Maneno ya Mungu ya Kila Siku: Kuingia Katika Uzima | Dondoo 496

Ushughulikiaji wa Mungu juu ya tabia za nje za watu ni sehemu moja ya kazi Yake; kwa mfano, kushughulikia ubinadamu wa watu wa nje, usiokuwa wa kawaida, au maisha na tabia zao, njia na desturi zao, na vilevile vitendo vyao vya nje, na hamasa zao. Lakini Anapowataka watu wauweke ukweli katika vitendo na wabadilishe tabia zao, kimsingi kinachoshughulikiwa hapa ni motisha na mawazo yaliyo ndani yao. Kushughulikia tabia zako za nje tu si kugumu; ni sawa na kukukataza kula vitu uvipendavyo, jambo ambalo ni rahisi. Kinachogusia dhana zilizo ndani yako, hata hivyo, si rahisi kukiachia: inakuhitaji uuasi mwili wako, na kulipa gharama, na kuteseka mbele za Mungu. Hii ndiyo hali hasa katika motisha za watu. Tangu wakati wa imani yao kwa Mungu mpaka leo, watu wamekuwa na motisha ambazo si sahihi. Wakati ambapo huweki ukweli katika vitendo, unahisi kuwa motisha zako ni sahihi, lakini jambo likikutokea, utaona kuwa kuna motisha nyingi ndani zisizo sahihi. Hivyo, Mungu akiwafanya watu kuwa wakamilifu, Anawafanya kugundua kuwa kuna dhana nyingi ndani yao ambazo zinawazuia kumfahamu Mungu. Ukitambua kuwa motisha zako zina makosa, kama unaweza kuacha kutenda kulingana na motisha na dhana zako, na unaweza kuwa na ushuhuda wa Mungu na kusimama imara katika msimamo wako kwa kila lifanyikalo kwako, hili linathibitisha kuwa umeuasi mwili wako. Ukiasi dhidi ya mwili wako, bila shaka kutakuwa na vita ndani yako. Shetani atajaribu kukufanya ufuate mwili wako, atakufanya ufuate dhana za kimwili na kutekeleza maslahi ya kimwili—ila maneno ya Mungu yatakupa nuru na kukuangazia kwa ndani, na wakati huu itakuwa juu yako ikiwa utamfuata Mungu au utamfuata Shetani. Mungu anawataka watu kuweka ukweli katika matendo kimsingi kushughulikia mambo yaliyo ndani yao, kushughulikiwa fikira zao, na dhana zao ambazo haziufuati moyo wa Mungu. Roho Mtakatifu anawagusa watu ndani, na kuendeleza kazi Yake ndani yao, na kwa hivyo katika tukio lolote kuna vita: kila wakati watu wanapoweka ukweli katika vitendo, au kuweka mapenzi ya Mungu katika vitendo, huwa kuna vita vikali, na japokuwa mambo yanaweza kuonekana shwari katika miili yao, ila ndani ya mioyo yao kutakuwa na vita vya kufa na kupona—na ni baada tu ya hivi vita vikali, baada ya kutafakari kwa kina, ndipo ushindi au kushindwa kunaweza kuamuliwa. Mtu anashindwa kujua ama acheke au alie. Kwa sababu motisha nyingi ndani ya watu zina makosa, ama kwa sababu kazi kubwa ya Mungu inakinzana na dhana zao, watu wakiuweka ukweli katika vitendo vita vikali huzuka kisirisiri. Baada ya kuuweka huu ukweli katika vitendo, kisirisiri watu watakuwa wamemwaga machozi mengi sana ya huzuni kabla ya kuamua kumridhisha Mungu. Ni kwa sababu ya vita hivi watu huvumilia shida na usafishaji; huku ni kuteseka kwa kweli. Vita vikikukabili, kama unaweza kusimama kweli upande wa Mungu, utaweza kumridhisha. Kuteseka katika harakati ya kutenda ukweli hakuepukiki; ikiwa, wanapoweka ukweli katika vitendo, kila kitu ndani yao kingekuwa sawa, basi wasingehitaji kufanywa wakamilifu na Mungu, na kusingekuwa na vita, na hawangeteseka. Ni kwa sababu kuna mambo mengi ndani ya watu ndipo hawafai kutumiwa na Mungu, na tabia nyingi za uasi wa mwili, ndipo watu wanapaswa kujifunza funzo la kuasi dhidi ya mwili kwa kina zaidi. Huku ndiko Mungu anaita kuteseka ambako Alimtaka mwanadamu kushiriki Naye. Ukikumbana na shida, fanya hima na umwombe Mungu: Ee Mungu! Ninataka kukuridhisha, ninataka kustahimili mateso ya mwisho ili kuuridhisha moyo Wako, na bila kujali kuwa vikwazo ninavyokumbana navyo ni vikubwa kiasi gani, bado ni sharti nikuridhishe. Hata ikiwa ni kuyatoa maisha yangu yote, bado ni sharti nikuridhishe! Ukiomba na hili azimio utaweza kusimama imara katika ushuhuda wako. Kila wawekapo ukweli katika vitendo, kila wapitiapo usafishaji, kila wanapojaribiwa, na kila wakati kazi ya Mungu inapowashukia, watu wanapitia mateso makubwa. Haya yote ni mtihani wa watu, na kwa hivyo ndani yao wote mna vita. Hii ndiyo gharama hasa wanayolipa. Kusoma zaidi neno la Mungu na kuzungukazunguka zaidi, kwa namna fulani ni gharama. Ndiyo watu wanapaswa kufanya, ndio wajibu wao, na jukumu ambalo ni sharti walitimize, lakini ni lazima watu waweke kando yale yanayofaa kuwekwa kando. Ikiwa hamwezi, basi haijalishi mateso yako yatakuwa makubwa kiasi gani, na utazunguka kiasi gani, yote yatakuwa bure! Hivi ni kusema, ni mabadiliko ndani yako tu yanaweza kuamua iwapo mateso yako ya nje yana thamani. Tabia yako ya ndani ikibadilika na ikiwa umeweka ukweli katika vitendo, basi mateso yako yote ya nje yatapata kibali cha Mungu; ikiwa hakujakuwa na mabadiliko katika tabia yako ya ndani, basi haijalishi unateseka kiasi gani au unazungukazunguka kiasi gani nje, hakutakuwa na kibali kutoka kwa Mungu—na mateso ambayo hayajaidhinishwa na Mungu ni bure! Hivyo, kama gharama unayoilipa itahesabika inaamuliwa na kama umekuwa na mabadiliko ndani yako, na kama unatia ukweli katika vitendo na kuasi dhidi ya motisha na dhana zako mwenyewe ili kupata ridhaa ya mapenzi ya Mungu, ufahamu wa Mungu, na uaminifu kwa Mungu. Haijalishi unazungukazunguka kiasi gani, ikiwa hujawahi kuasi dhidi ya motisha zako, unatafuta tu matendo na hamasa za nje, na usitilie maanani maisha yako, basi taabu yako yatakuwa yamepita bure. Ikiwa una kitu unachotaka kusema katika mazingira fulani, ila kwa ndani huhisi ni sawa, kwamba hakina faida kwa ndugu na dada zako, na kinaweza kuwadhuru, basi na usikiseme, uchague kuumia kwa ndani, kwa kuwa haya maneno hayawezi kuridhisha mapenzi ya Mungu. Wakati huu, kutakuwa na vita ndani yako, lakini utakuwa tayari kuumia na kuviacha uvipendavyo, utakuwa radhi kustahimili haya mateso ili kumridhisha Mungu na ingawa utaumia kwa ndani, hutautosheleza mwili, na moyo wa Mungu utakuwa umeridhishwa, hivyo utafarijika kwa ndani. Kwa hakika huku ni kulipa gharama, na ndiyo gharama inayotakiwa na Mungu. Ukitenda kwa njia hii, kwa hakika Mungu atakubariki; ikiwa huwezi kulifanikisha hili, basi haijalishi unaelewa kiasi gani, au unaweza kunena vyema kiasi gani, yote haya hayatafaa kitu! Katika njia ya kumpenda Mungu, ikiwa unaweza kusimama upande wa Mungu anapopigana na Shetani, na usimgeukie Shetani, basi utakuwa umefanikisha mapenzi ya Mungu, na utakuwa umesimama imara katika ushuhuda wako.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kumpenda Mungu tu Ndiko Kumwamini Mungu Kweli

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp