5. Kupata Mwili Mara Mbili Kunakamilisha Umuhimu wa Kupata Mwili
Maneno Husika ya Mungu:
Kupata mwili mara ya kwanza kulikuwa kumkomboa mwanadamu kutoka katika dhambi kupitia mwili wa Yesu, yaani, Alimwokoa mwanadamu kutoka msalabani, lakini tabia potovu ya kishetani bado ilibaki ndani ya mwanadamu. Kupata mwili mara ya pili si kwa ajili ya kuhudumu tena kama sadaka ya dhambi ila ni kuwaokoa kikamilifu wale waliokombolewa kutoka kwa dhambi. Hii inafanyika ili wale waliosamehewa wakombolewe kutoka kwa dhambi zao, na kufanywa safi kabisa, na kupata mabadiliko ya tabia, hivyo kujikwamua kutoka kwa ushawishi wa Shetani wa giza na kurudi mbele za kiti cha enzi cha Mungu. Hivyo tu ndivyo mwanadamu ataweza kutakaswa kikamilifu. Baada ya Enzi ya Sheria kufika mwisho, na kuanzia Enzi ya Neema, Mungu alianza kazi ya wokovu, ambayo inaendelea hadi siku za mwisho ambapo, katika kuhukumu na kuiadibu jamii ya binadamu kwa ajili ya uasi wao, Atawatakasa wanadamu kikamilifu. Ni hapo tu ndipo Mungu atakamilisha kazi Yake ya wokovu na kuingia katika pumziko. Kwa hivyo, katika hatua tatu za kazi, ni mara mbili tu ndipo Mungu amekuwa mwili ili kufanya kazi Yake kati ya mwanadamu Mwenyewe. Hiyo ni kwa sababu moja tu kati ya hatua tatu za kazi ni kuwaongoza wanadamu katika maisha yao, ilhali zingine mbili ni kazi ya wokovu. Mungu Anapokuwa mwili tu ndipo Atakapoishi pamoja na mwanadamu, kuzoea mateso ya dunia, na kuishi katika mwili wa kawaida. Ni kwa namna hii tu ndipo Ataweza kuwapa wanadamu njia ya vitendo wanayohitaji kama viumbe. Mwanadamu anapokea wokovu kamili kutoka kwa Mungu kwa sababu ya Mungu mwenye mwili, sio moja kwa moja kutoka kwa maombi yao kwenda mbinguni. Kwani mwanadamu ni mwenye mwili; mwanadamu hawezi kuona Roho wa Mungu na pia kutoweza kumkaribia. Kile tu mwanadamu anaweza kushiriki ni mwili wa Mungu; kupitia Yeye tu ndipo mwanadamu ataweza kuelewa njia zote, na ukweli wote, na kupokea wokovu kamili. Kupatikana kwa mwili mara ya pili kunatosha kumaliza dhambi za mwanadamu na kumtakasa mwanadamu. Hivyo, kupatikana kwa mwili mara ya pili kutafikisha tamati kazi yote ya Mungu mwenye mwili na kukamilisha umuhimu wa Mungu kupata mwili. Baada ya hapo, kazi ya Mungu mwenye mwili itakuwa imefika mwisho kabisa. Baada ya kupata mwili mara ya pili, hatakuwa mwili tena kwa kazi Yake. Kwani usimamizi Wake wote utakuwa umefika mwisho. Katika siku za mwisho, mwili Wake utakuwa umepata watu Wake teule kabisa, na wanadamu wotekatika siku za mwisho watakuwa wameainishwa kulingana na aina. Hatafanya kazi ya wokovu tena, wala Hatarudi kuwa mwili ili kutekeleza kazi yoyote.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (4)
Yesu Alipokuwa Akifanya kazi Yake, maarifa ya mwanadamu juu Yake yalikuwa bado hayakuwa bayana na hayakuwa wazi. Mwanadamu aliamini kila wakati kuwa Alikuwa Mwana wa Daudi na kumtangaza kuwa nabii mkuu na Bwana mwema Aliyezikomboa dhambi za mwanadamu. Wengine, wakiwa na msingi wa imani, wakaponywa tu kwa kugusa vazi Lake; vipofu wakaona na hata wafu kurejeshwa katika uhai. Hata hivyo, mwanadamu hangeweza kutambua tabia potovu za kishetani zilizokita mizizi ndani yake na pia mwanadamu hakujua jinsi ya kuitoa. Mwanadamu alipokea neema nyingi, kama amani na furaha ya mwili, baraka ya familia nzima juu ya imani ya mmoja, na kuponywa magonjwa, na mengine mengi. Yaliyobaki ni matendo mema ya mwanadamu na kuonekana kwa kiungu; kama mtu angeishi katika huo msingi, angechukuliwa kama muumini mzuri. Waumini hao tu ndio wangeingia mbinguni baada ya kifo, ambayo ilimaanisha kuwa walikuwa wameokolewa. Lakini katika maisha yao, hawakuelewa kamwe njia ya maisha. Walitenda tu dhambi, na kisha kukiri kila wakati bila njia yoyote ya kubadili tabia yao; hii ndiyo ilikuwa hali ya mwanadamu katika Enzi ya Neema. Je mwanadamu amepokea wokovu kamili? La! Kwa hivyo, hatua ilipokamilika, bado kuna kazi ya hukumu na kuadibu. Hatua hii ni ya kumfanya mwanadamu awea safi kupitia neno, na hivyo kumpa njia ya kufuata. Hatua hii haingekuwa na matunda ama ya maana kama ingeendelea na kukemea mapepo, kwani msingi wa dhambi wa mwanadamu haungetupwa mbali na mwanadamu angekoma tu baada ya msamaha wa dhambi. Kupitia kwa sadaka ya dhambi, mwanadamu amesamehewa dhambi zake, kwani kazi ya kusulubisha imefika mwisho na Mungu Ametawala juu ya Shetani. Lakini tabia potovu ya wanadamu bado imebaki ndani yao na mwanadamu anaweza kutenda dhambi na kumpinga Mungu; Mungu hajampata mwanadamu. Hiyo ndio sababu katika hatua hii ya kazi Mungu Anatumia neno kufichua tabia potovu ya mwanadamu na kumuomba mwanadamu kutenda kulingana na njia sahihi. Hatua hii ni ya maana zaidi kuliko zile za awali na pia yenye mafanikio zaidi, kwani wakati huu ni neno ambalo linatoa maisha moja kwa moja kwa mwanadamu na linawezesha tabia ya mwanadamu kubadilishwa kabisa; ni hatua ya kazi ya uhakika kabisa. Kwa hivyo, Mungu kupata mwili katika siku za mwisho imekamilisha umuhimu wa Mungu kupata mwili wa Mungu na kukamilisha usimamizi wa Mungu katika mpango wa kuokoa mwanadamu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (4)
Mungu katika kupata mwili Kwake kwa mara ya kwanza Hakukamilisha kazi ya kupata mwili; Alikamilisha tu hatua ya kwanza ya kazi iliyokuwa lazima kwa Mungu kuifanya katika mwili. Kwa hivyo, ili kuimaliza kazi ya kupata mwili, Mungu Amerudi katika mwili kwa mara nyingine tena, Akiishi kulingana na ukawaida na uhalisia wote wa mwili, yaani, anaifanya kazi ya Mungu ijitokeze katika mwili wa kawaida kabisa, na kwa njia hiyo Anahitimisha kazi Aliyoiacha bila kuikamilisha katika mwili. Mwili wa pili uliopatikana kimsingi ni sawa na ule wa kwanza, lakini ni halisi zaidi, wa kawaida kabisa kuliko ule wa kwanza. Kwa sababu hiyo, mateso yanayopitiwa na mwili wa pili uliopatikana ni makubwa kuliko yale ya ule wa kwanza, ila mateso haya ni kwa sababu ya huduma Yake katika mwili, ambayo ni tofauti na mateso ya mwanadamu mwovu. Vilevile yanayotokana na ukawaida na uhalisi wa mwili Wake. Kwa kuwa Anatekeleza huduma Yake katika mwili wa kawaida na halisi kabisa, ni lazima mwili upitie mateso makubwa. Kadiri mwili ulivyo wa kawaida na wa kivitendo, ndivyo unavyoteseka zaidi katika utekelezaji wa huduma Yake. Kazi ya Mungu inaonyeshwa katika mwili wa kawaida sana, mwili ambao si wa kimiujiza kabisa. Kwa kuwa mwili Wake ni wa kawaida, na ni lazima ubebe kazi ya kumwokoa mwanadamu, Anateseka hata zaidi kuliko ambavyo mwili wa kiroho unavyoweza kuteseka—mateso haya yote yanatokana na uhalisi na ukawaida wa mwili Wake. Kutokana na mateso yaliyopitiwa na hii miili miwili iliyopatikana wakati wa kutekeleza huduma Zao, mtu anaweza kuona kiini cha kupata mwili. Kadiri mwili ulivyo wa kawaida, ndivyo Anavyopata mateso mazito Anapofanya kazi, kadri mwili unaofanya kazi unavyokuwa halisi, ndivyo dhana za watu zinavyoendelea kuwa kubwa, na ndivyo hatari nyingi zaidi zinavyoweza kumpata Yeye. Lakini, kadiri mwili ulivyo halisi, kadiri mwili unavyokuwa na mahitaji na hisia kamili za mwanadamu wa kawaida, ndivyo Anavyoweza zaidi kuifanya kazi ya Mungu katika mwili. Ulikuwa mwili wa Yesu ulioangikwa msalabani, mwili Wake Alioutoa kama kafara kwa dhambi; yaani, ni kupitia kwa mwili wenye ubinadamu wa kawaida ndipo Alipoweza kumshinda Shetani na kumkomboa kabisa mwanadamu kutoka msalabani. Ni kwa njia ya mwili kamili ambapo mwili wa pili wa Mungu unafanya kazi ya ushindi na kumshinda Shetani. Ni mwili tu wa kawaida na halisi kabisa unaoweza kutekeleza kazi ya ushindi kwa ukamilifu wake na kutoa ushuhuda wenye nguvu. Hii ni sawa na kusema kwamba, ushindi juu ya mwanadamu unafanywa kuwa bora kupitia uhalisi na ukawaida wa mwili wa Mungu, si kupitia miujiza na mafunuo yasiyo ya kawaida. Huduma inayofanywa na huyu Mungu mwenye mwili ni kuzungumza, na ni kupitia kuzungumza ndipo Anapomshinda na kumkamilisha mwanadamu; kwa maneno mengine, kazi ya Roho inayodhihirika katika mwili ni kuzungumza na kazi ya mwili ni kuzungumza, na hivyo inafikia lengo la kuwashinda, kuwafichua, kuwakamilisha, na kuwaondoa watu kabisa. Kwa hivyo, ni katika kazi ya ushindi ambapo kazi ya Mungu katika mwili itatimizwa kikamilifu. Kazi ya upatanisho kwa ajili ya dhambi za wanadamu iliyofanywa mara ya kwanza ilikuwa tu ni mwanzo wa kazi ya kupata mwili; ni mwili tu unaofanya kazi ya ushindi ndio utakamilisha kazi yote ya kupata mwili. Kijinsia, mmoja ni mwanamke na mwingine ni mwanamume; kwa hili, maana ya kupata mwili kwa Mungu imekamilishwa. Dhana za mwanadamu kumhusu Mungu zimeondolewa: Mungu Anaweza kuwa mwanamke na mwanamume, na kimsingi Mungu mwenye mwili Hana jinsia. Alimuumba mwanamume na mwanamke, na Kwake, hakuna mgawanyiko wa jinsia. Katika hatua hii ya kazi, Mungu Hafanyi ishara na miujiza, ili kwamba kazi iweze kutimiza matokeo yake kupitia kwa maneno. Sababu ya jambo hili, aidha, ni kwa sababu kazi ya Mungu mwenye mwili kwa wakati huu si kuponya wagonjwa na kufukuza mapepo, ila ni kumshinda mwanadamu kupitia kunena, ikiwa na maana kwamba uwezo wa asili unaomilikiwa na mwili huu uliopatwa na Mungu ni kunena maneno na kumshinda mwanadamu, si kuponya wagonjwa na kufukuza mapepo. Kazi Yake katika ubinadamu wa kawaida si kutenda miujiza, si kuponya wagonjwa na kufukuza mapepo, ila ni kunena, na kwa hivyo kupata mwili kwa mara ya pili kunaonekana kwa watu kuwa kwa kawaida zaidi ya mara ya kwanza. Watu wanaona kuwa Mungu kupata mwili si uongo; lakini huyu Mungu mwenye mwili ni tofauti na Yesu Aliyekuwa mwili, na ingawa Wote ni kupata mwili kwa Mungu, Hawako sawa kabisa. Yesu Alikuwa na ubinadamu usio wa tofauti, ubinadamu wa kawaida, lakini Aliambatana na ishara nyingi na miujiza. Katika huyu Mungu mwenye mwili, macho ya mwanadamu hayataona ishara au miujiza, wala kuponya wagonjwa au kufukuza mapepo, wala kutembea juu ya bahari, wala kufunga kwa siku arobaini… Hafanyi kazi sawa na Aliyoifanya Yesu, si kwa kuwa mwili Wake kimsingi ni tofauti na ule wa Yesu, ila ni kwa sababu si huduma Yake kuponya wagonjwa na kufukuza mapepo. Haharibu kazi Yake mwenyewe, Havurugi kazi Yake mwenyewe. Kwa kuwa Anamshinda mwanadamu kupitia maneno Yake ya kivitendo, hakuna haja ya kumtiisha kwa miujiza, na hivyo hatua hii ni kukamilisha kazi ya kupata mwili.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kiini cha Mwili Uliovaliwa na Mungu
Kwa nini Ninasema kuwa maana ya kupata mwili haikukamilishwa katika kazi ya Yesu? Ni kwa sababu Neno halikuwa Mwili kikamilifu. Kilichofanywa na Yesu kilikuwa tu sehemu moja ya kazi ya Mungu katika mwili; Alifanya tu kazi ya ukombozi na Hakufanya kazi ya kumpata mwanadamu kikamilifu. Kwa sababu hii, Mungu amefanyika mwili kwa mara nyingine tena katika siku za mwisho. Hatua hii ya kazi, pia inafanywa katika mwili wa kawaida, ikifanywa na mwanadamu wa kawaida kabisa, ambaye ubinadamu wake haupiti mipaka ya ubinadamu. Kwa maneno mengine, Mungu Amekuwa mwanadamu kamili, na ni mtu ambaye utambulisho wake ni ule wa Mungu, mwanadamu kamili, mwili kamili, Ambaye Anatekeleza kazi. Macho ya mwanadamu huona umbo la mwili ambao haujavuka mipaka ya ubinadamu hata kidogo, ni, mwanadamu wa kawaida kabisa Anayeweza kuzungumza lugha ya mbinguni, Ambaye Haonyeshi ishara za kimiujiza, Hafanyi miujiza, sembuse kuweka wazi ukweli wa ndani kuhusu dini katika kumbi kuu za mikutano. Kazi ya kupata mwili kwa mara ya pili inaonekana kwa wanadamu kuwa tofauti kabisa na ile ya kwanza, kiasi kwamba kazi hizi mbili zinaonekana kutokuwa na uhusiano wowote, na hakuna chochote katika kazi ya kwanza kinachoweza kuonekana wakati huu. Japo kazi ya kupata mwili kwa mara ya pili ni tofauti na ile ya kwanza, hili halithibitishi kuwa chanzo Chao si kimoja na sawa. Iwapo chanzo Chao ni kimoja inategemea aina ya kazi iliyofanywa na miili na si katika maumbo Yao ya nje. Katika hatua tatu za kazi Yake, Mungu amefanyika mwili mara mbili, na mara zote kazi ya Mungu katika mwili inaanzisha enzi mpya, inaanzisha kazi mpya; kupata mwili kwa mara ya kwanza na ya pili kunakamilishana. Macho ya wanadamu hayawezi kugundua kuwa hii miili miwili kwa kweli imetoka kwenye chanzo kimoja. Ni wazi kwamba hili liko nje ya uwezo wa macho ya wanadamu au akili za wanadamu. Lakini katika kiini Chao, ni miili sawa, kwani kazi Zao zinatoka kwa Roho mmoja. Ikiwa hii miili miwili inatoka kwenye chanzo kimoja haiwezi kuamuliwa kutokana na enzi na sehemu Ilipozaliwa, au vigezo vingine kama hivyo, ila kwa kazi ya uungu iliyoonyeshwa Nayo. Kupata mwili kwa pili hakufanyi kazi yoyote iliyofanywa na Yesu, kwani kazi ya Mungu haifuati makubaliano, lakini kila wakati inafungua njia mpya. Kupata mwili kwa mara ya pili hakulengi kuongeza au kuimarisha maono ya kupata mwili kwa mara ya kwanza katika akili za watu, bali inautimiza na kuukamilisha, ili kuongeza maarifa ya mwanadamu kuhusu Mungu, kuvunja sheria zote ambazo zipo katika mioyo ya watu, na kufuta picha za uongo kuhusu Mungu mioyoni mwao. Ni wazi kuwa hakuna hatua moja ya kazi ya Mungu mwenyewe inayoweza kumpa mwanadamu ufahamu kamili wa Mungu; kila moja inatoa kwa sehemu tu, si ufahamu kamili. Ingawa Mungu ameonyesha tabia Yake kikamilifu, lakini kwa sababu ya upungufu wa ufahamu wa mwandamu, ufahamu wake kuhusu Mungu si kamili. Haiwezekani, kutumia lugha ya wanadamu, kuelezea tabia nzima ya Mungu; basi je hatua moja tu ya kazi Yake itawezaje kumwelezea Mungu kikamilifu? Anafanya kazi katika mwili kwa kujificha katika ubinadamu Wake wa kawaida, na mtu anaweza kumjua tu kupitia kwa maonyesho ya uungu Wake, si kupitia kwa umbo Lake la kimwili. Mungu Anakuja katika mwili kumruhusu mwanadamu Amjue kupitia kazi Zake mbalimbali, na hakuna hatua mbili za kazi Yake zinazofanana. Ni kwa njia hii tu mwanadamu anaweza kuwa na ufahamu kamili wa kazi ya Mungu katika mwili, si kwa kujifunga katika kipengele kimoja tu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kiini cha Mwili Uliovaliwa na Mungu
Hatua ya kazi ambayo Yesu alitekeleza ilitimiza tu kiini cha “Neno alikuwako kwa Mungu”: Ukweli wa Mungu ulikuwako kwa Mungu, na Roho wa Mungu alikuwa na mwili na alikuwa asiyetenganishwa kutoka katika mwili huo. Yaani, mwili wa Mungu mwenye mwili ulikuwa na Roho wa Mungu, ambalo ni thibitisho kuu zaidi kwamba Yesu mwenye mwili alikuwa kupata mwili wa kwanza wa Mungu. Hatua hii ya kazi hasa inatimiza maana ya ndani ya “Neno lakuwa mwili,” ilichangia kwenye maana ya kina zaidi ya “naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu,” na inakuruhusu wewe uamini kwa uthabiti maneno “Hapo mwanzo kulikuwako na Neno.” Ambalo ni kusema, wakati wa uumbaji Mungu alikuwa na maneno, Maneno Yake yalikuwa na Yeye na yasiyotenganishwa kutoka Kwake, na katika enzi ya mwisho, Yeye anafanya nguvu na mamlaka ya maneno Yake yawe hata wazi zaidi, na kumruhusu mwanadamu kuziona njia Zake zote—kuyasikia maneno Yake yote. Hiyo ndiyo kazi ya enzi ya mwisho. Lazima uelewe mambo haya yote kabisa. Si suala la kuujua mwili, bali la jinsi unavyouelewa mwili na Neno. Huu ndio ushuhuda unaopaswa kuwa nao, kile ambacho kila mtu lazima akijue. Kwa sababu hii ni kazi ya kupata mwili kwa pili—na mara ya mwisho ambapo Mungu anapata mwili—inakamilisha kwa ukamilifu umuhimu wa kupata mwili, inatekeleza kabisa na kutoa kazi yote ya Mungu katika mwili, na kuitamatisha enzi ya Mungu kuwa katika mwili.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Utendaji (4)
Haijalishi kama katika hatua hii Mungu mwenye mwili Anapitia ugumu au Anatekeleza huduma Yake, Anafanya hivyo ili kukamilisha maana ya kupata mwili, kwani huku ndiko Mungu kupata mwili kwa mara ya mwisho. Mungu anaweza kufanyika mwili mara mbili tu. Hakuwezi kuwa na mara ya tatu. Kupata mwili kwa mara ya kwanza kulikuwa ni mwanamume, mara ya pili ni mwanamke, na kwa hivyo sura ya mwili wa Mungu imekamilika katika akili za mwanadamu; zaidi ya hayo, kupata mwili mara mbili tayari kumekamilisha kazi ya Mungu katika mwili. Mara ya kwanza, Mungu mwenye mwili Alikuwa na ubinadamu wa kawaida, ili kukamilisha maana ya kupata mwili. Mara hii vilevile Ana ubinadamu wa kawaida lakini maana ya kupata mwili huku ni tofauti: ni kwa kina zaidi, na kazi Yake ni ya umuhimu mkubwa. Sababu ya Mungu kufanyika mwili kwa mara nyingine tena ni ili kukamilisha maana ya kupata mwili. Mungu atakapomaliza kabisa hatua hii ya kazi Yake, maana nzima ya kupata mwili, yaani, kazi ya Mungu katika mwili, itakuwa imekamilika, na hakutakuwa na kazi nyingine ya kufanywa katika mwili. Yaani, tangu sasa Mungu Hatawahi tena kuja katika mwili kufanya kazi Yake.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kiini cha Mwili Uliovaliwa na Mungu
Kupata Mwili Mara Mbili Kunakamilisha Umuhimu wa Kupata Mwili
(Sura Iliyochaguliwa ya Neno la Mungu)
Kila hatua ya kazi inayofanywa na Mungu ina umuhimu wake wa vitendo. Yesu alipokuja zamani, Alikuwa mwanaume, lakini Mungu anapokuja wakati huu Yeye ni mwanamke. Kutokana na hili, unaweza kuona kwamba Mungu aliwaumba mwanaume na mwanamke kwa ajili ya kazi Yake na Kwake hakuna tofauti ya jinsia. Roho Wake anapowasili, Anaweza kuchukua mwili wowote kwa matakwa Yake na mwili huo unaweza kumwakilisha Yeye. Uwe wa kiume au kike, unaweza kumwakilisha Mungu alimradi tu ni mwili Wake wa nyama. Kama Yesu angeonekana kama mwanamke alipokuja, kwa maneno mengine, iwapo mtoto wa kike, sio wa kiume, angezaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, hatua hiyo ya kazi ingekuwa imekamilika pia. Kama hali ingekuwa hivyo, basi hatua ya leo ya kazi ingelazimika kukamilishwa badala yake na mwanaume, lakini kazi ingekamilika pia. Kazi inayofanywa katika hatua hizi zote ni muhimu kwa kiwango sawa; hakuna hatua yoyote ya kazi inayojirudia au kupingana na nyingine. Wakati huo, Yesu alipokuwa akifanya kazi Yake aliitwa Mwana wa pekee, na “Mwana” inaashiria jinsia ya kiume. Basi kwa nini Mwana wa pekee halikutajwa katika hatua hii? Hii ni kwa sababu mahitaji ya kazi yamelazimisha badiliko la jinsia ambayo ni tofauti na ile ya Yesu. Kwa Mungu hakuna tofauti ya jinsia. Kazi Yake inafanywa kama Anavyotaka na katika kufanya kazi Yake hazuiliwi na kitu chochote kile, lakini hasa yupo huru. Hata hivyo, kila hatua ya kazi ina umuhimu wake wa vitendo. Mungu alipata mwili mara mbili, na ni dhahiri kwamba kupata mwili Kwake katika siku za mwisho ni mara ya mwisho. Amekuja kufichua matendo Yake yote. Iwapo katika hatua hii Hakuwa mwili ili binafsi kufanya kazi kwa ajili ya mwanadamu kushuhudia, mwanadamu angeshikilia milele dhana kwamba Mungu ni mwanamume tu, si mwanamke. Kabla ya hili, wanadamu wote waliamini kwamba Mungu angeweza kuwa tu mwanaume na kwamba mwanamke hawezi kuitwa Mungu, maana wanadamu wote walimchukulia mwanamume kuwa na mamlaka juu ya mwanamke. Waliamini kwamba hakuna mwanamke anayeweza kuchukua mamlaka, bali ni mwanamume tu. Aidha hata walisema kwamba mwanamume alikuwa ni mkuu wa mwanamke na kwamba mwanamke anapaswa kumtii mwanaume na asimshinde. Iliposemwa hapo nyuma kwamba mwanamume alikuwa mkuu wa mwanamke, ilielekezwa kwa Adamu na Hawa ambao walikuwa wamedanganywa na yule nyoka, na wala sio kwa mwanamume na mwanamke kama walivyoumbwa na Yehova hapo mwanzo. Bila shaka, mwanamke anapaswa kumtii na kumpenda mume wake, na mume anapaswa kujifunza kuilisha na kuiruzuku familia yake. Hizi ni sheria na kanuni zilizowekwa na Yehova ambazo kwazo wanadamu wanapaswa kuzifuata katika maisha yao ya hapa duniani. Yehova alimwambia mwanamke “Tamaayako itakuwa kwa mume wako, na atatawala juu yako.” Alisema hivyo tu ili kwamba wanadamu (yaani, mwanamume na mwanamke) waweze kuishi maisha ya kawaida chini ya utawala wa Yehova, na tu ili kwamba maisha ya wanadamu yaweze kuwa na mfumo na yasipoteze mwelekeo. Kwa hivyo, Yehova alitengeneza kanuni zinazofaa ya namna ambavyo mwanamume na mwanamke wanavyopaswa kutenda, lakini hili lilihusu tu viumbe wote wanaoishi duniani na halikuhusiana na mwili wa Mungu wa nyama. Inawezekanaje Mungu awe sawa na viumbe Wake? Maneno Yake yalielekezwa tu kwa wanadamu wa viumbe Wake; Alianzishia mwanamume na mwanamke kanuni ili wanadamu waweze kuishi maisha ya kawaida. Hapo mwanzo, Yehova alipoumba wanadamu, Aliwaumba wanadamu wa aina mbili, mwanamume na mwanamke; na kwa hiyo, kuna mgawanyo wa kike na kiume katika miili Yake. Hakuamua juu ya kazi Yake kulingana na maneno aliyozungumza kwa Adamu na Hawa. Mara mbili Alipopata mwili kuliamuliwa kwa kuzingatia kabisa mawazo Yake alipowaumba wanadamu kwa mara ya kwanza, yaani, Alikamilisha kazi ya kupata Kwake mwili mara mbili, kwa msingi wa mwanamke na mwanamume kabla ya wao kupotoshwa. Ikiwa wanadamu wangechukua maneno yaliyozungumzwa na Yehova kwa Adamu na Hawa, ambao walikuwa wamedanganywa na yule nyoka, na kuyatumia katika kazi ya mwili wa Mungu, je, si Yesu pia angepaswa kumpenda mke Wake kama Alivyotakiwa? Je, kwa njia hii, Mungu bado ni Mungu? Na ikiwa ni hivyo, je, bado Angeweza kukamilisha kazi Yake? Ikiwa ni vibaya kwa mwili wa Mungu kuwa mwanamke, je, basi lisingekuwa kosa kubwa sana pia kwa Mungu kumuumba mwanamke? Ikiwa mwanadamu bado anaamini kwamba Mungu kupata mwili kama mwanamke ni vibaya, je, basi Yesu, ambaye hakuoa na hivyo hakuweza kumpenda mke Wake, angekuwa na makosa kama kupata mwili wa sasa? Kwa kuwa unatumia maneno yaliyozungumzwa na Yehova kwa Hawa ili kupima ukweli wa Mungu kupata mwili leo, basi unapaswa kutumia maneno ya Yehova kwa Adamu kumhukumu Bwana Yesu ambaye alipata mwili katika Enzi ya Neema. Je, hawa wawili sio sawa? Kwa kuwa unampima Bwana Yesu kulingana na mwanamume ambaye hakuwa amedanganywa na yule nyoka, basi hupaswi kuhukumu ukweli wa kupata mwili leo hii kulingana na mwanamke ambaye alikuwa amedanganywa na yule nyoka. Hii itakuwa si haki! Ikiwa umefanya hukumu ya namna hiyo, inathibitisha kukosa urazini kwako. Yehova alipopata mwili mara mbili, jinsia ya mwili Wake ilikuwa inahusiana na mwanamume na mwanamke ambaye hakuwa amedanganywa na yule nyoka; Alipata mwili mara mbili kulingana na mwanamume na mwanamke ambaye hakuwa amedanganywa na yule nyoka. Usifikiri kwamba uanaume wa Yesu ulikuwa sawa na uanaume wa Adamu ambaye alidanganywa na yule nyoka. Hahusiani naye kabisa, na ni wanaume wawili wa asili tofauti. Hakika haiwezi kuwa kwamba uanaume wa Yesu unathibitisha Yeye ni mkuu wa wanawake wote lakini sio mkuu wa wanaume wote? Je, Yeye si Mfalme wa Wayahudi wote (ikiwa ni pamoja na wanaume na wanawake)? Yeye ni Mungu Mwenyewe, sio tu mkuu wa mwanamke bali mkuu wa mwanamume pia. Yeye ni Bwana wa viumbe vyote, na mkuu wa viumbe vyote. Unawezaje kuamua uanaume wa Yesu kuwa ishara ya mkuu wa mwanamke? Huku si kukufuru? Yesu ni mwanamume ambaye hajapotoshwa. Yeye ni Mungu; Yeye ni Kristo; Yeye ni Bwana. Anawezaje kuwa mwanamume kama Adamu ambaye alipotoshwa? Yesu ni mwili uliovaliwa na Roho wa Mungu aliye mtakatifu sana. Unawezaje kusema kuwa Yeye ni Mungu aliye na uanaume wa Adamu? Kama ni hivyo, kazi yote ya Mungu haingekuwa si sahihi? Je, Yehova angeweza kuuweka ndani ya Yesu uanaume wa Adamu ambaye alidanganywa na yule nyoka? Je, si kupata mwili kwa wakati huu ni tukio jingine la kazi ya Mungu mwenye mwili ambaye ni tofauti kijinsia na Yesu lakini aliye kama Yeye katika asili? Bado unathubutu kusema kwamba Mungu mwenye mwili hawezi kuwa mwanamke kwa kuwa mwanamke ndiye aliyedanganywa kwanza na yule nyoka? Bado unathubutu kusema kwamba, kwa kuwa mwanamke ndiye mwenye najisi sana na ni chanzo cha upotovu wa wanadamu, Mungu hawezi kabisa kupata mwili kama mwanamke? Bado unathubutu kuendelea kusema kwamba “mwanamke siku zote atamtii mwanamume na hawezi kamwe kudhihirisha au kumwakilisha Mungu moja kwa moja”? Hukuelewa hapo nyuma; lakini sasa bado unaweza kuendelea kukufuru kazi ya Mungu, hususan mwili wa nyama wa Mungu? Kama huwezi kuona hili kwa uwazi kabisa, ni vizuri zaidi ukawa makini na ulimi wako, la sivyo upumbavu na ujinga wako ufichuliwe na ubaya wako uwekwe wazi. Usidhani kwamba unaelewa kila kitu. Nakueleza kwamba yote uliyokwishayaona na kuyapitia hayakutoshelezi wewe kuelewa hata sehemu ndogo kabisa ya mpango Wangu wa usimamizi. Hivyo kwa nini basi unakuwa mwenye kiburi sana? Talanta ndogo hiyo uliyonayo na maarifa kidogo hayo uliyonayo hayatoshelezi kutumika na Yesu hata katika sekunde moja ya kazi Yake! Je, una uzoefu kiasi gani hasa? Yale uliyoyaona na yote uliyoyasikia katika maisha yako yote na yale uliyoyafikiria ni kidogo kuliko kazi Ninayoifanya kwa muda mfupi sana! Ni bora usichambue na kutafuta kosa. Haijalishi una kiburi kiasi gani, wewe bado ni kiumbe tu mdogo kuliko mchwa! Vyote vilivyomo katika tumbo lako ni vichache zaidi ya vile vilivyomo katika tumbo la mchwa! Usifikiri kwamba kwa kuwa tu umepata uzoefu na ukubwa kiasi, unaweza kuashiria kiburi na kuzungumza kwa maringo. Je, uzoefu wako na ukubwa wako sio matokeo ya maneno Niliyoyazungumza? Je, unaamini kwamba yalikuwa mbadala wa kufanya kwako kazi kwa bidii na kutokwa jasho? Siku hii, unaona kuwa nimepata mwili, na kwa sababu ya hili pekee unajawa na dhana nyingi hizo, na kutoka kwalo unakuwa na fikira nyingi zisizohesabika. Isingekuwa kwa kupata mwili Kwangu, bila kujali talanta ulizo nazo ni za ajabu kiasi gani, usingekuwa na dhana hizi nyingi; na si kutokana na haya ndipo dhana zako zinaibuka? Kama si kupata mwili kwa Yesu mara hiyo ya kwanza, je, hata ungejua kuhusu kupata mwili? Je, si kwa sababu ya maarifa yako kutoka kwa kupata mwili mara ya kwanza ndio una ufidhuli kuthubutu kuhukumu kupata mwili kwa mara ya pili? Kwa nini ukuchunguze badala ya kuwa mfuasi mtiifu? Wakati umeingia katika mkondo huu na kuja mbele ya Mungu mwenye mwili, je, Angekuruhusu kuchunguza hili? Ni sawa kwako kuchunguza historia ya familia yako, lakini ukijaribu kuchunguza “historia ya familia” ya Mungu, inawezekanaje Mungu wa leo akuruhusu kufanya uchunguzi kama huo? Je, wewe si kipofu? Je, hujiletei dharau kwako mwenyewe?
Laiti tu kazi ya Yesu ingefanywa bila kukamilishwa na kazi katika hatua hii ya siku za mwisho, basi mwanadamu angeshikilia milele dhana kwamba Yesu pekee ndiye Mwana pekee wa Mungu, yaani, Mungu ana mwana mmoja tu, na kwamba yeyote anayekuja baada yake akiwa na jina jingine hawezi kuwa Mwana pekee wa Mungu, sembuse Mungu Mwenyewe. Mwanadamu ana dhana kwamba yeyote ambaye anajitoa sadaka kwa ajili ya dhambi au yule ambaye anachukua mamlaka kwa niaba ya Mungu na anayewakomboa wanadamu wote ni Mwana wa Mungu wa pekee. Kuna baadhi ambao wanaamini kwamba alimradi Yeye anayekuja ni mwanamume, Anaweza kuchukuliwa kuwa ni Mwana wa Mungu wa pekee na mwakilishi wa Mungu, na hata kuna wale wanaosema kwamba Yesu ni Mwana wa Yehova, Mwana Wake wa pekee. Je, hii kweli siyo tu dhana iliyopita kiasi ya mwanadamu? Ikiwa hatua hii ya kazi haingefanywa katika enzi ya mwisho, basi wanadamu wote wangekuwa gizani sana kumhusu Mungu. Kama hii ingekuwa hivyo, mwanamume angejiona kuwa juu kuliko mwanamke, na wanawake hawangeweza kamwe kuinua vichwa vyao, na basi hakuna hata mwanamke mmoja ambaye angeweza kuokolewa. Watu siku zote wanaamini kwamba Mungu ni mwanamume, na aidha kwamba siku zote Amemchukia mwanamke na asingempa wokovu. Ingekuwa ni hivyo, isingekuwa ukweli kwamba wanawake wote walioumbwa na Yehova na pia ambao wamepotoshwa, wasingeweza kuwa na fursa ya kuokolewa? Je, basi isingekuwa bure kwa Yehova kumuumba mwanamke, yaani, kumuumba Hawa? Na je, mwanamke asingeangamia milele? Kwa sababu hii, hatua ya kazi katika siku za mwisho inafanywa ili kuwaokoa wanadamu wote, sio tu mwanamke. Ikiwa mtu yeyote angefikiri kwamba, ikiwa Mungu angepata mwili kama mwanamke, ingekuwa tu kwa ajili ya kuokoa mwanamke, basi mtu huyo kwa kweli angekuwa mpumbavu!
Kazi inayofanywa kwa sasa imesukuma mbele kazi ya Enzi ya Neema; yaani, kazi katika mpango mzima wa usimamizi wa miaka elfu sita imesonga mbele. Ingawa Enzi ya Neema imeisha, kazi ya Mungu imeendelea mbele. Kwa nini Ninasema mara kwa mara kwamba hatua hii ya kazi inajengwa juu ya Enzi ya Neema na Enzi ya Sheria? Hii ina maana kwamba kazi ya siku hii ni mwendelezo wa kazi iliyofanyika katika Enzi ya Neema na maendeleo ya kazi iliyofanyika katika Enzi ya Sheria. Hatua hizi tatu zinaingiliana kwa karibu na kuunganika moja kwa inayofuata kwa karibu. Kwa nini pia Ninasema kwamba hatua hii ya kazi inajengwa juu ya ile iliyofanywa na Yesu? Tuseme kwamba hatua hii haingejengwa juu ya kazi iliyofanywa na Yesu, ingebidi kusulubiwa kwingine kufanyike katika hatua hii, na kazi ya ukombozi ya hatua iliyopita ingelazimika kufanywa upya tena. Hii isingekuwa na maana yoyote. Kwa hiyo, sio kwamba kazi imekamilika kabisa, bali ni kwamba enzi imesonga mbele, na kiwango cha kazi kimewekwa juu kabisa kuliko kilivyokuwa kabla. Inaweza kusemwa kwamba hatua hii ya kazi imejengwa juu ya msingi wa Enzi ya Sheria na kwenye mwamba wa kazi ya Yesu. Kazi hii inajengwa hatua kwa hatua, na hatua hii sio mwanzo mpya. Ni muungano tu wa hatua tatu za kazi ndio unaweza kuchukuliwa kuwa mpango wa usimamizi wa miaka elfu sita. Kazi ya hatua hii inafanywa kwa msingi wa kazi ya Enzi ya Neema. Ikiwa hatua hizi mbili za kazi hazikuhusiana, kwa nini basi kusulubiwa hakurudiwi katika hatua hii? Kwa nini Sibebi dhambi za mwanadamu, lakini badala yake Naja kumhukumu na kumwadibu mwanadamu moja kwa moja? Ikiwa kazi Yangu ya kumhukumu na kumwadibu mwanadamu na kuja Kwangu saa hii si kwa njia ya Roho Mtakatifu na hakukufuata kusulubiwa, basi Nisingekuwa na sifa zinazostahili kumhukumu na kumwadibu mwanadamu. Kazi katika hatua hii imejengwa kabisa juu ya kazi katika hatua iliyotangulia. Hiyo ndiyo maana ni kazi kama hii tu ndiyo inaweza kumleta mwanadamu katika wokovu hatua kwa hatua. Yesu na Mimi tunatoka kwa Roho mmoja. Ingawa miili Yetu haina uhusiano, Roho Zetu ni moja; ingawa kile Tunachofanya na kazi Tulizo nazo hazifanani, kwa asili Tunafanana; Miili Yetu ina maumbo tofauti, lakini hii ni kwa sababu ya mabadiliko ya enzi na mahitaji tofauti ya kazi Yetu; huduma Zetu hazifanani, hivyo kazi Tunayoileta na tabia Tunayoifichua kwa mwanadamu pia ni tofauti. Ndiyo maana kile ambacho mwanadamu anakiona na kukielewa leo hii si kama kile cha wakati uliopita; ni hivyo kwa sababu ya mabadiliko ya enzi. Ingawa jinsia na maumbo ya miili Yao ni tofauti, na kwamba hawakuzaliwa katika familia moja, sembuse katika kipindi kimoja, hata hivyo Roho Zao ni moja. Ingawa miili Yao haina uhusiano wa damu au kimwili kwa namna yoyote ile, haipingiki kwamba Wao ni Mungu kupata mwili katika vipindi viwili tofauti vya nyakati. Ni ukweli usiopingika kwamba Wao ni miili ya nyama ya Mungu, ingawa hawatoki katika ukoo mmoja na hawatumii lugha moja ya binadamu (mmoja alikuwa mwanamume aliyezungumza lugha ya Wayahudi na mwingine ni mwanamke anayezungumza Kichina pekee). Ni kwa sababu hizi ndiyo Wameishi katika nchi tofauti kufanya kazi ambayo inampasa kila mmoja kufanya, na katika nyakati tofauti vilevile. Licha ya ukweli kwamba Wao ni Roho moja, wakiwa na asili inayofanana, hakuna mfanano wa wazi kabisa kati ya ngozi za nje za miili Yao. Wanashiriki tu ubinadamu sawa, lakini sura ya nje ya miili Yao na kuzaliwa Kwao hakufanani. Mambo haya hayana athari katika kazi Zao au maarifa aliyonayo mwanadamu juu Yao, maana, kimsingi, Wao ni Roho mmoja na hakuna anayeweza kuwatenganisha. Ingawa Hawana uhusiano wa damu, nafsi Zao zote zinaongoza Roho Zao, ambazo zinawapa kazi tofauti katika nyakati tofauti, na miili Yao kwa ukoo tofauti. Roho wa Yehova si baba wa Roho wa Yesu na Roho wa Yesu si mwana wa Roho wa Yehova: Ni Roho mmoja. Kama tu Mungu mwenye mwili wa leo na Yesu. Ingawa Hawahusiani kwa damu, ni Wamoja; hii ni kwa sababu Roho Zao ni moja. Mungu anaweza kufanya kazi ya rehema na wema, vilevile na ile kazi ya hukumu ya haki na kumwadibu mwanadamu, na ile ya kuleta laana kwa mwanadamu; na hatimaye, Anaweza kufanya kazi ya kuuharibu ulimwengu na kuwaadhibu waovu. Je, hafanyi haya yote Mwenyewe? Je, hii si kudura ya Mungu? Aliweza kutangaza sheria kwa ajili ya mwanadamu na kumpa amri, na aliweza pia kuwaongoza Waisraeli wa awali katika kuishi maisha yao duniani na kuwaongoza kujenga hekalu na madhabahu, Akiwatawala Waisraeli wote. Kwa kutegemea mamlaka Yake, Aliishi pamoja na Waisraeli duniani kwa miaka elfu mbili. Waisraeli hawakuthubutu kumwasi; wote walimheshimu Yehova na walifuata amri Zake. Hii ilikuwa Kazi iliyofanywa kwa kutegemea mamlaka Yake na kudura Yake. Kisha, katika Enzi ya Neema, Yesu alikuja kuwakomboa wanadamu wote walioanguka (sio Waisraeli pekee). Alionyesha rehema na wema kwa mwanadamu. Yesu ambaye mwanadamu alimwona katika Enzi ya Neema Alikuwa amejazwa na wema na siku zote Alikuwa mwenye upendo kwa mwanadamu, maana Alikuwa amekuja kuwakomboa wanadamu kutoka dhambini. Aliweza kuwasamehe wanadamu dhambi zao hadi pale ambapo kusulubiwa Kwake kuliwakomboa wanadamu kutoka dhambini kabisa. Wakati huo, Mungu alionekana kwa mwanadamu kwa rehema na wema; yaani, Alijitoa sadaka kwa ajili ya mwanadamu na Alisulubiwa kwa ajili ya dhambi za mwanadamu ili kwamba ziweze kusamehewa milele. Alikuwa mwenye rehema, mwenye huruma, mwenye upendo na mstahimilivu. Na wale wote waliomfuata Yesu katika Enzi ya Neema nao pia walitafuta kuwa wastahimilivu na wenye upendo katika mambo yote. Walistahimili mateso kwa muda mrefu, na hawakuwahi kulipiza kisasi hata walipopigwa, kulaaniwa au kupigwa mawe. Lakini haya hayawezi kuwa hivyo tena katika hatua ya mwisho. Vivyo hivyo, hata ingawa Roho Zao zilikuwa moja, kazi ya Yesu na Yehova hazikufanana kabisa. Kazi ya Yehova haikuwa kwa ajili ya kukamilisha enzi bali kuiongoza, kukaribisha maisha ya wanadamu duniani. Hata hivyo, kazi iliyopo sasa ni kuwashinda wale walio katika nchi ya Mataifa ambao wamepotoshwa sana, na kuongoza sio tu watu waliochaguliwa na Mungu nchini China, bali ulimwengu mzima na wanadamu wote. Inaweza kuonekana kwako kwamba kazi hii inafanywa Uchina pekee, lakini kwa kweli imekwishaanza kusambaa katika nchi za ughaibuni. Ni kwa nini wageni mara kwa mara wanatafuta njia ya kweli? Hiyo ni kwa sababu Roho tayari amekwishaanza kazi, na maneno yanayonenwa sasa yanaelekezwa kwa watu ulimwenguni kote. Kwa hili, nusu ya kazi tayari inaendelea. Kutoka kuumbwa kwa dunia hadi sasa, Roho wa Mungu ameendeleza hii kazi kubwa, na aidha Amefanya kazi tofauti katika enzi tofauti, na katika mataifa tofauti. Watu wa kila enzi wanaiona tabia Yake tofauti, ambayo kwa asili inafichuliwa kupitia kazi tofauti Anazozifanya. Yeye ni Mungu, aliye mwingi wa rehema na wema; Yeye ni sadaka ya dhambi kwa ajili ya mwanadamu na mchungaji wa mwanadamu; lakini pia Yeye ni hukumu, kuadibu, na laana kwa mwanadamu. Angeweza kumwongoza mwanadamu kuishi duniani kwa miaka elfu mbili na pia Angeweza kuwaokoa wanadamu waliopotoka kutoka dhambini. Leo, pia Anaweza kuwashinda wanadamu ambao hawamjui na kuwafanya wawe chini ya miliki Yake, ili kwamba wote wajinyenyekeze kwake kikamilifu. Mwishowe, Atachoma yote ambayo si safi na ambayo ni dhalimu ndani ya wanadamu katika ulimwengu mzima, ili kuwaonyesha kwamba Yeye si Mungu wa Rehema, na upendo tu, si Mungu wa hekima, na maajabu tu, si Mungu mtakatifu tu, bali, hata zaidi ni Mungu anayemhukumu mwanadamu. Kwa waovu miongoni mwa wanadamu, Yeye ni mwenye kuchoma, kuhukumu na kuadhibu; kwa wale ambao wanapaswa kukamilishwa, Yeye ni mateso, usafishaji, na majaribu, na vilevile faraja, ruzuku, utoaji wa maneno, kushughulika na kupogoa. Na kwa wale ambao wanaondolewa, Yeye ni adhabu na vilevile malipo. Niambie, je, Mungu si mweza yote? Ana uwezo wa kufanya kazi yoyote, sio tu kusulubishwa kama mlivyowazia. Unamfikiria Mungu kuwa ni wa chini sana! Je, unaamini kwamba Anachoweza kufanya ni kuwakomboa wanadamu wote kupitia kusulubishwa Kwake na ndivyo hivyo? Na baada ya hayo, utamfuata mbinguni kula tunda kutoka mti wa uzima na kunywa kutoka mto wa uzima? … Je, inaweza kuwa rahisi hivyo? Niambie, umekamilisha nini? Je, una uzima wa Yesu? Ni kweli ulikombolewa naye, lakini kusulubiwa kulikuwa ni kazi ya Yesu Mwenyewe. Ni wajibu gani umeukamilisha kama mwanadamu? Una uchamungu wa nje pekee lakini huielewi njia Yake. Hivyo ndivyo unavyomdhihirisha? Ikiwa hujapata maisha ya Mungu au kuona tabia Yake yote ya haki, basi huwezi kudai kuwa mtu aliye na uzima, na hustahili kupita katika lango la ufalme wa mbinguni.
Mungu si Roho pekee, Anaweza pia kuwa mwili. Aidha, Yeye ni mwili wa utukufu. Yesu, ingawa hamjamwona, alishuhudiwa na Waisraeli, yaani, Wayahudi wa wakati huo. Mwanzoni alikuwa mwili wa nyama, lakini baada ya kusulubiwa, Aligeuka mwili wa utukufu. Yeye ni Roho anayezunguka mambo yote na Anaweza kufanya kazi katika kila mahali. Anaweza kuwa Yehova, au Yesu au Masihi; hatimaye, Anaweza pia kuwa Mwenyezi Mungu. Yeye ni haki, hukumu, na kuadibu; Yeye ni laana na ghadhabu, lakini pia Yeye ni rehema na wema. Kazi zote ambazo Amezifanya zinaweza kumwakilisha. Unasema Yeye ni Mungu ni wa aina gani? Huwezi kuelezea kabisa. Iwapo huwezi kweli kueleza, hufai kufanya mahitimisho kumhusu Mungu. Usihitimishe kwamba Mungu milele ni Mungu wa rehema na wema, kwa sababu tu Yeye alifanya kazi ya ukombozi katika hatua moja. Je, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yeye ni Mungu wa rehema na upendo pekee? Ikiwa Yeye ni Mungu tu wa rehema na mwenye upendo, kwa nini Ataikomesha enzi katika siku za mwisho? Kutokana na fikira na mawazo ya watu Mungu anastahili kuwa mwenye rehema na upendo hadi katika enzi ya mwisho, ili kwamba kila mmoja wa wanadamu aweze kuokolewa. Lakini kwa nini, katika siku za mwisho, ndipo Atatuma chini majanga makubwa kama vile matetemeko ya ardhi, tauni na njaa ili kuwaangamiza wanadamu waovu, wanaomchukulia Mungu kama adui? Kwa nini anamruhusu mwanadamu kuteseka majanga haya? Hakuna yeyote kati wenu anayethubutu kusema Yeye ni Mungu wa aina gani, na hakuna anayeweza kuelezea. Je, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yeye ni Roho? Je, unathubutu kusema kuwa Yeye ni mwili wa Yesu pekee? Na unathubutu kusema kuwa Yeye ni Mungu ambaye milele atasulubiwa kwa ajili ya mwanadamu?
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu