Kwa nini inasemekana kwamba “Utatu” ni kauli ya upuuzi zaidi?

24/09/2018

Maneno Husika ya Mungu:

Baada ya ukweli wa Yesu aliyepata mwili kutokea, mwanadamu aliamini hili: Si Baba pekee aliye mbinguni, bali pia Mwana, na hata Roho Mtakatifu. Hii ndiyo dhana ya kawaida aliyonayo mwanadamu, kwamba kuna Mungu wa aina hii mbinguni: Utatu ambao ni Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu, wote katika nafsi moja. Wanadamu wote wana fikra hizi: Mungu ni Mungu mmoja, ila Anajumuisha sehemu tatu, kile ambacho wale wote waliofungwa kwa huzuni katika hizi dhana za kawaida wanachukulia kuwa kuna Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu. Ni sehemu hizo tatu pekee ambazo zimefanywa moja ambazo ni Mungu kamili. Bila Baba Mtakatifu, Mungu asingekuwa mkamilifu. Vivyo hivyo, wala Mungu asingekuwa mkamilifu bila Mwana au Roho Mtakatifu. Katika mawazo yao, wanaamini kuwa Baba au Mwana pekee hawezi kuwa Mungu. Ni Baba, Mwana na Roho Mtakatifu tu kwa pamoja wanaoweza kuwa Mungu Mwenyewe. Sasa, waumini wote wa kidini, akiwemo kila mfuasi miongoni mwenu, anashikilia hii imani. Ilhali, ikiwa hii imani ni sahihi, hakuna anayeweza kuelezea, kwani daima mmechanganyikiwa kuhusu masuala ya Mungu Mwenyewe. Japo hizi ni fikra tu, hamjui kama ni sawa au mbaya, kwani mmeathiriwa vibaya na mawazo ya kidini. Mmeyakubali kwa kina haya mawazo ya kidini yaliyozoeleka, na hii sumu imezama kwa kina ndani yenu. Hivyo basi, hata kwa hili mmeanguka katika huu ushawishi wenye madhara, kwani Utatu haupo. Yaani, Utatu wa Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu haupo. Hizi zote ni fikra za kawaida za mwanadamu, na imani za uongo za mwanadamu. Kwa karne nyingi, mwanadamu ameamini katika huu Utatu, ambao umebuniwa na mawazo katika akili za mwanadamu, ukatengenezwa na mwanadamu, na ambao haujawahi kuonekana na mwanadamu. Kwa miaka mingi, kumekuwa na watu maarufu wa kiroho ambao wameeleza “maana ya kweli” ya Utatu, ila maelezo hayo ya Utatu kama nafsi tatu dhahiri yamekuwa si yakini na hayapo wazi na watu wote wamepumbazwa na “ujenzi” wa Mungu. Hakuna mtu maarufu yeyote aliyewahi kutoa maelezo kamili; maelezo mengi yanafaa katika masuala ya mjadala na katika maandishi, ila hakuna hata mtu mmoja ambaye ana ufahamu kamili na wa wazi kuhusu maana ya Utatu. Hii ni kwa sababu huu Utatu huu mkuu ambao mwanadamu anashikilia moyoni kwa hakika haupo.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Je, Utatu Upo?

Ikiwa yeyote miongoni mwenu anasema kwamba hakika Utatu upo, basi eleza huyu Mungu mmoja katika nafsi tatu ni nini hasa. Baba Mtakatifu ni nini? Mwana ni nini? Roho Mtakatifu ni nini? Je, Yehova ni Baba Mtakatifu? Je, Yesu ni Mwana? Basi, Roho Mtakatifu je? Je, Baba si Roho? Je, kiini cha Mwana vilevile si Roho? Je, kazi ya Yesu haikuwa ya Roho Mtakatifu? Je, kazi ya Yehova haikufanywa wakati ule na Roho sawa tu na kazi ya Yesu? Mungu Anaweza kuwa na Roho wangapi? Kulingana na maelezo yako hizi nafsi tatu, yaani, Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu ni mmoja; kama ni hivyo, kuna Roho watatu lakini kuwa na Roho watatu kunamaanisha kuwa kuna Mungu Watatu. Hii inamaanisha kuwa hakuna Mungu Mmoja wa kweli; Mungu wa aina hii anawezaje kuwa kiini asili cha Mungu? Kama unakubali kuwa kuna Mungu mmoja tu, basi Anawezaje kuwa na Mwana na awe Baba? Je, hizi si fikra zako mwenyewe? Kuna Mungu Mmoja tu, nafsi moja katika Mungu huyu, na Roho mmoja tu wa Mungu sawa tu na ilivyoandikwa katika Biblia kwamba “Kuna tu Roho Mtakatifu mmoja na Mungu mmoja tu.” Haijalishi kama Baba na Mwana unaowazungumzia wapo, kuna Mungu mmoja tu, na kiini cha Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu mnaowaamini ni kiini cha Roho Mtakatifu. Kwa maneno mengine, Mungu ni Roho, ila Ana uwezo wa kupata Mwili na kuishi miongoni mwa wanadamu na vilevile kuwa juu ya vitu vyote. Roho Wake anajumuisha kila kitu na Anapatikana kila mahala. Anaweza kuwa katika mwili na wakati ule ule akawa kote duniani. Kwa kuwa watu wanasema kwamba Mungu ndiye tu Mungu wa kweli, basi kuna Mungu mmoja, ambaye hawezi kugawanywa kwa mapenzi ya awaye yote! Mungu ni Roho mmoja tu, na nafsi moja; na huyo ni Roho wa Mungu. Ikiwa ni kama usemavyo, Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu, basi Hawa si watatu? Roho Mtakatifu ni kitu kimoja, Mwana ni kingine, na Baba vilevile ni kingine. Ni nafsi tatu tofauti zenye viini tofauti, iweje basi ziwe kila moja sehemu ya Mungu mmoja? Roho Mtakatifu ni Roho; hili ni rahisi kueleweka kwa wanadamu. Ikiwa ni hivyo basi, Baba ni Roho zaidi. Hajawahi kushuka kuja duniani na Hajawahi kupata mwili; Yeye ni Yehova Mungu katika mioyo ya mwanadamu, na kwa hakika Yeye vilevile ni Roho. Basi kuna uhusiano gani kati Yake na Roho Mtakatifu? Je, ni uhusiano kati ya Baba na Mwana? Au ni uhusiano kati ya Roho Mtakatifu na Roho wa Mungu? Je, kiini cha kila Roho ni sawa? Au Roho Mtakatifu ni chombo cha Baba? Hili linaweza kuelezwaje? Aidha kuna uhusiano gani kati ya Mwana na Roho Mtakatifu? Je, ni uhusiano kati ya Roho wawili au ni uhusiano kati ya mwanadamu na Roho? Haya yote ni masuala ambayo hayawezi kuelezewa! Ikiwa Wote ni Roho mmoja, basi hapawezi kuwepo na mjadala kuhusu nafsi tatu, kwani zote zinamilikiwa na Roho mmoja. Kama Zingekuwa nafsi tofauti, basi Roho Zao Zingetofautiana katika nguvu zao na kamwe hawangekuwa Roho mmoja. Hii dhana ya Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu ni upuuzi mtupu! Hili linamweka Mungu katika vitengo na kumgawanya kuwa nafsi tatu, kila moja ikiwa na hadhi na Roho; basi Atawezaje kuwa Roho mmoja na Mungu mmoja?

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Je, Utatu Upo?

Hata hivyo, wengine wanaweza kusema: “Baba ni Baba; Mwana ni Mwana; Roho Mtakatifu ni Roho Mtakatifu, na mwishowe, Watafanywa kitu kimoja.” Je, Utawafanyaje kitu kimoja? Baba na Roho Mtakatifu Wawezaje kufanywa kitu kimoja? Ikiwa Walikuwa wawili kiasili, haijalishi Wamewekwa pamoja kwa namna gani, je, Hawataendelea kuwa sehemu mbili? Unaposema kuwa kuwafanya kuwa kitu kimoja, huko si kuunganisha sehemu mbili kutengeneza kitu kamili? Je, Hawakuwa sehemu mbili kabla ya kufanywa kitu kizima? Kila Roho ana kiini kinachotofautiana, na Roho wawili Hawawezi kufanywa kuwa kitu kimoja. Roho si chombo cha kutengenezwa, si kama chombo chochote katika ulimwengu. Kulingana na mitazamo ya wanadamu, Baba ni Roho mmoja, Mwana ni mwingine, na Roho Mtakatifu tena ni mwingine, halafu Roho Hawa huchanganyika sawa na glasi tatu za maji kuunda kitu kimoja kizima. Je, hizo si sehemu tatu zimefanywa kuwa kitu kimoja? Haya bila shaka ni maelezo ya kimakosa! Je, huku si kumgawa Mungu? Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu wanawezaje kufanywa kuwa kitu kimoja? Je, Wao si sehemu tatu zenye asili tofauti?

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Je, Utatu Upo?

Yesu alipomwita Mungu wa mbinguni kwa jina la Baba alipokuwa akiomba, hili lilifanywa katika mitazamo ya mwanadamu aliyeumbwa, kwa sababu Roho wa Mungu alikuwa amevaa mwili wa kawaida na wa desturi na Alikuwa na umbile la nje la mwanadamu aliyeumbwa. Hata ikiwa ndani yake mlikuwa na Roho wa Mungu, umbo Lake la nje bado lilikuwa lile la mwanadamu wa kawaida; kwa maana nyingine, Alikuwa “Mwana wa Adamu” jambo ambalo watu wote, akiwemo Yesu Mwenyewe, walilizungumzia. Na kwa sababu Anaitwa Mwana wa Adamu, Yeye ni mtu (Mwanamke au mwanamume, kwa vyovyote vile mwenye umbo la nje la mwanadamu) aliyezaliwa katika familia ya kawaida ya watu wa kawaida. Kwa hivyo, Yesu kumwita Mungu wa mbinguni kwa jina la Baba kulikuwa sawa na mlivyomwita mara ya kwanza Baba; Alifanya hivyo kutokana na mtazamo wa Mwanadamu aliyeumbwa. Je, mnakumbuka Sala ya Bwana ambayo Yesu aliwafundisha kukariri? “Baba Yetu Uliye mbinguni….” Aliwaambia wanadamu wote wamwite Mungu wa Mbinguni kwa jina la Baba. Na kwa kuwa Naye pia alimwita Baba, alifanya hivyo kutoka kwa mtazamo wa mtu aliye katika daraja moja nanyi nyote. Kwa kuwa mlimuita Mungu wa mbinguni Baba, hili linaonyesha kuwa Yesu alijichukulia kuwa katika daraja sawa nanyi, kama mwanadamu duniani aliyeteuliwa na Mungu (yaani, Mwana wa Mungu). Kama mnamwita Mungu “Baba,” je, hii si kwa sababu nyinyi ni wanadamu walioumbwa? Haijalishi Yesu alikuwa na mamlaka makubwa kiasi gani duniani, kabla ya kusulubiwa, Alikuwa tu Mwana wa Adamu, akiongozwa na Roho Mtakatifu (yaani, Mungu), Akiwa miongoni mwa viumbe wa duniani, kwani bado Alikuwa hajaikamilisha kazi Yake. Kwa hivyo, kumwita kwake Mungu wa mbinguni Baba kulikuwa tu unyenyekevu na utiifu Wake. Yeye kumwita Mungu (yaani, Roho aliye mbinguni) kwa namna ile, hata hivyo, hakudhibitishi kuwa Yeye ni Mwana wa Roho wa Mungu aliye mbinguni. Badala yake, ni kuwa mtazamo wake ni tofauti, si kwamba ni nafsi tofauti. Uwepo wa nafsi tofauti ni uongo. Kabla ya kusulubiwa kwake, Yesu alikuwa Mwana wa Adamu aliyefungwa katika udhaifu wa kimwili, na Hakuwa na mamlaka kamilifu ya Roho. Hiyo ndiyo maana Angeweza tu kutafuta mapenzi ya Mungu Baba kutoka katika mtazamo wa kiumbe. Ni kama tu Alivyoomba mara tatu huko Gethsemane: “Si kama Nitakavyo, bali kama utakavyo.” Kabla Atundikwe msalabani, Hakuwa zaidi ya Mfalme wa Wayahudi; alikuwa Kristo, Mwana wa Adamu, na wala si mwenye utukufu. Hiyo ndiyo maana, kutokana na mtazamo wa mwanadamu, Alimwita Mungu Baba. Sasa, huwezi kusema kuwa wote wamwitao Mungu Baba ni Wana. Ingekuwa kweli, basi wote si mngekuwa Mwana punde Yesu alipowafundisha Sala ya Bwana? Ikiwa bado hamjaridhika, basi niambieni hili, ni nani mmwitaye Baba? Ikiwa mnamrejelea Yesu, je, Baba ya Yesu ni nani kwenu? Baada ya Yesu kurudi mbinguni, hii dhana ya Baba na Mwana ilikoma. Hii dhana ilifaa tu kipindi ambacho Yesu alikuwa mwili; katika mazingira mengine yoyote, uhusiano ni ule wa kati ya Bwana wa uumbaji na kiumbe mnapomwita Mungu Baba. Hakuna wakati ambapo wazo hili la Utatu wa Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu linaweza kuwa na mashiko; ni uongo ambao ni nadra kuonekana na halipo!

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Je, Utatu Upo?

Kuna ukinzani mwingi katika maelezo ya mwanadamu. Kweli, haya ni mawazo ya mwanadamu; bila uchunguzi zaidi, ambayo nyote mngeamini kuwa yako sahihi. Je, hamjui hii dhana ya Mungu kama Utatu Mtakatifu ni mawazo ya mwanadamu tu? Hakuna ufahamu wa mwanadamu ulio mzima na kamili. Mara zote kuna madoa, na mwanadamu ana mawazo mengi mno; hili linaonyesha kuwa kiumbe hawezi kuieleza kazi ya Mungu. Kuna mengi sana katika akili ya mwanadamu, yote yakitokana na mantiki na tafakari, ambayo hukinzana na ukweli. Je, mantiki yako yaweza kuichangua kazi ya Mungu? Je, waweza kupata utambuzi wa kazi yote ya Yehova? Je, ni wewe kama mwanadamu uwezaye kubaini yote, au ni Mungu Mwenyewe awezaye kuona kutoka milele hadi milele? Je, ni wewe mwanadamu uwezaye kuona tangu milele ya zamani sana hadi milele ijayo, au Mungu ndiye Ana uwezo wa kufanya hivyo? Unasema nini? Unafaa vipi kumweleza Mungu? Maelezo yako yametegemezwa katika misingi gani? Wewe ni Mungu? Mbingu na dunia, na vyote vilivyomo viliumbwa na Mungu Mwenyewe. Si wewe uliyelifanya hili, basi ni kwa nini unatoa maelezo yasiyo sahihi? Sasa, unaendelea kuamini katika utatu mtakatifu? Hufikirii kuwa huu ni mzigo mkubwa kwa njia hii? Itakuwa bora kwako kuamini katika Mungu mmoja, si watatu. Ni bora zaidi kuwa mwepesi, kwani mzigo wa Bwana ni mwepesi.

Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Je, Utatu Upo?

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Leave a Reply

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp