneno haya. Una ufahamu kwa muhtasari? Ni kitu gani Mungu anahitaji kwa wanadamu? (Wakati wa huu ushirika mbalimbali, Mungu ametoa mkazo wa kututaka tumjue Mungu, tujue matendo Yake, tujue kuwa ni Yeye chanzo cha uhai kwa vitu vyote, tujue hadhi na utambulisho Wake, na kujua wajibu wetu kama viumbe wa Mungu. Mungu alikuwa na maneno wazi kuhusu ni kwa kitu gani tunapaswa kuweka jitihada zetu zote, mahitaji Yake kwetu, Anapenda aina gani ya watu, na aina Anayoichukia.) Na ni nini matokeo ya mwisho Mungu anapohitaji watu wamjue? (Wajue kwamba Mungu ndiye Muumbaji, na kuwa watu ni viumbe walioumbwa.) Wanapopata ufahamu kama huu, ni mabadiliko yapi yanakuwepo katika mwelekeo wa watu kwa Mungu, tabia zao na mbinu za utekelezaji, au tabia ya maisha yao? Umewahi kuwaza kuhusu hili? Inaweza kusemwa kuwa, baada ya kumjua Mungu, na kumfahamu, wanakuwa watu wazuri? (Imani katika Mungu sio kwa ajili ya kuwa mtu mzuri.) Na kwa hivyo wanapaswa wawe watu wa aina gani? (Lazima wawe viumbe stahili wa Mungu.) (Lazima wawe wa kweli.) Kuna kitu kingine chochote? (Baada ya kumjua Mungu kweli na kwa usahihi, tunaweza kumtendea Mungu kama Mungu, tunajua kuwa Mungu daima ni Mungu, kuwa sisi ni viumbe walioumbwa, tunapaswa kumwabudu Mungu, na kushikilia nafasi zetu.) Vizuri sana! Hebu tusikie kutoka kwa wengine. (Tunamjua Mungu, na hatimaye tunaweza kuwa watu ambao wanamtii Mungu kweli, kumheshimu Mungu sana, na kuepuka maovu.) Huo ni ukweli.

3. Mwelekeo Ambao Mungu Anahitaji Mwanadamu Awe Nao Kwake

Kwa kweli, Mungu hana mahitaji sana kwa wanadamu—au angalau, hana mahitaji kama watu wanavyodhani. Bila matamshi ya Mungu, au udhihirishaji wowote wa tabia Yake, matendo, au maneno, basi kumjua Mungu kungekuwa kugumu sana kwenu, kwa sababu watu wangelazimika kukisia nia ya Mungu na mapenzi Yake, kitu ambacho ni kigumu sana kwao. Lakini kutokana na hatua ya mwisho ya Kazi Yake, Mungu amenena maneno mengi, kufanya kiwango kikubwa cha kazi, na kufanya mahitaji mengi kwa wanadamu. Katika maneno Yake, na kiwango kikubwa cha kazi Yake, amejulisha watu anachokipenda, anachokichukia, na wanafaa kuwa aina gani ya watu. Baada ya kuelewa vitu hivi, ndani ya nyoyo watu wanafaa kuwa na maelezo sahihi ya mahitaji ya Mungu, kwa kuwa hawamwabudu tena yule Mungu asiye yakini, au kumfuata Mungu katika ukosefu uyakini na udhahania na utupu; badala yake, watu wanaweza kusikia maneno ya Mungu, wanaweza kuelewa viwango vya mahitaji ya Mungu, na kuvifikia, na Mungu hutumia lugha ya wanadamu kuwaambia watu yale yote wanafaa kujua na kulewa. Leo, kama watu hawafahamu mahitaji ya Mungu kwao, kile Mungu alicho, kwa nini wanamwamini Mungu, na jinsi wanafaa kumwamini Mungu na jinsi wanavyojichukulia mbele Zake, basi kuna shida hapa. Sasa hivi tu kila mmoja wenu amezungumza kuhusu kipengele kimoja; mnafahamu kuhusu mambo fulani, yawe ni mambo mahususi au ya jumla—lakini Ningependa kuwaambia mahitaji ya Mungu ya kweli, kamili, na mahususi kwa wanadamu. Ni maneno machache tu, na rahisi sana. Yawezekana tayari mnayajua haya maneno. Mahitaji sahihi ya Mungu kwa wanadamu na wale ambao wanamfuata ni kama ifuatavyo. Mungu anahitaji mambo matano kutoka kwa wale wanaomfuata; imani ya kweli, ufuasi wenye uaminifu, utiifu kamili, ufahamu wa kweli na heshima za kutoka moyoni.

Katika mambo haya matano, Mungu anahitaji kuwa watu wasimshuku tena, wala kumfuata wakitumia fikira zao au mitazamo ikosayo uyakini na iliyo dhahania; Ni lazima wamfuate Mungu bila fikira au dhana zozote. Mungu anahitaji kuwa wote wanaomfuata wafanye hivyo kwa uaminifu, sio kwa shingo upande au bila kujizatiti. Mungu anapokupa mahitaji yoyote, au kukujaribu, kukuhukumu, kukushughulikia na kukupogoa, au kukuadhibu na kukuangamiza, unapaswa kuwa mtiifu kabisa Kwake. Hufai kuuliza kilichosababisha, au kuweka masharti, au hata uongee kuhusu sababu. Utiifu wako lazima uwe usio na shaka. Kumjua Mungu ni kipengele ambacho watu wengi wanakosea. Mara kwa mara wanamlazimishia Mungu misemo, matamshi, na maneno ambayo hayahusiani na Yeye, wakiamini kuwa haya maneno ndiyo ya kweli kuhusu kumfahamu Mungu. Kumbe hawajui kuwa hii misemo, ambayo inatoka kwa fikira za watu, ung’amuzi wao, na busara zao, havina uhusiano wowote na kiini cha Mungu. Na kwa hiyo, Ninataka kukwambia kuwa, katika ufahamu wa watu unaotamaniwa na Mungu, Mungu haulizi tu kwamba umtambue Mungu na maneno Yake, lakini kuwa ufahamu wako juu ya Mungu ni sahihi. Hata kama unaweza kusema sentensi moja tu, au una ufahamu mdogo tu, huu ufahamu mdogo ni sahihi na wa kweli, na unalingana na kiini cha Mungu Mwenyewe. Kwa kuwa Mungu hapendi sifa na wao kumtukuza Yeye kwa hali isiyo halisi na yenye nia mbaya. Zaidi ya hayo, Anachukia watu wanapomchukulia kama hewa. Anachukia ambapo, wakati wa majadiliano juu ya mada kuhusu Mungu, watu wanazungumza kimzaha, wakiongea kwa hiari bila ya kujali, wakiongea wapendavyo; zaidi ya hayo, anawachukia wale wanaojifanya wanamjua Mungu, na wanaringa kuhusu ufahamu wa Mungu, wakijadili mada kuhusu Mungu bila mipaka au kipimo. La mwisho Kati ya yale mahitaji matano lilikuwa ni kumheshimu Mungu kutoka moyoni. Hili ndilo hitaji kuu la Mungu kwa wale wote wanaomfuata. Wakati mtu ana ufahamu wa kweli na sahihi kumhusu Mungu, anaweza kumheshimu Mungu na kuepuka maovu. Heshima hii hutoka ndani ya moyo wake, ni ya hiari, na sio kwa sababu Mungu amemshurutisha. Mungu hataki utoe zawadi ya mwelekeo wowote wa kupendeza, au tabia, au mienendo ya nje Kwake; badala yake, anataka kwamba umheshimu na umwogope kutoka ndani ya moyo wako. Heshima hii inaafikiwa kutokana na mabadiliko katika tabia ya maisha yako, kwa sababu una ufahamu juu ya Mungu, kwa sababu unaelewa matendo ya Mungu, kwa sababu ya uelewa wako wa kiini cha Mungu, na kwa sababu umetambua ukweli kuwa wewe ni mmoja wa viumbe wa Mungu. Na kwa hiyo, nia yangu ya kutumia neno “kutoka moyoni” kwa kurejelea heshima hapa ni kwamba wanadamu waelewe kuwa heshima ya watu kwa Mungu inapaswa kutoka ndani ya mioyo yao.

Sasa yafikirie hayo matakwa matano: kuna yeyote kati yenu anaweza kupata matatu ya kwanza? Ambapo Ninamaanisha uaminifu wa kweli, ufuasi wenye uaminifu, na utiifu kamili. Kuna wowote kati yenu wanaoweza mambo haya? Najua Nikisema yote matano, basi bila kuuliza hapatakuwa na hata mmoja kati yenu anayeweza—lakini nimeyapunguza hadi matatu. Tafakari kama umeyapata au la. Je, “uaminifu wa kweli” ni rahisi kuupata? (La, sio rahisi.) Sio rahisi, kwa kuwa mara nyingi watu humtilia Mungu mashaka. Na, je, “ufuasi wenye uaminifu”? Huu “uaminifu” una maana gani? (Sio kwa shingo upande ila kwa moyo wote.) Sio kwa shingo upande ila kwa moyo wote. Mmegonga ndipo! Kwa hiyo, je, mna uwezo wa kupata hili hitaji? Inabidi mjitahidi zaidi—siyo? Kwa sasa bado hamjapata hili hitaji. Kuhusu “utiifu kamili”—je, mmepata hilo? (Hapana.) Bado hamjapata hilo, pia. Mara nyingi nyinyi si watiifu na ni waasi, mara nyingi hamsikilizi, au kupenda kutii, au kutaka kusikia. Haya ndiyo mahitaji matatu ya msingi wanayopata watu baada ya kuingia katika maisha yao, na bado hamjayapata. Kwa hiyo, kwa wakati huu, mna uwezo mkubwa? Leo, baada ya kunisikia nikisema maneno haya, mna wasiwasi? (Ndiyo.) Ni sawa kuwa mna wasiwasi. Msiwe na wasiwasi Ninahisi wasiwasi kwa niaba yenu. Sitakwenda katika mahitaji hayo mengine mawili; bila shaka, hakuna anayeweza kuyafikia. Mna shauku. Kwa hivyo mmebaini malengo yenu? Malengo yapi, kuelekeza upande gani, mnapaswa kuyafuata, na kujitolea jitihada zenu? Mna lengo? Hebu niongee waziwazi: mnapofikia mahitaji haya matano, mtakuwa mmemridhisha Mungu. Kila mojawapo ni ishara, ishara ya watu wakiingia katika maisha wakiwa wamefikia ukomavu, na lengo la mwisho la hii. Hata kama Ningechukua moja kati ya mahitaji na kuongea kwa kina kulihusu na kinachohitajika, haiwezi kuwa rahisi kupata; ni lazima mpitie kiwango fulani cha matatizo na kufanya kiasi fulani cha juhudi. Na ni aina gani ya mawazo mnapaswa kuwa nayo? Yanapaswa kuwa sawa na yale ya mgonjwa wa saratani anayesubiri kwenda kwenye meza ya upasuaji. Na ni kwa nini Ninasema haya? Kama ungependa kumwamini Mungu, na kumpata Mungu na kupata ridhaa Yake, basi kama hutapitia katika kiasi fulani cha shida, au kufanya kiwango fulani cha juhudi, hutaweza kupata vitu hivi. Umesikia mahubiri mengi, lakini kuyasikia hakumaanishi kuwa haya mahubiri ni yako; ni lazima uyachukue na kuyageuza yawe kitu ambacho ni chako, ni lazima uyasimilishe maishani mwako, na kuyaleta katika uwepo wako, ukiyaruhusu maneno na mahubiri haya yakuongoze katika maisha yako, na kuleta dhamana na maana ya uhai katika maisha yako—na hivyo basi itakuwa ni thamani kuwa uliyasikia maneno haya. Kama maneno haya Ninayoyanena hayaleti mabadiliko yoyote katika maisha yenu, au thamani yoyote katika uwepo wako, basi hakuna haja ya kuyasikiliza. Mnaelewa haya, ndiyo? Baada ya kuelewa haya, basi kilichobaki ni juu yenu wenyewe. Ni lazima mfanye kazi! Ni lazima muwe na bidii katika kila jambo! Msiwe huku na kule—wakati unapita upesi! Wengi wenu wameamini kwa zaidi ya miaka kumi. Tazama nyuma kwa hii miaka zaidi ya kumi ya imani katika Mungu: Umenufaika kiasi gani? Na mmesalia na miongo mingapi ya haya maisha? Sio mirefu. Sahau kuhusu iwapo kazi ya Mungu inakusubiri, iwapo Amekuachia nafasi, iwapo Atafanya kazi ile ile tena; usizungumze kuhusu hili. Unaweza kurudisha nyuma miaka yako kumi iliyopita? Kwa kila siku inayopita, na kila hatua unayochukua, siku ambazo unazo hupunguzwa kwa siku moja. Muda haumsubiri mwanadamu yeyote! Utanufaika tu kutokana na imani kwa Mungu kama utaichukulia kama kitu kikubwa zaidi maishani mwako, muhimu zaidi kuliko chakula, mavazi, au kitu kingine chochote! Kama huwa unaamini tu unapokuwa na wakati, na huwezi kutoa umakini wako wote kwa imani yako, kama siku zote umetatizwa na vurugu, basi hutafaidi chochote. Unaelewa hili, ndio? Tutaishia hapa kwa leo. Tuonane wakati ujao! (Shukrani kwa Mungu!)

Februari 15, 2014

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp