Maneno ya Mungu ya Kila Siku: Kumjua Mungu | Dondoo 41

Shetani Anamjaribu Ayubu kwa Mara ya Kwanza (Mifugo Yake Yaibiwa na Janga Lawapata Watoto Wake)

a. Maneno Yaliyotamkwa na Mungu

Ayubu 1:8 Naye Yehova akasema kwa Shetani, je, umemfikiria mtumishi wangu Ayubu, kwamba hakuna hata mtu kama yeye duniani, mtu mtimilifu na mwaminifu, ambaye anamcha Mungu, na kuepuka maovu?

Ayubu 1:12 Naye Yehova akasema kwa Shetani, Tazama, vyote ambavyo anavyo vimo uwezoni mwako; lakini juu yake mwenyewe wewe usinyoshe mkono wako. Hivyo basi Shetani akaondoka mbele za uwepo wa Yehova.

b. Jibu la Shetani

Ayubu 1:9-11 Kisha Shetani akamjibu Yehova, na kusema, je, Ayubu anamcha Mungu bure? Wewe hujamzunguka kila upande na ukingo, na kila upande wa nyumba yake, na kila upande wa yote aliyo nayo? Umebariki kazi ya mikono yake, na mali yake inaongezeka nchini. Lakini nyosha mbele mkono wako sasa, na uguse yote aliyo nayo, na yeye atakulaani mbele ya uso wako.

Mungu Amruhusu Shetani Kumjaribu Ayubu ili Imani ya Ayubu iweze Kufanywa Kuwa Timilifu

Ayubu 1:8 ndiyo rekodi ya kwanza tunayoiona kwenye Biblia kuhusu mabadilishano kati ya Yehova Mungu na Shetani. Na ni nini alichosema Mungu? Maandishi asilia yanatupatia simulizi ifuatayo: “Naye Yehova akasema kwa Shetani, je, umemfikiria mtumishi wangu Ayubu, kwamba hakuna hata mtu kama yeye duniani, mtu mtimilifu na mwaminifu, ambaye anamcha Mungu, na kuepuka maovu?” Huu ulikuwa ukadiriaji wa Mungu kuhusu Ayubu kwa Shetani; Mungu alisema kwamba alikuwa binadamu mtimilifu na mnyofu, yule aliyemcha Mungu na kujiepusha na maovu. Kabla ya maneno haya kati ya Mungu na Shetani, Mungu alikuwa ameamua kwamba Angemtumia Shetani kujaribu Ayubu—kwamba Angemkabidhi Ayubu kwa Shetani. Kwa mkondo mmoja, hali hii ingethibitisha kwamba uangalizi na utathmini wa Mungu kwa Ayubu ulikuwa sahihi na bila kosa, na ungesababisha Shetani kuaibishwa kupitia kwa ushuhuda wa Ayubu, kwa mkondo mwingine, ingefanya imani ya Ayubu kwa Mungu na kumcha Mungu kuwa timilifu. Hivyo, wakati Shetani alipokuja mbele ya Mungu, Mungu hakutatiza maneno. Alienda moja kwa moja kwenye hoja na kumuuliza Shetani: “Je, umemfikiria mtumishi wangu Ayubu, kwamba hakuna hata mtu kama yeye duniani, mtu mtimilifu na mwaminifu, ambaye anamcha Mungu, na kuepuka maovu?” Katika swali la Mungu kunayo maana ifuatayo: Mungu alijua kwamba Shetani alizunguka kila pahali, na mara nyingi alikuwa amemnyemelea Ayubu, aliyekuwa mtumishi wa Mungu. Alikuwa mara nyingi amemjaribu na kumshambulia, akijaribu kupata njia ya kumwangamiza Ayubu ili kuthibitisha kwamba imani ya Ayubu katika Mungu na kumcha Mungu kwake kusingeweza kubadilika. Shetani pia alitafuta kwa haraka sana fursa za kumhangaisha Ayubu, ili Ayubu aweze kumkataa Mungu na kumruhusu Shetani kumpokonya kutoka kwenye mikono ya Mungu. Lakini Mungu aliuangalia moyo wa Ayubu na kuona kwamba alikuwa mtimilifu na mnyofu, na kwamba alimcha Mungu na kujiepusha na maovu. Mungu alitumia swali moja kumwambia Shetani kwamba Ayubu alikuwa binadamu mtimilifu na mnyofu aliyemcha Mungu na kujiepusha na maovu, kwamba Ayubu asingeweza kumwacha Mungu na kufuata Shetani. Baada ya kusikia utathmini wa Mungu kuhusu Ayubu, ndani ya Shetani kukatokea hasira kali iliyotokana na udhalilishaji, na akawa mwenye hasira zaidi, na aliyekosa subira ya kumpokonya Ayubu kutoka kwa Mungu, kwani Shetani alikuwa hajawahi kusadiki kwamba mtu angeweza kuwa mtimilifu na mnyofu, au kwamba angeweza kumcha Mungu na kujiepusha na maovu. Wakati huohuo, Shetani pia alichukizwa na utimilifu na unyofu kwa binadamu, na aliwachukia watu ambao wangeweza kumcha Mungu na kujiepusha na maovu. Na hivyo imeandikwa katika Ayubu 1:9-11 kwamba “Kisha Shetani akamjibu Yehova, na kusema, je, Ayubu anamcha Mungu bure? Wewe hujamzunguka kila upande na ukingo, na kila upande wa nyumba yake, na kila upande wa yote aliyo nayo? Umebariki kazi ya mikono yake, na mali yake inaongezeka nchini. Lakini nyosha mbele mkono wako sasa, na uguse yote aliyo nayo, na yeye atakulaani mbele ya uso wako.” Mungu alikuwa amezoea kwa undani asili ya kijicho ya Shetani, na Alijua vizuri kabisa kwamba Shetani alikuwa na mpango wa muda mrefu wa kumwangamiza Ayubu, na hivyo kwa haya Mungu alitaka, kwa kumwambia Shetani kwa mara nyingine kwamba Ayubu alikuwa mtimilifu na mnyofu na kwamba alimwogopa Mungu na kujiepusha na maovu, kumrudisha Shetani pale anapofaa, kumfanya Shetani kufichua uso wake wa kweli na kumshambulia na kumjaribu Ayubu. Kwa maneno mengine, Mungu alitilia mkazo makusudi kwamba Ayubu alikuwa mtimilifu na mnyofu na kwamba alimcha Mungu na kujiepusha na maovu, na kwa njia hii alimfanya Shetani kumshambulia Ayubu kwa sababu ya chuki na hasira za Shetani kutokana na vile ambavyo Ayubu alikuwa binadamu mtimilifu na mnyofu, yule aliyemcha Mungu na kujiepusha na maovu. Kutokana na haya, Mungu angemletea Shetani aibu kupitia kwa ukweli kwamba Ayubu alikuwa binadamu mtimilifu na mnyofu, yule aliyemcha Mungu na kujiepusha na maovu, na Shetani angeachwa akiwa amedhalilishwa kabisa na kushindwa. Baada ya hapo, Shetani asingekuwa tena na shaka au asingetoa mashtaka kuhusu utimilifu, unyofu, ucha Mungu au hali ya kujiepusha na maovu ya Ayubu. Kwa njia hii, majaribio ya Mungu na yale ya Shetani yalikuwa karibu yasiyoepukika. Yule tu aliye na uwezo wa kustahimili majaribio ya Mungu na yale ya Shetani alikuwa ni Ayubu. Kufuatia mabadilishano haya, Shetani alipewa ruhusa kumjaribu Ayubu. Na hivyo raundi ya kwanza ya mashambulizi ya Shetani ikaanza. Kilengwa cha mashambulizi haya kilikuwa mali ya Ayubu, kwani Shetani alikuwa ametoa mashtaka yafuatayo dhidi ya Ayubu: “Je, Ayubu anamcha Mungu bure? … Umebariki kazi ya mikono yake, na mali yake inaongezeka nchini.” Kutokana na haya, Mungu alimruhusu Shetani kuchukua kila kitu ambacho Ayubu alikuwa nacho—ambalo ndilo lilikuwa kusudio lenyewe la Mungu kuzungumza na Shetani. Hata hivyo, Mungu alitoa sharti moja kwa Shetani: “vyote ambavyo anavyo vimo uwezoni mwako; lakini juu yake mwenyewe wewe usinyoshe mkono wako” (Ayubu 1:12). Hili ndilo sharti ambalo Mungu alitoa baada ya kumruhusu Shetani kumjaribu Ayubu na akamweka Ayubu kwenye mikono ya Shetani, na hiyo ndiyo mipaka aliyomwekea Shetani: Alimwamuru Shetani kutodhuru Ayubu. Kwa sababu Mungu alijua kwamba Ayubu alikuwa mtimilifu na mnyofu, na kwamba Alikuwa na imani kwamba utimilifu na unyofu wa Ayubu kwake Yeye ulikuwa zaidi ya kutiliwa shaka, na kwamba angeweza kustahimili majaribio; hivyo, Mungu alimruhusu Shetani kumjaribu Ayubu, lakini akaweka hapo kizuizi kwa Shetani: Shetani aliruhusiwa kuchukua mali ya Ayubu yote, lakini asimguse hata kwa kidole. Hii inamaanisha nini? Inamaanisha kwamba Mungu hakumkabidhi Ayubu kabisa kwa Shetani wakati huo. Shetani angeweza kumjaribu Ayubu kwa mbinu zozote zile ambazo alitaka, lakini hakuweza kumdhuru Ayubu mwenyewe, hata unywele mmoja wa kichwa chake, kwa sababu kila kitu cha binadamu kinathibitiwa na Mungu, iwapo binadamu anaishi ama anakufa inaamuliwa na Mungu na Shetani hana leseni yoyote ya kuthibiti haya. Baada ya Mungu kumwambia Shetani maneno haya, Shetani asingeweza kusubiri kuanza. Alitumia kila mbinu kumjaribu Ayubu, na baada ya muda usiyokuwa mrefu Ayubu alipoteza kundi kubwa la kondoo na ng’ombe na mali yote aliyokuwa amepewa na Mungu…. Na hivyo majaribio ya Mungu yakamjia yeye.

Ingawa Biblia inatuambia asili ya jaribio la Ayubu, je Ayubu mwenyewe, ambaye alipatwa na majaribio haya, alijua kuhusu kile kilichokuwa kikiendelea? Ayubu alikuwa tu binadamu wa kawaida; bila shaka hakujua chochote kuhusu hadithi ile iliyokuwa ikiendelea nyuma yake. Hata hivyo, kumcha Mungu kwake na utimilifu pamoja na unyofu wake, ulimfanya kutambua kwamba majaribio ya Mungu yalikuwa yamemjia. Hakujua ni nini kilichokuwa kimefanyika kwenye ufalme wa kiroho, wala nia alizokuwa nazo Mungu katika majaribio hayo. Lakini alijua kwamba haijalishi ni nini ambacho kingemfanyikia yeye, alifaa kuendelea kushikilia ukweli wa utimilifu na unyofu wake, na kwamba alifaa kutii njia ya kumcha Mungu na kujiepusha na maovu. Mwelekeo na mwitikio wa Ayubu katika masuala haya uliweza kutazamwa waziwazi na Mungu. Naye Mungu aliona nini? Aliuona moyo wa Ayubu uliyomcha Mungu, kwa sababu kutoka mwanzo hadi wakati ambapo Ayubu alijaribiwa, moyo wa Ayubu ulibakia wazi kwa Mungu, uliwekwa mbele ya Mungu, naye Ayubu hakuwacha utimilifu wala unyofu wake, wala hakutupilia mbali au kugeuka katika njia ya kumcha Mungu na kujiepusha na maovu—na hakuna kingine chochote kilichokuwa cha kumtosheleza na kumfurahisha Mungu kama haya.

Kimetoholewa kutoka katika Neno Laonekana katika Mwili

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp