Mungu Ndiye Chanzo cha Uhai wa Mwanadamu

Tangu unapoingia katika dunia hii ukilia, unaanza kutekeleza wajibu wako. Unachukua jukumu lako katika mpango wa Mungu na katika utaratibu wa Mungu. Unaanza safari ya maisha. Licha ya asili yako na licha ya safari iliyoko mbele yako, hakuna kitakachoepuka mpango na utaratibu ambao mbingu imeweka, na hakuna aliye na udhibiti wa hatima yake, kwa maana Anayetawala juu ya kila kitu ndiye tu Aliye na uwezo wa kazi hiyo. Tangu siku aliyoumbwa binadamu, Mungu amekuwa thabiti katika kazi Yake, kusimamia ulimwengu huu na kuelekeza mabadiliko na harakati ya mambo yote. Kama kila kiumbe, mwanadamu bila kujua anapata lishe ya utamu na mvua na umande kutoka kwa Mungu. Kama vitu vyote, mwanadamu bila kujua anaishi chini ya mpango wa mkono wa Mungu. Moyo na roho ya mwanadamu vimeshikwa katika mkono wa Mungu, na maisha yote ya mwanadamu yanatunzwa machoni mwa Mungu. Haijalishi kama unayaamini mambo haya au la, vitu vyote, vilivyo hai au vilivyokufa, vitahamishwa, vitabadilika, kufanywa vipya, na kutoweka kulingana na mawazo ya Mungu. Hivi ndivyo Mungu anavyotawala juu ya kila kitu.

Usiku uingiapo kwa utulivu, mwanadamu huwa hafahamu, kwani moyo wa mwanadamu hauwezi kujua jinsi giza linapokaribia au linakotoka. Usiku unapotoweka polepole, mwanadamu anakaribisha mwanga wa mchana, lakini moyo wa mwanadamu haufahamu ilikotoka nuru hii na jinsi gani nuru yenyewe imeliondoa giza la usiku. Mabadiliko kama haya ya kawaida ya mchana na usiku humpitisha mwanadamu katika kipindi kimoja baada ya kingine, kupita katika nyakati, wakati huu wote ikihakikisha kwamba kazi ya Mungu na mpango wake unafanywa wakati wa kila kipindi na katika nyakati zote. Mwanadamu alitembea katika enzi nyingi na Mungu, lakini bado mwanadamu hafahamu kwamba Mungu ndiye kiongozi wa hatima ya mambo yote na viumbe hai au jinsi Mungu hupanga na kuelekeza mambo yote. Hili ni jambo ambalo limekwepa ufahamu wa binadamu tangu enzi za kale mpaka leo. Na juu ya ni kwa sababu ipi, sio kwa sababu njia za Mungu hazifahamiki, au kwa sababu mpango wa Mungu bado haujakamilika, lakini ni kwa sababu moyo na roho ya mwanadamu viko mbali sana na Mungu. Kwa hivyo, hata ingawa mwanadamu Anamfuata Mungu, bila kujua yeye hubaki katika huduma ya Shetani. Hakuna anayetafuta kwa ukamilifu nyayo au nafsi ya Mungu, na hakuna anayetaka kuwepo katika huduma na utunzaji wa Mungu. Badala yake, wao wako tayari kutegemea upotoshaji wa Shetani na yule mwovu ili kubadilishwa na dunia hii na kanuni za maisha ambazo watu waovu hufuata. Katika nafasi hii, moyo na roho za mwanadamu hutolewa kafara kwa shetani na kuwa riziki yake. Aidha, moyo wa binadamu na roho yake huwa mahali ambapo Shetani anaweza kuishi na kuufanya uwanja wake wa kuchezea. Kwa njia hii, mwanadamu kwa kutojua hupoteza ufahamu wake wa kanuni ya kuwa binadamu, na wa thamani na madhumuni ya kuwepo kwa binadamu. Sheria kutoka kwa Mungu na agano kati ya Mungu na mwanadamu huangamia hatua kwa hatua kutoka katika moyo wa mwanadamu mpaka mwishowe mwanadamu hawezi tena kuomba au kufuata na kumsikiza Mungu. Wakati upitapo, mwanadamu haelewi tena kwa nini Mungu alimuumba, wala haelewi maneno yanayotoka katika kinywa cha Mungu au kutambua kwamba yote hayo ni kutoka kwa Mungu. Mwanadamu huanza kupinga sheria na amri kutoka kwa Mungu; moyo na roho ya mwanadamu hufishwa…. Mungu humpoteza mwanadamu Aliyemuumba pale mwanzo, na mwanadamu hupoteza mizizi ya mwanzo wake. Hii ni huzuni ya uanadamu. Kwa uhakika, tangu mwanzo mpaka sasa, Mungu alilifanya janga la wanadamu ambalo mwanadamu ni mhusika mkuu na mwaathiriwa, na hakuna hata mmoja anayeweza kupata jibu kuhusu nani ndiye mwelekezi wa hadithi hii ya janga.

Katika dunia hii kubwa, mabadiliko yasiyo hesabika yamefanyika, tena na tena. Hapana aliye na uwezo wa kuongoza binadamu isipokuwa Yeye ambaye Anatawala juu ya kila kitu katika ulimwengu. Hakuna yeyote hodari kwa kazi au kufanya maandalizi kwa ajili ya binadamu, wala aliye na uwezo wa kuwaongoza wanadamu kurejelea mwanga na ukombozi kutokana na ukosefu wa haki duniani. Mungu Analalamikia wakati ujao wa wanadamu, na Anahuzunishwa na kuanguka kwa mwanadamu. Anahisi huzuni kwa kuangamia kwa mwanadamu polepole na kwenda katika njia isiyo na upande wa kurudi. Mwanadamu ameuvunja moyo wa Mungu, akamkana na kumfuata yule mwovu. Hakuna waliowahi kuwa na mawazo kuhusu mwelekeo ambao mwanadamu wa aina hii atafuata. Ni kwa sababu hii haswa ndio kwamba hakuna ambaye ameona hasira ya Mungu. Hakuna anayetafuta njia ya kumpendeza Mungu au kujaribu kuwa karibu na Mungu. Kadhalika, hakuna anayetafuta kufahamu huzuni na maumivu ya Mungu. Hata baada ya kusikia sauti ya Mungu, binadamu anaendelea tu kwenye njia yake mbali na Mungu, kukwepa neema na huduma ya Mungu, na kuepuka ukweli wa Mungu, akiona ni afadhali auuze mwili wake kwa Shetani, adui wa Mungu. Na ni nani amewahi kuwa na mawazo yoyote ya jinsi gani Mungu atamtendea mwanadamu asiyetubu na ambaye amempuuza? Hakuna anayejua kwamba ukumbusho wa mara kwa mara na nasaha za Mungu ni kwa sababu Yeye anayo katika mikono yake maafa Aliyowaandalia yasiyokuwa ya kawaida, maafa ambayo yatakuwa magumu kwa mwili na nafsi ya mwanadamu kustahimili. Janga hili sio tu adhabu ya mwili bali ya roho pia. Lazima ujue hili: Mpango wa Mungu unapokataliwa na wakati kuwakumbusha kwake na nasaha hazileti mabadiliko, Atakuwa na hasira ya aina gani? Hii itakuwa kama kitu ambacho hakijawahi kushuhudiwa hapo awali au hata kusikika na viumbe vyovyote. Na hivyo Nasema, janga hili ni kubwa mno na kamwe hayatawahi kurudiwa. Hii ni kwa sababu uumbaji mmoja tu na wokovu mmoja wa mwanadamu ndio ulio ndani ya mpango wa Mungu. Hii ni mara ya kwanza na pia ni ya mwisho. Kwa hivyo, hakuna anayeweza kuelewa nia ya huruma na hamu ya Mungu kwa matarajio yake ya kuwaokoa wanadamu.

Mungu aliumba dunia hii na kuleta mwanadamu, kiumbe hai ambacho alitia uhai ndani yake. Baadaye, mwanadamu akaja kuwa na wazazi na jamaa na hakuwa mpweke tena. Tangu mwanadamu alipotua macho kwa mara ya kwanza katika dunia hii tunayoishi, ilibainika kuwa angeishi ndani ya utaratibu wa Mungu. Ni pumzi ya uhai kutoka kwa Mungu ndiyo hustawisha kila kiumbe hai katika ukuaji wake hadi kinapokomaa. Wakati wa mchakato huu, hakuna hata mmoja anayeamini kwamba mwanadamu huishi na kukua chini ya uangalizi wa Mungu. Badala yake, anashikilia kwamba mwanadamu hukua chini ya upendo na utunzaji wa wazazi wake, na kwamba ukuaji wake unaongozwa na silika ya maisha. Hii ni kwa sababu mwanadamu hajui aliyeleta maisha au kulikotoka maisha hayo, pia hafahamu jinsi silika ya maisha husababisha miujiza. Mwanadamu anajua tu kwamba chakula ndicho msingi wa kuendelea kwa maisha, kwamba uvumilivu ni chanzo cha kuwepo kwa maisha, na kwamba imani iliyomo akilini mwake ni utajiri wa maisha yake. Mwanadamu haihisi neema na riziki itokayo kwa Mungu. Mwanadamu huyatumia kwa uharibifu maisha aliyopewa na Mungu…. Hapana hata mwanadamu mmoja ambaye Mungu Anamwangazia usiku na mchana amechukua jukumu la kuanza Kumwabudu. Mungu Anaendelea kufanya kazi kama Alivyopanga juu ya mwanadamu Akiwa hana matarajio yoyote kutoka kwa mwanadamu. Anafanya hivyo kwa matumaini kwamba siku moja, mwanadamu ataamka kutoka katika ndoto yake na ghafla kuelewa thamani na madhumuni ya maisha, kuelewa gharama Aliyopitia Mungu ili Ampe mwanadamu kila kitu alicho nacho, na kujua jinsi Mungu anavyotamani kwa ari mwanadamu ageuke na Kumrudia. Hakuna yeyote amewahi kufikiria juu ya siri ya asili na endelezo la maisha ya mwanadamu. Na bila shaka, Mungu tu Ambaye Anaelewa yote haya na kwa kimya huvumilia mapigo na maumivu kutoka kwa binadamu, ambaye alipokea kila kitu kutoka kwa Mungu bila shukurani. Binadamu huchukulia kila kitu kinacholetwa na maisha kimzaha, na tena kama “kama jambo lisilo na shaka,” Mungu amesalitiwa, amesahaulika, na kukataliwa na binadamu. Je, mpango wa Mungu ni wa maana namna hii? Je mwanadamu, kiumbe hai ambaye alitoka katika mkono wa Mungu, ni wa maana namna hiyo? Mpango wa Mungu ni wa umuhimu kabisa; hata hivyo, maisha ya viumbe vya mkono wa Mungu vipo kwa ajili ya mpango Wake. Kwa hivyo, Mungu hawezi kuuharibu mpango wake kwa sababu ya chuki Yake kwa mwanadamu. Ni kwa ajili ya mpango Wake na pumzi aliyotoa ndiyo maana Mungu Hustahimili mateso yote, siyo kwa ajili ya mwili wa mwanadamu ila ni kwa sababu ya uhai wa mwanadamu. Mungu ana hamu ya kuchukua pumzi aliyopuliza ndani mwa mwanadamu, wala sio nyama za mwili. Huu ndio mpango wake.

Wote wanaokuja duniani lazima wapitie maisha na kifo, na wengi wamepitia mzunguko wa kifo na kuzaliwa upya. Wale wanaoishi watakufa hivi karibuni na wafu watarejea karibuni. Yote haya ni mwendo wa maisha uliopangwa na Mungu kwa kila kiumbe hai. Hata hivyo, njia hii na mzunguko huu ni ukweli ambao Mungu Anataka binadamu aone, kwamba maisha aliyopewa na Mungu hayana kikomo na hayazuiliwi na mwili, wakati, au nafasi. Hii ni siri ya maisha aliyopewa binadamu na Mungu na dhihirisho kwamba maisha yalikuja kutoka Kwake. Ingawa watu wengi wanaweza kosa kuamini kwamba maisha yalitoka kwa Mungu, binadamu bila ya kufahamu wanafurahia yote yatokayo kwa Mungu, iwe wanaamini au wanakana uwepo Wake. Iwapo siku moja Mungu kwa ghafla Atabadili moyo na Atake kurudisha yote yaliyomo duniani na kuchukua maisha Aliyotoa, basi yote duniani yataisha. Mungu Hutumia maisha Yake kukimu vitu vyote vilivyo hai na visivyo na uhai, na kuleta yote kwa utaratibu mzuri kwa mujibu wa madaraka na mamlaka Yake. Huu ni ukweli ambao hakuna anayeweza kuufahamu au kuuelewa kwa urahisi, na kweli hizi zisizoeleweka kwa fikira zetu ni dhihirisho halisi na ushahidi wa nguvu za Mungu katika maisha. Sasa hebu nikupe siri: Ukuu na nguvu ya uhai wa Mungu hauwezi kueleweka na kiumbe chochote. Hii ilikuwa hivyo awali, iko hivyo wakati huu, na itakuwa hivyo wakati ujao. Siri ya pili Nitakayotoa ni hii: chanzo cha uhai hutoka kwa Mungu, kwa viumbe vyote, haijalishi tofauti katika maumbile au muundo. Hata uwe kiumbe hai cha aina gani, huwezi kwenda kinyume na njia ya maisha ambayo Mungu ameweka. Katika hali yoyote, kile Napenda ni kuwa mwanadamu aelewe kwamba bila huduma, utunzaji, na utoaji wa Mungu, mwanadamu hawezi kupokea yote aliyokusudiwa kupokea, haijalishi juhudi au mapambano yake. Bila ruzuku ya uhai kutoka kwa Mungu, mwanadamu hupoteza maana ya thamani katika maisha na kupoteza madhumuni ya kusudi katika maisha. Mungu angewezaje kuruhusu mwanadamu anayepoteza thamani ya uhai wake kuishi hivyo bila ya kujali? Kisha tena, usisahau kwamba Mungu Ndiye chanzo cha maisha yako. Iwapo mwanadamu atashindwa kuthamini yote ambayo Mungu Amemfanyia, Mungu Hatachukua kile Alichotoa pekee, lakini zaidi ya hayo, mwanadamu atalipa mara mbili kufanya fidia kwa yote ambayo Mungu Ametumia.

Mei 26, 2003

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp