Kuwa Mzingatifu wa Mapenzi ya Mungu ili Upate Utimilifu

Kadiri unavyozingatia mapenzi ya Mungu, ndivyo unavyokuwa na mzigo zaidi; kadiri unavyokuwa na mzigo, ndivyo uzoefu wako utakuwa mwingi zaidi. Unapokuwa mzingatifu wa mapenzi ya Mungu, Mungu atakupa mzigo huu, na Mungu atakupa nuru ya mambo ambayo amekuaminia. Baada ya Mungu kukupa mzigo huu, utaangalia ukweli wa kipengele hiki unapokula na kunywa maneno ya Mungu. Kama una mzigo unaohusiana na hali ya maisha ya ndugu, huu ni mzigo ulioaminiwa kwako na Mungu, na sala zako za kila siku daima zitaubeba mzigo huu. Kile ambacho Mungu hufanya kimeaminiwa kwako, uko radhi kutekeleza kile ambacho Mungu anataka kufanya, na hivi ndivyo inavyomaanisha kuuchukua mzigo wa Mungu kama wako. Wakati huu, kula na kunywa kwako maneno ya Mungu kutalenga masuala katika vipengele hivi, na utafikiri: Nitayatatuaje masuala haya? Nitawaruhusu vipi ndugu kufunguliwa, wawe na furaha katika nafsi zao? Utalenga kusuluhisha masuala haya unapokuwa katika ushirika, utalenga kula na kunywa maneno yanayohusiana na masuala haya wakati ambapo unakula na kunywa maneno ya Mungu, utakuwa ukila na kunywa maneno ya Mungu na wakati huo ukiubeba mzigo huu, na utaelewa matakwa ya Mungu. Wakati huu, utakuwa wazi zaidi kuhusu njia ya kutembelea. Huku ni kupata nuru na mwangaza wa Roho Mtakatifu kunakosababishwa na mzigo wako, na huku ni Mungu kukupa mwongozo Wake. Kwa nini Nasema hili? Ikiwa huna mzigo, basi huzingatii unapokula na kunywa maneno ya Mungu; unapokuwa ukila na kunywa maneno ya Mungu na wakati huo kuubeba mzigo, unakuwa na uwezo wa kuelewa kiini cha maneno ya Mungu, kutafuta njia yako, na kuzingatia mapenzi ya Mungu. Kwa hivyo, unapaswa kumsihi Mungu akuongezee mizigo zaidi katika sala zako ili aweze kukuaminia mambo makuu zaidi, unaweza vyema zaidi kupata njia ya utendaji mbele, unakuwa wa kufaa zaidi katika kula na kunywa maneno ya Mungu, unakuwa na uwezo wa kuelewa kiini cha maneno Yake, na unaweza zaidi kukubali kuguswa hisi na Roho Mtakatifu.

Kula na kunywa maneno ya Mungu, kufanya maombi, kukubali mzigo wa Mungu, kukubali Anachokuaminia—haya yote ni kwa ajili ya kuwa na njia mbele yako. Kadiri unavyozidi kuwa na mzigo mwingi wa agizo la Mungu, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwako kufanywa mtimilifu na Mungu. Wengine hawako tayari kushirikiana katika kumtumikia Mungu hata wakati ambapo wameshurutishwa; hao ni watu wavivu ambao hutamani kufurahia faraja. Kadiri unavyotakiwa kushirikiana katika kumhudumia Mungu, ndivyo utakavyopata uzoefu zaidi. Kwa sababu una mizigo zaidi na una uzoefu zaidi, utakuwa na nafasi zaidi ya kufanywa mtimilifu. Kwa hivyo, ikiwa unaweza kumhudumia Mungu kwa uaminifu utazingatia mzigo wa Mungu, na kwa njia hii utakuwa na nafasi nyingi zaidi za kufanywa mtimilifu na Mungu. Kundi kama hili la watu linafanywa kamilifu na Mungu wakati huu. Kadiri Roho Mtakatifu anavyokugusa hisia, ndivyo utakavyotenga muda zaidi wa kuzingatia mzigo wa Mungu, ndivyo utakavyofanywa mtimilifu na Mungu zaidi, ndivyo Mungu atakavyokupata zaidi, na mwishowe, utakuwa mtu anayetumiwa na Mungu. Sasa, kuna baadhi ambao hawalibebei kanisa mzigo. Watu hawa ni wazembe na wenye ubwege, na wanajali tu miili yao. Wao ni wenye ubinafsi sana na ni vipofu pia. Hutakuwa na mzigo wowote ikiwa huna uwezo wa kuona suala hili kwa dhahiri. Kadiri unavyozidi kuwa mzingatifu wa mapenzi ya Mungu, ndivyo mzigo ambao Mungu atakuaminia utakavyozidi kuwa mzito. Watu wenye ubinafsi hawako tayari kuyapitia mambo kama haya, na hawako radhi kulipa gharama, na kwa sababu hiyo watakosa nafasi ya kufanywa wakamilifu na Mungu. Je, si huku ni kujiumiza? Ikiwa wewe ni mtu ambaye ni mzingatifu wa mapenzi ya Mungu, utakuza mzigo wa kweli kwa ajili ya kanisa. Kwa kweli, badala ya kuuita huu mzigo wa kanisa, badala yake ni mzigo wa maisha yako, kwa sababu mzigo unaoukuza kwa ajili ya kanisa ni kwa ajili yako kufanywa mtimilifu na Mungu kwa kupitia uzoefu kama huu. Kwa hivyo, yeyote anayelibebea kanisa mzigo mzito zaidi na yeyote abebaye mzigo wa kuingia katika maisha watakuwa wale ambao wanafanywa watimilifu na Mungu. Je, umeona hili kwa dhahiri? Ikiwa kanisa unaloshiriki limetawanyika kama mchanga, lakini bado huna wahaka wala wasiwasi, na hata unajitia hamnazo wakati kina ndugu zako hawali au kunywa maneno ya Mungu kwa kawaida, basi huibebi mizigo yoyote. Watu kama hawa hawapendwi na Mungu. Wale wanaopendwa na Mungu huwa na shauku na kiu ya haki na ni wazingatifu wa mapenzi Yake. Kwa hivyo mnapaswa kuwa wazingatifu wa mzigo wa Mungu sasa. Hupaswi kusubiri tabia ya Mungu yenye haki ifunuliwe kwa watu wote kabla ya wewe kuwa mzingatifu wa mzigo wa Mungu. Je, si muda utakuwa umeshapita wakati huo? Sasa ni nafasi nzuri ya kufanywa mtimilifu na Mungu. Ukiruhusu nafasi hii ipotee, utajuta katika maisha yako yote, kama vile Musa alivyoshindwa kuingia katika nchi nzuri ya Kanani na alijuta katika maisha yake yote, akifa kwa majuto. Mara tu Mungu ameifichua tabia Yake yenye hakikwa watu wote, utajawa na majuto. Hata kama Mungu hakuadibu, utajiadibu kutokana na majuto yako mwenyewe. Wengine hawaridhishwi na hili. Ikiwa huamini, basi subiri uone. Watu wengine watatumika kama utimizaji wa maneno haya. Je, uko tayari kuwa sadaka ya dhabihu kwa maneno haya?

Usipotafuta fursa za kufanywa mtimilifu na Mungu, na usipojitahidi kuwa mbele katika kutafuta kwako kukamilishwa, basi hatimaye utajawa na majuto. Sasa ni fursa nzuri ya kufanywa mtimilifu—huu ni wakati mzuri. Usipotafuta kwa bidii kufanywa mtimilifu na Mungu, mara tu kazi Yake itakapokuwa imekamilika utakuwa umechelewa—utakuwa umekosa fursa hii. Bila kujali jinsi matarajio yako yalivyo makuu, ikiwa Mungu hatendi kazi tena, bila kujali jitihada unazotia, hutaweza kamwe kufanywa mtimilifu. Lazima uchukue fursa hii na ushirikiane kupitia huku Roho Mtakatifu akiwa anafanya kazi Yake kuu. Ukipoteza fursa hii, hutapewa nyingine bila kujali juhudi unazotia. Watu wengine hulia: “Mungu, niko radhi kuzingatia mzigo Wako, na niko radhi kuyaridhisha mapenzi Yako.” Ilhali hawana njia ya utendaji, kwa hivyo mizigo yao haitadumu. Ikiwa kuna njia, utapata uzoefu hatua kwa hatua, na itakuwa na muundo na ratiba. Baada ya mzigo mmoja kukamilika, mwingine unakabidhiwa kwako. Kupitia kuongezeka kwa uzoefu wako wa maisha, mizigo yako inakua pia. Watu wengine hubeba mzigo tu wanapoguswa hisia na Roho Mtakatifu, na baada ya kipindi cha muda, hawaubebi tena mizigo yoyote wakati ambapo hakuna njia ya utendaji. Huwezi kupata mizigo kwa kula na kunywa tu maneno ya Mungu. Kwa kuelewa ukweli mwingi, utapata umaizi, utakuwa na uwezo wa kutatua matatizo kwa kutumia ukweli, na ufahamu mzuri zaidi wa maneno ya Mungu na mapenzi ya Mungu. Kwa mambo haya, utakuza mizigo, na utaweza kufanya kazi nzuri mara tu unapokuwa na mzigo. Ikiwa una mzigo tu lakini huna ufahamu wa ukweli ulio wazi, hiyo pia haitasaidia. Lazima wewe mwenyewe uwe na uzoefu wa maneno ya Mungu, na ujue jinsi ya kuyatenda, na lazima kwanza uingie katika hali halisi kabla ya kuwakimu wengine, kuwaongoza wengine, na kufanywa mtimilifu na Mungu.

Katika “Njia … (4)”, imeandikwa kwamba ninyi nyote ni watu wa ufalme, waliojaaliwa na Mungu kabla ya enzi, na haliwezi kuchukuliwa na mtu yeyote. Pia inasema kwamba Mungu anataka kila mtu atumiwe na Mungu na kufanywa mtimilifu na Mungu, na Anawataka kusimama kama watu Wake, na kwamba kuwa tu watu wa Mungu kutaweza kutimiza mapenzi Yake. Mlikuwa na ushirika juu ya suala hili wakati huo, ushirika juu ya njia ya kuingia kulingana na vigezo kwa watu wa Mungu, kwa hivyo kazi iliyofanywa na Roho Mtakatifu wakati huo ilikuwa kumwondoa kila mtu kutoka kwa hali yake mbaya na kumwongoza katika hali nzuri. Wakati huo, mwenendo wa kazi ya Roho Mtakatifu ulikuwa kumfanya kila mtu afurahie maneno ya Mungu kama watu wa Mungu, na kuruhusu kila mmoja wenu kuelewa kwa wazi kwamba ninyi ni watu wa Mungu waliojaaliwa kabla ya enzi, na Shetani hawezi kukuchukua. Kwa hivyo, nyote mliomba, “Mungu! Niko tayari kuwa mmoja wa watu Wako, kwa sababu tumejaaliwa na Wewe kabla ya enzi, kwa sababu umetupa haya. Tuko tayari kuchukua nafasi hii na kukuridhisha.” Ulipomwomba kwa namna hiyo, Roho Mtakatifu angekusisimua—huo ndio mwelekeo wa kazi ya Roho Mtakatifu. Katika kipindi hiki cha muda ni kuomba na kufanya mazoezi ya kutuliza moyo wako mbele ya Mungu ili uweze kufuatilia maisha na kufuatilia kuingia katika mafunzo ya ufalme. Hii ndiyo hatua ya kwanza. Kwa sasa, kazi ya Mungu ni kuwa kila mtu aingie kwenye njia sahihi, awe na maisha ya kawaida ya kiroho na uzoefu wa kweli, aongozwe na Roho Mtakatifu, na kwa msingi wa msingi huu, kukubali kile kilichowekwa na Mungu. Kusudi la kuingilia katika mafunzo ya ufalme ni kuruhusu kila neno lenu, kila tendo, kila mwendo na kila mawazo na wazo la kuingilia katika maneno ya Mungu, kuwawezesha kuguswa na Mungu mara nyingi zaidi na kukuza upendo kwa Mungu na kukuza mzigo mzito zaidi kwa ajili ya mapenzi ya Mungu, ili kila mtu awe kwenye njia ya kufanywa mtimilifu na Mungu, na kila mtu awe kwenye njia sahihi. Mara unapokuwa kwenye njia ya kufanywa mtimilifu na Mungu, basi uko kwenye njia sahihi. Wakati ambapo mawazo yako na dhana zako pamoja na malengo yako mabaya yanaweza kurekebishwa na unaweza kugeuka kutoka katika kuzingatia mwili wako hadi kuzingatia mapenzi ya Mungu, na wakati ambapo malengo mabaya yanajitokeza na unaweza kutosumbuliwa nayo na kutenda kwa mujibu wa mapenzi ya Mungu—ikiwa unaweza kufikia mageuzo hayo, basi uko kwenye njia sahihi ya uzoefu wa maisha. Utendaji wako wa sala unapokuwa kwenye njia sahihi, hapo ndipo utakapoongozwa na Roho Mtakatifu katika sala zako. Kila wakati unapoomba, utaguswa hisia na Roho Mtakatifu; kila wakati utakapoomba, utakuwa na uwezo wa kutuliza moyo wako mbele ya Mungu. Kila wakati ambapo unakula na kunywa kifungu cha neno la Mungu, ikiwa unaweza kuelewa kazi ambayo anafanya sasa, na unaweza kujua jinsi ya kuomba, jinsi ya kushirikiana, na jinsi ya kuingia ndani, huku tu ndiko kufikia matokeo kutokana na kula na kunywa maneno ya Mungu. Unapoweza kupata njia ya kuingia kutoka kwa maneno ya Mungu, na unaweza kuelewa mienendo ya sasa ya kazi ya Mungu na mwenendo wa kazi ya Roho Mtakatifu kwa maneno Yake, hii inaonyesha kwamba wewe u kwenye njia sahihi. Ikiwa hujafahamu hoja muhimu unapokula na kunywa maneno ya Mungu, ikiwa huwezi kupata njia ya kutenda baada ya kula na kunywa maneno ya Mungu, inaonyesha kuwa bado hujui jinsi ya kula na kunywa maneno Yake na kwamba wewe hujapata njia au kanuni ya kula na kunywa maneno Yake. Ikiwa hamjaelewa kazi iliyofanywa na Mungu kwa sasa, hutaweza kukubali Agizo la Mungu. Kazi ambayo sasa inafanywa na Mungu ni ile wanapaswa kuingia ndani na kuwa na ujuzi kuhusu kwa sasa. Je, mnaelewa mambo haya?

Ukila na kunywa maneno ya Mungu kwa njia inayofaa, maisha yako ya kiroho yanakuwa ya kawaida, na bila kujali ni majaribu gani unayoweza kukabili, ni hali gani unazoweza kukumbana nazo, ni magonjwa gani ya kimwili unayoweza kuvumilia, ni mafarakano gani kutoka kwa ndugu au ni shida zipi za kifamilia unazoweza kupitia, unaweza kula na kunywa maneno ya Mungu kwa kawaida, kuomba kawaida, na kuendelea na maisha yako ya kanisa kawaida; ikiwa unaweza kutimiza haya yote, itaonyesha kuwa uko kwenye njia sahihi. Watu wengine ni dhaifu sana na hawana uvumilivu. Wanapokutana na kizuizi kidogo, wao hunung’unika na kuwa hasi. Ufuatiliaji wa ukweli unahitaji uvumilivu na uamuzi. Ikiwa huwezi kuyakidhi mapenzi ya Mungu wakati huu, lazima uweze kujidharau, kwa kimya kuwa na uamuzi ndani ya moyo wako kwamba utayaridhisha mapenzi ya Mungu wakati mwingine ujao. Ikiwa wakati huu hukuwa mzingatifu wa mzigo wa Mungu, unapaswa kuwa na azimio la kuasi dhidi ya mwili wakati ambapo unakabiliwa na kile kikwazo sawa katika siku zijazo, na kukusudia kuyaridhisha mapenzi ya Mungu. Hivi ndivyo unavyokuwa wa kustahili sifa. Watu wengine hata hawajui kama mawazo yao na dhana zao ni sawa—watu kama hao ni wapumbavu! Ikiwa ungependa kuuhini moyo wako na kuasi dhidi ya mwili, lazima kwanza ujue kama malengo yako ni sahihi, na hapo tu ndipo utaweza kuuhini moyo wako. Ikiwa hujui ikiwa nia yako ni sawa, unaweza kuuhini moyo wako na kuasi dhidi ya mwili? Hata ukiasi, unafanya hivyo kwa njia ya kuchanganyikiwa. Unapaswa kujua jinsi ya kuasi dhidi ya malengo yako potovu; hii ndiyo maana ya kuasi dhidi ya mwili. Unapojua kwamba malengo yako, mawazo yako na dhana zako si sahihi, unapaswa kukimbilia kurudi nyuma na kutembea kwenye njia sahihi. Tatua tatizo hili kwanza na ujifunze kufikia uingiaji kwa namna hii, kwa sababu unajua bora zaidi kama nia yako ni sawa au la. Wakati malengo mabaya yanarekebishwa na ni kwa ajili ya Mungu, basi umefikia lengo la kuuhini moyo wako.

Cha muhimu kwenu sasa ni kuwa na maarifa ya Mungu, kuwa na maarifa ya kazi ya Mungu, na lazima ujue jinsi Roho Mtakatifu anavyofanya kazi Yake kwa mwanadamu; huu ndio ufunguo wa kuingia kwenye njia sahihi. Itakuwa rahisi kwako kuingia kwenye njia sahihi baada ya kufahamu ufunguo huu. Unamwamini Mungu na kumjua Mungu, ambayo inaonyesha kwamba imani yako kwake ni ya kweli. Ikiwa utaendelea kupata uzoefu mpaka mwisho lakini bado huna uwezo wa kumjua Mungu, basi wewe hakika ni mtu anayempinga Mungu. Wale ambao huamini tu katika Yesu Kristo lakini hawaamini katika Mungu mwenye mwili wa leo wote wamehukumiwa. Wote ni Mafarisayo wa wakati wa sasa, kwa kuwa hawamtambui Mungu wa leo; wote wanampinga Mungu. Bila kujali imani yao katika Yesu ni ya kujitolea kiasi gani, itakuwa bure; hawatapata sifa ya Mungu. Wote wanaosema kuwa wanaamini katika Mungu ilhali hawana maarifa ya kweli ya Mungu katika mioyo yao ni wanafiki!

Ili kutafuta kufanywa mtimilifu na Mungu, mtu lazima kwanza aelewe maana ya kufanywa mtimilifu na Yeye, ni hali gani ambazo mtu anapaswa kumiliki ili kufanywa mtimilifu, na kisha kutafuta njia ya kutenda mara mtu ameelewa mambo kama hayo. Mtu lazima awe na ubora fulani wa tabia ili afanywe mtimilifu na Mungu. Wengi wenu hawana ubora muhimu wa tabia, ambao unahitaji wewe kulipa gharama fulani na jitihada zako za nafsi. Kadiri ubora wako wa tabia unavyozidi kuwa wa chini, ndivyo lazima utie juhudi zaidi za binafsi. Kadiri ufahamu wako wa maneno ya Mungu ulivyo mkuu na kadiri unavyoyatia kwenye matendo, ndivyo unavyoweza kuingia kwenye njia ya kufanywa mtimilifu na Mungu haraka. Kupitia katika maombi, unaweza pia kufanywa mtimilifu katika maombi; pia unaweza kufanywa mtimilifu kwa kula na kunywa maneno ya Mungu, kuelewa kiini cha maneno hayo, na kuishi kwa kudhihirisha ukweli wa maneno ya Mungu, unaweza kufanywa kuwa mtimilifu. Kupitia uzoefu wa maneno ya Mungu kila siku, unapaswa kujua kile unachokosa ndani yako, na, zaidi ya hayo, unapaswa kujua dosari yako kubwa na upungufu wako, na umwombe na kumsihi Mungu. Kwa kufanya hivyo, utafanywa mtimilifu polepole. Njia za kufanywa mtimilifu: kuomba, kula na kunywa maneno ya Mungu, kuelewa kiini cha maneno ya Mungu, kuingia katika uzoefu wa maneno ya Mungu, kuja kujua kinachokosa ndani yako, kuitii kazi ya Mungu, kuzingatia mzigo wa Mungu na kuunyima mwili kwa kupitia upendo wako kwa Mungu, na kuwa na ushirika wa mara kwa mara na ndugu, ambayo yanaboresha uzoefu wako. Iwe ni maisha ya jumuiya au maisha yako binafsi, na iwe ni makusanyiko makubwa au madogo, yote yanaweza kukuwezesha kupata uzoefu na kupata mafunzo ili moyo wako uwe na utulivu mbele ya Mungu na kurudi kwa Mungu. Haya yote ni mchakato wa kufanywa mtimilifu. Kuyapitia maneno ya Mungu ambayo yamesemwa kunamaanisha kuwa na uwezo wa kwa kweli kuyaonja maneno ya Mungu na kuyaruhusu yaweze kuishi kwa kudhihirishwa ndani yako ili uwe na imani kubwa na upendo kwa Mungu. Kupitia njia hii, utaondoa tabia potovu ya kishetani polepole, utaachana na motisha isiyofaa polepole, na kuishi kwa kudhihirisha mfano wa mtu wa kawaida. Kadiri upendo kwa Mungu ndani yako unavyozidi kuwa mkuu—yaani, kadiri unavyozidi kufanywa mtimilifu na Mungu mara nyingi—ndivyo unayopotoshwa na Shetani kwa kiasi kidogo. Kupitia uzoefu wako wa vitendo, utaingia kwenye njia ya kufanywa mtimilifu polepole. Hivyo, ikiwa unataka kufanywa mtimilifu, kuzingatia mapenzi ya Mungu na kuyapitia maneno ya Mungu hasa ni muhimu sana.

Iliyotangulia: Kuhusu Kuutuliza Moyo Wako Mbele ya Mungu

Inayofuata: Mungu Anawakamilisha Wale Wanaoupendeza Moyo Wake

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp