Maneno ya Mungu ya Kila Siku: Hatua Tatu za Kazi | Dondoo 16

Kazi inayofanywa kwa sasa imesukuma mbele kazi ya Enzi ya Neema; yaani, kazi katika mpango mzima wa usimamizi wa miaka elfu sita imesonga mbele. Ingawa Enzi ya Neema imekoma, kazi ya Mungu imeendelea sana. Kwa nini Ninazungumza mara kwa mara kwamba hatua hii ya kazi inajenga juu ya Enzi ya Neema na Enzi ya Sheria? Hii ina maana kwamba kazi ya wakati huu ni mwendelezo wa kazi iliyofanyika katika Enzi ya Neema na kuinua kazi ile iliyofanyika katika Enzi ya Sheria. Hatua hizi tatu zinaingiliana kwa karibu na kuunganika moja kwa inayofuata. Kwa nini pia Ninasema kwamba hatua hii ya kazi inajenga juu ya kile kilichofanywa na Yesu? Tuseme kwamba hatua hii haingeongezea juu ya kazi iliyofanywa na Yesu, ingebidi Asulubiwe tena katika hatua hii, na kazi ya ukombozi ya hatua iliyopita ingelazimika kufanywa upya tena. Hii isingekuwa na maana yoyote. Kwa hiyo, sio kwamba kazi imekamilika kabisa, bali ni kwamba enzi imesonga mbele, na kazi imekuwa ya juu kabisa kuliko ilivyokuwa kabla. Inaweza kusemwa kwamba hatua hii ya kazi imejengwa juu ya msingi wa Enzi ya Sheria na katika mwamba wa kazi ya Yesu. Kazi hii imejengwa hatua kwa hatua, na hatua hii sio mwanzo mpya. Ni muungano tu wa hatua tatu za kazi ndio unaweza kuchukuliwa kuwa mpango wa usimamizi wa miaka elfu sita. Hatua hii inafanywa katika msingi wa kazi ya Enzi ya Neema. Ikiwa hatua hizi mbili za kazi hazihusiani, kwa nini hakuna msalaba katika hatua hii? Kwa nini Sibebi dhambi za wanadamu? Siji kupitia kuzaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu na wala Sitosulubiwa ili kubeba dhambi za wanadamu; badala yake, Nipo hapa moja kwa moja kumwadibu mwanadamu. Ikiwa Mimi kumwadibu mwanadamu na kuja Kwangu si kwa njia ya Roho Mtakatifu na hakukufuata usulubisho, basi Nisingekuwa na sifa zinazostahili kumwadibu mwanadamu. Ni hasa kwa sababu Mimi ni mmoja na Yesu ndiyo Nimekuja moja kwa moja kumwadibu na kumhukumu mwanadamu. Hatua hii ya kazi inajenga kwa ujumla juu ya hatua iliyotangulia. Hii ndiyo maana ni kazi kama hiyo tu inaweza ikamletea mwanadamu wokovu hatua kwa hatua. Yesu pamoja na Mimi tunatoka katika Roho Mmoja. Ingawa miili Yetu haina uhusiano, Roho Zetu ni moja; ingawa kile Tunachofanya na kazi Tulizonazo hazifanani, kwa asili Tunafanana; miili Yetu ina maumbo tofauti, na hii ni kwa sababu ya mabadiliko ya enzi na mahitaji ya kazi Yetu; huduma Zetu hazifanani, hivyo kazi Tunayoileta na tabia Tunayoifichua kwa mwanadamu pia ni tofauti. Ndio maana kile ambacho mwanadamu anakiona na kukipokea leo hii si kama kile cha wakati uliopita; hii ni kwa sababu ya mabadiliko ya enzi. Ingawa jinsia na maumbo ya miili Yao ni tofauti, na ingawa hawakuzaliwa kutoka katika familia moja, achilia mbali katika kipindi kimoja, Roho Zao ni moja. Ingawa miili Yao haina uhusiano wa damu au kimwili kwa namna yoyote ile, hii haipingi kwamba Wao ni Mungu kupata mwili katika vipindi viwili tofauti vya nyakati. Ni ukweli usiopingika kwamba Wao ni Mungu katika miili, ingawa hawatoki katika ukoo mmoja au hawatumii lugha moja ya binadamu (mmoja alikuwa mwanamume aliyezungumza lugha ya Kiyahudi na mwingine ni mwanamke anayezungumza Kichina pekee). Ni kwa sababu hizi ndiyo maana Wameishi katika nchi tofauti kufanya kazi ambayo inampasa kila mmoja kufanya, na katika nyakati tofauti vilevile. Licha ya ukweli kwamba ni Roho moja, wakiwa na asili inayofanana, hakuna mfanano wa wazi kabisa kati ya ngozi ya nje ya miili Yao. Wanashiriki tu ubinadamu sawa, lakini umbo na kuzaliwa kwa miili Yao hakufanani. Haya hayana athari katika kazi Zao au maarifa aliyonayo mwanadamu juu yao, maana, hata hivyo, ni Roho moja na hakuna anayeweza kuwatenganisha. Ingawa Hawana uhusiano wa damu, nafsi zao zinaongozwa na Roho Zao, ili kwamba waweze kufanya kazi tofauti katika nyakati tofauti, wakiwa na miili Yao isiyokuwa na undugu wa damu. Kwa namna ile ile, Roho wa Yehova sio baba wa Roho ya Yesu na Roho wa Yesu sio mwana wa Roho wa Yehova. Ni wa Roho moja. Kama tu Mungu katika mwili wa leo na Yesu. Ingawa Hawahusiani kwa damu, ni Wamoja; hii ni kwa sababu Roho Zao ni moja. Anaweza kufanya kazi ya rehema na wema, vilevile na ile kazi ya hukumu ya haki na kumwadibu mwanadamu, na ile ya kuleta laana kwa mwanadamu. Hatimaye, Anaweza kufanya kazi ya kuuharibu ulimwengu na kuwaadhibu waovu. Je, hafanyi haya yote Mwenyewe? Je, huu si ukuu wa Mungu? Angeweza kutangaza sheria kwa ajili ya mwanadamu na kutoa amri, na angeweza pia kuwaongoza Waisraeli wa awali katika maisha yao duniani na kuwaongoza kujenga hekalu na madhabahu, kutawala Israeli yote. Kwa sababu ya mamlaka Yake, Aliishi pamoja nao duniani kwa miaka elfu mbili. Waisraeli hawakuthubutu kuasi; wote walimheshimu sana Yehova na walifuata amri Zake. Kazi hii ilifanywa kwa sababu ya mamlaka Yake na ukuu Wake. Katika Enzi ya Neema, Yesu alikuja kuwakomboa wanadamu wote walioanguka (sio Waisraeli pekee). Alionyesha rehema na wema kwa mwanadamu. Yesu ambaye mwanadamu alimwona katika Enzi ya Neema Alikuwa amejazwa na wema na siku zote Alikuwa mwenye upendo, maana Alikuja kumkomboa mwanadamu kutoka dhambini. Angeweza kuwasamehe wanadamu dhambi zao hadi pale ambapo msalaba Wake ungeweza kumkomboa mwanadamu kutoka dhambini. Wakati huo, Mungu alionekana kwa mwanadamu katika rehema na wema; yaani, Alijitoa sadaka kwa ajili ya mwanadamu na Alisulubiwa kwa ajili ya dhambi za mwanadamu ili kwamba waweze kusamehewa milele. Alikuwa mwenye rehema, mwenye huruma, mwenye upendo na mstahimilivu. Na wale wote waliomfuata Yesu katika Enzi ya Neema nao pia walionekana kuwa wastahimilivu na wenye upendo katika mambo yote. Walistahimili mateso yote, na hawakuweza kulipiza kisasi hata walipopigwa, kulaaniwa au kupigwa mawe. Lakini haipo hivyo tena katika hatua hii ya mwisho, kama vile kazi ya Yesu na Yehova hazikufanana ingawa Roho Zao zilikuwa moja. Kazi ya Yehova haikuwa kwa ajili ya kukamilisha enzi bali kuiongoza na kuipeleka katika maisha ya mwanadamu duniani. Hata hivyo, kazi sasa ni kuwashinda wale wanadamu walioharibiwa sana katika nchi za Wamataifa na kuongoza sio tu familia ya China bali ulimwengu mzima. Unaona kazi hii ikifanywa sasa China pekee, lakini kwa kweli imekwishaanza kusambaa katika nchi za ughaibuni. Ni kwa nini wageni mara kwa mara wanatafuta njia ya kweli? Hiyo ni kwa sababu Roho tayari amekwishaanza kazi Yake, na maneno sasa yameelekezwa kwa watu wa ulimwengu mzima. Hii tayari ni nusu ya kazi. Roho wa Mungu amefanya kazi kubwa hiyo tangu dunia ilipoumbwa; Amefanya kazi tofauti katika enzi tofautitofauti, na katika mataifa tofauti. Watu wa kila enzi wanaiona tabia Yake tofauti, ambayo kwa asili inafichuliwa kupitia kazi tofauti Anazozifanya. Yeye ni Mungu, mwingi wa rehema na wema; Yeye ni sadaka ya dhambi kwa ajili ya mwanadamu na mchungaji wa mwanadamu, pia Yeye ni hukumu, kuadibu, na laana kwa mwanadamu. Angeweza kumwongoza mwanadamu kuishi duniani kwa miaka elfu mbili na pia kumwokoa mwanadamu aliyepotoka. Na siku hii, pia Anaweza kumshinda mwanadamu ambaye hamjui na kumfanya awe chini ya utawala Wake, ili kwamba wote wajinyenyekeze kwake kikamilifu. Mwishoni, Atachoma yote ambayo si safi na ambayo si ya haki ndani ya wanadamu katika ulimwengu mzima, kuwaonyesha kwamba Yeye si Mungu wa Rehema, wema, hekima, maajabu na utakatifu pekee, bali pia ni Mungu anayemhukumu mwanadamu. Kwa waovu miongoni mwa wanadamu wote, Yeye ni moto, hukumu na adhabu; kwa wale ambao wanapaswa kukamilishwa, Yeye ni mateso, usafishaji, na majaribu, vilevile faraja, ustahimilivu, kutoa maneno, kushughulika na kupogoa. Na kwa wale ambao wameondolewa, Yeye ni adhabu, vilevile mapatilizo.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kupata Mwili Mara Mbili Kunakamilisha Umuhimu wa Kupata Mwili

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp