Maneno ya Mungu ya Kila Siku: Kuingia Katika Uzima | Dondoo 416

02/09/2020

Nyinyi hamtilii maanani sala katika maisha yenu ya kila siku. Watu daima wamepuuza sala. Hapo awali sala zilikuwa za uzembe, huku mwanadamu akifanya tu mambo kwa namna isiyo ya dhati mbele za Mungu, na hakuna mtu aliyeupeana moyo wake kwa ukamilifu mbele ya Mungu na kumwomba Mungu kweli. Watu humwomba Mungu tu wakati kitu kinawatendekea. Katika wakati huu wote, umewahi kweli kumwomba Mungu? Je, umewahi kutoa machozi ya uchungu mbele ya Mungu? Je, umewahi kujijua mwenyewe mbele ya Mungu? Je, umewahi kumwomba Mungu maombi ya kutoka? Sala huja kupitia kufanya mazoezi: Ikiwa kwa kawaida huombi nyumbani, basi hutakuwa na njia yoyote ya kuomba kanisani, na kama kwa kawaida huombi wakati wa mikusanyiko midogo, basi hutaweza kusali wakati wa mikusanyiko mikubwa. Ikiwa kwa kawaida humkaribii Mungu au kutafakari juu ya maneno ya Mungu, basi hutakuwa na chochote cha kusema wakati wa kuomba—na hata kama utaomba, utakuwa tu unaunga mkono kwa maneno matupu; hutakuwa unaomba kwa kweli.

Ni nini maana ya kuomba kwa kweli? Ina maana ya kuzungumza maneno yaliyo ndani ya moyo wako kwa Mungu, na kuwasiliana na Mungu baada ya kufahamu mapenzi Yake na kutegemea maneno Yake; ina maana ya kuhisi kuwa karibu na Mungu hasa, kuhisi kwamba Yeye yuko mbele yako, na kwamba una kitu cha kumwambia; na inamaanisha kuwa mwangavu hasa ndani ya moyo wako, na kuhisi kwamba Mungu ni wa kupendeza hasa. Utajisikia kutiwa moyo sana, na baada ya kusikia maneno yako ndugu zako watajisikia kufurahishwa, watahisi kwamba maneno unayosema ni maneno yaliyo ndani ya mioyo yao, maneno ambayo wangependa kusema, na kwamba kile unachosema kinawakilisha kile wanachotaka kusema. Hii ndiyo maana ya kuomba kwa kweli. Baada ya kuomba kwa kweli, moyoni mwako utahisi kuwa na amani, na kufurahishwa; nguvu ya kumpenda Mungu itaongezeka, na utahisi kwamba hakuna kitu chochote katika maisha yako yote kinachostahili au ni muhimu zaidi kuliko kumpenda Mungu—na yote haya yatathibitisha kuwa maombi yako yamekuwa yenye ufanisi. Je, umewahi kuomba kwa njia hiyo?

Na je, kuhusu maudhui ya sala? Unapaswa kuomba, hatua kwa hatua, kwa mujibu wa hali yako ya kweli na kile kinachotakiwa kufanywa na Roho Mtakatifu, na unapaswa kuwasiliana kwa karibu na Mungu kulingana na mapenzi ya Mungu na mahitaji Yake kwa mwanadamu. Unapoanza kufanya mazoezi ya maombi yako, kwanza peana moyo wako kwa Mungu. Usijaribu kufahamu mapenzi ya Mungu; jaribu tu kuzungumza maneno yaliyo ndani ya moyo wako kwa Mungu. Unapokuja mbele za Mungu, sema hivi: “Ee Mungu! Leo tu ndio natambua kuwa nilikuwa nikikuasi. Mimi kweli ni mpotovu na mwenye kustahili dharau. Awali, nilikuwa nikipoteza muda wangu; kuanzia leo nitaishi kwa ajili Yako, nitaishi kwa kudhihirisha maisha ya maana, na kuridhisha mapenzi Yako. Ningependa Roho Wako afanye kazi ndani yangu daima, na daima aniangaze na kunipa nuru, ili nipate kuwa na ushuhuda wenye nguvu na unaosikika mbele Zako, unaomruhusu Shetani kuuona utukufu Wako, ushuhuda Wako, na thibitisho la ushindi Wako ndani yetu.” Wakati unapoomba kwa njia hii, moyo wako utawekwa huru kabisa, baada ya kuomba kwa njia hii, moyo wako utakuwa karibu na Mungu, na kwa kuomba hivi mara kwa mara, Roho Mtakatifu atafanya kazi ndani yako bila shaka. Ikiwa daima wewe humwita Mungu kwa njia hii na kufanya azimio lako mbele ya Mungu, siku itawadia ambapo azimio lako litaweza kukubalika mbele ya Mungu, wakati moyo wako na nafsi yako vyote vitapokelewa na Mungu, na hatimaye utakamilishwa na Mungu. Sala ni ya muhimu sana kwenu. Unapoomba, unapokea kazi ya Roho Mtakatifu, hivyo moyo wako unaguswa na Mungu, na nguvu za upendo kwa Mungu ndani yako huchipuka. Ikiwa hutaomba kwa moyo wako, ikiwa hutafungua moyo wako kuwasiliana kwa karibu na Mungu, basi Mungu hatakuwa na njia ya kufanya kazi ndani yako. Ikiwa, baada ya kusali, umesema maneno yote yaliyo ndani ya moyo wako na Roho wa Mungu hajafanya kazi, ikiwa huhisi kutiwa moyo ndani, basi hili linaonyesha kwamba moyo wako hauna ari, kwamba maneno yako si ya kweli, na bado wewe ni mchafu. Ikiwa, baada ya kusali, unafurahishwa, basi sala zako zimekubaliwa na Mungu na Roho wa Mungu amefanya kazi ndani yako. Kama mtu ambaye huhudumu mbele ya Mungu, huwezi kuwa bila sala. Ikiwa unaona ushirika na Mungu kama kitu ambacho kina maana na cha thamani, ungeweza kuacha sala? Hakuna mtu anayeweza kuwa bila mawasiliano ya karibu na Mungu. Bila sala, unaishi katika mwili, unaishi katika utumwa wa Shetani; bila sala ya kweli, unaishi chini ya ushawishi wa giza. Natumaini kwamba ndugu wanaweza kuomba kila siku. Huku si kuzingatia mafundisho ya dini, hata hivyo, bali matokeo ambayo yanapaswa kutimizwa. Je, uko tayari kuacha usingizi kidogo na anasa, kusema sala za asubuhi wakati wa alfajiri na kisha kufurahia maneno ya Mungu? Ukiomba kwa moyo safi na kula na kunywa maneno ya Mungu hivi, basi utakubalika zaidi na Mungu. Ukifanya hivi kila asubuhi, ukifanya mazoezi ya kumpa Mungu moyo wako kila siku na kuwasiliana kwa karibu na Mungu, basi ufahamu wako wa Mungu utaongezeka bila shaka, na utaweza kufahamu vizuri zaidi mapenzi ya Mungu. Unapaswa kusema: “Ee Mungu! Ningependa kutimiza wajibu wangu. Ili Uweze kutukuzwa ndani yetu, na Uweze kufurahia ushuhuda ulio ndani yetu, kikundi hiki cha watu, naweza tu kutoa nafsi yangu yote kwako. Nakuomba Ufanye kazi ndani yetu, ili niweze kukupenda na kukuridhisha kwa kweli, na kukufanya Uwe lengo ambalo ninafuatilia.” Wakati ambapo unakuwa na mzigo huu, Mungu atakufanya uwe mkamilifu bila shaka; hupaswi tu kuomba kwa ajili yako mwenyewe, bali pia kwa ajili ya kufanya mapenzi ya Mungu, na kwa ajili ya kumpenda Yeye. Hiyo ndiyo aina ya sala ya kweli kabisa. Je, wewe huomba ili kutenda mapenzi ya Mungu?

Hapo awali, nyinyi hamkujua jinsi ya kuomba, na mlipuuza maombi; leo, lazima mjitahidi kabisa kujifundisha kuomba. Ikiwa huwezi kuwa na ujasiri wa kumpenda Mungu, basi unawezaje kuomba? Unapaswa kusema: “Ee Mungu! Moyo wangu hauwezi kukupenda kweli, nataka kukupenda lakini sina nguvu. Napaswa kufanya nini? Napenda Ufungue macho ya roho yangu, napenda Roho Wako auguse moyo wangu, ili mbele Yako nivuliwe hali zote za kutoonyesha hisia, na nisishurutishwe na mtu yeyote, jambo, au kitu; nauweka moyo wangu wazi kabisa mbele Yako, ili nafsi Yangu yote ijitoe mbele Yako, na Uweze kunijaribu vile Utakavyo. Sasa, siwazii matarajio yangu, wala sifungwi na kifo. Kwa kuutumia moyo wangu ambao unakupenda, napenda kutafuta njia ya uzima. Vitu vyote na matukio viko mikononi Mwako, majaliwa yangu yako mikononi Mwako, na, zaidi ya hayo, maisha yangu yanadhibitiwa na mikono Yako. Sasa, nafuatilia kukupenda Wewe, na bila kujali kama Wewe unaniruhusu kukupenda, haijalishi jinsi Shetani anavyoingilia, nimeamua kukupenda Wewe.” Unapokabiliwa na mambo kama hayo, unasali kwa njia hii. Ikiwa utafanya hivyo kila siku, nguvu ya kumpenda Mungu itaongezeka polepole.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kuhusu Desturi ya Sala

Tazama zaidi

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Shiriki

Ghairi

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp