Wale Wanaopaswa Kukamilishwa Lazima Wapitie Usafishaji

Kama unamwamini Mungu, basi ni lazima umtii Mungu, uweke ukweli katika vitendo na utimize wajibu wako wote. Zaidi ya hayo, ni lazima uelewe mambo unayopaswa kupitia. Ikiwa unapitia tu kushughulikiwa, kufundishwa nidhamu na kuhukumiwa, kama wewe unaweza tu kumfurahia Mungu lakini usalie usiyeweza kuhisi wakati Mungu anakufundisha nidhamu au kukushughulikia—hili halikubaliki. Labda katika wakati huu wa usafishaji, unaweza kushikilia msimamo wako, bali hili bado halitoshi; ni lazima bado uendelee kusonga mbele. Funzo la kumpenda Mungu halikomi kamwe na halina mwisho. Watu huona kumwamini Mungu kama jambo lililo rahisi mno, lakini mara tu wanapopata uzoefu kiasi wa vitendo, wao kisha hutambua kwamba imani katika Mungu si rahisi kama watu wanavyofikiria. Wakati Mungu anafanya kazi ili kumsafisha mwanadamu, mwanadamu huteseka. Kadiri usafishaji wa mtu ulivyo mkubwa, ndivyo upendo wake kwa Mungu utakavyokuwa mkubwa zaidi na ndivyo nguvu za Mungu zitakavyofichuliwa zaidi kwake. Kinyume chake, kadiri mtu apokeavyo usafishaji mdogo zaidi, ndivyo upendo wake kwa Mungu utakavyokuwa kwa kiwango kidogo zaidi, na ndivyo nguvu za Mungu zitakavyofichuliwa kwake kwa kiwango kidogo zaidi. Kadiri usafishaji na uchungu wa mtu kama huyo ulivyo mkubwa na kadiri anavyopitia mateso mengi zaidi, ndivyo upendo wake kwa Mungu utakavyokuwa, ndivyo imani yake kwa Mungu itakavyokuwa ya kweli zaidi, na ndivyo maarifa yake ya Mungu yatakavyokuwa ya kina zaidi. Katika matukio unayopitia, utawaona watu wanaoteseka sana wanapokuwa wakisafishwa, wanaoshughulikiwa na kufundishwa nidhamu sana, na utaona kwamba ni watu hao ndio walio na upendo mkubwa kwa Mungu na maarifa ya kina na elekevu ya Mungu. Wale ambao hawajapitia kushughulikiwa wanayo maarifa ya juu juu tu, na wao wanaweza tu kusema: “Mungu ni mzuri sana, Yeye huwapa watu neema ili waweze kumfurahia Yeye.” Kama watu wamepitia kushughulikiwa na kufundishwa nidhamu, basi hao wanaweza kuzungumza kuhusu maarifa ya kweli ya Mungu. Hivyo kazi ya Mungu katika mwanadamu ilivyo ya ajabu zaidi, ndivyo ilivyo ya thamani zaidi na ni muhimu zaidi. Kadiri inavyokosa kupenyeza kwako zaidi na kadiri isivyolingana na mawazo yako, ndivyo kazi ya Mungu inavyoweza kukushinda, kukupata, na kukufanya mkamilifu. Umuhimu wa kazi ya Mungu ni mkubwa ulioje! Kama Mungu hangemsafisha mwanadamu kwa njia hii, kama Hangefanya kazi kulingana na njia hii, basi kazi Yake haingekuwa na ufanisi na ingekuwa isiyo na maana. Ilisemwa hapo awali kwamba Mungu angelichagua na kulipata kundi hili na kuwakamilisha katika siku za mwisho; hili lina umuhimu mkubwa sana. Kadiri kazi Anayofanya ndani yenu ilivyo kuu, ndivyo upendo wenu kwa Mungu ulivyo mkubwa na safi. Kadiri kazi ya Mungu ilivyo kuu zaidi, ndivyo mwanadamu anavyoweza kuelewa kitu kuhusu hekima Yake na ndivyo maarifa ya mwanadamu Kwake yalivyo ya kina zaidi. Katika siku za mwisho, miaka elfu sita ya mpango wa Mungu wa usimamizi itafika kikomo. Je, kweli inaweza kufika mwisho kwa urahisi? Baada ya Yeye kuwashinda wanadamu, je, kazi Yake itakuwa imefika mwisho? Je, inaweza kuwa rahisi vile? Watu kweli hufikiria kwamba ni rahisi hivi, lakini kile ambacho Mungu hufanya si rahisi vile. Bila kujali ni sehemu gani ya kazi ya Mungu unayojali kutaja, yote ni isiyoeleweka kwa mwanadamu. Ikiwa ungeweza kuifahamu, basi kazi ya Mungu ingekuwa isiyo na maana au thamani. Kazi inayofanywa na Mungu ni isiyoeleweka; ni kinyume kabisa na mawazo yako, na kadiri isivyopatana na mawazo yako, ndivyo inavyoonyesha zaidi kwamba kazi ya Mungu ni ya maana; kama ingekuwa inalingana na mawazo yako, basi ingekuwa isiyo maana. Leo, unahisi kwamba kazi ya Mungu ni ya ajabu sana, na kadiri unavyohisi kuwa ni ya ajabu, ndivyo unahisi kwamba Mungu ni asiyeeleweka, na kuona jinsi matendo ya Mungu yalivyo makubwa. Kama Angefanya tu kazi fulani ya juu juu ya kutimiza wajibu kumshinda mwanadamu na Asifanye chochote zaidi baadaye, basi mwanadamu hangeweza kuona umuhimu wa kazi ya Mungu. Ingawa unapokea usafishaji kidogo sasa, ni wa faida kubwa sana kwa ukuaji wako katika maisha; hivyo ni jambo linalohitajika sana wewe kupitia ugumu wa aina hiyo. Leo, unapokea usafishaji kidogo, lakini baadaye utaweza kwa kweli kuyaona matendo ya Mungu, na hatimaye utasema: “Matendo ya Mungu ni ya ajabu mno!” Haya ndiyo yatakuwa maneno moyoni mwako. Baada ya kupitia usafishaji wa Mungu kwa muda (majaribu ya watendaji huduma na wakati wa kuadibu), baadhi ya watu hatimaye walisema: “Kuamini katika Mungu ni jambo gumu kweli!” Ukweli kwamba wao hutumia maneno “jambo gumu kweli”, unaonyesha kwamba matendo ya Mungu ni yasiyoeleweka, kuwa kazi ya Mungu ni yenye umuhimu na thamani kubwa, na kwamba kazi Yake ni yenye kustahili sana kuthaminiwa na mwanadamu. Ikiwa, baada ya Mimi kufanya kazi nyingi hivi, hukuwa na maarifa hata kidogo, basi kazi Yangu ingeweza kuwa na thamani bado? Itakufanya useme: “Huduma kwa Mungu ni ngumu kweli, matendo ya Mungu ni ya ajabu mno, na Mungu kweli ni mwenye hekima! Mungu ni mwenye kupendeza kweli!” Kama, baada ya kupitia kipindi cha uzoefu, una uwezo wa kusema maneno kama haya, basi hii inathibitisha kuwa umepata kazi ya Mungu ndani yako. Siku moja, ukiwa unaeneza injili ughaibuni na mtu akuulize: “Imani yako katika Mungu inaendeleaje?” Utaweza kusema: “Matendo ya Mungu ni ya ajabu kweli!” Mtu huyo atahisi kwamba maneno yako yanazungumza kuhusu matukio halisi uliyopitia. Huku kweli ni kutoa ushahidi. Utasema kuwa kazi ya Mungu imejaa hekima, na kazi Yake ndani yako imekushawishi kwa kweli na kuushinda moyo wako. Wewe daima utampenda kwa maana Yeye anastahili zaidi upendo wa wanadamu! Kama unaweza kuzungumza kwa vitu hivi, basi unaweza kuigusa mioyo ya watu. Haya yote ni kutoa ushahidi. Kama unaweza kuwa shahidi wa ajabu, kuwagusa watu hadi watoe machozi, hiyo inaonyesha kwamba kwa kweli wewe ni mmoja anayempenda Mungu, kwa sababu unaweza kushuhudia kuhusu kumpenda Mungu, na kupitia kwako, matendo ya Mungu yanaweza kushuhudiwa. Kupitia ushuhuda wako, wengine wanafanywa watafute kazi ya Mungu, wapitie kazi ya Mungu, na katika mazingira yoyote wanayopitia, wataweza kusimama imara. Hii pekee ndiyo njia ya kweli ya kuwa shahidi, na hili hasa ndilo linalohitajika kutoka kwako sasa. Unafaa kuona kwamba kazi ya Mungu ni muhimu sana na inastahili kuthaminiwa na watu, kwamba Mungu ni wa thamani mno na mwenye Mengi, Hawezi tu kusema, lakini pia Anaweza kutoa uamuzi juu ya watu, kusafisha mioyo yao, kuwaletea starehe, kuwapata, kuwashinda, na kuwakamilisha. Kutoka katika kupitia kwako utaona kwamba Mungu ni mwenye kupendwa sana. Hivyo unampenda Mungu kiasi gani sasa? Je, unaweza kweli kusema mambo haya kutoka moyoni mwako? Wakati unaweza kuonyesha maneno haya kutoka kwenye kina cha moyo wako, basi utaweza kuwa na ushuhuda. Mara tu uzoefu wako unapofikia kiwango hiki utakuwa na uwezo wa kuwa shahidi wa Mungu, na utakuwa umestahili. Kama huwezi kufika kiwango hiki katika uzoefu wako, basi wewe bado utakuwa mbali sana. Ni jambo la kawaida kwa watu kuonyesha udhaifu katika mchakato wa usafishaji, lakini baada ya usafishaji unapaswa kuweza kusema: “Mungu ni mwenye hekima sana katika kazi Yake!” Kama wewe kweli unaweza kufikia ufahamu wa vitendo wa maneno haya, basi kitakuwa kitu unachokithamini, na uzoefu wako utakuwa wa thamani.

Je, ni nini unachopaswa kufuatilia sasa? Iwapo unaweza kushuhudia kazi ya Mungu au la, iwapo unaweza kuwa ushuhuda na udhihirisho wa Mungu au la, na iwapo unastahili kutumiwa na Yeye au la—hivi ndivyo vitu unavyopaswa kutafuta. Ni kiasi gani cha kazi ambacho Mungu hakika amefanya kwako? Ni kiasi gani ambacho umeona, ni kiasi gani ambacho umegusa? Umepitia kiasi gani, na kuonja kiasi gani? Bila kujali iwapo Mungu amekujaribu, kukushughulikia, au kukuadhibu, matendo Yake na kazi Yake vimetekelezwa juu yako. Lakini kama muumini katika Mungu na kama mtu ambaye ana nia ya kufuatilia kukamilishwa na Yeye, je, unaweza kushuhudia kazi ya Mungu kwa msingi wa uzoefu wako wa vitendo? Je, Je, unaweza kuishi kwa kudhihirisha neno la Mungu kupitia kwa uzoefu wako wa vitendo? Je, unaweza kuwakimu wengine kupitia uzoefu wako mwenyewe wa vitendo, na kutumia maisha yako yote kushuhudia kazi ya Mungu? Ili kushuhudia kazi ya Mungu, lazima utegemee uzoefu na maarifa yako, na gharama ambayo umelipa. Unaweza kuyaridhisha mapenzi Yake kwa njia hii pekee. Je, wewe ni mtu ambaye hushuhudia kazi ya Mungu? Je, una matamanio haya? Kama unaweza kulishuhudia jina Lake, na hata zaidi, kazi Yake, na kama unaweza kuishi kwa kudhihirisha sura ambayo Yeye anataka kutoka kwa watu Wake, basi wewe ni shahidi wa Mungu. Je, unashuhudia kwa ajili ya Mungu vipi kwa hakika? Unafanya hivyo kwa kutafuta na kuwa na hamu sana ya kuishi kwa kulidhihirisha neno la Mungu na, kwa kuwa na shahidi kwa maneno yako, kuwaruhusu watu wajue kazi Yake na kuona matendo Yake. Kama kweli unatafuta yote haya, basi Mungu atakukamilisha. Ikiwa yote unayotafuta ni kukamilishwa na Mungu na kubarikiwa mwishoni kabisa, basi mtazamo wa imani yako katika Mungu si safi. Unapaswa kuwa ukifuatilia jinsi ya kuona matendo ya Mungu katika maisha ya kweli, jinsi ya kumridhisha Yeye Anapokufichulia mapenzi Yake, na kutafuta jinsi unavyopaswa kushuhudia maajabu na hekima Yake, na jinsi ya kushuhudia jinsi Anavyokufundisha nidhamu na kukushughulikia. Haya yote ni mambo unayopaswa kuwa ukiyatafakari sasa. Kama upendo wako kwa Mungu ni ili tu uweze kushiriki katika utukufu wa Mungu baada ya Yeye kukukamilisha, basi bado hautoshi na hauwezi kukidhi mahitaji ya Mungu. Unahitaji kuwa na uwezo wa kushuhudia kazi ya Mungu, kutosheleza mahitaji Yake, na kuwa na uzoefu wa kazi ambayo Amefanya kwa watu kwa njia ya utendaji. Iwe ni uchungu, majonzi, au huzuni, lazima upitie vitu hivi vyote katika kutenda kwako. Vitu hivi vinanuiwa kukukamilisha kama Yule anayemshuhudia Mungu. Ni nini hasa kinachokushurutisha sasa kuteseka na kutafuta kukamilishwa? Je, mateso yako ya sasa kweli ni kwa ajili ya kumpenda Mungu na kumshuhudia? Ama ni kwa ajili ya Baraka za mwili na matarajio na kudura yako ya baadaye? Dhamira zako zote, nia, na malengo unayofuatilia lazima yarekebishwe na hayawezi kuongozwa na mapenzi yako mwenyewe. Kama mtu mmoja anatafuta ukamilifu ili apokee baraka na kutawala mamlakani, wakati mtu mwingine anafuatilia ukamilifu ili amridhishe Mungu, awe na ushuhuda wa vitendo wa kazi ya Mungu, je, ni ipi kati ya njia hizi mbili za ufuatiliaji ndiyo ungechagua? Ikiwa utachagua ya kwanza, basi utakuwa mbali sana na viwango vya Mungu. Nilisema wakati mmoja kwamba matendo Yangu yatajulikana wazi katika ulimwengu wote na kwamba Ningetawala kama Mfalme katika ulimwengu. Kwa upande mwingine, kilichoaminiwa kwenu ni kuenda kushuhudia kazi ya Mungu, sio kuwa wafalme na kuonekana ulimwenguni wote. Hebu matendo ya Mungu yajazee ulimwengu na anga. Hebu kila mtu ayaone na ayakiri. Maneno haya yanasemwa kuhusiana na Mungu Mwenyewe, na kile ambacho wanadamu wanapaswa kufanya ni kutoa ushuhuda kwa ajili ya Mungu. Je, unajua kiasi gani kuhusu Mungu sasa? Je, unaweza kutoa ushuhuda kwa Mungu kiasi gani? Je, ni lengo gani la Mungu kumkamilisha mwanadamu? Mara baada ya kuelewa mapenzi ya Mungu, je, unapaswa kuonyeshaje kujali kuelekea mapenzi Yake? Kama uko tayari kukamilishwa na uko tayari kushuhudia kazi ya Mungu kupitia kile unachoishi kwa kudhihirisha, kama una hii nguvu ya msukumo, basi hakuna lililo gumu sana. Wanachohitaji watu sasa ni imani. Kama una hii nguvu ya msukumo, basi ni rahisi kuachilia chochote chenye uhasi, cha kukaa tu, uvivu na mawazo ya mwili, falsafa za kuishi, tabia ya uasi, hisia, na mengineyo.

Wakati wanapitia majaribu, ni kawaida kwa watu kuwa dhaifu, au kuwa na uhasi ndani yao, au kukosa uwazi juu ya mapenzi ya Mungu au njia yao ya kutenda. Lakini katika hali yoyote, lazima uwe na imani katika kazi ya Mungu, na usimkane Mungu, kama tu Ayubu. Ingawa Ayubu alikuwa dhaifu na aliilaani siku yake ya kuzaliwa, yeye hakukana kwamba vitu vyote katika maisha ya binadamu vilikuwa vimetolewa na Yehova, na kwamba Yehova pia Ndiye anayeyachukua vyote. Haijalishi jinsi alivyojaribiwa, alidumisha imani hii. Katia kupitia kwako, haijalishi ni usafishaji gani unaopitia katika maneno ya Mungu, kile Mungu anahitaji kutoka kwa wanadamu kwa ufupi ni imani yao na upendo wao Kwake. Anachokamilisha kwa kufanya kazi kwa njia hii ni imani, upendo na matarajio ya watu. Mungu hufanya kazi ya ukamilisho kwa watu, nao hawawezi kuiona, hawawezi kuihisi; katika hali kama hizi imani yako inahitajika. Imani ya watu inahitajika wakati ambao kitu hakiwezi kuonekana kwa macho tu, na imani yako inahitajika wakati huwezi kuziachilia dhana zako mwenyewe. Wakati ambapo huna uwazi kuhusu kazi ya Mungu, kinachohitajika kutoka kwako ni kuwa na imani uchukue msimamo imara na kuwa shahidi. Wakati Ayubu alifikia hatua hii, Mungu alimwonekania na kuzungumza naye. Yaani, ni kutoka ndani ya imani yako tu ndipo utaweza kumwona Mungu, na wakati una imani Mungu atakukamilisha. Bila imani, Hawezi kufanya hivyo. Mungu ataweka juu yako chochote ulicho na matumaini ya kupata. Kama huna imani, basi huwezi kukamilishwa na hutakuwa na uwezo wa kuona matendo ya Mungu, sembuse kudura Yake. Wakati una imani kwamba utaona matendo Yake katika uzoefu wako wa utendaji, basi Mungu atakuonekania, na Atakupa nuru na kuongoza kutoka ndani. Bila hiyo imani, Mungu hataweza kufanya hivyo. Kama umepoteza matumaini katika Mungu, utawezaje kupata uzoefu wa kazi Yake? Kwa hiyo, ni wakati tu una imani na huweki mashaka kumhusu Mungu, ni wakati una imani ya kweli Kwake tu bila kujali Anachokifanya ndipo Atakuangazia na kukupa nuru kupitia katika mapito yako, na ni hapo tu ndipo utaweza kuona matendo Yake. Mambo haya yote yanafanikishwa kupitia kwa imani. Imani huja kupitia tu usafishaji, na wakati hakuna usafishaji, imani haiwezi kukua. Je, neno hili “imani”, linarejelea nini? Imani ni kusadiki kwa kweli na moyo wa dhati ambao wanadamu wanapaswa kumiliki wakati wao hawawezi kuona au kugusa kitu, wakati kazi ya Mungu haiambatani na za binadamu, wakati inazidi uwezo wa binadamu. Hii ndiyo imani Ninayozungumzia. Watu wanahitaji imani katika nyakati za shida na usafishaji, na imani ni kitu kinachofuatwa na usafishaji; usafishaji na imani haviwezi kutenganishwa. Haijalishi jinsi Mungu anavyofanya kazi, na haijalishi mazingira uliyomo, unaweza kufuatilia maisha na kutafuta ukweli, na kutafuta maarifa ya kazi ya Mungu, na kuwa na ufahamu wa matendo Yake, na unaweza kutenda kulingana na ukweli. Kufanya hivi ndiko kuwa na imani ya kweli, na kufanya hivyo kunaonyesha kwamba hujapoteza imani katika Mungu. Unaweza tu kuwa na imani ya kweli katika Mungu ikiwa bado unaweza kuendelea kufuatilia ukweli kupitia ukiwa katika usafishaji, ikiwa unaweza kumpenda Mungu kwa kweli na huna na mashaka kumhusu Yeye, ikiwa bila kujali Anachokifanya bado unatenda ukweli kumridhisha Yeye, na ikiwa unaweza kutafuta kwa dhati mapenzi Yake na ujali mapenzi Yake. Zamani, wakati Mungu alisema kwamba ungetawala kama mfalme, ulimpenda, na wakati Alijionyesha hadharani kwako, ulimfuata. Lakini sasa Mungu amejificha, huwezi kumwona, na shida zimekujia—je, hapo unapoteza matumaini kwa Mungu? Hivyo, lazima ufuatilie uzima wakati wote na kutafuta kuyaridhisha mapenzi ya Mungu. Hii inaitwa imani ya kweli, na huu ndio aina ya upendo ulio wa kweli na mzuri zaidi.

Hapo zamani, watu wote walikuja mbele za Mungu kufanya maazimio yao na walisema: “Hata kama hakuna mtu mwingine anayempenda Mungu, ni lazima mimi nimpende.” Lakini sasa, usafishaji unakujia, na kwa sababu hili halilingani na fikira zako, hivyo unapoteza imani katika Mungu. Je, huu ni upendo wa kweli? Umesoma mara nyingi kuhusu matendo ya Ayubu—Je, umesahau kuyahusu? Upendo wa kweli unaweza tu kukua kutoka ndani ya imani. Unakuza upendo wa kweli kwa Mungu kupitia katika usafishaji unaopitia, na ni kupitia kwa imani yako ndiyo unaweza kuyadhukuru mapenzi ya Mungu katika matukio yako ya vitendo, na pia ni kupitia kwa imani yako ndiyo unautelekeza mwili wako mwenyewe na kufuatilia uzima; hili ndilo watu wanapaswa kufanya. Ukifanya hivi, basi utaweza kuona matendo ya Mungu, lakini ukikosa imani, basi hutaweza kuona matendo ya Mungu au kuipitia kazi Yake. Iwapo unataka kutumika na kukamilishwa na Mungu, ni lazima umiliki kila kitu: uwe tayari kuteseka, imani, uvumilivu, utiifu na uwezo wa kupitia kazi ya Mungu, kufahamu mapenzi Yake kujali huzuni Yake, na kadhalika. Kumkamilisha mtu si rahisi, na kila kisa cha usafishaji unachopitia kinahitaji imani na upendo wako. Kama unataka kukamilishwa na Mungu, haitoshi kukimbia tu mbele kwenye njia, wala haitoshi kujitumia tu kwa ajili ya Mungu. Ni lazima umiliki mambo mengi ili uweze kuwa mtu ambaye anakamilishwa na Mungu. Unapokabiliwa na mateso ni lazima uweze kuweka kando masilahi ya mwili na usifanye malalamiko dhidi ya Mungu. Wakati Mungu anajificha kutoka kwako, ni lazima uweze kuwa na imani ya kumfuata Yeye, kudumisha upendo wako wa awali bila kuuruhusu ufifie au kutoweka. Haijalishi anachofanya Mungu, ni lazima utii mpango Wake na uwe tayari kuulaani mwili wako mwenyewe badala ya kulalamika dhidi Yake. Wakati unakabiliwa na majaribu, lazima umridhishe Mungu, ingawa unaweza kulia kwa uchungu au uhisi kusita kuhusu kuacha kitu unachopenda. Huu tu ndio upendo wa kweli na imani. Haijalishi kimo chako halisi ni kipi, ni lazima kwanza umiliki nia ya kupitia ugumu na imani ya kweli, na ni pia lazima uwe na nia ya kuutelekeza mwili. Unapaswa kuwa tayari kuvumilia ugumu wa kibinafasi na kupata hasara kwa maslahi yako binafsi ili kuridhisha mapenzi ya Mungu. Lazima pia uwe na uwezo wa kuhusi majuto kujihusu moyoni mwako: Hapo zamani, hukuweza kumridhisha Mungu, na sasa unaweza kujuta mwenyewe. Ni lazima usipungukiwe katika yoyote ya hali hizi—Ni kupitia katika vitu hivi ndiyo Mungu atakukamilisha. Usipoweza kufikia viwango hivi, basi huwezi kukamilishwa.

Mtu anayemtumikia Mungu lazima asijue jinsi ya kuteseka kwa ajili Yake; zaidi ya hayo, anapaswa kuelewa kwamba kusudi la kuamini katika Mungu ni kwa ajili ya kufuatilia kumpenda Mungu. Mungu hukutumia si kwa sababu tu ya kukusafisha au kwa sababu ya kukufanya uteseke, lakini badala yake ni Yeye hukutumia ili uweze kujua matendo Yake, kujua umuhimu halisi wa maisha ya binadamu, na hasa, ili uweze kujua kwamba kumtumikia Mungu si kazi rahisi. Kupata uzoefu wa kazi ya Mungu hakuhusu kufurahia neema Yake, bali kuhusu kuteseka kwa sababu ya upendo wako Kwake. Kwa kuwa unafurahia neema ya Mungu, lazima pia ufurahie kuadibu Kwake; lazima upitie haya yote. Unaweza kupata uzoefu wa nuru ya Mungu ndani yako, na unaweza pia kupitia jinsi Anavyokushughulikia na Anavyokuhukumu. Kwa njia hii, uzoefu wako utakuwa mkamilifu. Mungu ametekeleza kazi Yake ya hukumu na kuadibu kwako. Neno la Mungu limekushughulikia, lakini si hilo yu; pia limekupa nuru, na kukuangazia. Wakati wewe ni hasi na dhaifu, Mungu ana wasiwasi kwa ajili yako. Hizi kazi zote ni za kukufahamisha kwamba kila kitu kuhusu mwanadamu kimo katika udhibiti wa Mungu. Unaweza kufikiri kwamba kuamini katika Mungu ni kuhusu mateso, au kumfanyia mambo ya kila aina; unaweza kufikiri kwamba sababu ya kumwamini Mungu ni ili mwili wako uwe na amani, au ili kwamba kila kitu maishani mwako kiende vizuri, au ili kwamba uweze kuwa na raha na utulivu katika kila kitu. Hata hivyo, hakuna kati ya haya ambayo watu wanapaswa kuhusisha na imani yao katika Mungu. Ukiamini kwa ajili ya sababu hizi, basi mtazamo wako si sahihi na haiwezekani kabisa wewe kukamilishwa. Matendo ya Mungu, tabia ya Mungu ya haki, hekima Yake, maneno Yake, na maajabu Yake na kutoeleweka kwa kina Kwake yote ni mambo ambayo watu wanapaswa kuelewa. Kuwa na ufahamu huu, unapaswa kuutumia kuondoa moyoni mwako madai, matumaini na fikiza za kibinafsi. Ni kwa kuondoa mambo haya tu ndiyo unaweza kukidhi masharti yanayotakiwa na Mungu, na ni kwa kufanua hivi tu ndiyo unaweza kuwa na uzima na kumridhisha Mungu. Kusudi la kumwamini Mungu ni ili kumridhisha na kuishi kwa kudhihirisha tabia ambayo Yeye anahitaji, ili matendo na utukufu Wake viweze kudhihirishwa kupitia kundi hili la watu wasiostahili. Huu ndio mtazamo sahihi wa kuamini katika Mungu, na hili pia ndilo lengo unalopaswa kutafuta. Unapaswa kuwa na mtazamo sahihi kuhusu kuamini katika Mungu na unapaswa kutafuta kupata maneno ya Mungu. Unahitaji kula na kunywa maneno ya Mungu na lazima uwe na uwezo wa kuishi kwa kudhihirisha ukweli, na hasa lazima uweze kuona matendo Yake ya vitendo, matendo Yake ya ajabu kotekote katika ulimwengu mzima, pamoja na kazi ya vitendo Yeye hufanya katika mwili. Kupitia katika uzoefu wao wa vitendo, watu wanaweza kufahamu ni jinsi gani hasa Mungu hufanya kazi Yake kwao na mapenzi Yake kwao ni yapi. Kusudi la haya yote ni ili kuondoa tabia potovu ya kishetani ya watu. Baada ya kuondoa uchafu na udhalimu wote ulio ndani mwako, na baada ya kuondoa nia zako mbaya, na baada ya kukuza imani ya kweli kwa Mungu—ni kwa kuwa na imani ya kweli tu ndiyo unaweza kumpenda Mungu kweli. Unaweza tu kweli kumpenda Mungu kwa msingi wa imani yako Kwake. Je, unaweza kufanikisha upendo wa kweli kwa Mungu bila kumwamini? Kwa kuwa unaamini katika Mungu, huwezi kukanganyika kuhusu jambo hilo. Baadhi ya watu hujawa na nguvu mara tu wanapoona kwamba imani katika Mungu itawaletea baraka, lakini kisha hupoteza nguvu zote mara tu wanapoona kwamba wanafaa kupitia kusafishwa. Je, huko ni kuamini katika Mungu? Mwishowe, lazima upate utiifu kamili na mzima mbele ya Mungu katika imani yako. Unaamini katika Mungu lakini bado una madai Kwake, una mawazo mengi ya kidini ambayo huwezi kuyapuuza, maslahi ya kibinafsi huwezi kuacha, na bado unatafuta baraka za mwili na unataka Mungu auokoe mwili wako, kuiokoa nafsi yako—hizi zote ni tabia za watu walio na mtazamo usio sahihi. Hata kama watu wenye imani za kidini wana imani katika Mungu, hawatafuti kubadilisha tabia zao na hawafuatilii maarifa ya Mungu, lakini badala yake wanatafuta tu masilahi ya miili yao. Wengi kati yenu wana imani ambazo ni za kikundi cha kusadiki kidini; hii siyo imani ya kweli katika Mungu. Kuamini katika Mungu, watu lazima wamiliki moyo ulio tayari kuteseka kwa ajili Yake na radhi ya kujitoa wenyewe. Watu wasipokidhi haya masharti mawili, imani yao katika Mungu haihesabiki, na hawataweza kufanikisha mabadiliko katika tabia yao. Ni watu tu wanaotafuta ukweli kwa kweli, wanaotafuta maarifa ya Mungu, na kufuatilia maisha ndio wale ambao kweli wanaamini katika Mungu.

Wakati majaribu yanakujia, utaitumiaje kazi ya Mungu kushughulikia majaribu hayo? Je, utakuwa hasi au utaelewa jaribu na usafishaji wa Mungu wa mwanadamu kutoka kwa kipengele chema? Utapata faida gani kutoka kwa majaribu na usafishaji wa Mungu? Je, upendo wako kwa Mungu utaongezeka? Wakati unapitia usafishaji, je, utaweza kutumia majaribu ya Ayubu na ujishughulishe kwa ari na kazi ambayo Mungu anafanya ndani yako? Je, unaweza kuona jinsi Mungu anavyompima mwanadamu kwa njia ya majaribu ya Ayubu? Ni aina gani ya mvuto ambao majaribu ya Ayubu yanaweza kuleta kwako? Je, utakuwa tayari kuwa shahidi kwa Mungu katikati ya usafishaji wako, au utataka kuuridhisha mwili katika mazingira ya starehe? Mtazamo wako kuhusu imani kwa Mungu ni upi kwa kweli? Je, kweli ni kwa ajili Yake, na si kwa ajili ya mwili? Je, kweli una lengo ambalo unafuatilia katika kutafuta kwako? Je, uko tayari kupitia usafishaji ili uweze kufanywa mkamilifu na Mungu, au badala yake ungeona heri kuadibiwa na kulaaniwa na Mungu? Mtazamo wako juu ya suala la kuwa na ushuhuda wa Mungu? Watu wanapaswa kufanya nini katika mazingira fulani ili wamshuhudie Mungu kwa kweli? Kwa kuwa Mungu wa utendaji amefichua mengi sana kazi Yake ya hakika ndani yako, kwa nini siku zote una mawazo ya kuondoka? Je, imani yako katika Mungu ni kwa ajili ya Mungu? Kwa wengi wenu, imani yeny ni sehemu ya hesabu mnayofanya kwa niaba yenu wenyewe, kwa ajili ya ufuatiliaji wa faida zenu binafsi. Watu wachache sana wanaamini katika Mungu kwa ajili ya Mungu; je, huu sio ukaidi?

Kusudi la kazi ya usafishaji kimsingi ni ya kukamilisha imani ya watu. Mwishowe, kile kinachofanikishwa ni kwamba unataka kuondoka lakini, wakati huo huo, huwezi; baadhi ya watu bado wanaweza kuwa na imani hata wakati wanaondolewa hata chembe kidogo cha matumaini; na watu hawana tena tumaini kabisa kuhusu matarajio ya siku za zao za usoni. Ni katika wakati huu tu ndipo usafishaji wa Mungu utafikia kikomo. Mwanadamu bado hajafikia hatua ya kuelea kati ya maisha na kifo, na hajaonja mauti, hivyo mchakato wa usafishaji bado haujakamilika. Hata wale ambao walikuwa katika hatua ya watenda huduma hawakuwa wamesafishwa kabisa. Ayubu alipitia usafishaji mkali sana, na hakuwa na kitu cha kutegemea. Watu lazima wapitie usafishaji mpaka ile hatua ambayo hawana matumaini na kitu cha kutegemea—huu tu ndio usafishaji wa kweli. Wakati wa watenda huduma, ikiwa moyo wako daima ulikuwa umetulia mbele ya Mungu, na ikiwa pasipo kujali Alichofanya na pasipo kujali mapenzi Yake kwa ajili yako yalikuwa nini, wewe daima ulitii mipango Yake, basi mwishoni ungeelewa kila kitu ambacho Mungu alikuwa amefanya. Unapitia majaribu ya Ayubu, na wakati uo huo unapitiaa majaribu ya Petro. Wakati Ayubu alijaribiwa, yeye alikuwa shahidi, na mwishowe, Yehova alidhihirishwa kwake. Ni baada tu ya kuwa shahidi ndipo alistahili kuona uso wa Mungu. Kwa nini inasemwa: “Mimi najificha kutoka nchi ya uchafu lakini Najionyesha kwa ufalme mtakatifu”? Hiyo ina maana kwamba wakati tu uko mtakatifu na kuwa shahidi ndipo unaweza kuwa na hadhi ya kuuona uso wa Mungu. Kama huwezi kuwa shahidi kwa ajili Yake, hauna hadhi ya kuuona uso Wake. Ukijiondoa au kufanya malalamiko kwa Mungu ukikabiliwa na usafishaji, hivyo ushindwe kuwa shahidi Wake na uwe kichekesho cha Shetani, basi hutapata sura ya Mungu. Kama wewe ni kama Ayubu, ambaye katikati ya majaribu aliulaani mwili wake na wala hakulalamika dhidi ya Mungu, na aliweza kuuchukia mwili wake bila kulalamika au kutenda dhambi kwa njia ya maneno yake, basi utakuwa shahidi. Unapopitia usafishaji kwa kiasi fulani na bado unaweza kuwa kama Ayubu, mtiifu kabisa mbele ya Mungu na bila mahitaji mengine Kwake au dhana zako mwenyewe, basi Mungu atakuonekania. Sasa Mungu hakuonekanii kwa sababu una nyingi za dhana zako mwenyewe, maoni binafsi, mawazo ya ubinafsi, mahitaji ya binafsi na maslahi ya kimwili, na wewe hustahili kuuona uso Wake. Kama ungemwona Mungu, ungempima kupitia katika mawazo yako mwenyewe na, kwa kufanya hivyo, Angesulubishwa msalabani nawewe. Kama mambo mengi yanakuja kwako ambayo si sambamba na dhana zako lakini bado unaweza kuyaweka kando na kupata ufahamu wa matendo ya Mungu kutoka kwa mambo haya, na katikati ya usafishaji unadhihirisha moyo wako wa upendo kwa Mungu, basi huku ni kuwa shahidi. Kama nyumba yako ina amani, unafurahia starehe za mwili, hakuna mtu anayekutesa, na ndugu na dada zako katika kanisa wanakutii, je, unaweza kuonyesha moyo wako wa upendo kwa Mungu? Je, hali hii inaweza kukusafisha? Ni kwa kupitia katika usafishaji tu ndiyo upendo wako kwa Mungu unaweza kuonyeshwa, na ni kwa mambo yasiyo sambamba na fikira zako kutokea tu ndiyo unaweza kukamilishwa. Akitumia mambo mengi yasiyofaa na mabaya na kwa kutumia kila aina ya maonyesho ya Shetani—matendo yake, lawama yake, usumbufu wake na udanganyifu wake—Mungu hukuonyesha sura mbaya ya Shetani vizuri, na hivyo Anakamilisha uwezo wako wa kumbainisha Shetani, ili uweze kumchukua Shetani na uachane naye.

Uzoefu wako mwingi wa kushindwa, udhaifu, nyakati zako za uhasi, vyote vinaweza kusemekana kuwa majaribu ya Mungu. Hii ni kwa sababu kila kitu hutoka kwa Mungu, na mambo yote na matukio yako katika mikono Yake. Kama unashindwa au kama wewe ni dhaifu na unajikwaa, yote yako kwa Mungu na vipo katika mfumbato Wake. Kutoka kwa mtazamo wa Mungu, haya ni majaribu yako, na kama huwezi kutambua hivyo, yatageuka majaribu. Kuna aina mbili za hali ambazo watu wanapaswa kutambua: Moja inatoka kwa Roho Mtakatifu, na chanzo cha nyingine huenda ni Shetani. Moja ni hali ambamo Roho Mtakatifu anakuangazia na Anakuruhusu upate kujijua mwenyewe, kuchukia na kuhisi majuto kujihusu mwenyewe na kuweza kuwa na upendo wa kweli kwa Mungu, kuweka moyo wako katika kumridhisha Yeye. Nyingine ni hali ambamo unajijua mwenyewe, lakini wewe ni hasi na dhaifu. Inaweza kusemwa pia kuwa hii ni hali ya usafishaji wa Mungu, na pia kuwa ni ushawishi wa Shetani. Ukitambua kuwa huu ni wokovu wa Mungu kwako na ukihisi kuwa wewe sasa ni mdeni Wake mkubwa, na kama kuanzia sasa utajaribu kulipa deni Lake na usianguke tena katika upotovu kama huo, kama utaweka juhudi katika kula na kunywa maneno Yake, na kama siku zote unajichukua kama anayekosa, na kuwa na moyo wa hamu, basi haya ni majaribu ya Mungu. Baada ya mateso kumalizika na wewe kwa mara nyingine tena unasonga mbele, Mungu bado atakuongoza, atakuangazia, atakupa nuru, na kukusitawisha. Lakini kama hulitambui na wewe ni hasi, kujiachilia tu kukata tamaa, kama unafikiri hivi, basi kishawishi cha Shetani kimekufikia. Wakati Ayubu alipitia majaribu, Mungu na Shetani walikuwa wanawekeana dau, na Mungu alimruhusu Shetani amtese Ayubu. Hata ingawa ilikuwa ni Mungu aliyekuwa anamjaribu Ayubu, hakika alikuwa ni Shetani ndiye aliyemjia. Kwa Shetani, ilikuwa ni kumjaribu Ayubu, lakini Ayubu alikuwa upande wa Mungu. Kama haingekuwa vile, basi Ayubu angeanguka katika kishawishi. Mara baada ya watu kuanguka katika kishawishi, wao huanguka katika hatari. Kupitia usafishaji inaweza kusemwa kuwa jaribu kutoka kwa Mungu, lakini kama hauko katika hali nzuri inaweza kusemwa kuwa kishawishi kutoka kwa Shetani. Kama hauko na uwazi juu ya maono, Shetani atakushutumu na kukuvuruga katiza mtazamo wa maono. Kabla ya kujua, utaanguka katika majaribu.

Kama hupitii kazi ya Mungu, basi kamwe hutaweza kufanywa mkamilifu. Katika uzoefu wako, lazima pia uingie katika maelezo. Kwa mfano, ni vitu vipi hukuongoza kukuza dhana na nia za kupita kiasi, na ni aina gani za matendo yanayofaa uliyo nayo kushughulikia matatizo haya? Kama unaweza kupitia kazi ya Mungu, hii ina maana kwamba una kimo. Kama unaonekana tu kuwa na nguvu, hiki si kimo halisi na hutaweza kusimama imara hata kidogo. Ni wakati tu unaweza kupitia kazi ya Mungu na uweze kuipitia na kuitafakari wakati wowote na mahali popote, wakati unaweza kuwaacha wachungaji na uishi peke yako ukimtegemea Mungu, na uweze kuona matendo halisi ya Mungu—ni hapo tu ndipo mapenzi ya Mungu yatatimizwa. Sasa hivi, watu wengi hawajui jinsi ya kupitia, na wanapokumbana na suala, hawajui jinsi ya kulishughulikia; hawawezi kuipitia kazi ya Mungu, na hawezi kuishi maisha ya kiroho. Lazima uchukue maneno ya Mungu na kuyafanya ndani ya maisha yako ya utendaji.

Wakati mwingine Mungu hukupa aina fulani ya hisia, hisia inayokusababisha upoteze starehe yako ya ndani kabisa, na unapoteza uwepo wa Mungu, kiasi kwamba unatumbukia gizani. Hii ni aina ya usafishaji. Wakati wowote unapofanya kitu chochote, hicho huenda mrama, au kugonga ukuta. Hii ni nidhamu ya Mungu. Wakati mwingine, unapofanya kitu ambacho si cha utiifu na cha uasi kwa Mungu, huenda hakuna mtu mwingine anajua kukihusu—lakini Mungu anajua. Yeye hatakuachilia, na Atakufundisha nidhamu. Kazi ya Roho Mtakatifu ni yenye kina sana. Kwa makini sana Anatazama kila neno na tendo la watu, kila tendo na mwendo wao, na kila wazo lao na fikira ili watu waweze kupata ufahamu wa ndani wa vitu hivi. Unafanya kitu mara moja na kinaenda mrama, unakifanya kitu tena na bado kinaenda mrama, na hatua kwa hatua utapata kuelewa kazi ya Roho Mtakatifu. Kupitia kufundishwa nidhamu mara nyingi, utajua cha kufanya ili kuwa sambamba na mapenzi ya Mungu na kile kisichoambatana na mapenzi Yake. Mwishowe, utakuwa na majibu sahihi kwa uongozi wa Roho Mtakatifu ndani yako. Wakati mwingine utakuwa muasi na utakemewa na Mungu kutoka ndani. Haya yote hutoka kwa nidhamu ya Mungu. Kama huthamini neno la Mungu, kama unaidharau kazi Yake, Hatashughulika na wewe hata kidogo. Kadiri unavyoyachukulia maneno ya Mungu kwa makini, ndivyo Atakavyokupa nuru zaidi. Sasa hivi, kuna baadhi ya watu katika kanisa ambao wana imani iliyovurugwa na yenye kuchanganyikiwa, na wao hufanya mambo mengi yasiyofaa na kutenda bila nidhamu, na hivyo kazi ya Roho Mtakatifu haiwezi kuonekana wazi ndani yao. Baadhi ya watu huacha nyuma wajibu wao kwa ajili ya kuchuma pesa, kwenda nje kuendesha biashara bila kuwa na nidhamu; mtu wa aina hiyo yuko katika hatari zaidi. Siyo tu kwamba sasa hawana kazi ya Roho Mtakatifu, lakini katika siku zijazo itakuwa vigumu kwa wao kukamilishwa. Kuna watu wengi ambao kwao kazi ya Roho Mtakatifu haiwezi kuonekana na ambao nidhamu ya Mungu haiwezi kuonekana kwao. Wao ni wale ambao hawako wazi juu ya mapenzi ya Mungu na ni wasiojua kazi Yake. Wale ambao wanaweza kusimama imara katikati ya usafishaji, wanaofuata Mungu bila kujali Anachofanya, na angalau wanaweza kusalia, au kutimiza 0.1% ya kile ambacho Petro alitimiza wanafanya vyema, lakini hawana thamani kuhusiana na Mungu kuwatumia. Watu wengi huelewa mambo haraka, wana upendo wa kweli kwa Mungu, na wanaweza kuzidi kiwango cha Petro, na Mungu huwafanyia kazi ya kukamilisha. Nidhamu na nuru huja kwa watu kama hawa, na iwapo kuna jambo ndani yao lisiloambatana na mapenzi ya Mungu, wanaweza kulitupilia mbali mara moja. Watu kama hawa ni dhahabu, fedha na vito—wana thamani ya juu kabisa! Kama Mungu amefanya aina nyingi za kazi lakini bado uko kama mchanga au jiwe, basi huna thamani!

Kazi ya Mungu katika nchi ya joka kubwa jekundu ni ya ajabu na isiyoeleweka. Yeye atalikamilisha kundi moja la watu na kuondoa wengine, kwani kuna kila aina ya watu kanisani—kuna wale wanaopenda ukweli, na wale wasiopenda; kuna wale wanaopitia kazi ya Mungu, na wale wasiopitia; kuna wale wanaofanya wajibu wao, na wale wasiofanya; kuna wale wanaomshuhudia Mungu, na wale wasiomshuhudia—na wengine wao ni wasioamini na watu waovu, na hakika wataondolewa. Kama hujui vizuri kazi ya Mungu, basi utakuwa hasi; hii ni kwa sababu kazi ya Mungu inaweza tu kuonekana katika watu wachache. Wakati huu, itakuwa wazi ni nani ambao wanampenda Mungu kwa kweli na wasiompenda. Wale ambao kweli wanampenda Mungu wana kazi ya Roho Mtakatifu, huku wale ambao hawampendi kwa kweli watafichuliwa kupitia kila hatua ya kazi Yake. Watakuwa walengwa wa kuondolewa. Watu hawa watafichuliwa katika kipindi cha kazi ya ushindi, na wao ni watu ambao hawana thamani ya kufanywa wakamilifu. Wale ambao wamekamilishwa wamepatwa na Mungu katika ukamilifu wao wote, na wana uwezo wa kumpenda Mungu kama vile alivyokuwa nao Petro. Wale ambao wameshindwa hawana upendo wa hiari, lakini wana upendo usioonyesha hisia, na wao wanalazimika kumpenda Mungu. Upendo wa hiari unakuzwa kwa njia ya uelewa uliopatikana kupitia uzoefu wa vitendo. Upendo huu unachukua moyo wa mtu na unamfanya kujitolea kwa Mungu kwa hiari; maneno ya Mungu yanakuwa msingi wao na wanaweza kuteseka kwa ajili ya Mungu. Bila shaka haya ni mambo yanayomilikiwa na mtu ambaye amekamilishwa na Mungu. Kama unataka tu kushindwa, basi huwezi kuwa na ushuhuda kwa Mungu; kama Mungu angetimiza tu lengo Lake la wokovu kwa njia ya kuwashinda watu, basi hatua ya watenda huduma ingemaliza kazi. Hata hivyo, kuwashinda watu si lengo la mwisho la Mungu, ambalo ni kuwakamilisha watu. Hivyo badala ya kusema kwamba hatua hii ni kazi ni ya kuwashinda watu, sema kuwa ni kazi ya kukamilisha na kuondoa. Baadhi ya watu hawajashindwa kabisa, na katika harakati ya kuwashinda, kundi la watu watafanywa wakamilifu. Vipande hivi viwili vya kazi vinafanywa kwa pamoja. Watu hawajaondoka hata kwa muda mrefu sana kama huu wa kazi, na hili linaonyesha kuwa lengo la ushindi limekuwa na mafanikio—huu ni ukweli wa kushindwa. Usafishaji si kwa ajili ya kushindwa, lakini ni kwa ajili ya kukamilishwa. Bila usafishaji, watu hawangeweza kukamilishwa. Hivyo usafishaji kweli ni wa thamani! Leo kundi moja la watu linakamilishwa na kupatwa. Baraka kumi zilizotajwa hapo awali zote zililengwa kwa wale ambao wamekamilishwa. Kila kitu kuhusu kubadilisha sura zao duniani kunalenga wale ambao wamekamilishwa. Wale ambao hawajakamilishwa hawastahili kupokea ahadi za Mungu.

Iliyotangulia: Wale Wanaompenda Mungu Kwa Kweli Ni Wale Wanaoweza Kutii Utendaji Wake Kabisa

Inayofuata: Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp