Kwenye Siku ya Kwanza, Mchana na Usiku wa Mwanadamu Vinazaliwa na Kujitokeza Waziwazi kwa Msaada wa Mamlaka ya Mungu

15/07/2018

Hebu na tuweze kuangalia fungu la kwanza: “Na Mungu akasema, Na kuwe na mwanga; kukawa na mwanga. Mungu akauona mwanga, na kuwa ulikuwa mzuri: na Mungu akautenga mwanga na kiza. Naye Mungu akauita mwanga Mchana, na kiza akaliita Usiku. Na jioni na asubuhi yalikuwa siku ya kwanza” (Mwa 1:3-5). Fungu hili linafafanua kitendo cha kwanza cha Mungu wakati wa mwanzo wa uumbaji, na siku ya kwanza ambayo Mungu alipitisha ambapo kulikuwa na jioni na asubuhi. Lakini ilikuwa siku ya kipekee: Mungu alianza kutayarisha nuru ya viumbe vyote, na, vilevile, Akagawa nuru kutoka kwa giza. Kwenye siku hii, Mungu alianza kunena, na matamshi na mamlaka Yake vyote vilikuwa pamoja. Mamlaka Yake yalianza kujitokeza miongoni mwa viumbe vyote, na nguvu Zake zikaenea miongoni mwa viumbe vyote kutokana na maneno Yake. Kuanzia siku hii kuendelea mbele, viumbe vyote viliumbwa na vikawa viko tayari kwa sababu ya maneno ya Mungu, mamlaka ya Mungu na nguvu za Mungu, na vikaanza kufanya kazi kwa msaada wa maneno ya Mungu, mamlaka ya Mungu na nguvu za Mungu. Wakati Mungu aliposema maneno haya “Na kuwe na mwanga,” kulikuwepo na nuru. Mungu hakuanza kushughulikia shughuli yoyote; nuru ilikuwa imeonekana kama matokeo ya maneno Yake. Hii ilikuwa nuru ambayo Mungu aliita mchana, na ambayo binadamu angali anaitegemea kwa minajili ya kuwepo kwake leo. Kwa amri ya Mungu, hali yake halisi na thamani havijawahi kubadilika na havijawahi kutoweka. Uwepo wake unaonyesha mamlaka na nguvu za Mungu, na unatangaza uwepo wa Mungu, na unathibitisha, tena na tena, utambulisho na hadhi ya Muumba. Haiwezi kushikika, au kuonekana, lakini ni nuru halisi inayoweza kuonekana na binadamu. Kuanzia wakati huo kusonga mbele, kwenye ulimwengu huu mtupu ambao “nchi ilikuwa ya ukiwa na tupu; na kulikuwa na giza sehemu ya juu ya vilindi,” kulikuwepo kiumbe kile cha kwanza cha kushikika. Kiumbe hiki kilitokana na maneno ya kinywa cha Mungu na kikaonekana kwenye tukio la kwanza la kuumbwa kwa viumbe vyote kwa sababu ya mamlaka na matamshi ya Mungu. Muda mfupi baadaye, Mungu aliamuru nuru na giza kutengana…. Kila kitu kilibadilika na kilikamilishwa kwa sababu ya maneno ya Mungu…. Mungu akaiita nuru hii “Mchana,” na giza hili Akaliita “Usiku.” Kuanzia wakati huo, jioni ya kwanza na asubuhi ya kwanza ziliweza kuumbwa katika ulimwengu ambao Mungu alinuia kuumba, na Mungu akasema hii ndiyo iliyokuwa siku ya kwanza. Siku hii ilikuwa siku ya kwanza ya vile vilivyoumbwa na Muumba wa viumbe vyote, na ilikuwa mwanzo wa kuumbwa kwa viumbe vyote, na ndio wakati wa kwanza ambao mamlaka na nguvu za Muumba vilikuwa vimeonyeshwa katika ulimwengu huu ambao Alikuwa ameumba.

Kwenye Siku ya Kwanza, Mchana na Usiku wa Mwanadamu Vinazaliwa na Kujitokeza Waziwazi kwa Msaada wa Mamlaka ya Mungu

Kupitia maneno haya, binadamu anaweza kutazama mamlaka ya Mungu, na mamlaka ya maneno ya Mungu, na nguvu za Mungu. Kwa sababu Mungu tu ndiye anayemiliki nguvu kama hizo, na kwa hivyo Mungu pekee ndiye aliye na mamlaka, na kwa sababu Mungu ndiye anayemiliki mamlaka kama hayo, kwa hivyo Mungu pekee ndiye aliye na nguvu kama hizo. Je, binadamu au kifaa chochote kingeweza kumiliki mamlaka na nguvu kama hizi? Je, kunalo jibu katika moyo wako? Mbali na Mungu, je, kuna kiumbe chochote kilichoumbwa au kile ambacho hakikuumbwa kinachomiliki mamlaka kama hayo? Umewahi kuona mfano wa kiumbe kama hiki kwenye vitabu vingine vyovyote au machapisho? Kunayo rekodi yoyote kwamba mtu aliumba mbingu na ulimwengu na viumbe vyote? Jambo hili halionekani katika vitabu au rekodi nyingine zozote; haya ndiyo, bila shaka, maneno ya kipekee yenye mamlaka na nguvu kuhusu uumbaji wa kupendeza wa Mungu wa ulimwengu, yaliyorekodiwa kwenye Biblia, na maneno haya yanazungumzia mamlaka ya kipekee ya Mungu, na utambulisho wa kipekee wa Mungu. Je, mamlaka na nguvu kama hizi zinaweza kusemekana kuwa zinaashiria utambulisho wa kipekee wa Mungu? Yanaweza kusemwa yanamilikiwa na Mungu, na Mungu pekee? Bila shaka, Mungu Mwenyewe pekee ndiye anayemiliki mamlaka na nguvu kama hizi! Mamlaka na nguvu hizi vyote haviwezi kumilikiwa au kubadilishwa na kiumbe chochote kingine kilichoumbwa au kile ambacho hakikuumbwa! Je, hii ni mojawapo ya sifa za Mungu Mwenyewe wa kipekee? Je, umewahi kuishuhudia? Maneno haya yanaruhusu watu kuelewa kwa haraka na waziwazi hoja hii kwamba Mungu anamiliki mamlaka ya kipekee, na nguvu za kipekee, na Anamiliki utambulisho na hadhi isiyo ya kawaida. Kutokana na ushirika wa hapa juu, je, unaweza kusema kwamba Mungu unayemsadiki ndiye Mungu Mwenyewe wa kipekee?

Neno, Vol. 2. Kuhusu Kumjua Mungu. Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee I

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Leave a Reply

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp