Ni kwa Kupitia Usafishaji tu Ndiyo Mwanadamu Anaweza Kuwa na Upendo wa Kweli

Nyote mko katikati ya majaribu na usafishaji. Mnapaswa kumpendaje Mungu wakati wa usafishaji? Baada ya kupitia usafishaji, watu wanaweza kumtolea Mungu sifa ya kweli, na katika usafishaji, wanaweza kuona kwamba wamepungukiwa sana. Kadiri usafishaji wako ulivyo mkubwa, ndivyo unaweza zaidi kukana mwili; kadiri usafishaji wao ulivyo mkubwa, ndivyo zaidi ulivyo upendo wa watu kwa Mungu, Hili ndilo mnapaswa kuelewa. Je, kwa nini ni lazima watu wasafishwe? Linalenga kutimiza matokeo gani? Je, umuhimu wa kazi ya Mungu ya usafishaji kwa mwanadamu ni gani? Ukimtafuta Mungu kwa kweli, basi baada ya kupitia usafishaji Wake hadi kiwango fulani utahisi kwamba ni mzuri sana, na ni wa umuhimu mkubwa kabisa. Je, mwanadamu anapaswa kumpenda Mungu jinsi gani wakati wa usafishaji? Kwa kutumia azimio la kumpenda Mungu kukubali usafishaji Wake: Wakati wa usafishaji, unateseka ndani, kana kwamba kisu kinasokotwa moyoni mwako, ilhali uko tayari kumridhisha Mungu kwa kutumia moyo wako, ambao unampenda, na hauko tayari kuutunza mwili. Hii ndiyo maana ya kutenda upendo wa Mungu. Unaumia ndani, na mateso yako yamefikia kiwango fulani, lakini bado uko tayari kuja mbele ya Mungu na kuomba ukisema: “Ee Mungu! Siwezi kukuacha. Ingawa kuna giza ndani yangu, ningependa kukuridhisha; Unaujua moyo wangu, na ningependa kwamba Uwekeze zaidi ya upendo Wako ndani yangu.” Huu ndio utendaji wakati wa usafishaji. Ukitumia upendo wa Mungu kama msingi, usafishaji unaweza kukuleta karibu zaidi na Mungu na kukufanya mwandani zaidi wa Mungu. Kwa kuwa unamwamini Mungu, ni lazima uukabidhi moyo wako mbele ya Mungu. Ukiutoa moyo wako na kuuweka mbele ya Mungu, basi wakati wa usafishaji, haitawezekana wewe kumkana Mungu, au kumwacha Mungu. Kwa njia hii, uhusiano wako na Mungu utakuwa wa karibu hata zaidi, na wa kawaida hata zaidi, na mawasiliano yako na Mungu yatakuwa ya mara kwa mara zaidi. Ikiwa wewe daima hutenda kwa jinsi hii, basi utashinda wakati zaidi katika mwanga wa Mungu, na wakati zaidi chini ya mwongozo wa maneno Yake, kutakuwa pia na mabadiliko zaidi na zaidi katika tabia yako, na ufahamu wako utaongezeka kila siku. Siku itakapokuja na majaribu ya Mungu yakufike kwa ghafla, hutaweza tu kusimama kando ya Mungu, bali pia utaweza kuwa na ushuhuda kwa Mungu. Wakati huo, utakuwa kama Ayubu, na Petro. Baada ya kuwa na ushuhuda kwa Mungu, utampenda kwa kweli, na utamtolea maisha yako kwa furaha; utakuwa shahidi wa Mungu, na yule ambaye ni mpendwa wa Mungu. Upendo ambao umepitia usafishaji ni wa nguvu, na sio dhaifu. Haijalishi ni lini au vipi Mungu anakufanya upatwe na majaribu Yake, unaweza kutojali ikiwa unaishi au unaangamia, kuachana na kila kitu kwa furaha kwa ajili ya Mungu, na kuvumilia chochote kwa furaha kwa ajili ya Mungu—na hivyo upendo wako utakuwa safi, na imani yako halisi. Ni hapo tu ndipo utakuwa mtu anayependwa na Mungu kwa kweli, na ambaye amefanywa kamili na Mungu kwa kweli.

Watu wakijipata chini ya ushawishi wa Shetani, basi hawana upendo kwa Mungu ndani yao, na maono, upendo na azimio yao ya awali yamepotea. Watu walikuwa wakihisi kwamba walifaa kuteseka kwa ajili ya Mungu, lakini leo wanafikiri kwamba ni aibu na hawakosi malalamiko. Hii ni kazi ya Shetani; inaonyesha kwamba mwanadamu amemilikiwa na Shetani. Ukikabiliwa na hali hii ni sharti uombe, na uibadilishe haraka uwezavyo—hii itakulinda dhidi ya mashambulizi ya Shetani. Ni wakati wa usafishaji mkali ambapo mwanadamu anaweza kujipata chini ya ushawishi wa Shetani kwa urahisi zaidi—kwa hivyo ni jinsi gani unapaswa kumpenda Mungu wakati wa usafishaji kama huu? Unapaswa kuyaita mapenzi yako, kuuweka moyo wako mbele ya Mungu na kutenga muda wako wa mwisho Kwake. Haijalishi jinsi gani Mungu hukusafisha, unafaa kuwa na uwezo wa kutia ukweli katika vitendo kutimiza mapenzi ya Mungu, na unafaa kujitolea kumtafuta Mungu na kutafuta mawasiliano. Nyakati kama hizi, zaidi unavyokaa tu, ndivyo utakuwa mtu hasi zaidi, na ndivyo itakuwa rahisi zaidi kwako kurudi nyuma. Wakati ambapo inakulazimu kutenda kazi yako, ingawa huitendi vyema, unafanya kila unachoweza, na unaifanya kwa kutumia tu upendo wako wa Mungu; bila kujali kile ambacho wengine husema—ikiwa wanasema umetenda vyema, au kwamba umetenda vibaya—motisha zako ni sahihi, na wewe sio wa kujidai, kwani unatenda kwa niaba ya Mungu. Wengine wanapokuelewa vibaya, unaweza kumwomba Mungu na kusema: “Ee Mungu! Siombi kwamba wengine wanivumilie au kunitendea vyema, wala kwamba wanielewe au kunikubali. Naomba tu kwamba niweze kukupenda moyoni mwangu, kwamba niwe na utulivu moyoni mwangu, na kwamba dhamiri yangu ni safi. Siombi kwamba wengine wanisifu, au kuniheshimu, ninatafuta tu kukuridhisha kutoka moyoni mwangu, ninatenda wajibu wangu kwa kufanya kila ninachoweza, na ingawa mimi ni mpumbavu na mjinga, na mwenye ubora wa tabia duni, na kipofu, najua kwamba Unapendeza, na niko tayari kukutolea kila ninacho.” Punde tu unapoomba kwa jinsi hii, upendo wako kwa Mungu huibuka, na unahisi utulivu zaidi moyoni mwako. Hili ndilo linalomaanishwa na kutenda upendo wa Mungu. Unavyopata uzoefu, utashindwa mara mbili na kufaulu mara moja, au pia ushindwe mara tano na kufaulu mara mbili, na unavyopata uzoefu kwa jinsi hii, ni katikati ya kushindwa tu ndipo utaweza kuona uzuri wa Mungu na kugundua kinachokosa ndani yako. Unapopitia hali kama hizi tena, unafaa kujitahadharisha, kutuliza mwendo wako, na kuomba mara nyingi zaidi. Polepole utakuza uwezo wa kushinda katika hali kama hizi. Hilo linapofanyika, maombi yako yamekuwa yenye matokeo yanayotarajiwa. Unapoona umefanikiwa wakati huu, utafurahishwa ndani yako, na unapoomba utaweza kumhisi Mungu, na kuhisi kwamba uwepo wa Roho Mtakatifu haujakutoka—na ni hapo tu ndipo utajua jinsi Mungu hufanya kazi ndani yako. Kutenda kwa njia hii kutakupa njia inayoelekea katika uzoefu. Usipoutia ukweli katika vitendo, basi utakuwa bila uwepo wa Roho Mtakatifu ndani yako. Lakini ukiutia ukweli katika vitendo unapokumbana na mambo jinsi yalivyo, basi, ingawa unaumia ndani, Roho Mtakatifu atakuwa nawe baadaye, utaweza kuhisi uwepo wa Mungu unapoomba, utakuwa na nguvu ya kutenda maneno ya Mungu, na wakati wa mawasiliano na ndugu zako, hakutakuwa na chochote kinachosumbua dhamiri yako, na utahisi amani, na kwa jinsi hii, utaweza kufunua yale ambayo umefanya. Bila kujali yale ambayo wengine husema, utaweza kuwa na uhusiano wa kawaida na Mungu, hutazuiliwa na wengine, hutashindwa na lolote—na katika hili, utaonyesha kwamba kutenda kwako maneno ya Mungu kumekuwa kwa matokeo yanayotarajiwa.

Kadiri usafishaji wa Mungu ulivyo mkubwa, ndivyo mioyo ya watu inaweza kumpenda Mungu zaidi. Mateso ndani ya mioyo yao ni ya manufaa kwa maisha yao, wanaweza zaidi kuwa na amani mbele ya Mungu, uhusiano wao na Mungu ni wa karibu zaidi, na wanaweza kuona vizuri zaidi upendo wa juu kabisa wa Mungu na wokovu Wake wa juu kabisa. Petro alipitia usafishaji mamia ya mara, na Ayubu alipitia majaribio kadhaa. Ikiwa mngependa kufanywa kamili na Mungu, nyinyi pia sharti mpitie usafishaji mamia ya mara; ni ikiwa tu mtapitia mchakato huu, na mtegemee hatua hii, ndiyo mnaweza kuridhisha mapenzi ya Mungu, na kufanywa kamili na Mungu. Usafishaji ndio njia bora zaidi ambayo Mungu hutumia kuwafanya watu kamili; usafishaji na majaribio makali pekee ndiyo yanaweza kusababisha kuonekana upendo wa kweli kwa Mungu ndani ya mioyo ya watu. Bila taabu, watu hukosa upendo wa kweli kwa Mungu; ikiwa hawajaribiwi ndani, na hawapitii usafishaji kwa kweli, basi mioyo yao daima itakuwa ikielea kwa nje. Baada ya kusafishwa hadi kiwango fulani, utayaona mapungufu na matatizo yako mwenyewe, utaona kiasi ambacho unakosa na kwamba huwezi kuzishinda zile shida nyingi unazokabiliwa nazo, na utaona jinsi kutotii kwako kulivyo kukubwa. Ni katika majaribu pekee ndipo watu wataweza kujua kwa kweli hali zao halisi, na majaribu huwafanya watu waweze kufanywa kamili vyema.

Katika maisha yake, Petro alipitia usafishaji mamia ya mara na alipitia majaribu mengi ya uchungu. Usafishaji huu ukawa msingi wa upendo wake mkubwa kabisa kwa Mungu na ukawa uzoefu muhimu zaidi katika maisha yake yote. Kwamba aliweza kuwa na upendo mkubwa kabisa wa Mungu ilikuwa, kwa namna moja, kwa sababu ya uamuzi wake kumpenda Mungu; la muhimu zaidi, hata hivyo, ilikuwa kwa sababu ya usafishaji na mateso aliyopitia. Mateso haya yakawa mwongozo wake katika njia ya kumpenda Mungu, na yakawa jambo lililokumbukwa zaidi kwake. Ikiwa watu hawapitii uchungu wa usafishaji wanapompenda Mungu, basi upendo wao umejaa uchafu na mapendeleo yao wenyewe; upendo kama huu umejaa mawazo ya Shetani, na hauwezi hata kabisa kuridhisha mapenzi ya Mungu. Kuwa na azimio la kumpenda Mungu sio sawa na kumpenda Mungu kwa kweli. Hata ingawa yote wanayofikiria mioyoni mwao ni kwa ajili ya kumpenda Mungu, na kumridhisha Mungu, kana kwamba fikira zao hazina mawazo yoyote ya kibinadamu, kana kwamba zote ni kwa ajili ya Mungu, fikira zao zinapoletwa mbele ya Mungu, fikira kama hizi hazisifiwi wala kubarikiwa na Mungu. Hata wakati watu wameelewa kikamilifu ukweli wote—wakati wamekuja kuujua wote—hili haliwezi kusemwa kuwa ishara ya kumpenda Mungu, haiwezi kusemwa kwamba watu hawa hakika wanampenda Mungu. Licha ya kuelewa ukweli mwingi bila kupitia usafishaji, watu hawana uwezo wa kutia ukweli huu katika vitendo; ni wakati wa usafishaji tu ndipo watu wanaweza kuelewa maana halisi ya ukweli huu, hapo tu ndipo watu wanaweza kufahamu kwa kweli maana yao ya ndani. Wakati huo, wanapojaribu tena, wanaweza kutia ukweli katika vitendo kwa njia ya kufaa, na kulingana na mapenzi ya Mungu; wakati huo, mawazo yao ya kibinadamu yanapunguzwa, upotovu wao wa kibinadamu unapunguzwa, na hisia zao za kibinadamu zinapunguzwa; ni wakati huo tu ndipo utendaji wao ni onyesho la ukweli la upendo wa Mungu. Athari ya ukweli wa upendo wa Mungu haitimizwi kupitia ufahamu wa kusemwa au kuwa tayari kiakili, wala haiwezi kutimizwa kwa kueleweka tu. Inahitaji kwamba watu walipe gharama, na kwamba wapitie uchungu mwingi wakati wa usafishaji, na hapo tu ndipo upendo wao utakuwa safi, na wa kuupendeza moyo wa Mungu. Katika hitaji Lake kwamba mwanadamu ampende, Mungu hadai kwamba mwanadamu ampende kwa kutumia mapenzi makali, au mapenzi yake mwenyewe; kwa uaminifu tu na utumiaji wa ukweli kumtumikia ndipo mwanadamu anaweza kumpenda kwa kweli. Lakini mwanadamu huishi katikati ya upotovu, na hivyo hana uwezo wa kutumia ukweli na uaminifu kumtumikia Mungu. Yeye ama ni mwenye kutekwa na hisia kali kumhusu Mungu au hana hisia zozote na hajali; anampenda Mungu kwa kiwango cha juu zaidi au anamchukia kabisa. Wale ambao huishi katikati ya upotovu daima huishi katikati ya vipeo hivi viwili, daima wakiishi kwa kufuata mapenzi yao wenyewe lakini wakiamini kwamba wako sahihi. Ingawa Nimetaja hili mara kwa mara, watu hawana uwezo wa kulichukulia kwa uzito, hawawezi kuelewa kabisa umuhimu wake, na hivyo wanaishi katikati ya imani ya kujidanganya, katika madanganyo ya upendo kwa Mungu unaotegemea mapenzi yao wenyewe. Kotekote katika historia, kadiri mwanadamu ameendelea na enzi zimepita, mahitaji ya Mungu kwa mwanadamu yamekuwa ya juu zaidi, na Amezidi kudai kwamba mwanadamu awe kamili Kwake. Ilhali ufahamu wa mwanadamu kuhusu Mungu umekuwa usio yakini na wa dhahania zaidi na zaidi, na upendo wake wa Mungu kwa kufuatana umekuwa mchafu zaidi na zaidi. Hali ya mwanadamu na yote afanyayo yanazidi kubishana na mapenzi ya Mungu, kwa maana mwanadamu amepotoshwa kwa kina zaidi na Shetani. Hili linahitaji kwamba Mungu afanye kazi zaidi, na kazi kubwa zaidi, ya wokovu. Mwanadamu anazidi kulipisha kwa nguvu katika mahitaji yake kwa Mungu, na upendo wake wa Mungu unapunguka zaidi na zaidi. Watu wanaishi katika uasi, bila ukweli, na wanaishi maisha yasiyo na ubinadamu; hawana tu upendo hata kidogo kwa Mungu, lakini pia wamejaa tele uasi na upinzani. Ingawa wanafikiri kuwa tayari wana upendo mkubwa kabisa kwa Mungu, na hawawezi kuwa wa hisani zaidi Kwake, Mungu haamini hivyo. Ni dhahiri kabisa Kwake jinsi upendo wa mwanadamu Kwake umeoza, na Hawajawahi kubadilisha maoni Yake ya mwanadamu kwa sababu ya ushawishi wa mwanadamu, wala kuwahi kulipiza ukarimu wa mwanadamu kwa sababu ya kujitolea kwake. Tofauti na binadamu, Mungu anaweza kutofautisha: Anajua yule anayempenda kwa kweli na yule asiyempenda, na badala ya kujawa na ari na kupotea kwa sababu ya mvuto wa ghafla wa mwanadamu, Anamtendea mwanadamu kulingana na asili na tabia ya mwanadamu. Mungu, hata hivyo, ni Mungu, na Ana hadhi Yake na utambuzi Wake; mwanadamu, hata hivyo, ni mwanadamu na Mungu hatapumbazwa na upendo wa mwanadamu ambao unazozana na ukweli. Kinyume chake, Anachukulia yote ambayo mwanadamu hufanya kwa jinsi ifaayo.

Anapokabiliwa na hali ya mwanadamu na mtazamo wake kwa Mungu, Mungu amefanya kazi mpya, Akimruhusu mwanadamu kuwa na ufahamu Wake na utiifu Kwake, na upendo pia na ushahidi. Hivyo, mwanadamu lazima apitie usafishaji wa Mungu kwake, na pia hukumu, ushughulikiaji na upogoaji Wake kwake, ambazo pasi nazo mwanadamu hangewahi kumjua Mungu, na hangewahi kuwa na uwezo wa kumpenda kwa kweli na kuwa na ushuhuda Kwake. Usafishaji wa Mungu kwa mwanadamu sio tu kwa ajili ya athari inayoegemea upande mmoja, bali kwa ajili ya athari inayogusia pande nyingi. Ni kwa jinsi hii tu ndiyo Mungu hufanya kazi ya usafishaji kwa wale ambao wako tayari kutafuta ukweli, ili upendo na uamuzi wao ufanywe timilifu na Mungu. Kwa wale walio tayari kuutafuta ukweli na wanaomtamani Mungu, hakuna kilicho cha maana zaidi, au cha usaidizi zaidi, kuliko usafishaji kama huu. Tabia ya Mungu haijulikani wala kueleweka kwa urahisi sana na mwanadamu, kwani Mungu, hatimaye, ni Mungu. Mwishowe, haiwezekani kwa Mungu kuwa na tabia sawa na mwanadamu, na hivyo si rahisi kwa mwanadamu kujua tabia Yake. Ukweli haumilikiwi kwa asili na mwanadamu, na hauleweki kwa urahisi na wale ambao wamepotoshwa na Shetani; mwanadamu hana ukweli na hana azimio la kutia ukweli katika vitendo, na asipoteseka, na asisafishwe au kuhukumiwa, basi uamuzi wake hautawahi kufanywa timilifu. Kwa watu wote, usafishaji ni wa kutesa sana na ni mgumu sana kukubali—ilhali ni katika usafishaji ndipo Mungu huweka wazi tabia Yake ya haki kwa mwanadamu, na Huweka hadharani mahitaji Yake kwa mwanadamu, na Hutoa nuru zaidi, na upogoaji na ushughulikiaji halisi zaidi; kwa kulinganisha mambo ya hakika na ukweli, Yeye humpa mwanadamu ufahamu mkubwa zaidi kujihusu na ukweli, na Humpa mwanadamu ufahamu mkubwa zaidi wa mapenzi ya Mungu, hivyo kumruhusu mwanadamu kuwa na upendo wa kweli zaidi na safi zaidi wa Mungu. Haya ndiyo malengo ya Mungu katika kutekeleza usafishaji. Kazi yote Afanyayo Mungu kwa mwanadamu ina malengo yake na maana yake; Mungu hafanyi kazi isiyo na maana, wala Hafanyi kazi isiyo na manufaa kwa mwanadamu. Usafishaji haumaanishi kuondoa watu kutoka mbele ya Mungu, wala haumaanishi kuwaangamiza katika kuzimu. Unamaanisha kubadilisha tabia ya mwanadamu wakati wa usafishaji, kubadilisha motisha zake, mitazamo yake ya kale, kubadilisha upendo wake kwa Mungu, na kubadilisha maisha yake yote. Usafishaji ni jaribio la kweli la mwanadamu, na aina ya mafunzo halisi na ni wakati wa usafishaji tu ndipo upendo wake unaweza kutimiza wajibu wake wa asili.

Iliyotangulia: Namna Petro Alivyopata Kumjua Yesu

Inayofuata: Wanaompenda Mungu Wataishi Milele Katika Mwangaza Wake

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp