Yule tu Anayepitia Kazi ya Mungu Ndiye Anayemwamini Mungu Kweli

Ingawa watu wengi wanaamini katika Mungu, ni wachache wanaoelewa ni nini maana ya imani katika Mungu, na ni nini wanachopaswa kufanya ili waupendeze moyo wa Mungu. Hii ni kwa sababu, hata ingawa watu wengi wanalifahamu neno “Mungu” na mafungu ya maneno kama “kazi ya Mungu”, hawamjui Mungu, sembuse kujua kazi ya Mungu. Si ajabu, basi, kwamba wale wote wasiomjua Mungu wamejawa na imani iliyovurugika. Watu hawachukulii imani kwa Mungu kwa uzito kwa kuwa kuamini Mungu ni jambo geni, jambo lisilo la kawaida sana kwao. Kwa njia hii, hawafikii mahitaji ya Mungu. Kwa maneno mengine, ikiwa watu hawamjui Mungu, hawajui kazi Yake, basi hawafai kwa matumizi na Mungu, sembuse kuweza kutimiza hamu ya Mungu. “Imani katika Mungu” inamaanisha kuamini kuwa kuna Mungu; hii ndiyo dhana rahisi zaidi ya imani katika Mungu. Zaidi ya hayo, kuamini kuwa kuna Mungu si sawa na kuamini katika Mungu kwa ukweli; bali, ni aina ya imani sahili ikiwa na vipengee vya uzito vya kidini. Imani ya kweli katika Mungu ina maana kupitia maneno na kazi ya Mungu kwa msingi wa imani kuwa Mungu ndiye mkuu juu ya vitu vyote. Kwa hivyo mtawekwa huru kutokana na tabia yenu ya upotovu, mtatimiza hamu ya Mungu, na mtapata kumjua Mungu. Ni kwa kupitia safari ya aina hii tu ndio mnaweza kusemekana kuwa mnaamini katika Mungu. Ilhali watu mara nyingi huona kuamini katika Mungu kama jambo rahisi sana na la kipuuzi tu. Imani ya watu wa aina hii haina maana na haitawahi kupata idhini ya Mungu, kwa sababu wanatembea katika njia mbaya. Leo, kuna wale ambao bado wanaamini Mungu katika nyaraka, katika mafundisho ya dini yaliyo matupu. Hawana habari kuwa imani yao katika Mungu haina dutu, na hawawezi kupata idhini ya Mungu, na bado wanaomba kupata amani na neema ya kutosha kutoka kwa Mungu. Tunafaa kuweka kituo na kujiuliza wenyewe: Je, kuamini kwa Mungu linaweza kuwa jambo rahisi ya yote duniani? Je, kuamini kwa Mungu hakumaanishi chochote zaidi ya kupokea neema nyingi kutoka kwa Mungu? Je, watu wanaoamini kwa Mungu na hawamjui, na wanaamini kwa Mungu ila wanamuasi; je watu kama hawa wanaweza kutimiza hamu ya Mungu?

Mungu na mwanadamu hawawezi kuzungumziwa kama wa kulingana. Dutu ya Mungu na kazi Yake ni vitu visivyoeleweka na kufahamika kwa mwanadamu. Ikiwa Mungu hawezi kufanya kazi Yake binafsi na kuzungumza maneno Yake katika ulimwengu wa mwanadamu, basi mwanadamu hangeweza kuelewa mapenzi ya Mungu, na kwa hivyo, hata wale waliotoa maisha yao yote kwa ajili ya Mungu hawataweza kupata idhini ya Mungu. Bila kazi ya Mungu, haijalishi jinsi gani mwanadamu anatenda mema, haitahesabika kama chochote, kwa maana fikira za Mungu daima zitakuwa juu ya fikira za mwanadamu, na hekima ya Mungu haieleweki kwa mwanadamu. Na kwa hivyo Nasema kwamba wale ambao “wanaona kwa wazi” Mungu na kazi Yake ni wasioweza kufanikisha chochote, wao wote ni wenye kiburi na wapumbavu. Mwanadamu hafai kufafanua kazi ya Mungu; zaidi ya hayo, mwanadamu hawezi kufafanua kazi ya Mungu. Katika macho ya Mungu, mwanadamu ni mdogo kushinda mchwa, kwa hivyo mwanadamu atawezaje kuelewa kazi ya Mungu? Wale wasemao daima, “Mungu hafanyi kazi kwa njia hii ama ile” au “Mungu yuko hivi ama vile”—je hawa wote si wenye kiburi? Tunafaa sote kujua kwamba watu, ambao ni wa mwili, wote wamepotoshwa na Shetani. Ni katika hali yao asili kumuasi Mungu, na hawako katika usawa na Mungu, sembuse kuweza kutoa mawaidha kwa kazi ya Mungu. Jinsi Mungu anavyomwelekeza mwanadamu ni kazi ya Mungu mwenyewe. Mwanadamu anafaa kunyenyekea, na hafai kuwa na wazo hili ama lile, kwani mwanadamu ni mchanga tu. Kwa sababu tunajaribu kumtafuta Mungu, hatufai kuwekelea dhana zetu katika kazi ya Mungu ili Mungu Aziwaze, na zaidi hatufai kutumia tabia zetu potovu kwa kupinga kazi ya Mungu kwa makusudi. Je hili halitatufanya wapinga Kristo? Je, watu kama hawa watawezaje kusema kuwa wanamwamini Mungu? Kwa maana tunaamini kuwa kuna Mungu, na kwa maana tunatamani kumtosheleza na kumwona, tunapaswa kutafuta njia ya ukweli, na tunapaswa kutafuta njia ya kulingana na Mungu. Hatupaswi kuwa katika upinzani sugu kwa Mungu; Matendo kama haya yatakuwa na matokeo gani mazuri?

Leo hii, Mungu Anayo kazi mpya. Unaweza kuyakataa maneno haya, yanaweza kuhisi yasiyo ya kawaida kwako, lakini Nakushauri usifichue asili yako halisi, kwa maana wale tu walio na njaa ya kweli na kiu cha haki mbele za Mungu ndio wanaweza kupata ukweli, na wale wanaomcha Mungu kwa ukweli tu ndio wanaweza kupata nuru na kuongozwa na Mungu. Hakuna litakalotoka kwa kutafuta ukweli kupitia ugomvi. Ni kwa kutafuta kwa utulivu ndio tunaweza kupata matokeo. Ninaposema kwamba “Leo, Mungu Anayo kazi mpya,” Ninaashiria Mungu kurudi katika mwili. Pengine huyajali maneno haya, pengine unayachukia, au pengine una haja kubwa sana nayo. Haijalishi ni hali gani, Natumai kuwa wote walio na tamaa ya kweli ya kuonekana kwa Mungu wataweza kuukabili ukweli huu na kutafakari juu yake kwa makini. Ni vyema usiamue jambo upesi bila kuzingatia suala zima. Hivi ndivyo watu wenye hekima wanapaswa kutenda.

Kuchunguza kitu cha aina hii sio vigumu, lakini kunahitaji kila mmoja wetu ajue ukweli huu: Yeye Aliye mwili wa Mungu Atakuwa na dutu ya Mungu, na Yule Aliye Mungu katika mwili Atakuwa na maonyesho ya Mungu. Kwa maana Mungu Hupata mwili, Ataleta mbele kazi Anayopaswa kufanya, na kwa maana Mungu Amepata mwili, Ataonyesha kile Alicho na Ataweza kuuleta ukweli kwa mwanadamu, kumpa mwanadamu uhai, na Amwonyeshe mwanadamu njia. Mwili usio na dutu ya Mungu kwa kweli sio Mungu mwenye mwili; kwa hili hakuna tashwishi. Kupeleleza kama kweli ni mwili wa Mungu mwenye Mwili, mwanadamu lazima aamue haya kutoka kwa tabia Yeye huonyesha na maneno Yeye hunena. Ambayo ni kusema, kama ni mwili wa Mungu mwenye mwili au la, na kama ni njia ya kweli au la, lazima iamuliwe kutokana na dutu Yake. Hivyo, katika kudadisi[a] iwapo ni mwili wa Mungu mwenye mwili, cha msingi ni kuwa makini kuhusu dutu Yake (Kazi Yake, Maneno Yake, Tabia Yake, na mengine mengi), bali sio hali ya sura Yake ya nje. Mwanadamu akiona tu sura Yake ya nje, na aipuuze dutu Yake, basi hilo linaonyesha upumbavu na ujinga wa mwanadamu. Sura ya nje haiamulii dutu; na zaidi, kazi ya Mungu haijawahi kuambatana na dhana za mwanadamu. Je, si sura ya nje ya Yesu ilikinzana na dhana za mwanadamu? Je sura Yake na mavazi Yake hayakuweza kutoa dalili yoyote ya utambulisho Wake? Je, si sababu ya Mafarisayo wa zamani kabisa kumpinga Yesu hasa ilikuwa ni kwa sababu waliiangalia tu sura Yake ya nje, na hawakuyaweka moyoni maneno Aliyoongea? Ni matumaini Yangu kuwa ndugu wanaotafuta kuonekana kwa Mungu hawatarudia tanzia ya kihistoria. Hampaswi kuwa Mafarisayo wa wakati huu na kumsulubisha Mungu msalabani tena. Mnafaa kufikiria kwa makini jinsi ya kukaribisha kurudi kwa Mungu, na kuwa na mawazo dhahiri ya jinsi ya kuwa mtu anayetii ukweli. Hili ni jukumu la kila mtu anayengoja Yesu arudi na mawingu. Tunafaa kusugua macho yetu ya kiroho, na tusiwe waathiriwa wa maneno yaliyojaa mambo ya kufurahisha masikio. Tunafaa kuwaza juu ya kazi ya Mungu ya matendo, na tunafaa kuangalia upande wa hakika wa Mungu. Msijisahau ama kupotelea ndotoni, mkitazamia daima ile siku ambayo Bwana Yesu atashuka kwa ghafla juu ya mawingu kuwachukua nyinyi ambao hamjawahi kumjua wala kumwona Yeye, na msiojua kutenda mapenzi Yake. Ni vyema kufikiri juu ya mambo ya kiutendaji!

Unaweza kuwa umefungua kitabu hiki kwa ajili ya utafiti, au ukiwa na nia ya kukubali; haijalishi mwelekeo wako, Natumaini kuwa utakisoma mpaka mwisho, na hutakiweka kando kwa urahisi. Pengine, baada ya kuyasoma maneno haya, mwelekeo wako utabadilika, lakini hilo linategemea jinsi ulivyo na motisha, na jinsi unavyoathiriwa na mambo kwa urahisi. Kunalo jambo moja hata hivyo unalotakiwa kujua: Neno la Mungu haliwezi kuzungumzwa kama neno la mwanadamu, sembuse neno la mwanadamu kuzungumzwa kama neno la Mungu. Mwanadamu anayetumiwa na Mungu siye Mungu mwenye mwili, na Mungu mwenye mwili siye mwanadamu anayetumiwa na Mungu; katika hili, kunayo tofauti kubwa sana. Pengine, baada ya kusoma maneno haya, hukubali kuwa ni maneno ya Mungu, na kuyakubali tu kama maneno ya mwanadamu ambaye amepewa nuru. Ikiwa hivyo, basi umepofushwa na ujinga. Maneno ya Mungu yatawezaje kuwa sawa na maneno ya mwanadamu ambaye amepewa nuru? Maneno ya Mungu mwenye mwili yanaanzisha enzi mpya, yanaongoza wanadamu wote, yanafichua mafumbo, na kumwonyesha mwanadamu mwelekeo mbele katika enzi mpya. Nuru anayoipata mwanadamu ni utendaji au elimu rahisi. Haiwezi kuelekeza binadamu wote kuingia enzi mpya au kufichua fumbo la Mungu Mwenyewe. Mungu, hata hivyo, ni Mungu, na mwanadamu ni mwanadamu. Mungu yuko na dutu ya Mungu, na mwanadamu yuko na dutu ya mwanadamu. Iwapo mwanadamu anachukulia maneno yanayonenwa na Mungu kama kupewa nuru tu na Roho Mtakatifu, na kuchukua maneno yaliyonenwa na mitume na manabii kama maneno yaliyonenwa na Mungu Mwenyewe, basi mwanadamu anakosea. Licha ya haya, hufai kamwe kubadili jambo sahihi liwe baya, ama kuzungumzia lililo juu kama la chini, au kuzungumzia jambo kubwa kama lisilo na kina; haijalishi ni nini, hupaswi kamwe kwa makusudi kupinga lile unalojua kuwa ni ukweli. Kila anayeamini kuwa kuna Mungu anapaswa kufikiri juu ya tatizo hili kwa msimamo ulio sahihi, na anapaswa kukubali kazi Yake mpya na maneno Yake kama kiumbe wa Mungu—la sivyo aondolewe na Mungu.

Baada ya kazi ya Yehova, Yesu Alipata mwili ili Afanye kazi Yake miongoni mwa wanadamu. Kazi Yake haikutekelezwa kivyake, ila ilijengwa juu ya misingi ya kazi ya Yehova. Ilikuwa kazi ya enzi mpya baada ya Mungu kukamilisha Enzi ya Sheria. Vivyo hivyo, baada ya kazi ya Yesu kukamilika, Mungu bado Aliendeleza kazi Yake ya enzi iliyofuata, kwa sababu usimamizi wote wa Mungu huendelea mbele siku zote. Enzi nzee ikipita, itabadilishwa na enzi mpya, na mara tu kazi nzee imekamilika, kazi mpya itaendeleza usimamizi wa Mungu. Kupata mwili huku ni kupata mwili kwa Mungu mara ya pili kufuatia kukamilika kwa kazi ya Yesu. Bila shaka, kupata mwili huku hakufanyiki kivyake, bali ni hatua ya tatu ya kazi baada ya Enzi ya Sheria na Enzi ya Neema. Kila hatua mpya ya kazi ya Mungu kila mara huleta mwanzo mpya na enzi mpya. Vivyo hivyo kuna mabadiliko yanayokubaliana katika tabia ya Mungu, katika njia Yake ya kufanya kazi, katika sehemu Yake ya kufanya kazi, na katika jina Lake. Ndiyo maana basi ni vigumu kwa mwanadamu kukubali kazi ya Mungu katika enzi mpya. Lakini licha ya jinsi anapingwa na mwanadamu, Mungu huendelea kufanya kazi Yake, na daima Yeye huwa Akiongoza wanadamu wote kuendelea mbele. Yesu Alipokuja katika ulimwengu wa mwanadamu, Alileta Enzi ya Neema na Akatamatisha Enzi ya Sheria. Wakati wa siku za mwisho, Mungu kwa mara nyingine Alipata mwili, na Alipopata mwili mara hii, Alikamilisha Enzi ya Neema na Akaleta Enzi ya Ufalme. Wale wote wanaokubali kupata mwili kwa Mungu kwa mara ya pili wataongozwa mpaka Enzi ya Ufalme, na wataweza kukubali kibinafsi uongozi wa Mungu. Hata ingawa Yesu Alifanya kazi nyingi miongoni mwa wanadamu, Yeye Alimaliza tu ukombozi wa wanadamu wote na akawa sadaka ya dhambi ya mwanadamu, na Hakumwondolea mwanadamu tabia yake yote ya upotovu. Kumwokoa mwanadamu kikamilifu kutokana na ushawishi wa Shetani hakukumlazimu Yesu kuchukua dhambi zote za mwanadamu kama sadaka ya dhambi tu, lakini pia kulimlazimu Mungu kufanya kazi kubwa zaidi ili kumwondolea mwanadamu tabia yake kikamilifu, ambayo imepotoshwa na Shetani. Na kwa hivyo, baada ya mwanadamu kusamehewa dhambi zake, Mungu Amerudi katika mwili kumwongoza mwanadamu katika enzi mpya, na kuanza kazi ya kuadibu na hukumu, na kazi hii imemleta mwanadamu katika ulimwengu wa juu zaidi. Wote wanaonyenyekea chini ya utawala Wake watapata kufurahia ukweli wa juu na kupata baraka nyingi mno. Wataishi katika mwanga kwa kweli, na watapata ukweli, njia na uzima.

Watu wakibaki katika Enzi ya Neema, basi hawatawahi kujiweka huru kutokana na tabia zao za upotovu, sembuse kujua tabia ya asili ya Mungu. Wanadamu wakiishi daima katika wingi wa neema ila hawana njia ya maisha inayowaruhusu kumjua Mungu na kumridhisha Mungu, basi kamwe hawataweza kumpata Mungu kwa kweli hata ingawa wanaamini Kwake. Hiyo ni aina ya imani ya kutia huruma. Wakati umemaliza kusoma kitabu hiki, wakati umepitia matukio yote ya kazi ya Mungu mwenye mwili katika Enzi ya Ufalme, utahisi kwamba matumaini ya miaka mingi hatimaye yametimika. Utahisi kwamba ni sasa tu ndipo umemwona Mungu uso kwa uso; ni sasa tu ndipo umeutazama uso wa Mungu, umesikia matamshi ya Mungu Mwenyewe, umeifahamu hekima ya kazi ya Mungu, na kuhisi kwa kweli jinsi Mungu ni wa kweli na mwenye nguvu. Utafahamu kuwa umepata vitu vingi ambavyo watu wa nyakati zilizopita hawajawahi kuviona wala kuwa navyo. Wakati huu, utajua kwa uhakika ni nini hasa kuamini katika Mungu, na ni nini kupendeza nafsi ya Mungu. Bila shaka, ukikwamilia maoni ya kitambo, na ukatae au ukane ukweli wa kupata mwili kwa Mungu mara ya pili, basi utabaki mkono mtupu na hutapata chochote, na mwishowe utakuwa na hatia ya kumpinga Mungu. Wale wanaotii ukweli na kunyenyekea kwa kazi ya Mungu watakuja chini ya jina la Mungu mwenye mwili wa pili—Mwenyezi. Wataweza kukubali uelekezi binafsi wa Mungu, na watapata ukweli zaidi na wa juu zaidi na watapokea maisha ya kweli ya mwanadamu. Wataona maono ambayo watu wa zamani hawajawahi kuona kamwe: “Na nikapinduka ili kuiona sauti hiyo iliyonizungumzia. Na baada ya kupinduka, nikatazama vinara saba vya taa vilivyokuwa vya dhahabu; Na hapo katikati ya hivyo vinara saba vya taa nilimwona mtu aliyefanana na Mwana wa Adamu, aliyekuwa amevalia nguo iliyofika katika miguu yake, na kifuani alikuwa amefungwa kanda ya dhahabu. Kichwa chake na nywele zilikuwa nyeupe mithili ya sufu, nyeupe mithili ya theluji; na macho yake yalikuwa mithili ya ulimi wa moto; Na miguu yake mithili ya shaba safi, kama kwamba ilikuwa imechomwa ndani ya tanuru; na sauti yake ilikuwa mithili ya sauti ya maji mengi. Na katika mkono wake wa kulia kulikuwa na nyota saba: na alitoa kinywani mwake upanga mkali wenye sehemu mbili za makali: nao uso wake ulikuwa mithili ya jua liangazavyo kupitia nguvu zake yeye” (Ufunuo 1:12-16). Maono haya ni maonyesho ya tabia kamilifu ya Mungu, na maonyesho ya aina hii ya tabia Yake nzima pia ndiyo maonyesho ya kazi ya Mungu Anapopata mwili mara hii. Katika mibubujiko ya kuadibu na hukumu, Mwana wa Adamu Anaonyesha tabia Yake ya asili kupitia kuzungumza kwa maneno, Akiwaruhusu wale wote wanaokubali kuadibu Kwake na hukumu kuuona uso wa kweli wa Mwana wa Adamu, uso ulio mfano wa kuaminika wa Mwana wa Adamu Alivyooneka na Yohana. (Bila shaka, yote haya hayatawaonekania wote wasioikubali kazi ya Mungu katika Enzi ya Ufalme.) Uso wa kweli wa Mungu hauwezi kuelezwa kikamilifu na maneno ya mwanadamu, na hivyo Mungu Hutumia maonyesho ya tabia Yake asili kuuonyesha uso Wake wa kweli kwa mwanadamu. Ambayo ni kusema wote ambao wamepitia tabia asili ya Mwana wa Adamu wameuona uso wa kweli wa Mwana wa Adamu, kwa kuwa Mungu ni mkuu zaidi na Hawezi kuelezwa kikamilifu na maneno ya mwanadamu. Mara tu mwanadamu amepitia kila hatua ya kazi ya Mungu katika Enzi ya Ufalme, basi atapata kujua maana kamili ya maneno ya Yohana alipozungumza kuhusu Mwana wa Adamu kati ya vinara vya taa: “Kichwa chake na nywele zilikuwa nyeupe mithili ya sufu, nyeupe mithili ya theluji; na macho yake yalikuwa mithili ya ulimi wa moto; Na miguu yake mithili ya shaba safi, kama kwamba ilikuwa imechomwa ndani ya tanuru; na sauti yake ilikuwa mithili ya sauti ya maji mengi. Na katika mkono wake wa kulia kulikuwa na nyota saba: na alitoa kinywani mwake upanga mkali wenye sehemu mbili za makali: nao uso wake ulikuwa mithili ya jua liangazavyo kupitia nguvu zake yeye.” Wakati huo, utajua bila shaka yoyote kwamba mwili huu wa kawaida uliozungumza maneno mengi ni kwa hakika Mungu mwenye mwili mara ya pili. Na utahisi ni jinsi gani kwa kweli umebarikiwa, na kujiona mwenyewe kama mwenye bahati kubwa. Je, ungekuwa huna radhi kuikubali baraka hii?

Sehemu ya kwanza ya kitabu hiki ni maneno ya Roho kwa makanisa. Maneno haya yanawakilisha mpito kutoka mwisho wa Enzi ya Neema hadi kwa mwanzo wa Enzi ya Ufalme, na ni ushuhuda wa wazi wa Roho wa Mwana wa Adamu kwa makanisa. Pia ni utimizo wa maneno katika Ufunuo wa Yohana kwamba “Yeye ambaye ana sikio, na asikie yale ambayo makanisa yaliambiwa na Roho.” Hii ni kazi ambayo Mungu alianza katika Enzi ya Ufalme. Sehemu ya pili ya kitabu hiki ni maneno ambayo yaliyonenwa binafsi na Mwana wa Adamu baada ya Yeye kujifichua kirasmi. Inajumuisha maudhui kubwa ya matamshi kadhaa tofauti na maneno kama vile unabii, ufunuo wa mafumbo, na njia ya maisha. Kuna utabiri wa siku za usoni ya ufalme, ufunuo wa mafumbo ya mpango wa usimamizi wa Mungu, uchunguzi wa asili ya mwanadamu, ushawishi na maonyo, hukumu kali, maneno ya dhati ya kuliwaza, mazungumzo ya maisha, mazungumzo ya kuingia na kadhalika. Kwa ufupi, kile Mungu Anacho, kile Alicho, na tabia ya Mungu yote imeonyeshwa ndani ya kazi na maneno Yake. Bila shaka, Mungu Anapopata mwili mara hii, kazi Yake ni kuonyesha tabia Yake, kimsingi kupitia kuadibu na hukumu. Akitumia haya kama msingi, Analeta ukweli zaidi kwa mwanadamu, kuonyesha njia zaidi za matendo, na hivyo Hufikia lengo Lake la kumshinda mwanadamu na kumwokoa mwanadamu kutokana na tabia yake potovu. Hili ndilo liko katika kazi ya Mungu katika Enzi ya Ufalme. Je, unatamani kuingia katika enzi mpya? Je, unatamani kujiondolea tabia yako potovu? Je, unatamani kupata ukweli wa juu? Je, unatamani kuuona uso wa kweli wa Mwana wa Adamu? Je unatamani kuishi maisha yaliyo na thamani? Je, unatamani kufanywa mkamilifu na Mungu? Basi, je, utakaribisha vipi kurudi kwa Yesu?

Tanbihi:

a. Nakala halisi ya mwanzo inasema “na kwa.”

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp