IX. Maneno Juu ya Tofauti Kati ya Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
310. Kazi ya Mungu Mwenyewe inahusisha kazi ya wanadamu wote, na pia inawakilisha kazi ya enzi nzima. Hii ni kusema kwamba, kazi ya Mungu mwenyewe inawakilisha harakati na mwelekeo wa kazi yote ya Roho Mtakatifu, ilhali kazi ya mitume inafuata kazi ya Mungu na wala haiongozi enzi, na wala haiwakilishi mielekeo ya kazi ya Roho Mtakatifu katika enzi nzima. Huwa wanafanya tu kazi ambayo mwanadamu anapaswa kufanya, ambayo haihusishi kabisa kazi ya usimamizi. Kazi ya Mungu Mwenyewe ni mradi uliopo ndani ya kazi ya usimamizi. Kazi ya mwanadamu ni wajibu tu ambao watu wanaotumiwa wanatekeleza, na wala haina uhusiano na kazi ya usimamizi. Licha ya ukweli kwamba zote ni kazi za Roho Mtakatifu, kutokana na utofauti katika utambulisho na uwakilishi wa kazi, kuna tofauti za wazi na muhimu kati ya kazi ya Mungu Mwenyewe na kazi ya mwanadamu. Zaidi ya hayo, kiwango cha kazi inayofanywa na Roho Mtakatifu kwa watu wenye tambulisho tofauti inatofautiana. Hizi ni kanuni na mawanda ya kazi ya Roho Mtakatifu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
311. Kazi ya Mungu mwenye mwili huanzisha enzi mpya, na wale wanaoiendeleza kazi Yake ni watu wanaotumiwa na Yeye. Kazi inayofanywa na mwanadamu yote ipo ndani ya huduma ya Mungu mwenye mwili, na haina uwezo wa kwenda zaidi ya mawanda haya. Ikiwa Mungu mwenye mwili haji kufanya kazi Yake, mwanadamu hana uwezo wa kuhitimisha enzi ya zamani, na hana uwezo wa kuikaribisha enzi mpya. Kazi inayofanywa na mwanadamu ipo tu ndani ya wajibu wake ambao unawezekana kibinadamu, na haiwakilishi kazi ya Mungu. Ni Mungu mwenye mwili pekee ndiye anayeweza kuja na kukamilisha kazi ambayo Anapaswa kuifanya, na mbali na Yeye, hakuna anayeweza kuifanya kazi hii badala Yake. Bila shaka, kile Ninachozungumzia ni kuhusiana na kazi ya kufanyika mwili.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mwanadamu Aliyepotoka Anahitaji Zaidi Wokovu wa Mungu Mwenye Mwili
312. Neno la Mungu haliwezi kuzungumzwa kama neno la mwanadamu, sembuse neno la mwanadamu kuzungumzwa kama neno la Mungu. Mwanadamu anayetumiwa na Mungu siye Mungu mwenye mwili, na Mungu mwenye mwili siye mwanadamu anayetumiwa na Mungu; katika hili, kunayo tofauti kubwa sana. Pengine, baada ya kusoma maneno haya, hukubali kuwa ni maneno ya Mungu, na kuyakubali tu kama maneno ya mwanadamu ambaye amepewa nuru. Ikiwa hivyo, basi umepofushwa na ujinga. Maneno ya Mungu yatawezaje kuwa sawa na maneno ya mwanadamu ambaye amepewa nuru? Maneno ya Mungu mwenye mwili yanaanzisha enzi mpya, yanaongoza wanadamu wote, yanafichua mafumbo, na kumwonyesha mwanadamu mwelekeo mbele katika enzi mpya. Nuru anayoipata mwanadamu ni utendaji au elimu rahisi. Haiwezi kuelekeza binadamu wote kuingia enzi mpya au kufichua fumbo la Mungu Mwenyewe. Mungu, hata hivyo, ni Mungu, na mwanadamu ni mwanadamu. Mungu yuko na dutu ya Mungu, na mwanadamu yuko na dutu ya mwanadamu. Iwapo mwanadamu anachukulia maneno yanayonenwa na Mungu kama kupewa nuru tu na Roho Mtakatifu, na kuchukua maneno yaliyonenwa na mitume na manabii kama maneno yaliyonenwa na Mungu Mwenyewe, basi mwanadamu anakosea. Licha ya haya, hufai kamwe kubadili jambo sahihi liwe baya, ama kuzungumzia lililo juu kama la chini, au kuzungumzia jambo kubwa kama lisilo na kina; haijalishi ni nini, hupaswi kamwe kwa makusudi kupinga lile unalojua kuwa ni ukweli. Kila anayeamini kuwa kuna Mungu anapaswa kufikiri juu ya tatizo hili kwa msimamo ulio sahihi, na anapaswa kukubali kazi Yake mpya na maneno Yake kama kiumbe wa Mungu—la sivyo aondolewe na Mungu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Dibaji
313. Kazi inayotekelezwa na yule anayetumiwa na Mungu ni kwa ajili ya kushirikiana na kazi ya Kristo au Roho Mtakatifu. Mtu huyu anainuliwa na Mungu miongoni mwa wanadamu, yuko pale kuongoza wateule wote wa Mungu, na pia yeye anainuliwa na Mungu ili kufanya kazi ya ushirikiano wa mwanadamu. Na mtu kama huyu, ambaye anaweza kufanya kazi ya ushirikiano wa mwanadamu, matakwa mengi zaidi ya Mungu kwa mwanadamu na kazi ambayo Roho Mtakatifu lazima Afanye miongoni mwa wanadamu inaweza kutimizwa kupitia kwake. Njia nyingine ya kulisema ni hivi: Lengo la Mungu katika kumtumia mtu huyu ni ili wote wanaomfuata Mungu waweze kuelewa bora mapenzi ya Mungu, na waweze kufikia matakwa zaidi ya Mungu. Kwa vile watu hawawezi kuyaelewa maneno ya Mungu na mapenzi ya Mungu moja kwa moja, Mungu amemuinua mtu fulani ambaye anatumiwa kutekeleza kazi kama hiyo. Mtu huyu anayetumiwa na Mungu anaweza kuelezwa kama chombo ambacho Mungu hutumia kuwaongoza watu, kama “mfasiri” anayewasiliana kati ya Mungu na watu. Hivyo, mtu kama huyo hayuko kama yeyote kati ya wale wanaofanya kazi katika nyumba ya Mungu au ambao ni mitume Wake. Kama wao, anaweza kusemekana kuwa mtu anayemhudumia Mungu, lakini katika kiini cha kazi yake na usuli wa kutumiwa kwake na Mungu anatofautiana sana na wafanyakazi wengine na mitume. Kuhusu kiini cha kazi yake na usuli wa kutumiwa kwake, mwanadamu anayetumiwa na Mungu huinuliwa na Yeye, hutayarishwa na Mungu kwa kazi ya Mungu, na yeye hushirikiana katika kazi ya Mungu Mwenyewe. Hakuna mtu anayeweza kufanya kazi yake badala yake—huu ni ushirikiano wa mwanadamu ambao ni wa lazima pamoja na kazi takatifu. Kazi inayofanywa na wafanyakazi wengine au mitume, wakati huo huo, ni uwasilishaji na utekelezaji wa vipengele vingi vya mipango ya makanisa katika kila kipindi, au sivyo ni kazi ya utoaji fulani rahisi wa maisha ili kudumisha maisha ya kanisa. Wafanyakazi hawa na mitume hawateuliwi na Mungu, seuze kuweza kuitwa wale wanaotumiwa na Roho Mtakatifu. Wao huchaguliwa kutoka miongoni mwa makanisa na, baada ya kufunzwa na kukuzwa kwa kipindi cha wakati, wale wanaofaa hubaki, huku wale wasiofaa hurudishwa walikotoka. Kwa vile watu hawa huchaguliwa kutoka miongoni mwa makanisa, wengine huonyesha tabia zao halisi baada ya kuwa viongozi, na wengine hata hufanya mambo mengi mabaya na huishia kufutwa. Mtu anayetumiwa na Mungu, kwa upande mwingine, ni mtu ambaye ametayarishwa na Mungu, na aliye na ubora fulani wa tabia, na ana ubinadamu. Ametayarishwa na kukamilishwa mapema na Roho Mtakatifu, na anaongozwa kabisa na Roho Mtakatifu, na, inapofikia kazi yake hasa, yeye huongozwa na kuamriwa na Roho Mtakatifu—kutokana na hilo hakuna mkengeuko katika njia ya kuwaongoza wateule wa Mungu, kwani Mungu kwa hakika huwajibikia kazi Yake mwenyewe, na Mungu hufanya kazi Yake nyakati zote.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kuhusu Mungu Kumtumia Mwanadamu
314. Kama, katika kupata mwili, Mungu anafanya kazi ya uungu tu bila kuwa na wanadamu wachache wa ziada wanaopendeza moyo Wake kushirikiana na Yeye, basi mwanadamu hangekuwa na uwezo kabisa wa kuelewa mapenzi ya Mungu au kuwasiliana na Mungu. Mungu lazima atumie wanadamu wa kawaida wanaopendeza moyo Wake ili kukamilisha kazi hii, kutunza na kuchunga makanisa, ili kufikia kiwango ambapo mchakato wa ufahamu wa mwanadamu, ubongo wake unaweza kubuni. Kwa maneno mengine, Mungu anatumia wanadamu wachache wanaopendeza moyo wake “kutafsiri” kazi anayofanya katika uungu Wake, ili iweze kufunuliwa, yaani, kubadilisha lugha ya Mungu kuwa lugha ya binadamu, hivyo kwamba wanadamu wote waweze kuielewa, wote waifahamu. Kama Mungu hangefanya hivyo, hakuna mwanadamu angeweza kuelewa lugha takatifu ya Mungu, kwa sababu idadi ya wanadamu wanaoupendeza moyo wa Mungu, ni chache mno, na uwezo wa mwanadamu kufahamu ni dhaifu. Hiyo ndiyo maana Mungu hutumia njia hii wakati wa kufanya kazi katika mwili wa nyama. Kama kungekuwa na kazi ya uungu peke yake, mwanadamu hangeweza kabisa kujua au kuwasiliana na Mungu, kwa sababu mwanadamu haelewi lugha ya Mungu. Mwanadamu anaweza kuelewa lugha hii tu kupitia tu kwa nguvu ya wanadamu wanaopendeza moyo wa Mungu kufafanua maneno Yake. Hata hivyo, kama kungekuwa na wanadamu kama hao pekee wakifanya kazi katika ubinadamu, hilo lingeweza tu kudumisha maisha ya kawaida ya mwanadamu; lisingeweza kubadilisha tabia ya mwanadamu. Kazi ya Mungu basi haingekuwa na mwanzo mpya; kungekuwa tu na nyimbo zile zile za zamani, maelezo yale yale ya kawaida ya zamani. Ni kupitia kwa nguvu ya Mungu mwenye mwili pekee, Anayesema yote yanayohitajika kusemwa na kufanya yote ambayo yanafaa kufanywa katika kipindi cha Yeye kupata mwili, ambapo baadaye watu hufanya kazi na kupata uzoefu kulingana na maneno Yake, ndipo tabia ya maisha yao itaweza kubadilika na waweze kusonga na nyakati. Yeye ambaye Anafanya kazi katika uungu Anawakilisha Mungu, ilhali wale wanaofanya kazi katika ubinadamu ni wanadamu wanaotumiwa na Mungu. Yaani, Mungu mwenye mwili ana tofauti kubwa na wanadamu wanaotumiwa na Mungu. Mungu mwenye mwili Anaweza kufanya kazi ya uungu, lakini wanadamu wanaotumiwa na Mungu hawawezi. Mwanzoni mwa kila enzi, Roho wa Mungu huongea binafsi kuzindua enzi mpya na kuleta mwanadamu kwenye mwanzo mpya. Wakati Yeye Amemaliza kuongea, hili linaashiria kwamba kazi ya Mungu katika uungu Wake imekamilika. Baada ya hapo, wanadamu wote hufuata mwongozo wa wale ambao wametumiwa na Mungu kuingia katika uzoefu wa maisha. Vile vile, hii pia ni enzi ambapo Mungu huleta mwanadamu katika enzi mpya na Anampa kila mwanadamu mwanzo mpya. Kwa hilo, kazi ya Mungu katika mwili inahitimishwa.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Tofauti Muhimu Kati ya Mungu Mwenye Mwili na Watu Wanaotumiwa na Mungu
315. Hata mwanadamu anayetumiwa na Roho Mtakatifu hawezi kumwakilisha Mungu Mwenyewe. Na mwanadamu huyu hawezi tu kumwakilisha Mungu bali pia kazi yake haiwezi kumwakilisha Mungu moja kwa moja. Kwa maneno mengine, uzoefu wa mwanadamu hauwezi kuwekwa moja kwa moja ndani ya usimamizi wa Mungu, na hauwezi kuwakilisha usimamizi wa Mungu. Kazi yote ambayo Mungu Mwenyewe hufanya ni kazi Anayolenga Kufanya katika mpango Wake wa usimamizi na inahusiana na usimamizi mkuu. Kazi ifanywayo na mwanadamu (mwanadamu anayetumiwa na Roho Mtakatifu) hukidhi uzoefu wake binafsi. Anapata njia mpya ya uzoefu mbali na ile iliyotembelewa na wale waliomtangulia na anawaongoza ndugu zake chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu. Kinachotolewa na watu hawa ni uzoefu wao ama maandishi ya kiroho ya watu wa kiroho. Ingawa wanatumiwa na Roho Mtakatifu, kazi ya watu kama hao haina uhusiano na kazi ya usimamizi mkuu katika mpango wa miaka elfu sita. Wamesimamishwa na Roho Mtakatifu katika wakati tofauti kuongoza watu katika mkondo wa Roho Mtakatifu hadi wakamilishe kazi yao ama maisha yao yafike mwisho. Kazi wanayofanya ni kutayarisha njia ifaayo kwa ajili ya Mungu Mwenyewe ama kuendeleza kitu kimoja kwa usimamizi wa Mungu Mwenyewe katika dunia. Watu hao hawawezi kufanya kazi kuu katika usimamizi Wake, na hawawezi kufungua njia mpya, ama kumaliza kazi yote ya Mungu kutoka enzi ya kitambo. Kwa hivyo, kazi wafanyayo inawakilisha kiumbe aliyeumbwa pekee akifanya kazi Yake na hawezi kuwakilisha Mungu Mwenyewe Akifanya huduma Yake. Hii ni kwa sababu kazi wanayofanya haifanani na ile inayofanywa na Mungu Mwenyewe. Kazi ya kukaribisha enzi mpya haiwezi kufanywa na mwanadamu kwa niaba ya Mungu. Haiwezi kufanywa na mwingine ila Mungu Mwenyewe. Kazi yote inayofanywa na mwanadamu ni kufanya wajibu wake kama mmoja wa viumbe na inafanywa akiguswa au kupewa nuru na Roho Mtakatifu. Mwongozo ambao watu hawa hutoa unajumuisha kabisa kumwonyesha mwanadamu njia ya utendaji katika maisha ya kila siku na jinsi anavyopaswa kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu. Kazi ya mwanadamu haihusishi usimamizi wa Mungu ama kuwakilisha kazi ya Roho. Kama mfano, kazi ya Witness Lee na Watchman Nee ilikuwa ni kuongoza njia. Njia iwe mpya au nzee, kazi ilifanywa kwa misingi ya kanuni ya kutozidi Biblia. Haijalishi kama makanisa ya mitaa yalirejeshwa yalivyokuwa awali au yalijengwa, kazi yao ilikuwa ni kuanzisha makanisa. Kazi waliyofanya iliendeleza kazi ambayo Yesu Kristo na mitume Wake walikuwa hawajamaliza au kuendeleza zaidi kwenye Enzi ya Neema. Kile walichofanya katika kazi yao kilikuwa ni kurejesha kile ambacho Yesu Kristo Alikuwa Ameomba katika kazi Yake ya vizazi vitakavyokuja baada Yake Yeye, kama vile kufunika vichwa vyao, kupokea ubatizo, umegaji mkate, au unywaji divai. Inaweza kusemekana kwamba kazi yao ilikuwa kubakia tu kwenye Biblia na kutafuta njia zinazotokana tu na Biblia. Hawakupiga hatua yoyote mpya kamwe. … kwa sababu kazi ya wanadamu wanaotumiwa na Roho Mtakatifu si sawa na kazi ifanywayo na Mungu Mwenyewe, utambulisho wao na wanayefanya kazi kwa niaba yake ni tofauti. Hii ni kwa sababu kazi ambayo Roho Mtakatifu Analenga Kufanya ni tofauti, na hapo kutoa utambulisho tofauti na hadhi kwa wale wote wafanyao kazi. Wanadamu wanaotumiwa na Roho Mtakatifu wanaweza pia kufanya kazi fulani ambayo ni mpya na wanaweza pia kuondoa kazi fulani iliyofanywa katika enzi iliyopita, lakini wanachofanya hakiwezi kueleza tabia na mapenzi ya Mungu katika enzi mpya. Wanafanya kazi ili kuondoa kazi ya enzi iliyopita tu, sio kufanya kazi mpya kuwakilisha moja kwa moja tabia ya Mungu Mwenyewe. Hivyo, haijalishi matendo mangapi yaliyopitwa na wakati wanakomesha ama matendo mapya wanaanzisha, bado wanawakilisha mwanadamu na viumbe vilivyoumbwa. Mungu Mwenyewe Akifanya kazi, hata hivyo, Hatangazi wazi kukomeshwa kwa matendo ya enzi ya zamani au kutangaza moja kwa moja kuanzishwa kwa enzi mpya. Yeye hufanya kazi Yake moja kwa moja na kwa njia ya moja kwa moja. Yeye hufanya kazi Anayolenga kufanya moja kwa moja; hivyo, yeye hueleza moja kwa moja kazi Aliyoleta, Anafanya kazi Yake moja kwa moja Alivyokusudia hapo awali, Akionyesha nafsi na tabia Yake. Jinsi mwanadamu anavyoiona, tabia Yake na vivyo hivyo kazi Yake hutofautiana na zile za enzi zilizopita. Hata hivyo, kutoka kwa mtazamo wa Mungu Mwenyewe, huu ni mwendelezo tu na maendeleo zaidi ya kazi Yake. Mungu Mwenyewe Akifanya kazi, Anaeleza neno Lake na Analeta kazi mpya moja kwa moja. Tofauti ni, mwanadamu akifanya kazi, ni kwa ukombozi na kusoma, ama ni kwa maendeleo ya maarifa na mpangilio wa mazoezi iliyojengwa juu ya msingi wa kazi za wengine. Hiyo ni kusema, kiini cha kazi inayofanywa na mwanadamu ni kufuata utaratibu uliowekwa na “kutembea njia za zamani kwa viatu vipya.” Hii ina maana kwamba hata njia wanayotembea wanadamu wanaotumiwa na Roho Mtakatifu imejengwa juu ya ile iliyofunguliwa na Mungu mwenyewe. Kwa hivyo, yote yanaposemwa na kufanywa, mwanadamu angali mwanadamu, na Mungu angali Mungu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (1)
316. Wakati wa Enzi ya Neema, Yesu alinena baadhi ya maneno na kutekeleza hatua moja ya kazi. Yote yalikuwa na muktadha, na yote yalikuwa ya kufaa kwa hali za watu wa wakati huo; Yesu alinena na kufanya kazi kama ilivyostahili muktadha wa wakati huo. Pia Alinena unabii kiasi. Alitabiri kwamba Roho wa ukweli angekuja katika siku za mwisho na angetekeleza hatua fulani ya kazi. Ambayo ni kusema, Hakuelewa chochote zaidi ya kazi ambayo Yeye Mwenyewe alipaswa kufanya wakati wa enzi hiyo; kwa maneno mengine, kazi iliyoletwa na Mungu mwenye mwili ni yenye mipaka. Hivyo, Yeye hufanya tu kazi ya enzi ambayo Yeye yumo na Hafanyi kazi nyingine ambayo haihusiani na Yeye. Wakati huo, Yesu hakufanya kazi kulingana na hisia au maono, bali ilivyostahili wakati na muktadha. Hakuna aliyemwongoza au kumwelekeza Yeye. Kazi Yake nzima ilikuwa nafsi Yake—ilikuwa ni kazi iliyopaswa kutekelezwa na Roho wa Mungu mwenye mwili, ambayo ilikuwa kazi yote iliyokaribishwa na kupata mwili. Yesu alifanya kazi tu kulingana na kile ambacho Yeye Mwenyewe aliona na kusikia. Kwa maneno mengine, Roho alifanya kazi moja kwa moja; hakukuwa na haja ya wajumbe kumwonekania na kumpa ndoto, wala kwa nuru yoyote kubwa kumwangazia na kumkubalia Aone. Alifanya kazi kwa uhuru na bila vizuizi, ambayo ilikuwa kwa sababu kazi Yake haikutegemea hisia. Kwa maneno mengine, Alipofanya kazi, Hakutafuta kwa kupapasa na kubahatisha, lakini Alitimiza mambo kwa urahisi, Akifanya kazi na kunena kulingana na mawazo Yake mwenyewe na kile Alichoona kwa macho Yake mwenyewe, Akitoa riziki ya papo hapo kwa kila mwanafunzi aliyemfuata Yeye. Hii ndiyo tofauti kati ya kazi ya Mungu na kazi ya watu: Watu wanapofanya kazi, wao hutafuta na kupapasa huku na kule, kila mara wakiiga na kufikiria sana kwa kutegemea msingi uliowekwa na wengine ili kutimiza kuingia kwa ndani zaidi. Kazi ya Mungu ni utoaji wa kile Alicho, na Yeye hufanya kazi ambayo Yeye Mwenyewe anapaswa kufanya. Hatoi riziki kwa kanisa kwa kutumia ufahamu kutoka katika kazi ya mwanadamu yeyote. Badala yake, Yeye hufanya kazi ya sasa kwa kutegemea hali za watu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Utendaji (5)
317. Kazi ya mwanadamu inawakilisha uzoefu wake na ubinadamu wake. Kile ambacho mwanadamu anatoa na kazi ambayo anafanya vinamwakilisha yeye. Kuona kwa mwanadamu, kufikiri kwa mwanadamu, mantiki ya mwanadamu na uwezo wake mkubwa wa kufikiri vyote vinajumuishwa katika kazi yake. Kimsingi, uzoefu wa mwanadamu, unaweza zaidi kuwakilisha kazi yake na kile ambacho mtu amekipitia kitakuwa ni sehemu ya kazi yake. Kazi ya mwanadamu inaweza kuonyesha uzoefu wake. Pale ambapo baadhi ya watu wanapitia hali ya kukaa tu bila kujishughulisha, sehemu kubwa ya ushirika wao inakuwa na vipengele vya uhasi. Kama uzoefu wao kwa kipindi cha muda ni mzuri na wanapita katika njia ya upande mzuri, kile wanachoshiriki kinatia moyo sana, na watu wanaweza kupokea mambo mazuri kutoka kwao. Mfanyakazi akiwa katika hali ya kukaa tu kwa kipindi cha muda, ushirika wake siku zote utakuwa na vipengele vya uhasi. Ushirika wa aina hii ni wa kuvunja moyo, na wengine watavunjika mioyo bila kujua kwa kufuata ushirika wa yule mfanyakazi. Hali ya wafuasi inabadilika kutegemea na hali ya kiongozi. Vile ambavyo mfanyakazi alivyo ndani, ndicho kile anachoonyesha, na kazi ya Roho Mtakatifu mara nyingi inabadilika kulingana na hali ya mwanadamu. Anafanya kazi kulingana na uzoefu wa mwanadamu na wala hamshurutishi mwanadamu, bali Anaweka mahitaji kwa mwanadamu kulingana na njia ya kawaida ya uzoefu wake. Hii ni kusema kwamba ushirika wa mwanadamu unatofautiana na neno la Mungu. Kile ambacho mwanadamu hushiriki kinahusisha kile alichoona binafsi na uzoefu wake, kinaonyesha kile walichokiona na kupata uzoefu kwa msingi wa kazi ya Mungu. Wajibu wao ni kutafuta, baada ya Mungu kufanya kazi au kuzungumza, kile wanachopaswa kufanya au kuingia ndani yake, halafu kukiwasilisha kwa wafuasi. Hivyo, kazi ya mwanadamu inawakilisha kuingia au matendo yake. Bila shaka, kazi hiyo imechanganyika na masomo ya kibinadamu na uzoefu au mawazo ya kibinadamu. Haijalishi namna ambavyo Roho Mtakatifu anafanya kazi, iwe Anafanya kazi kwa mwanadamu au kwa Mungu mwenye mwili, siku zote wafanyakazi ndio wanaoonyesha vile walivyo. Ingawa ni Roho Mtakatifu ambaye hufanya kazi, kazi hiyo imejengwa katika msingi wa mwanadamu alivyo kiasili, kwa sababu Roho Mtakatifu hafanyi kazi bila msingi. Kwa maneno mengine, kazi haifanyiki pasipokuwa na kitu, lakini siku zote hufanyika kulingana na mazingira halisi na hali halisi. Ni kwa njia hii pekee ndiyo tabia ya mwanadamu inaweza kubadilishwa, kwamba mitazamo yake ya zamani na mawazo yake ya zamani yanaweza kubadilishwa. Kile ambacho mwanadamu huonyesha ni kile anachokiona, anachopitia, na anachoweza kufikiria. Hata kama ni mafundisho au dhana, haya yote yanaweza kufikiwa na fikira za mwanadamu. Bila kujali ukubwa wa kazi ya mwanadamu, haiwezi kuzidi mawanda ya uzoefu wa mwanadamu, kile ambacho mwanadamu huona, au kile ambacho mwanadamu anaweza kukitafakari au kukiingiza akilini mwake. Kile ambacho Mungu anaonyesha ni vile ambavyo Mungu Mwenyewe alivyo, na hii ipo nje ya uwezo wa mwanadamu, yaani, nje ya uwezo wa kufikiri kwa mwanadamu. Anaonyesha kazi Yake ya kuwaongoza wanadamu wote, na hii haihusiani na undani wa uzoefu wa mwanadamu, badala yake inahusu usimamizi Wake. Mwanadamu anaonyesha uzoefu wake wakati Mungu anaonyesha nafsi Yake—nafsi hii ni tabia Yake ya asili na iko nje ya uwezo wa mwanadamu. Uzoefu wa mwanadamu ni kuona kwake na kupata maarifa kwa msingi wa maonyesho ya Mungu ya nafsi Yake. Kuona kama huko na maarifa kama hayo yanaitwa nafsi ya mwanadamu. Yanaonyeshwa kwa msingi wa tabia ya asili ya mwanadamu na ubora wa tabia yake halisi; hivyo pia vinaitwa nafsi ya mwanadamu. Mwanadamu anaweza kushiriki kile anachokipitia na kukiona. Kile ambacho hajawahi kukipitia au kukiona au akili yake haiwezi kukifikia, yaani, vitu ambavyo havipo ndani yake, hawezi kuvishiriki. Ikiwa kile ambacho mwanadamu anakionyesha sio uzoefu wake, basi ni mawazo yake au mafundisho ya kidini. Kwa ufupi, hakuna ukweli wowote katika maneno yake. Kama hujawahi kukutana na maswala ya kijamii, hutaweza kushiriki kwa uwazi kuhusu mahusiano tata katika jamii. Kama huna familia na watu wengine wanazungumza juu ya masuala ya familia, huwezi kuelewa kwa kiasi kikubwa kuhusu kile walichokuwa wakizungumzia. Kwa hivyo, kile ambacho mwanadamu anashiriki na kazi anayofanya vinawakilisha nafsi yake ya ndani.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
318. Usemi Wangu unawakilisha nafsi Yangu, lakini kile Ninachokisema kiko nje ya uwezo wa mwanadamu. Kile Ninachosema sio kile ambacho mwanadamu anakipitia, na sio kitu ambacho mwanadamu anaweza kukiona, pia si kitu ambacho mwanadamu anaweza kukigusa, lakini ndicho Nilicho. Baadhi ya watu wanakiri tu kwamba kile Ninachoshiriki ndicho kile Nilichopitia, lakini hawatambui kwamba ni maonyesho ya moja kwa moja ya Roho. Ni kweli, kile Ninachokisema ndicho kile Nilichokipitia. Ni Mimi ndiye Niliyefanya kazi ya usimamizi kwa kipindi cha zaidi ya miaka elfu sita. Nimepitia kila kitu kuanzia mwanzo wa uumbaji wa mwanadamu hadi leo; Nitashindwaje kuvizungumzia? Inapokuja kwa suala la asili ya mwanadamu, Nimeiona waziwazi, na Nimeiangalia toka zamani; sasa Nitashindwaje kuiongelea? Kwa kuwa Nimeiona asili ya mwanadamu kwa uwazi, Nina sifa za kumwadibu mwanadamu na kumhukumu, kwa sababu wanadamu wote wametoka Kwangu lakini wameharibiwa na Shetani. Kwa kweli, Nimehitimu kutathmini kazi ambayo Nimeifanya. Ingawa kazi hii haijafanywa na mwili Wangu, ni uonyeshaji wa moja kwa moja wa Roho, na hiki ndicho Nilicho nacho na kile Nilicho. Kwa hivyo, Nina sifa za kuonyesha na kufanya kazi ambayo Napaswa kufanya. Kile ambacho mwanadamu anakisema ni kile alichokipitia. Ni kile ambacho wamekiona, kile ambacho akili zao zinaweza kukifikia, na kile ambacho milango yao ya fahamu inaweza kuhisi. Hicho ndicho wanachoweza kukifanyia ushirika. Maneno yaliyosemwa na mwili wa Mungu ni onyesho la moja kwa moja la Roho na huonyesha kazi ambayo imefanywa na Roho. Mwili haujaipitia au kuiona, lakini bado unaonyesha nafsi Yake kwa sababu kiini cha mwili ni Roho, na huonyesha kazi ya Roho. Ingawa mwili hauwezi kuifikia, ni kazi ambayo tayari imefanywa na Roho. Baada ya kupata mwili, kupitia maonyesho ya mwili, Anawasaidia watu kujua nafsi ya Mungu na kuwafanya watu waione tabia ya Mungu na kazi ambayo Ameifanya. Kazi ya mwanadamu inawawezesha watu kuelewa kwa uwazi kuhusu kile wanachopaswa kuingia ndani yake na kile wanachopaswa kuelewa; inahusisha kuwaongoza watu kupata ufahamu na kuujua ukweli. Kazi ya mwanadamu ni kuwaendeleza watu; kazi ya Mungu ni kufungua njia mpya na kufungua enzi mpya kwa ajili ya binadamu, na kuwafunulia watu kile ambacho hakijafahamika kwa watu wenye mwili wa kufa, ikiwasaidia kuelewa tabia Yake. Kazi ya Mungu ni kuwaongoza wanadamu wote.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
319. Kazi ya Roho Mtakatifu inakusudiwa kuwasaidia watu kunufaika; inakusudiwa kuwaadilisha watu; hakuna kazi ambayo haiwanufaishi watu. Haijalishi kama ukweli ni wa kina au wa juu juu, na haijalishi ubora wa tabia wa wale wanaopokea ukweli huo ulivyo, chochote ambacho Roho Mtakatifu anafanya, yote hayo huwanufaisha watu. Lakini kazi ya Roho Mtakatifu haiwezi kufanywa moja kwa moja; ni lazima idhihirishwe kupitia kwa wanadamu wanaoshirikiana na Yeye. Ni kwa njia hii pekee ndiyo matokeo ya kazi ya Roho Mtakatifu yanaweza kupatikana. Bila shaka, inapokuwa ni kazi ya moja kwa moja ya Roho Mtakatifu, haijachanganywa na kitu chochote kabisa; lakini Roho Mtakatifu anapomtumia mwanadamu kama chombo, inakuwa imechanganywa sana na sio kazi halisi ya Roho Mtakatifu. Kwa njia hii, ukweli hubadilika katika viwango tofauti. Wafuasi hawapokei nia halisi ya Roho Mtakatifu bali wanapokea mchanganyiko wa kazi ya Roho Mtakatifu na uzoefu na maarifa ya mwanadamu. Sehemu ya kazi ya Roho Mtakatifu inayopokelewa na wafuasi ni sahihi. Uzoefu na maarifa ya mwanadamu yanayopokewa yanatofautiana kwa sababu wafanyakazi ni tofauti. Wafanyakazi wanapokuwa na nuru na uongozi wa Roho Mtakatifu, wanakuwa wanapata uzoefu kulingana na nuru na uongozi huu. Ndani ya uzoefu huu kunachanganyika akili ya mwanadamu na uzoefu, vile vile nafsi ya wanadamu, ambapo wanapata maarifa na kuona vile walivyopaswa kuona. Hii ndiyo njia ya kutenda baada ya mwanadamu kuujua ukweli. Njia hii ya kutenda siku zote haifanani kwa sababu watu wana uzoefu tofauti na vitu ambavyo watu wanavipitia ni tofauti. Kwa njia hii, nuru ile ile ya Roho Mtakatifu inaleta maarifa tofauti na utendaji kwa sababu wale wanaopokea nuru hiyo ni tofauti. Baadhi ya watu hufanya makosa madogo wakati wa utendaji ilhali wengine hufanya makosa makubwa, na baadhi hawafanyi chochote ila ni makosa tu. Hii ni kwa sababu uwezo wa kuelewa mambo unatofautiana na kwa sababu ubora wa tabia zao halisi pia unatofautiana. Baadhi ya watu wanaelewa hivi baada ya kuusikia ujumbe, na baadhi ya watu wanaelewa vile baada ya kuusikia ukweli. Baadhi ya watu wanapotoka kidogo; na baadhi hawaelewi kabisa maana ya ukweli. Kwa hiyo, vyovyote vile mtu anavyoelewa ndivyo atakavyowaongoza wengine; hii ni kweli kabisa, kwa sababu kazi yake inaonyesha tu nafsi yake. Watu wanaoongozwa na watu wenye ufahamu sahihi wa ukweli pia watakuwa na ufahamu sahihi wa ukweli. Hata kama kuna watu ambao uelewa wao una makosa, ni wachache sana, na sio watu wote watakuwa na makosa. Ikiwa mtu ana uelewa wa kipuuzi wa ukweli, wale wanaomfuata bila shaka pia watapotoshwa, na watu hawa watakuwa na makosa kwa kila maana ya neno. Kiwango cha kuuelewa ukweli miongoni mwa wafuasi kinategemea kwa kiasi kikubwa wafanyakazi. Bila shaka, ukweli kutoka kwa Mungu ni sahihi na hauna makosa, na ni hakika. Lakini, wafanyakazi hawako sahihi kabisa na hatuwezi kusema kwamba ni wa kutegemewa kabisa. Ikiwa wafanyakazi wana njia ya kuuweka ukweli katika vitendo, basi wafuasi pia watakuwa na njia ya kuutenda. Ikiwa wafanyakazi hawawezi kuuweka ukweli katika vitendo bali wanashikilia mafundisho tu, wafuasi hawatakuwa na uhalisia wowote. Ubora wa tabia na asili ya wafuasi inaamuliwa na kuzaliwa na haihusiani na wafanyakazi. Lakini kiwango ambacho wafuasi wanauelewa ukweli na kumfahamu Mungu inategemeana na wafanyakazi (hii ni kwa baadhi ya watu tu). Vyovyote vile alivyo mfanyakazi, hivyo ndivyo wafuasi anaowaongoza watakavyokuwa. Kile ambacho mfanyakazi anakionyesha ni vile alivyo mwenyewe, bila kuacha chochote. Yale anayowaambia wafuasi wake wafanye ni yale ambayo yeye mwenyewe yuko tayari kuyatimiza au yale anayoweza kuyafikia. Wafanyakazi wengi huweka mahitaji kwa wafuasi wao kulingana na kile ambacho wao wenyewe wanafanya, licha ya kuwa kuna mengi ambayo watu hawawezi kuyafikia kabisa—kile ambacho watu hawawezi kufanikisha kinakuwa kizuizi katika kuingia kwao.
Kuna upotoshaji mdogo zaidi katika kazi za wale ambao wamepitia kupogolewa, kushughulikiwa, kuhukumiwa na kuadhibiwa, na maonyesho ya kazi zao ni sahihi zaidi. Wale wanaotegemea asili zao katika kufanya kazi wanafanya makosa makubwa sana. Kazi za watu ambao hawajakamilishwa zinadhihirisha kiasi kikubwa cha asili zao wenyewe, kitu ambacho kinaweka kizuizi kikubwa katika kazi ya Roho Mtakatifu. Bila kujali jinsi ubora wa tabia ya mtu ulivyo mzuri, lazima pia apitie upogoaji, ashughulikiwe, na kuhukumiwa kabla ya kuweza kufanya kazi ya agizo la Mungu. Kama hawajapitia hukumu kama hiyo, haijalishi jinsi wanavyoifanya vizuri, haiwezi kupatana na kanuni za ukweli na daima ni zao la asili yao wenyewe na wema wa kibinadamu. Kazi za wale ambao wamepitia kupogolewa, kushughulikiwa, na kuhukumiwa ni sahihi zaidi kuliko kazi za wale ambao hawajapogolewa, kushughulikiwa, na kuhukumiwa. Wale ambao hawajapitia hukumu hawaonyeshi chochote isipokuwa mawazo ya kibinadamu, yakiwa yamechanganyika na ufahamu wa kibinadamu na talanta za ndani. Haya si maonyesho sahihi ya mwanadamu kwa kazi ya Mungu. Wale watu wanaowafuata wanaletwa mbele yao kwa tabia zao za asili. Kwa sababu wanaonyesha vitu vingi vyenye ufahamu na uzoefu wa mwanadamu, ambavyo karibia vimetenganishwa na nia ya asili ya Mungu, na hutofautiana sana nayo, kazi ya mtu wa aina hii haiwezi kuwaleta watu mbele za Mungu, bali inawaleta mbele ya mwanadamu. Kwa hivyo, wale ambao hawajapitia hukumu na kuadibu, hawana sifa za kufanya kazi ya agizo la Mungu. … Ikiwa mwanadamu hajakamilishwa na tabia yake potovu haijapogolewa na kushughulikiwa, kutakuwa na pengo kubwa kati ya kile anachokionyesha na ukweli; anachoonyesha kitachanganywa na mambo yasiyoeleweka, kama vile mawazo yake na uzoefu wa upande mmoja, na kadhalika. Aidha, bila kujali jinsi anavyofanya kazi, watu wanahisi kwamba hakuna lengo la jumla na hakuna ukweli ambao unafaa kwa kuingia kwa watu wote. Matakwa mengi yanawekwa kwa watu wakitakiwa kufanya kile ambacho ni nje ya uwezo wao, kama vile kumfanya bata asimame juu ya tawi jembamba ambalo ndege wanatulia. Hii ni kazi ya matakwa ya binadamu. Tabia potovu ya mwanadamu, mawazo yake na fikira zinaenea katika sehemu zote za mwili wake. Mwanadamu hakuzaliwa na tabia ya kutenda ukweli, na wala hana tabia ya kuuelewa ukweli moja kwa moja. Ikiongezewa na tabia hio potovu ya mwanadamu—mtu wa aina hii anapofanya kazi, je, haisababishi matatizo? Lakini mwanadamu ambaye amekamilishwa ana uzoefu wa ukweli ambao watu wanapaswa kuuelewa, na maarifa ya tabia yao potovu, ili kwamba vitu visivyoeleweka vizuri na visivyokuwa halisi katika kazi yake vipungue taratibu, uchafu wa binadamu upungue, na kazi na huduma yake ikaribie zaidi viwango vinavyohitajika na Mungu. Kwa njia hiyo, kazi yake imeingia katika uhalisi wa ukweli na pia imekuwa halisi zaidi. Mawazo katika akili ya mwanadamu yanazuia kazi ya Roho Mtakatifu. Mwanadamu ana mawazo mengi na mantiki za kuridhisha, na amekuwa na uzoefu wa muda mrefu wa kushughulikia mambo. Kama haya yote hayatapitia kupogolewa na kusahihishwa, yote yanakuwa vizuizi katika kazi. Hivyo kazi ya mwanadamu haiwezi kufikia kiwango cha juu cha usahihi, hususan kazi ya watu ambao hawajakamilishwa.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
320. Kazi ya mwanadamu ina upeo mdogo na ina mipaka. Mtu mmoja anaweza tu kufanya kazi ya wakati fulani na hawezi kufanya kazi ya enzi nzima—vinginevyo, angewaongoza watu katika kanuni. Kazi ya mwanadamu inaweza kufaa tu katika kipindi au awamu fulani. Hii ni kwa sababu uzoefu wa mwanadamu una upeo wake. Mtu hawezi kulinganisha kazi ya mwanadamu na kazi ya Mungu. Njia za utendaji wa mwanadamu na maarifa yake ya ukweli yote yanatumika tu katika mawanda fulani. Huwezi kusema kwamba njia ambayo mwanadamu anaiendea ni matakwa ya Roho Mtakatifu kabisa, kwa sababu mwanadamu anaweza kupewa nuru na Roho Mtakatifu tu na hawezi kujazwa kikamilifu na Roho Mtakatifu. Vitu ambavyo mwanadamu anaweza kuvipitia vyote vipo ndani ya mawanda ya ubinadamu na haviwezi kuzidi kiwango cha fikira zilizopo katika akili ya kawaida ya mwanadamu. Wale wote wanaoweza kuishi kwa kudhihirisha uhalisi wa ukweli hupitia ndani ya mawanda haya. Wanapoupitia ukweli, siku zote ni uzoefu wa maisha ya kawaida ya mwanadamu chini ya nuru ya Roho Mtakatifu, sio kupitia uzoefu kwa namna ambayo inakwenda nje ya maisha ya kawaida ya mwanadamu. Wanapitia uzoefu wa ukweli ambao unatiwa nuru na Roho Mtakatifu katika msingi wa kuishi maisha yao ya kibinadamu. Aidha, ukweli huu unatofautiana kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine, na kina chake kinahusiana na hali ya mtu huyo. Mtu anaweza kusema kwamba njia anayoipitia ni maisha ya kawaida ya kibinadamu ya mtu ambaye anafuatilia ukweli, na inaweza kuitwa njia inayotembewa na mtu wa kawaida ambaye amepata nuru ya Roho Mtakatifu. Huwezi kusema kwamba njia wanayoipitia ni njia ambayo inafuatwa na Roho Mtakatifu. Katika uzoefu wa kawaida wa binadamu, kwa sababu watu wanaoutafuta ukweli hawafanani, kazi ya Roho Mtakatifu pia haifanani. Aidha, kwa sababu mazingira wanayoyapitia na kiwango cha uzoefu wao haufanani, kwa sababu ya mchanganyiko wa akili na mawazo yao, uzoefu wao pia umechanganyika kwa viwango tofauti. Kila mtu anaelewa ukweli kulingana na hali yake tofauti ya kibinafsi. Ufahamu wao wa maana halisi ya ukweli hauko kamili, na ni kwa kipengele kimoja tu au vichache. Mawanda ambayo ukweli unaeleweka kwa mwanadamu siku zote umejikita katika hali tofauti tofauti za watu, na hivyo hazifanani. Kwa njia hii, maarifa yanayoonyesha ukweli ule ule kwa watu tofauti hayafanani. Hii ni kusema, uzoefu wa mwanadamu siku zote una mipaka, na hauwezi kuwakilisha kikamilifu matakwa ya Roho Mtakatifu, na kazi ya mwanadamu haiwezi kuchukuliwa kama kazi ya Mungu, hata kama kile kinachoonyeshwa na mwanadamu kinafanana kwa karibu sana na mapenzi ya Mungu, hata kama uzoefu wa mwanadamu unakaribiana sana na kazi ya ukamilishaji itakayofanywa na Roho Mtakatifu. Mwanadamu anaweza kuwa tu mtumishi wa Mungu, akifanya kazi ambayo Mungu amemwaminia. Mwanadamu anaweza kuonyesha maarifa tu chini ya nuru ya Roho Mtakatifu na ukweli alioupata kutokana na uzoefu wake binafsi. Mwanadamu hana sifa na hana vigezo vya kuwa msemaji wa Roho Mtakatifu. Hana uwezo wa kusema kuwa kazi ya mwanadamu ni kazi ya Mungu. Mwanadamu ana kanuni za kufanya kazi za mwanadamu, na wanadamu wote wana uzoefu tofauti na wana hali zinazotofautiana. Kazi ya mwanadamu inajumuisha uzoefu wake wote chini ya nuru ya Roho Mtakatifu. Uzoefu huu unaweza tu kuwakilisha nafsi ya mwanadamu na hauwakilishi nafsi ya Mungu, au mapenzi ya Roho Mtakatifu. Kwa hivyo, njia inayotembewa na mwanadamu haiwezi kusemwa kuwa ndio njia inayotembewa na Roho Mtakatifu, kwa sababu kazi ya mwanadamu haiwezi kuwakilisha kazi ya Mungu na kazi ya mwanadamu na uzoefu wa mwanadamu sio matakwa ya Roho Mtakatifu. Kazi ya mwanadamu ina hatari ya kuangukia katika kanuni, na mbinu za kazi yake zinafungwa kirahisi kwa upeo mdogo, na haziwezi kuwaongoza watu katika njia huru. Wafuasi wengi wanaishi ndani ya mawanda finyu, na uzoefu wao pia unakuwa ni finyu. Uzoefu wa mwanadamu siku zote ni finyu; mbinu ya kazi yake pia ni finyu na haiwezi kulinganishwa na kazi ya Roho Mtakatifu au kazi ya Mungu Mwenyewe—hii ni kwa sababu uzoefu wa mwanadamu, mwishowe, ni mdogo. Hata hivyo Mungu anafanya kazi Yake, hakuna kanuni kwa kazi hiyo; vyovyote vile inavyofanywa, haifungwi na njia moja. Hakuna kanuni za aina yoyote ile katika kazi ya Mungu—kazi Yake yote imeachiliwa na ipo huru. Haijalishi ni muda gani mwanadamu aliotumia kumfuata Yeye, hawawezi kufanya muhtasari wa sheria zozote za mbinu Zake za kufanya kazi. Ingawa kazi Yake inaongozwa na kanuni, siku zote inafanywa katika njia mpya na siku zote inakuwa na maendeleo mapya ambayo yanazidi uwezo wa mwanadamu. Katika kipindi kimoja, Mungu anaweza kuwa na aina kadhaa tofauti za kazi na njia tofauti za kuwaongoza watu, Akiwaruhusu watu daima wawe na uingiaji mpya na mabadiliko mapya. Huwezi kuelewa sheria za kazi Yake kwa sababu siku zote Anafanya kazi katika njia mpya. Ni kwa njia hii tu ndiyo wafuasi wa Mungu hawawezi kuanguka katika kanuni. Kazi ya Mungu Mwenyewe siku zote ipo mbali na dhana za watu na kupinga mitazamo yao. Ni wale tu ambao wanamfuata Yeye kwa moyo wote ndio wanaoweza kubadilishwa tabia zao na wanaweza kuishi kwa uhuru bila kuwa chini ya kanuni zozote au kufungwa na dhana za kidini. Matakwa ambayo kazi ya mwanadamu inawawekea watu yamejikita katika uzoefu wake mwenyewe na kile ambacho yeye mwenyewe anaweza kutimiza. Kiwango cha matakwa haya kina mipaka ndani ya mawanda fulani, na mbinu za utendaji pia ni chache sana. Kwa hivyo wafuasi bila kujua wanaishi ndani ya mawanda finyu; kadiri muda unavyokwenda, zinakuwa kanuni na taratibu. Ikiwa kazi ya kipindi fulani inaongozwa na mtu ambaye hajapitia kukamilishwa na Mungu na hakupokea hukumu, wafuasi wake wote watakuwa wakidini na wataalamu wa kumpinga Mungu. Kwa hivyo, ikiwa mtu fulani ni kiongozi aliyehitimu, mtu huyo lazima awe amepitia hukumu na kukubali kukamilishwa. Wale ambao hawajapitia mchakato wa hukumu, hata kama wanaweza kuwa na kazi ya Roho Mtakatifu, wanaonyesha vitu ambavyo si dhahiri na visivyokuwa halisi. Kadiri muda unavyozidi kwenda, watawaongoza watu katika kanuni zisizoeleweka vizuri na zisizowezekana. Kazi ambayo Mungu anafanya haiambatani na mwili wa mwanadamu; haiambatani na mawazo ya mwanadamu bali inapinga dhana za mwanadamu; haijachanganyika na mitazamo ya kidini isiyoeleweka vizuri. Matokeo ya kazi Yake hayawezi kupatikana kwa mwanadamu ambaye hajakamilishwa na Yeye na yapo nje ya uwezo wa fikira za mwanadamu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
321. Kazi iliyopo katika akili ya mwanadamu inatimizwa kwa urahisi sana na mwanadamu. Wachungaji na viongozi waliopo katika ulimwengu wa kidini, kwa mfano, wanategemea karama zao na nafasi zao katika kufanya kazi zao. Watu wanaowafuata kwa muda mrefu wataambukizwa na karama zao na kuvutiwa na vile walivyo. Wanazingatia karama za watu, uwezo na maarifa ya watu, na wanamakinikia mambo ya kimiujiza na mafundisho mengi yasiyokuwa na uhalisi (kimsingi, haya mafundisho ya kina hayawezi kutekelezeka). Hawalengi mabadiliko ya tabia za watu, badala yake wanalenga kuwafundisha watu uwezo wao wa kuhubiri na kufanya kazi, kuboresha maarifa ya watu na mafundisho yao mengi ya kidini. Hawalengi kuona ni kwa kiasi gani tabia za watu zimebadilika au ni kwa kiasi gani watu wanauelewa ukweli. Wala hawajali kuhusu viini vya watu, wala kujua hali za watu za kawaida na zisizo za kawaida. Hawapingi mitazamo ya dhana za watu au kufichua dhana zao, sembuse kuwapogoa watu kwa sababu ya mapungufu au upotovu wao. Wengi ambao wanawafuata wanahudumu kwa vipaji vyao, na yote wanayotoa ni fikira za kidini na nadharia za theolojia, ambazo haziambatani na uhalisi na haziwezi kabisa kuwapa watu uzima. Kwa kweli, kiini cha kazi yao ni kulea talanta, kumlea mtu kuwa mhitimu mwenye talanta aliyemaliza mafunzo ya kidini ambaye baadaye anakwenda kufanya kazi na kuongoza. Kwa miaka elfu sita ya kazi ya Mungu, je, unaweza kupata sheria zozote kuihusu? Kuna kanuni na vizuizi vingi katika kazi ambayo mwanadamu hufanya, na ubongo wa mwanadamu umejawa na mafundisho mengi ya kidini. Hivyo mwanadamu anachokionyesha ni kiasi cha maarifa na utambuzi ndani ya uzoefu wake wote. Mwanadamu hawezi kuonyesha kitu chochote zaidi ya hiki. Uzoefu au maarifa ya mwanadamu hayatokani na vipawa vyake vya asili au silika yake; unatokea kwa sababu ya uongozi wa Mungu na uchungaji wa moja kwa moja wa Mungu. Mwanadamu ana uwezo tu wa kupokea uchungaji huu na sio uwezo wa kuonyesha moja kwa moja uungu ni nini. Mwanadamu hana uwezo wa kuwa chanzo, anaweza kuwa tu chombo ambacho kinapokea maji kutoka kwenye chanzo; hii ni silika ya mwanadamu, uwezo ambao mtu anapaswa kuwa nao kama mwanadamu. Ikiwa mtu anapoteza uwezo wa kukubali neno la Mungu na kupoteza silika ya kibinadamu, mtu huyo anapoteza pia kile ambacho ni cha thamani sana, na anapoteza wajibu wa mwanadamu aliyeumbwa. Ikiwa mtu hana maarifa au uzoefu wa neno la Mungu au kazi Yake, mtu huyo anapoteza wajibu wake, wajibu anaopaswa kuutimiza kama kiumbe aliyeumbwa, na anapoteza heshima ya kiumbe aliyeumbwa. Ni silika ya Mungu kuonyesha uungu ni nini, iwe unaonyeshwa katika mwili au moja kwa moja na Roho Mtakatifu; hii ni huduma ya Mungu. Mwanadamu anaonyesha uzoefu wake mwenyewe au maarifa (yaani, anaonyesha kile alicho) wakati wa kazi ya Mungu au baada yake; hii ndiyo silika ya mwanadamu na wajibu wa mwanadamu, ndicho kitu ambacho mwanadamu anapaswa kukifikia. Ingawa maonyesho ya mwanadamu ni duni sana kuliko kile ambacho Mungu anaonyesha, na kuna kanuni nyingi katika kile ambacho mwanadamu huonyesha, mwanadamu anapaswa kutimiza wajibu anaopaswa kutimiza na kufanya kile anachopaswa kufanya. Mwanadamu anapaswa kufanya kitu chochote kinachowezekana kwa mwanadamu kufanya ili kutimiza wajibu wake, na hapaswi kuacha kitu hata kidogo.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
322. Watu wengine watauliza, “Kuna tofauti gani kati ya kazi iliyofanywa na Mungu mwenye mwili na ile ya manabii na mitume wa zamani? Daudi pia aliitwa Bwana, sawa tu na Yesu alivyoitwa; ingawa kazi walizofanya zilikuwa tofauti, waliitwa kwa jina sawa. Kwa nini unasema, utambulisho wao haukuwa sawa? Kile Yohana alichoshuhudia ni maono, ambayo pia yalitoka kwa Roho Mtakatifu, na aliweza kuyasema maneno ambayo Roho Mtakatifu alikusudia kuyasema; kwa nini utambulisho wa Yohana ni tofauti na ule wa Yesu?” Maneno aliyoyasema Yesu yaliweza kumwakilisha Mungu kikamilifu, na kuwakilisha kikamilifu kazi ya Mungu. Kile alichokiona Yohana kilikuwa maono, na hakuweza kuwakilisha kikamilifu kazi ya Mungu. Ni kwa nini Yohana, Petro na Paulo walizungumza maneno mengi—kama alivyofanya Yesu—lakini bado hawakuwa na utambulisho sawa na Yesu? Ni hasa kwa sababu kazi waliyoifanya ilikuwa tofauti. Yesu alimwakilisha Roho wa Mungu, na Alikuwa Roho wa Mungu Akifanya kazi moja kwa moja. Alifanya kazi ya enzi mpya, kazi ambayo hakuna aliyekuwa amewahi kuifanya hapo awali. Yeye Alifungua njia mpya, Alimwakilisha Yehova, na Alimwakilisha Mungu Mwenyewe. Ilhali kwa Petro, Paulo na Daudi, bila kujali walichoitwa, waliwakilisha tu utambulisho wa kiumbe wa Mungu, na walitumwa na Yesu na Yehova. Kwa hivyo bila kujali kiasi cha kazi waliyofanya, bila kujali jinsi walivyofanya miujiza kubwa, walikuwa bado tu viumbe wa Mungu, na hawakuweza kumwakilisha Roho Mtakatifu. Walifanya kazi kwa jina la Mungu ama baada ya kutumwa na Mungu; zaidi ya hayo, walifanya kazi katika enzi iliyoanzishwa na Yesu ama Yehova, na kazi waliyoifanya haikuwa tofauti. Walikuwa, hatimaye, viumbe wa Mungu tu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kuhusu Majina na Utambulisho
323. Katika Enzi ya Neema, Yesu pia Alinena mengi na kufanya kazi nyingi. Alikuwaje tofauti na Isaya? Alikuwaje tofauti na Danieli? Je, Alikuwa nabii? Ni kwa nini inasemekana kwamba Yeye ni Kristo? Kuna tofauti gani baina yao? Wote walikuwa wanadamu walionena maneno, na maneno yao yalionekana sawa kwa wanadamu. Wote walinena na kufanya kazi. Manabii wa Agano la Kale walitoa unabii, na vivyo hivyo, pia na Yesu. Ni kwa nini iwe hivi? Tofauti hapa inapatikana katika aina ya kazi zao. Ili kutambua suala hili, huwezi kuzingatia asili ya mwili na hufai kuzingatia upurukushani wa maneno ya mtu. Daima ni sharti kwanza uzingatie kazi yake na athari ambayo kazi yake inafanikisha ndani ya mwanadamu. Unabii uliotolewa na manabii wakati ule, haukuyaruzuku maisha ya mwanadamu, na ujumbe uliopokelewa na watu kama Isaya na Danieli ulikuwa tu unabii na si njia ya uzima. Ingekuwa si kuonekana moja kwa moja kwa Yehova, hakuna ambaye angefanya hiyo kazi, ambayo haiwezekani kwa wanadamu. Yesu pia Alisema mengi, lakini maneno yake yalikuwa njia ya uzima ambayo kwayo mwanadamu angepata njia ya kutenda. Hiyo ni kusema, kwanza, Angeukimu uzima wa mwanadamu, kwa kuwa Yesu ni uzima; pili, Angeweza kuugeuza upotovu wa mwanadamu; tatu, kazi Yake ingeweza kuifuata ile ya Yehova ili kuendeleza enzi; nne, Angeweza kutambua mahitaji ya mwanadamu kwa ndani na kufahamu anachokosa mwanadamu; tano, Angeweza kuanzisha enzi mpya na kutamatisha enzi ya zamani. Ndiyo maana Anaitwa Mungu na Kristo; Yeye si tofauti na Isaya tu; bali pia na manabii wengine wote. Chukua Isaya kama ulinganisho wa kazi za manabii. Kwanza, asingeweza kuukimu uzima wa mwanadamu; pili, asingeweza kuanzisha enzi mpya. Alikuwa akifanya kazi chini ya uongozi wa Yehova wala si kuanzisha enzi mpya. Tatu, alichokizungumza yeye mwenyewe kilikuwa nje ya ufahamu wake. Alikuwa akipata ufunuo moja kwa moja kutoka kwa Roho wa Mungu, na wengine wasingeelewa hata baada ya kuusikiliza ufunuo huo. Haya machache yanatosha kuthibitisha kuwa kazi yake haikuwa zaidi ya unabii, si zaidi ya kazi iliyofanywa kwa niaba ya Yehova. Hata hivyo, asingeweza kumwakilisha Yehova kikamilifu. Alikuwa mtumishi wa Yehova, chombo katika kazi ya Yehova. Aidha alikuwa anafanya kazi katika Enzi ya Sheria tu na katika mawanda ya kazi ya Yehova; hakufanya kazi nje ya Enzi ya Sheria. Kinyume na haya, kazi ya Yesu ilikuwa tofauti. Alivuka mipaka ya kazi ya Yehova; Alifanya kazi kama Mungu mwenye mwili na kupitia mateso ili amkomboe mwanadamu. Hiyo ni kusema kuwa Alifanya kazi mpya nje ya ile iliyofanywa na Yehova. Huku kulikuwa kukaribisha kwa enzi mpya. Jambo jingine ni kuwa Aliweza kuyazungumzia mambo ambayo mwanadamu asingeweza kupata. Kazi Yake ilikuwa kazi ndani ya usimamizi wa Mungu na ilijumuisha wanadamu wote. Hakufanya kazi miongoni mwa watu wachache tu, na wala kazi yake haikuwa kuwaongoza watu wachache tu. Kuhusu jinsi Mungu alivyopata mwili ili kuwa mwanadamu, jinsi Roho alivyotoa ufunuo wakati huo, na jinsi Roho alivyomshukia mwanadamu kufanya kazi, haya ni mambo ambayo mwanadamu hawezi kuona au kugusa. Haiwezekani kabisa ukweli huu kutumika kama uthibitisho kwamba Yeye ni Mungu mwenye mwili. Kwa sababu hii, tofauti inaweza kupatikana tu kwenye maneno na kazi ya Mungu ambayo ni mambo dhahiri kwa mwanadamu. Hili tu ndilo halisi. Hii ni kwa sababu masuala ya Roho hayaonekani kwako na yanafahamika wazi na Mungu Mwenyewe peke Yake, wala hata mwili wa Mungu haufahamu yote; unaweza kuthibitisha tu kama Yeye ni Mungu[a] kutokana na kazi Aliyoifanya tu. Kutokana na kazi Yake, inaweza kuonekana kuwa, kwanza, Anaweza kufungua enzi mpya; pili, Yeye ana uwezo wa kuyaruzuku maisha ya mwanadamu na kumwonyesha mwanadamu njia ya kufuata. Hii inatosha kuthibitisha kuwa Yeye ni Mungu Mwenyewe. Angalau kazi Aifanyayo yaweza kumwakilisha kikamilifu Roho Mtakatifu wa Mungu na kutokana na kazi hiyo inaonekana kuwa Roho wa Mungu yupo ndani Yake. Kwa kuwa kazi iliyofanywa na Mungu mwenye mwili ilikuwa kuanzisha enzi mpya, kuongoza kazi mpya, na kuanzisha na kufungua mazingira mapya, haya mambo machache tu yanatosha kuthibitisha kuwa Yeye ni Mungu Mwenyewe. Hili kwa hivyo linamtofautisha na Isaya, Danieli, na manabii wengine wakuu.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Tofauti Kati ya Huduma ya Mungu Mwenye Mwili na Wajibu wa Mwanadamu
324. Katika Enzi ya Neema, Yohana alimwandalia Yesu njia. Hangeweza kufanya kazi ya Mungu Mwenyewe ila alitimiza tu kazi ya mwanadamu. Ingawa Yohana alikuwa mtangulizi wa Bwana; hangeweza kumwakilisha Mungu; alikuwa tu binadamu aliyetumiwa na Roho Mtakatifu. Baada ya ubatizo wa Yesu, “Roho Mtakatifu alimshukia Yeye kwa mfano wa njiwa.” Kisha Akaanza kazi Yake, hivyo, Alianza kufanya huduma ya Kristo. Hiyo ndiyo maana Alichukua utambulisho wa Mungu, kwa sababu Alitoka Kwa Mungu. Haijalishi jinsi imani Yake ilivyokuwa kabla ya hii—labda wakati mwingine ilikuwa dhaifu, au wakati mwingine ilikuwa na nguvu—hayo ndiyo yalikuwa maisha Yake ya kawaida ya binadamu kabla Afanye huduma Yake. Baada ya kubatizwa (kuteuliwa), mara moja Alikuwa na nguvu na utukufu wa Mungu pamoja Naye, na hivyo Akaanza Kufanya huduma Yake. Angeweza kufanya ishara na maajabu, kufanya miujiza, na Alikuwa na uwezo na mamlaka, kwani Alikuwa akifanya kazi moja kwa moja kwa niaba ya Mungu Mwenyewe; Alifanya kazi ya Roho badala Yake na kuonyesha sauti ya Roho Mtakatifu; kwa hivyo Alikuwa Mungu Mwenyewe. Hili halina pingamizi. Yohana alitumiwa na Roho Mtakatifu. Hangemwakilisha Mungu, na hakungekuwa na uwezekano wa yeye kumwakilisha Mungu. Kama angetaka kufanya hivyo, Roho Mtakatifu hangelikubali, kwani hangeweza kufanya kazi ambayo Mungu Mwenyewe alinuia kukamilisha. Labda kulikuwa na mengi ndani yake yaliyokuwa ya mapenzi ya mwanadamu, ama kitu kilichokuwa cha mwacha maadili; hakuna hali yoyote ambapo angemwakilisha Mungu moja kwa moja. Makosa Yake na mambo yasiyo sahihi yalimwakilisha yeye pekee, lakini kazi Yake ilikuwa uwakilishi wa Roho Mtakatifu. Ilhali, huwezi kusema kuwa yeye mzima alimwakilisha Mungu. Je upotovu na kuwa kwake na makosa kungemwakilisha Mungu pia? Kuwa na makosa katika kumwakilisha mwanadamu ni kawaida, lakini kama alikuwa na upotovu katika kumwakilisha Mungu, basi si hiyo ingekuwa kutomheshimu Mungu? Je hilo halingekuwa kufuru dhidi ya Roho Mtakatifu? Roho Mtakatifu hawezi kumruhusu mwanadamu asimame mahali pa Mungu anavyotaka, hata kama anasifiwa na wengine. Kama yeye si Mungu, basi hataweza kubaki akiwa amesimama mwishowe. Roho Mtakatifu hamkubali mwanadamu amwakilishe Mungu vile mwanadamu atakavyo! Kwa mfano, Roho Mtakatifu alimshuhudia Yohana na pia kumtambulisha kuwa mmoja wa wale watakaomwandalia Yesu njia, lakini kazi iliyofanywa ndani Yake na Roho Mtakatifu ilikuwa imepimwa vizuri. Kilichotakiwa kwa Yohana ilikuwa awe wa kutayarisha njia ya Yesu tu, kumtayarishia Yesu njia. Hiyo ni kusema, Roho Mtakatifu Aliiunga mkono kazi yake katika kutengeneza njia na kumruhusu afanye kazi ya aina hiyo pekee, hakuna nyingine yoyote. Yohana alimwakilisha Eliya, na alimwakilisha nabii aliyetengeneza njia. Hili liliungwa mkono na Roho Mtakatifu; bora kazi yake iwe kutengeneza njia, Roho Mtakatifu aliiunga mkono. Hata hivyo, kama angedai kuwa yeye ni Mungu Mwenyewe na kusema kwamba amekuja kumaliza kazi ya ukombozi, Roho Mtakatifu angalilazimika kumwadibu. Haijalishi ukuu wa kazi ya Yohana, na ingawa iliungwa mkono na Roho Mtakatifu, kazi Yake ilibaki katika mipaka. Ni ukweli hakika kuwa kazi yake iliungwa mkono na Roho Mtakatifu, lakini nguvu aliyopewa katika wakati huo iliwekewa mipaka tu katika kutengeneza njia. Hangeweza, hata kidogo, kufanya kazi nyingine, kwani alikuwa tu Yohana aliyetengeneza njia, ila si Yesu. Kwa hivyo ushuhuda wa Roho Mtakatifu ni muhimu, lakini kazi ambayo mwanadamu anaruhusiwa kufanya na Roho Mtakatifu ni muhimu zaidi. Je, Yohana hakushuhudiwa sana? Kazi yake haikuwa kuu pia? Lakini kazi aliyofanya haingeshinda ile ya Yesu, kwani alikuwa mwanadamu tu aliyetumiwa na Roho Mtakatifu na hangeweza kumwakilisha Mungu moja kwa moja, na kwa hiyo kazi aliyofanya ilikuwa yenye mipaka. Baada ya yeye kuimaliza kazi ya kuandaa njia, Roho Mtakatifu hakuthibitisha ushuhuda wake tena, hakuna kazi mpya iliyomfuata yeye tena, na aliondoka kazi ya Mungu Mwenyewe ilipoanza.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (1)
325. Ingawa Yohana alisema kuwa, “Ninyi tubuni: kwa kuwa ufalme wa mbinguni uko karibu,” na kuhubiri pia injili ya ufalme wa mbinguni, kazi yake haikuwa yenye kina na ilijumuisha tu mwanzo. Kinyume, Yesu Alikaribisha enzi mpya na kuikamilisha enzi ya kitambo, lakini pia Alitimiza sheria ya Agano la Kale pia. Kazi Aliyofanya ni kubwa kuliko ile ya Yohana, na Alikuja kuwakomboa wanadamu wote—Alifanya hatua hii ya kazi. Yohana alitayarisha tu njia. Ingawa kazi yake ilikuwa kubwa, maneno yake mengi, na wale wafuasi waliomfuata wengi, kazi yake haikufanya kitu kingine ila kuletea mwanadamu mwanzo mpya. Mwanadamu hakupokea maisha, njia, ama ukweli wa ndani kutoka kwake, wala mwanadamu hakupata kupitia kwake ufahamu wa mapenzi ya Mungu. Yohana alikuwa nabii mkuu (Eliya) ambaye alifungua uwanja mpya kwa ajili ya kazi ya Yesu na kuwatayarisha waliochaguliwa; alikuwa mtangulizi wa Enzi ya Neema. Mambo kama haya hayawezi kutambuliwa kirahisi kwa kuchunguza kuonekana kwao kwa kawaida. Hasa sana, Yohana alifanya kazi kubwa; zaidi ya hayo, alizaliwa kutoka kwa ahadi ya Roho Mtakatifu, na kazi yake ikashikiliwa na Roho Mtakatifu. Hivyo, kutofautisha kati ya utambulisho wao inaweza kufanywa tu kupitia kazi zao, kwa kuwa sura tu ya nje ya mwanadamu haiwezi kuonyesha dutu yake, na mwanadamu hawezi kuhakikisha ushuhuda wa kweli wa Roho Mtakatifu. Kazi iliyofanywa na Yohana na ile iliyofanywa na Yesu si sawa na ilikuwa ya asili tofauti. Hii ndiyo inafaa kuonyesha kama yeye ni Mungu ama sio Mungu. Kazi ya Yesu ilikuwa kuanza, kuendelea, kuhitimisha na kukamilisha. Kila moja ya hatua hizi zilichukuliwa na Yesu, ilhali kazi ya Yohana haikuwa zaidi ya kuanzisha. Hapo mwanzo, Yesu Alieneza injili na kuhubiri njia ya toba, na kisha Akaendelea kumbatiza mwanadamu, kuponya wagonjwa, na kutoa mapepo. Mwishowe, Alimkomboa mwanadamu kutoka kwa dhambi na kukamilisha kazi Yake ya enzi yote. Alimhubiria mwanadamu na kueneza injili ya ufalme wa mbinguni katika sehemu zote. Hii ilikuwa sawa na Yohana, tofauti ikiwa kwamba Yesu Alikaribisha enzi mpya na kuleta Enzi ya Neema kwa mwanadamu. Kutoka kwa Mdomo Wake lilitoka neno jinsi mwanadamu anavyopaswa kutenda na njia mwanadamu anayopaswa kufuata katika Enzi ya Neema, na mwishowe, Akamaliza kazi ya Ukombozi. Kazi kama hiyo haingeweza kutekelezwa na Yohana. Kwa hivyo, ni Yesu ndiye Aliyefanya Kazi Ya Mungu Mwenyewe, na ni Yeye ndiye Mungu Mwenyewe na Anamwakilisha Mungu moja kwa moja.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (1)
326. Maneno na kazi za manabii na za wale waliotumiwa na Roho Mtakatifu zote zilikuwa zinafanya wajibu wa mwanadamu, kutekeleza jukumu lake kama kiumbe na kufanya ambacho mwanadamu anapaswa kufanya. Hata hivyo, maneno na kazi za Mungu mwenye mwili ilikuwa ni kuendeleza huduma Yake. Ingawa umbo Lake lilikuwa lile la kiumbe, kazi Yake haikuwa kutimiza majukumu Yake bali Huduma Yake. Dhana “wajibu” inarejelea viumbe ilhali “huduma” inarejelea mwili wa Mungu mwenye mwili. Kuna tofauti kubwa kati ya haya mawili, na haya mawili hayabadilishani nafasi. Kazi ya mwanadamu ni kufanya wajibu wake, ilhali kazi ya Mungu ni kusimamia, na kuendeleza huduma Yake. Kwa hivyo, ingawa mitume wengi walitumiwa na Roho Mtakatifu na manabii wengi wakajazwa na Yeye, kazi zao na maneno yao yalikuwa tu kutimiza wajibu wao kama viumbe. Ingawa unabii wao ungeweza kuwa mkubwa kuliko maisha kama yanavyozungumziwa na Mungu mwenye mwili, na hata ubinadamu wao ulikuwa wa hali ya juu kuliko wa Mungu kuwa mwenye mwili, walikuwa bado wanafanya wajibu wao na wala si kutimiza huduma yao. Wajibu wa mwanadamu unarejelea majukumu yake, na ni kitu kinachoweza kufanikishwa na mwanadamu. Hata hivyo, huduma ifanywayo na Mungu mwenye mwili inahusiana na usimamizi Wake, na haiwezi kufanikishwa na mwanadamu. Hata kama Mungu mwenye mwili hunena, kufanya kazi, au kutenda miujiza, Anafanya kazi kubwa katika usimamizi Wake, kazi ambayo haiwezi kufanywa na mwanadamu kwa niaba Yake. Kazi ya mwanadamu ni kufanya tu wajibu wake kama kiumbe katika hatua fulani ya usimamizi wa Mungu. Bila usimamizi kama huo, yaani, ikiwa huduma ya Mungu mwenye mwili itapotea, pia wajibu wa viumbe utapotea. Kazi ya Mungu kuendeleza huduma Yake ni kumsimamia mwanadamu, ilhali mwanadamu afanyapo wajibu wake ni kutimiza wajibu wake ili kuafikia masharti ya Muumba na haiwezi kwa vyovyote vile kuchukuliwa kwamba ameendeleza huduma ya mtu yeyote. Kwa kiini asili cha Mungu, yaani, Roho, kazi ya Mungu ni usimamizi wake, bali kwa Mungu mwenye mwili akiwa na umbile la nje la kiumbe, kazi yake ni kuendeleza huduma Yake. Kazi yoyote Aifanyayo ni ya kuendeleza huduma Yake, na mwanadamu anaweza tu kufanya awezalo ndani ya upeo Wake wa usimamizi na chini ya uongozi Wake.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Tofauti Kati ya Huduma ya Mungu Mwenye Mwili na Wajibu wa Mwanadamu
327. Hata hivyo, kazi ya Mungu ni tofauti na kazi ya mwanadamu, na aidha, maonyesho Yake yanawezaje kuwa sawa na ya mwanadamu? Mungu ana tabia Yake Mwenyewe ya kipekee, ilhali mwanadamu ana wajibu ambao anapaswa kutimiza. Tabia ya Mungu inaonyeshwa katika kazi Yake, ilhali wajibu wa mwanadamu unadhihirishwa katika uzoefu wa mwanadamu na kuonyeshwa katika kazi za mwanadamu. Kwa hiyo inakuwa dhahiri kupitia kazi inayofanywa iwapo jambo fulani ni maonyesho ya Mungu ama maonyesho ya mwanadamu. Halihitaji kufafanuliwa na Mungu Mwenyewe, wala halihitaji mwanadamu ajitahidi kushuhudia; aidha, halimhitaji Mungu Mwenyewe kumkandamiza mtu yoyote. Yote haya yanakuja kama ufunuo wa kawaida; hayalazimishwi wala silo jambo ambalo mwanadamu anaweza kuingilia kati. Wajibu wa mwanadamu unaweza kujulikana kupitia uzoefu wake, na hauhitaji watu wafanye kazi yoyote ya ziada inayohusu uzoefu wao. Nafsi yote ya mwanadamu inaweza kufichuliwa wakati anapotimiza wajibu wake, wakati Mungu anaweza kuonyesha tabia Yake ya asili anapotekeleza kazi Yake. Ikiwa ni kazi ya mwanadamu basi haiwezi kufichika. Ikiwa ni kazi ya Mungu, basi haiwezekani hata zaidi kwa tabia ya Mungu kufichwa na yeyote, sembuse kudhibitiwa na mwanadamu. Hakuna mwanadamu anayeweza kusemekana kuwa Mungu, wala kazi na maneno yake kuonekana kuwa matakatifu ama kuchukuliwa kuwa yasiyobadilika. Mungu anaweza kusemekana kuwa mwanadamu kwa sababu Amejivika mwili, lakini kazi Yake haiwezi kuchukuliwa kuwa kazi ya mwanadamu ama wajibu wa mwanadamu. Aidha, matamshi ya Mungu na nyaraka za Paulo hayawezi kulinganishwa, wala hukumu na kuadibu kwa Mungu na maneno ya mwanadamu ya kuagiza kuzungumziwa kuwa sawa. Kwa hiyo, kuna kanuni zinazotofautisha kazi ya Mungu na kazi ya mwanadamu. Zinatofautishwa kulingana na viini vyao, sio kwa upana wa kazi ama ustadi wake wa muda. Watu wengi hufanya makosa ya kanuni kuhusiana na hili. Hii ni kwa sababu mwanadamu anaangalia mambo ya nje, ambayo anaweza kutimiza, ilhali Mungu anaangalia kiini, ambacho hakiwezi kuonekana na macho ya mwanadamu. Ukichukulia maneno na kazi ya Mungu kama wajibu wa mtu wa kawaida, na kuona kazi kubwa ya mwanadamu kama kazi ya Mungu aliyejivika mwili badala ya wajibu ambao mwanadamu anatimiza, je, basi hujakosea kimsingi? Barua na wasifu wa mwanadamu vinaweza kuandikwa kwa urahisi, lakini kwa msingi tu wa kazi ya Roho Mtakatifu. Hata hivyo, matamshi na kazi ya Mungu haviwezi kufanikishwa kwa urahisi na mwanadamu ama kutimizwa kwa hekima na fikira za binadamu, na watu hawawezi kuvieleza kikamilifu baada ya kuvichunguza. Masuala haya ya kimsingi yasipowaletea hisia yoyote, basi ni dhahiri kwamba imani yenu si ya kweli ama safi sana. Inaweza tu kusemekana kwamba imani yenu imejaa mashaka, na imekanganyikiwa na ni isiyo na maadili. Bila hata kuelewa masuala ya msingi kabisa ya Mungu na mwanadamu, je, imani kama hii haijakosa utambuzi kabisa?
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Msimamo Wako Kuhusu Nyaraka Kumi na Tatu ni Upi?
328. Mnapaswa kujua jinsi ya kutofautisha kazi ya Mungu na kazi ya mwanadamu. Je, mnaweza kuona nini katika kazi ya mwanadamu? Kuna vitu vingi ambavyo ni uzoefu wa mwanadamu katika kazi ya mwanadamu; kile ambacho mwanadamu anakionyesha ni kile alicho. Kazi ya Mungu pia inaonyesha kile Alicho, lakini kile Alicho ni tofauti na mwanadamu alivyo. Kile mwanadamu alicho ni kiwakilishi cha uzoefu na maisha ya mwanadamu (kile ambacho mwanadamu anakipitia au kukabiliana nacho katika maisha yake, au falsafa za kuishi alizo nazo), na watu wanaoishi katika mazingira tofauti huonyesha nafsi tofauti. Kama una uzoefu wa kijamii au la na jinsi ambavyo unaishi na kupitia uzoefu katika familia yako inaweza kuonekana katika kile unachokionyesha, lakini huwezi kuona kutoka kwa kazi ya Mungu mwenye mwili kama Ana uzoefu wa maisha ya kijamii au Hana. Anatambua vizuri kiini cha mwanadamu, Anaweza kufunua aina za matendo yote yanayohusiana na kila aina ya watu. Yeye ni bora zaidi katika kufichua tabia potovu ya mwanadamu na tabia yake ya uasi. Haishi miongoni mwa watu wa kidunia, lakini Anatambua asili ya watu wenye mwili wa kufa na upotovu wote wa watu wa duniani. Hicho ndicho Alicho. Ingawa Hashughuliki na dunia, Anajua kanuni za kushughulika na dunia, kwa sababu Anaielewa vizuri asili ya mwanadamu. Anajua kuhusu kazi ya Roho ambayo jicho la mwanadamu haliwezi kuiona na ambayo masikio ya mwanadamu hayawezi kusikia, kwa wanadamu wa leo na wa zamani. Hii inajumuisha hekima ambayo sio falsafa ya kuishi na maajabu ambayo ni magumu kwa watu kuyaelewa. Hiki ndicho Alicho, kimewekwa wazi kwa watu na pia kimefichwa kwa watu. Kile Anachoonyesha sio kile ambacho mwanadamu asiye wa kawaida alicho, bali ni tabia za asili na nafsi ya Roho. Hasafiri ulimwenguni kote lakini anajua kila kitu kuhusu ulimwengu. Anawasiliana na “sokwe” ambao hawana maarifa au utambuzi, lakini Anaonyesha maneno ambayo ni ya kiwango cha juu kuliko maarifa na yapo juu ya watu wakubwa duniani. Anaishi miongoni mwa kundi la wanadamu wapumbavu na wasiojali ambao hawana ubinadamu na ambao hawaelewi desturi na maisha ya ubinadamu, lakini Anaweza kuwaambia wanadamu waishi ubinadamu wa kawaida, na kwa wakati huo huo Anafichua ubinadamu duni na wa chini wa wanadamu. Haya yote ni nafsi Yake, iliyo juu zaidi kuliko nafsi ya mwanadamu yeyote wa damu na nyama. Kwa Yeye, si lazima Apitie maisha ya kijamii yaliyo magumu, changamani na duni, ili Aweze kufanya kazi Anayotaka kufanya na kufichua kikamilifu viini vya wanadamu waliopotoka. Maisha duni ya kijamii hayawezi kuadilisha mwili Wake. Kazi Yake na maneno Yake hufichua tu kutotii kwa mwanadamu na hayampi mwanadamu uzoefu na masomo kwa ajili ya kushughulika na ulimwengu. Hahitaji kuipeleleza jamii au familia ya mwanadamu wakati Anapompa mwanadamu uzima. Kumweka wazi na kumhukumu mwanadamu si maonyesho ya uzoefu wa mwili Wake; ni ufichuzi Wake wa kutokuwa na haki kwa mwanadamu baada ya kuujua uasi wa mwanadamu kwa muda mrefu na kuchukia upotovu wa mwanadamu. Kazi yote Anayoifanya ni kufichua tabia Yake kwa mwanadamu na kuonyesha nafsi Yake. Ni Yeye tu ndiye anayeweza kuifanya kazi hii, sio kitu ambacho mtu mwenye mwili na damu anaweza kuifanya.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu
329. Mungu anakuwa mwili ili tu kuongoza enzi na kuanzisha kazi mpya. Lazima muelewe hoja hii. Hii ni tofauti kabisa na kazi ya mwanadamu, na mawili haya hayawezi kuzungumzwa kwa pamoja. Mwanadamu anahitaji muda mrefu wa kukuzwa na kufanywa mkamilifu kabla mwanadamu aweze kutumiwa kutekeleza kazi, na ubinadamu wa hali ya juu unahitajika. Mwanadamu hapaswi kudumisha hali yake ya ubinadamu wa kawaida tu, bali pia mwanadamu zaidi ya hapo lazima aelewe kanuni nyingi na sheria za tabia kabla ya mengine, na zaidi ya hayo lazima ajifunze zaidi kuhusu hekima na maadili ya mwanadamu. Haya ndiyo mwanadamu lazima kujengwa nayo. Hata hivyo, hivi sivyo ilivyo na Mungu mwenye mwili, kwa maana kazi Yake haimwakilishi mwanadamu na wala si ya binadamu; bali ni dhihirisho la moja kwa moja la hali Yake na utekelezaji wa moja kwa moja wa kazi Anayopaswa kufanya. (Kwa kawaida, kazi Yake hufanyika wakati inapaswa kufanyika, na sio tu wakati wowote kiholela. Badala Yake, kazi Yake hufanyika wakati ambapo ni wakati wa kukamilisha huduma Yake). Yeye hajihusishi katika maisha ya mwanadamu wala katika kazi ya mwanadamu, hiyo inamaanisha, ubinadamu Wake haujengwi na yoyote kati ya haya (lakini hili haliathiri kazi Yake). Anatimiza huduma Yake tu ikiwa wakati umewadia wa kufanya hivyo; haijalishi hali Aliyomo, Yeye huendelea mbele na kazi Anayopaswa kufanya. Haijalishi mwanadamu anajua nini kumhusu, au maoni ya mwanadamu kumhusu, kazi Yake haiathiriki.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Fumbo la Kupata Mwili (3)
330. Kazi ambayo Mungu anafanya haiwakilishi uzoefu wa mwili Wake; kazi ambayo mwanadamu anafanya inawakalisha uzoefu wa mwanadamu. Kila mtu anazungumza kuhusu uzoefu wake binafsi. Mungu anaweza kuonyesha ukweli moja kwa moja, wakati mwanadamu anaweza tu kuonyesha uzoefu unaolingana na huo baada ya kupata uzoefu wa ukweli. Kazi ya Mungu haina masharti na haifungwi na muda au mipaka ya kijiografia. Anaweza kuonyesha kile Alicho wakati wowote, mahali popote. Anafanya kazi vile Anavyopenda. Kazi ya mwanadamu ina masharti na muktadha; vinginevyo hana uwezo wa kufanya kazi na hawezi kuonyesha ufahamu wake wa Mungu au uzoefu wake wa ukweli. Unatakiwa tu kulinganisha tofauti baina yao ili kuonyesha kama ni kazi ya Mungu mwenyewe au kazi ya mwanadamu. Kama hakuna kazi inayofanywa na Mungu Mwenyewe, na kuna kazi tu ya mwanadamu, utajua tu kwamba mafundisho ya mwanadamu ni makuu, zaidi ya uwezo wa mtu yeyote yule; toni yao ya kuzungumza, kanuni zao katika kushughulikia mambo na uwezo wao katika kufanya kazi ni zaidi ya uwezo wa wengine. Nyinyi nyote mnavutiwa na watu hawa wa ubora mzuri wa tabia na maarifa ya juu, lakini hamwezi kuona kutoka katika kazi na maneno ya Mungu jinsi ubinadamu Wake ulivyo wa juu. Badala yake, Yeye ni wa kawaida, na Anapofanya kazi, Yeye ni wa kawaida na halisi lakini pia hawezi kupimwa na watu wenye mwili wa kufa, kitu ambacho kinawafanya watu wahisi kumheshimu sana. Pengine uzoefu wa mtu katika kazi yake ni mkubwa sana, au mawazo na fikira zake ni za juu sana, na ubinadamu wake ni mzuri hasa; hivi vinaweza kutamaniwa na watu tu, lakini haviwezi kuamsha kicho na hofu yao. Watu wote wanawatamani wale ambao wana uwezo wa kufanya kazi na ambao wana uzoefu wa kina na wanaweza kuutenda ukweli, lakini hawawezi kuibua kicho, bali tu kutamani na wivu. Lakini watu ambao wamepitia uzoefu wa kazi ya Mungu hawamtamani Mungu, badala yake wanahisi kwamba kazi Yake haiwezi kufikiwa na mwanadamu na haiwezi kueleweka na mwanadamu, na kwamba ni mpya na ya kushangaza. Watu wanapopitia uzoefu wa kazi ya Mungu, ufahamu wao wa kwanza kumhusu ni kwamba Yeye ni asiyeeleweka, ni mwenye hekima na wa ajabu na wanamcha bila kujua na kuihisi siri ya kazi Anayoifanya, ambayo inapita akili ya mwanadamu. Watu wanataka tu kuwa na uwezo wa kukidhi matakwa Yake, kuridhisha matamanio Yake; hawatamani kumpita Yeye, kwa sababu kazi Anayoifanya inazidi fikira za mwanadamu na haiwezi kufanywa na mwanadamu kama mbadala. Hata mwanadamu mwenyewe hayajui mapungufu yake, wakati Amefungua njia mpya na kumleta mwanadamu katika dunia mpya zaidi na nzuri zaidi, na hivyo mwanadamu amefanya maendeleo mapya na kuwa na mwanzo mpya. Kile ambacho watu wanahisi kumhusu Mungu, sio matamanio, au sio matamanio tu. Uzoefu wake wa kina ni kicho na upendo, hisia zake ni kwamba Mungu kweli ni wa ajabu sana. Anafanya kazi ambayo mwanadamu hawezi kufanya na kusema mambo ambayo mwanadamu hawezi kusema. Watu ambao wamepitia kazi ya Mungu daima wana hisia isiyoweza kuelezeka. Watu wenye uzoefu wa kina wa kutosha wanaweza kuelewa ukweli wa Mungu; wanaweza kuhisi uzuri Wake, kwamba kazi Yake ni ya hekima sana, ya ajabu sana, na hivyo hii inazalisha nguvu isiyokoma ndani yao. Si woga au upendo wa mara moja moja na heshima, bali hisia za ndani za upendo wa Mungu na uvumilivu kwa mwanadamu. Hata hivyo, watu ambao wamepata uzoefu wa kuadibu na hukumu Yake wanahisi kuwa Yeye ni mkuu na Asiyekosewa. Hata watu ambao wamepitia uzoefu mkubwa wa kazi Yake pia hawawezi kumwelewa; watu wote wanaomcha wanajua kwamba kazi Yake hailingani na fikira za watu lakini siku zote inakwenda kinyume na fikira zao. Haihitaji watu wamtamani kabisa au wawe na mwonekano wa kunyenyekea Kwake; badala yake, wanapaswa kufikia uchaji wa kweli na utiifu wa kweli. Katika kazi Zake nyingi, mtu yeyote mwenye uzoefu wa kweli anahisi heshima Kwake, ambayo ni ya juu kuliko matamanio. Watu wameiona tabia Yake kwa sababu ya kazi Yake ya kuadibu na hukumu, na kwa hiyo wanamcha mioyoni mwao. Mungu anapaswa kuogopwa na kunyenyekewa, kwa sababu nafsi Yake na tabia Yake si sawa na za viumbe vilivyoumbwa, na ziko juu ya zile za viumbe vilivyoumbwa. Mungu hategemei chochote ili kuwepo na ni wa milele, Yeye siye kiumbe Aliyeumbwa, na ni Mungu tu anayestahili uchaji na utiifu; mwanadamu hana sifa ya kupewa hivi.
Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi ya Mungu na Kazi ya Mwanadamu