Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee IV

Utakatifu wa Mungu (I)

Tumekuwa na ushirika wa ziada wa mamlaka ya Mungu wakati wa mkutano wetu wa mwisho, na hatutazungumza kuhusu haki ya Mungu sasa hivi. Leo tutazungumza kuhusu mada nzima mpya—utakatifu wa Mungu. Utakatifu wa Mungu pia ni kipengele kingine cha kiini cha kipekee cha Mungu, hivyo kuna umuhimu mkubwa wa kushiriki mada hii hapa. Hiki kipengele cha kiini cha Mungu ambacho Nitashiriki, pamoja na vile vipengele viwili tulivyoshiriki mbeleni cha tabia ya haki ya Mungu na mamlaka ya Mungu—yote ni ya kipekee? (Ndiyo.) Utakatifu wa Mungu pia ni wa kipekee, kwa hivyomaudhui ya ushirika wetu wa leo ndiyo yatakayojumuisha msingi na kiini cha upekee huu. Leo tunaenda kushiriki kuhusu kiini cha kipekee cha Mungu—utakatifu Wake. Labda baadhi yenu wana wasiwasi kidogo, na wanauliza, “Mbona kushiriki utakatifu wa Mungu?” Msijali, Nitawazungumzia kuuhusu polepole. Punde tu mtakapousikia mtajua mbona ni muhimu Kwangu kushiriki mada hii.

Kwanza wacha tufafanue neno “takatifu.” Mkitumia utambuzi wenu na kutoka kwa maarifa yenu mmefunzwa, mnaelewa ufafanuzi wa “takatifu” kuwa nini? (“Takatifu” inamaanisha bila doa, bila upotovu au dosari yoyote ya binadamu. Kila kitu inachonururisha—kiwe kwa mawazo, matamshi ama vitendo, kila kitu inafanya—ni chema kabisa.) Vizuri kabisa. (“Takatifu” ni ya Mungu, haijanajisiwa, isiyokosewa na mtu. Ni ya kipekee, ni ishara ya tabia ya Mungu.) Huu ni ufafanuzi wako. Katika moyo wa kila mtu, neno hili “takatifu” lina wigo, ufafanuzi na fasiri. Kwa kiwango cha chini kabisa, mnapoona neno “takatifu” akili zenu si tupu. Mna wigo fulani uliofafanuliwa wa neno hili, na misemo ya watu wengine inakaribiana kiasi na misemo inayofafanua kiini cha tabia ya Mungu. Hii ni vizuri sana. Watu wengi zaidi wanaamini neno “takatifu” ni neno njema, na hii inaweza kuthibitishwa. Lakini utakatifu wa Mungu Ninaotaka kushiriki leo hautafafanuliwa tu, ama kuelezwa tu. Badala yake, Nitatumia baadhi ya ukweli kudhihirisha ili kukuruhusu kuona kwa nini Nasema Mungu ni mtakatifu, na mbona Natumia neno “takatifu” kuelezea kiini cha Mungu. Kabla ya ushirika wetu kuisha, utahisi kwamba matumizi ya neno “takatifu” kuelezea kiini cha Mungu na matumizi ya neno hili kumrejelea Mungu yanastahili sana na yanafaa. Kwa kiwango cha chini zaidi, kuhusiana na lugha za sasa za binadamu, kutumia neno hili kumrejelea Mungu kunafaa hasa—ni neno pekee kwa lugha ya binadamu linalofaa kabisa kumrejelea Mungu. Si neno tupu linapotumika kumrejelea Mungu, wala si sifa bila sababu au pongezi tupu. Madhumuni ya ushirika wetu ni kumruhusu kila mtu kuutambua ukweli wa kipengele hiki cha kiini cha Mungu. Mungu haogopi uelewa wa watu, bali kutoelewa kwao tu. Mungu anataka kila mtu ajue kiini Chake na kile Anacho na alicho. Hivyo kila wakati tunapotaja kipengele cha kiini Cha Mungu, tunaweza kutumia ukweli mwingi kuwaruhusu watu kuona kwamba kipengele hiki cha kiini cha Mungu kweli kipo.

Kwa sababu sasa tuna ufafanuzi wa neno “takatifu,” wacha tuangalie baadhi ya mifano. Katika fikira za watu, wanafikiria vitu na watu wengi kuwa “takatifu”. Kwa mfano, wavulana na wasichana mabikira wanaelezwa kama watakatifu katika kamusi za binadamu. Lakini je, kweli ni watakatifu? Je, hivi vinavyoitwa takatifu na “vitakatifu” tutakayoshiriki kuhusu leo ni kitu kimoja? Wale miongoni mwa wanadamu walio na maadili ya juu, wale walio na matamshi bora na ya maarifa, wasiomwumiza yeyote, na ambao, kupitia kwa maneni wanayozungumza, wanawafanya wengine kustareheka na kufurahia—ni watakatifu? Wale wanaofanya mazuri mara nyingi, wanaopenda kutoa na kuwasaidia wengine, wale wanaoleta raha tele ndani ya maisha ya watu—ni watakatifu? Wale wasio na fikira za kujihudumia, wasioweka madai makali juu ya yeyote, wanaomvumilia yeyote—ni watakatifu? Wale ambao hawajawahi kuwa na mzozo na yeyote wala kujinufaisha na yeyote—ni watakatifu? Basi wale wanaofanya kazi kwa minajili ya uzuri wa wengine, wanaofaidi wengine na kuleta uboreshaji kwa wengine kwa namna zote—ni watakatifu? Wanaowapa wengine akiba zao zote za maisha na kuishi maisha rahisi, walio wakali kwa wao wenyewe lakini wanawashughulikia wengine kwa ukarimu—ni watakatifu? (La.) Mnakumbuka kwamba mama zenu waliwatunza na kuwalinda kwa njia zote zinazoweza kufikiriwa—ni watakatifu? Vijimungu mnaopenda sana, wawe watu maarufu, mashuhuri ama watu wakubwa—ni watakatifu? (La.) Hebu sasa tuangalie wale manabii katika Biblia walioweza kuelezea siku za baadaye ambazo hazikujulikana na wengine wengi—mtu wa aina hii alikuwa mtakatifu? Watu walioweza kurekodi maneno ya Mungu na ukweli wa kazi Yake katika Biblia—walikuwa watakatifu? Musa alikuwa mtakatifu? Ibrahimu alikuwa mtakatifu? (La.) Ayubu je? Alikuwa mtakatifu? (La.) Ayubu aliitwa mtu mwenye haki na Mungu, basi mbona hata yeye anasemekana kutokuwa mtakatifu? Watu wanaomcha Mungu na kuepukana na maovu kweli si watakatifu? Ni watakatifu ama si watakatifu? (La.) Mna wasiwasi kidogo, hamna uhakika sana, na hamthubutu kusema “La,” lakini pia hamthubutu kusema “Ndiyo,” kwa hivyo mwishowe mnasema “La” shingo upande. Acha Niulize swali lingine. Wajumbe wa Mungu—wajumbe ambao Mungu huwatuma chini duniani—ni watakatifu? Malaika ni watakatifu? (La.) Binadamu wasio na upotoshaji wa Shetani—ni watakatifu? (La.) Nyinyi mnajibu “La” kila mara kwa kila swali. Kwa msingi upi? Mmechanganyikiwa, sivyo? Basi mbona hata malaika wanasemekana sio watakatifu? Mna wasiwasi hapa, sio? Basi mnaweza kugundua ni kwa msingi upi watu, vitu ama viumbe wasioumbwa tuliotaja mbeleni si watakatifu? Nina uhakika hamwezi. Hivyo, si kusema kwenu “La” basi ni kukosekana kwa uwajibikaji kidogo? Hamjibu bila kujali? Watu wengine wanafikiria: “Unauliza kwa namna hii, kwa hivyo si lazima iwe hivyo hakika.” Msijibu tu bila kujali. Fikirieni kwa makini iwapo jibu ni ndiyo au la. Mtajua tutakaposhiriki mada ifuatayo mbona ni “La.” Nitawapa jibu hivi punde. Hebu kwanza tusome baadhi ya maandiko.

1. Amri ya Yehova Mungu kwa Mwanadamu

Mwa 2:15-17 Naye Yehova Mungu akamchukua mtu huyo, na kumweka ndani ya bustani ya Edeni ili ailime na kuihifadhi. Yehova Mungu akamwamrisha mtu huyo, akisema, Unaweza kula kwa uhuru matunda kutoka miti yote ya bustani: Lakini kutoka mti wa maarifa ya mema na maovu, usiyale: kwa kuwa katika siku ambapo utakula matunda kutoka mti huo bila shaka utakufa.

2. Nyoka Anamshawishi Mwanamke

Mwa 3:1-5 Sasa nyoka alikuwa mwenye hila kuliko wanyama wote wa mwitu ambao Yehova Mungu alikuwa amewaumba. Naye akamwambia mwanamke, Naam, Mungu amesema, Msile matunda ya miti yote ya bustani? Naye mwanamke akamwambia nyoka, Tunaweza kula matunda ya miti katika bustani: Mungu amesema, Lakini msile wala kuyagusa matunda ya mti ulio katikati ya bustani, msije mkafa. Naye nyoka akamwambia mwanamke, Bila shaka hamtakufa: Kwa kuwa Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunuliwa, nanyi mtakuwa kama miungu, mkijua mema na maovu.

Hivi vifungu viwili ni dondoo kutoka kwa kitabu cha Mwanzo katika Biblia. Je, nyinyi nyote mnavijua vifungu hivi viwili? Hiki ni kitu kilichofanyika mwanzoni wakati binadamu kwanza aliumbwa; lilikuwa ni tukio halisi. Kwanza hebu tuangalie ni amri ya aina gani ambayo Yehova Mungu aliwapa Adamu na Hawa, kwani yaliyomo katika amri hii ni muhimu sana kwa mada yetu ya leo. “Yehova Mungu akamwamrisha mtu huyo, akisema, Unaweza kula kwa uhuru matunda kutoka miti yote ya bustani: Lakini kutoka mti wa maarifa ya mema na maovu, usiyale: kwa kuwa katika siku ambapo utakula matunda kutoka mti huo bila shaka utakufa.” Amri ya Mungu kwa mwanadamu katika kifungu hiki ina nini? Kwanza, Mungu anamwambia mwanadamu kile anachoweza kula, yakiwa ni matunda ya miti ya aina nyingi. Hakuna hatari na hakuna sumu, yote yanaweza kulika na kulika atakavyo mtu, bila wasiwasi wowote. Hii ni sehemu moja. Sehemu nyingine ni onyo. Onyo hili linamwambia mwanadamu mti ambao hawezi kula tunda kutoka—lazima asile tunda kutoka kwa mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Nini itafanyika akifanya hivyo? Mungu alimwambia mwanadamu: Ukilila hakika utakufa. Maneno haya yanaeleweka kwa urahisi? Iwapo Mungu angekwambia jambo hili lakini hukuelewa kwa nini, ungelichukulia kama kanuni ama amri ya kufuatwa? Linapaswa kufuatwa, sivyo? Lakini iwapo mwanadamu anaweza ama hawezi kulifuata, maneno ya Mungu hayaachi shaka. Mungu alimwambia mwanadamu kwa uwazi kabisa kile anachoweza kula na kile asichoweza, na kile kitakachofanyika akila kile hapaswi kula. Umeona tabia yoyote ya Mungu katika haya maneno machache ambayo Alisema? Haya maneno ya Mungu ni ya ukweli? Kuna udanganyifu wowote? Kuna uongo wowote? Kuna chochote kinachotisha? (La.) Mungu kwa uaminifu, kwa kweli, kwa dhati Alimwambia mwanadamu kile anachoweza kula na kile asichoweza kula, wazi na dhahiri. Kuna maana iliyofichwa katika maneno haya? Maneno haya yanaeleweka kwa urahisi? Je, kuna haja yoyote ya dhana? Hakuna haja ya kukisia. Maana yake ni wazi kwa mtazamo mmoja, na unaelewa punde tu unapoyaona. Ni wazi kabisa. Yaani, kile Mungu anataka kusema na Anachotaka kuonyesha kinatoka katika moyo Wake. Mambo ambayo Mungu anaonyesha ni safi, yanaeleweka kwa urahisi na ni wazi. Hakuna nia za siri ama maana zilizofichwa. Alizungumza moja kwa moja na mwanadamu, Akimwambia kile anachoweza kula na kile asichoweza kula. Hivyo ni kusema, kupitia maneno haya ya Mungu mwanadamu anaweza kuona kwamba moyo wa Mungu ni angavu, kwamba moyo wa Mungu ni wa kweli. Hakuna uwongo kabisa hapa; si kukwambia kwamba huwezi kula kile kinacholika ama kukwambia “Ifanye na uone kitakachofanyika” na vitu ambavyo huwezi kula. Hamaanishi hivi. Chochote afikiriacho Mungu katika moyo Wake ndicho Anachosema. Nikisema Mungu ni mtakatifu kwa sababu Anaonyesha na kujifichua Mwenyewe ndani ya maneno haya kwa njia hii, unaweza kuhisi kana kwamba Nimefanya jambo lisilokuwa kubwa ama Nimenyoosha ufasiri Wangu mbali kiasi. Kama ni hivyo, usijali, hatujamaliza bado.

Hebu tuzungumze kuhusu “Nyoka Anamshawishi Mwanamke.” Nyoka ni nani? Shetani. Anashikilia jukumu la foili katika mpango wa usimamizi wa Mungu wa miaka elfu sita, na ni jukumu ambalo hatuwezi kosa kutaja wakati tunaposhiriki utakatifu wa Mungu. Mbona Nasema hivi? Iwapo hujui uovu na upotovu wa Shetani ama asili ya Shetani, basi huna njia ya kumtambua, wala huwezi kujua utakatifu kweli ni nini. Katika mkanganyiko, watu wanaamini kwamba kile anachofanya Shetani ni chema, kwa sababu wanaishi ndani ya aina hii ya tabia potovu. Bila foili, bila kitu cha kulinganisha nacho, huwezi kujua utakatifu ni nini. Hiyo ndiyo maana lazima Shetani atajwe hapa. Matamko kama hayo si maneno matupu. Kupitia katika maneno na matendo ya Shetani, tutaona jinsi Shetani anavyotenda, jinsi Shetani anavyowapotosha binadamu, na asili na uso wa Shetani ni upi. Basi mwanamke alimwambia nini nyoka? Mwanamke alimweleza nyoka kile Yehova Mungu alikuwa amemwambia. Kwa kufuata alichosema, alikuwa amethibitisha uhalali wa yote ambayo Mungu alikuwa amemwambia? Hangeweza kuthibitisha haya, angeweza? Kama mtu ambaye alikuwa ameumbwa karibuni, hakuwa na uwezo wa kutambua mema kutoka kwa maovu, wala hakuwa na uwezo wa kufahamu chochote karibu naye. Kwa kutathmini maneno aliyomwambia nyoka hakuwa amethibitisha maneno ya Mungu kuwa kweli katika moyo wake; huu ulikuwa mtazamo wake. Hivyo wakati nyoka aliona kwamba mwanamke huyo hakuwa na mtazamo wa uhakika kwa maneno ya Mungu, alisema: “Bila shaka hamtakufa: Kwa kuwa Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunuliwa, nanyi mtakuwa kama miungu, mkijua mema na maovu.” Kuna chochote kibaya na maneno haya? Mlipomaliza kusoma sentensi hii, mlipata hisia ya nia za nyoka? Nyoka ana nia gani? Anataka kumjaribu mwanamke huyu kumfanya aache kusikiza maneno ya Mungu, lakini hakuongea moja kwa moja. Kwa hivyo tunaweza kusema kwamba ana ujanja sana. Anaonyesha maana yake kwa njia ya udanganyifu na ya kukwepa ili kufikia malengo anayonuia ambayo anaficha kutoka kwa mwanadamu ndani yake—huu ndio ujanja wa nyoka. Shetani amewahi kuzungumza na kutenda hivi. Anasema “sio kwa uhakika,” bila kuthibitisha kwa njia moja au nyingine. Lakini baada ya kusikia haya, moyo wa huyu mwanamke mjinga uliguswa. Nyoka alifurahia kwa sababu maneno yake yalikuwa na matokeo yaliyotarajiwa—hii ilikuwa nia ya ujanja ya Nyoka. Zaidi ya hayo, kwa kuahidi matokeo ambayo mwanadamu aliamini kuwa mema, alimshawishi, akisema, “siku mtakayokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunuliwa.” Hivyo mwanamke anafikiria: “Kufumbuliwa macho yangu ni jambo zuri!” Na kisha akasema kitu kizuri zaidi, maneno yasiyojulikana na mwanadamu, maneno yaliyo na nguvu kubwa ya majaribu juu ya wale wanaoyasikia: “nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na maovu.” Je, maneno haya hayamvutii mwanadamu sana? Ni kama mtu kukwambia: “Uso wako una umbo nzuri. Ni mfupi kidogo katika daraja la pua, lakini ukiirekebisha, utakuwa mrembo wa kupindukia!” Kwa mtu ambaye hajawahi kutaka kufanya upasuaji wa mapambo, moyo wake utaguswa kusikia maneno haya? Je, maneno haya ni ya kushawishi? Ushawishi huu unakuvutia? Ni wa kujaribu? (Ndiyo.) Je, Mungu husema mambo kama haya? Kulikuwa na dokezo lolote la haya katika maneno ya Mungu tuliyoyaangalia sasa hivi? Je, Mungu husema Anachofikiria katika moyo Wake? Mwanadamu anaweza kuona moyo wa Mungu kupitia maneno Yake? (Ndiyo.) Lakini wakati nyoka alikuwa amesema maneno haya kwa mwanamke, uliweza kuona moyo wake? La. Na kwa sababu ya ujinga wa mwanadamu, mwanadamu alishawishiwa kwa urahisi na maneno ya nyokana alidanganywa kwa urahisi. Hivyo uliweza kuona nia za Shetani? Uliweza kuona madhumuni nyuma ya kile alichosema? Uliweza kuona njama na mpango wake wa ujanja? (La.) Ni aina gani ya tabia inayowakilishwa na njia ya mazungumzo ya Shetani? Ni aina gani ya kiini ulichoona ndani ya Shetani kupitia maneno haya? Je, ni mwenye kudhuru kwa siri? Pengine juujuu anakupa tabasamu ama kutofichua maonyesho yoyote. Lakini katika moyo wake anahesabu jinsi ya kufikia lengo lake, na ni lengo hili ambalo huwezi kuliona. Kisha unashawishiwa na ahadi zote anazokupa, manufaa yote anayozungumzia. Unayaona kuwa mazuri, na unahisi kwamba kile anachosema ni cha kufaa zaidi, kikubwa zaidi kuliko asemacho Mungu. Wakati haya yanafanyika, je, mwanadamu basi hawi mfungwa mtiifu? Je, mbinu hizi zinazotumiwa na Shetani si za kikatili? Unajikubali kuzama chini. Bila ya Shetani kusongeza kidole, kwa sentensi hizi mbili unafurahia kumfuata na kumtii. Lengo lake limefikiwa. Nia hii si ya husuda? Huu sio uso wa kimsingi kabisa wa Shetani? Kutoka kwa maneno ya Shetani, mwanadamu anaweza kuona nia zake za husuda, kuona uso wake wenye sura mbaya na kiini chake. Sivyo? Kwa kulinganisha sentensi hizi, bila uchambuzi pengine unaweza kuhisi kana kwamba maneno ya Yehova Mungu ni ya kuchusha, ya kawaida na ya wote, kwamba hayastahili kuhangaikiwa kuusifu uaminifu wa Mungu. Tunapochukua maneno ya Shetani na uso wake wenye sura mbaya na kuvitumia kama foili, hata hivyo, je, haya maneno ya Mungu yanabeba uzito mwingi kwa watu wa leo? (Ndiyo.) Kupitia foili hii, mwanadamu anaweza kuhisi kutokuwa na dosari kwa Mungu. Kila neno analosema Shetani pamoja na nia zake, malengo yake na jinsi anavyoongea—yote yamepotoshwa. Ni nini sifa muhimu ya njia yake ya kuzungumza? Anatumia maneno yasiyo dhahiri kukushawishi bila kukuruhusu kumwona, wala hakuruhusu kutambua lengo lake ni nini; anakuacha uchukue chambo, akikufanya umsifu na kuimba uzuri wake. Hii siyo hila ya daima ya Shetani? (Ndiyo.) Hebu sasa tuangalie maneno na maonyesho mengine ya Shetani yanayomruhusu mwanadamu kuona uso wake wenye sura mbaya. Hebu tuendelee kusoma baadhi ya maandiko.

3. Mazungumzo kati ya Shetani na Yehova Mungu

Ayubu 1:6-11 Sasa kulikuweko na siku ambapo wana wa Mungu walikuja kujidhihirisha mbele za Yehova, naye Shetani akaja pia kati yao. Naye Yehova akasema kwa Shetani, Ni wapi umetoka? Basi Shetani akamjibu Yehova, na kunena, Natoka katika kuenda hapa na pale duniani, na katika kutembea juu chini humo. Naye Yehova akasema kwa Shetani, je, umemfikiria mtumishi Wangu Ayubu, kwamba hakuna hata mtu kama yeye duniani, mtu mtimilifu na mwaminifu, ambaye anamcha Mungu, na kuepuka maovu? Kisha Shetani akamjibu Yehova, na kusema, je, Ayubu anamcha Mungu bure? Wewe hujamzunguka kila upande na ukingo, na kila upande wa nyumba yake, na kila upande wa yote aliyo nayo? Umebariki kazi ya mikono yake, na mali yake inaongezeka nchini. Lakini nyosha mbele mkono Wako sasa, na uguse yote aliyo nayo, na yeye atakulaani mbele ya uso Wako.

Ayubu 2:1-5 Tena kulikuweko na siku ambapo wana wa Mungu walikuja kujidhihirisha mbele za Yehova, naye Shetani akaja pia kati yao ili kujidhihirisha mbele za Yehova. Naye Yehova akasema kwa Shetani, Ni wapi umetoka? Na Shetani akamjibu Yehova, na kunena, Natoka katika kuenda hapa na pale duniani, na katika kutembea juu chini humo. Naye Yehova akasema kwa Shetani, je, umemfikiria mtumishi Wangu Ayubu, kwamba hakuna hata mtu kama yeye duniani, mtu mtimilifu na mwaminifu, ambaye anamcha Mungu, na kuepuka maovu? Na bado anashikilia ukamilifu wake, ingawa ulinichochea dhidi yake, ili mimi nimwangamize bila sababu. Naye Shetani akamjibu Yehova, na akasema, Ngozi kwa ngozi, ndiyo, yote ambayo mtu anayo atayatoa kwa sababu ya uhai wake. Lakini nyosha mbele mkono Wako sasa, na uguse mfupa wake na nyama yake, na yeye atakulaani mbele ya uso Wako.

Vifungu hivi viwili vinajumuisha kikamilifu mazungumzo kati ya Mungu na Shetani; vinarekodi kile alichosema Mungu na kile alichosema Shetani. Mungu hakuzungumza sana, na Aliongea kwa urahisi sana. Tunaweza kuona utakatifu wa Mungu katika maneno rahisi ya Mungu? Wengine watasema “hii si rahisi.” Hivyo tunaweza kuona ubaya wa Shetani katika majibu yake? Kwanza wacha tuangalie ni aina gani ya swali ambalo Yehova Mungu alimwuliza Shetani. “Ni wapi umetoka?” Hili ni swali linaloeleweka kwa urahisi? Kuna maana iliyofichwa? La; ni swali la moja kwa moja tu. Kama Ningekuuliza: “Unatoka wapi wewe?” mngejibu vipi? Ni swali gumu kujibu? Mngesema: “Natoka katika kuzungukazunguka, na katika kutembea huku na huku”? (La.) Hamngejibu namna hii, kwa hivyo mnahisi aje mnapomwona Shetani akijibu kwa njia hii? (Tunahisi kwamba Shetani ni mpumbavu na mjanja.) Unaweza kusema ni nini Ninachohisi? Kila wakati Ninapoona maneno haya Nahisi kuchukizwa kwa sababu anazungumza bila kusema lolote. Alijibu swali la Mungu? Maneno yake hayakuwa jibu, hakukuwa na matokeo yoyote. Hayakuwa jibu lililoelekezwa kwa swali la Mungu. “Natoka katika kuenda hapa na pale duniani, na katika kutembea juu chini humo.” Unaelewa nini kutoka kwa maneno haya? Shetani ametoka wapi duniani? Mmepata jibu? (La.) Hii ndiyo “akili” ya ujanja wa Shetani, kutomwacha yeyote kujua anachosema. Baada ya kuyasikia maneno haya, bado huwezi kutambua ni nini amesema, ilhali amemaliza kujibu. Anaamini kwamba amejibu vizuri sana. Basi unahisi vipi? Kuchukizwa? (Ndiyo.) Sasa unaanza kuchukizwa na maneno haya. Maneno ya Shetani yana tabia ya aina fulani: Kile anachosema Shetani hukuacha ukikuna kichwa chako , usiweze kutambua chanzo cha maneno yake. Wakati mwingine Shetani huwa na nia na huzungumza kimakusudi, na wakati mwingine akitawaliwa na asili yake, maneno ya aina hiyo hutokea ghafla, na kutoka moja kwa moja kinywani mwa Shetani. Shetani hatumii muda mrefu kuyapima maneno ya aina hiyo; badala yake, yeye huyatoa bila kufikiri. Mungu alipouliza alipokuwa anatoka, Shetani alijibu kwa maneno machache yasiyo na maana kamili. Unahisi kuchanganyikiwa, bila kujua ametoka wapi hasa. Kuna wowote kati yenu wanaozungumza hivi? Hii ni njia ya aina gani ya kuzungumza? (Si dhahiri na haina jibu la uhakika.) Tunapaswa kutumia aina gani ya maneno kuelezea namna hii ya kuzungumza? Ni ya kupotosha na kudanganya, au siyo? Tuseme mtu hataki wengine wajue kile alichofanya jana. Unamwuliza: “Nilikuona jana. Ulikuwa unaelekea wapi?” Hakwambii moja kwa moja alikokwenda. Badala yake anasema: “Jana ilikuwa siku ya ajabu kweli. Nimechoka sana!” Je, walijibu swali lako? Walijibu, lakini hilo si jibu ulilokuwa unataka. Huu ni “werevu” wa ujanja wa mwanadamu. Huwezi kugundua wanachomaanisha ama kutambua chanzo ama nia nyuma ya maneno yao. Hujui ni nini wanachojaribu kuepuka kwa sababu ndani ya mioyo yao wanayo hadithi yao wenyewe—hili ni jambo lenye kudhuru kwa siri. Je, kunao wowote kati yenu wanaozungumza namna hii mara kwa mara? (Ndiyo.) Basi madhumuni yenu ni yapi? Je, huwa ni kulinda maslahi yenu wakati mwingine, wakati mwingine kudumisha fahari, nafasi na taswira zenu, kuweka siri za maisha yenu ya binafsi? Licha ya madhumuni, hayatenganishwi na maslahi yenu, yanahusiana na maslahi yenu. Hii sio asili ya mwanadamu? Wote walio na asili ya aina hii wana uhusiano wa karibu na Shetani nusra wawe jamaa wake. Tunaweza kulisema namna hiyo, siyo? Kuzungumza kwa ujumla, huu udhihirisho ni wenye makuruhu na wa kusinya. Mnahisi pia sasa kuchukizwa, sivyo? (Ndiyo.)

Tukiangalia tena kifungu cha kwanza, Shetani anamjibu tena Yehova, akisema: “Je, Ayubu anamcha Mungu bure?” Shetani anaanzisha mashambulizi juu ya tathmini ya Yehova kwa Ayubu, na shambulio hili linapakwa rangi na uhasama. “Wewe hujamzunguka kila upande na ukingo, na kila upande wa nyumba yake, na kila upande wa yote aliyo nayo?” Huu ndio uelewa na tathmini ya Shetani ya kazi ya Yehova kwa Ayubu. Shetani anaitathmini hivi, akisema: “Umebariki kazi ya mikono yake, na mali yake inaongezeka nchini. Lakini nyosha mbele mkono Wako sasa, na uguse yote aliyo nayo, na yeye atakulaani mbele ya uso Wako.” Shetani huongea kwa utata kila mara, lakini hapa anaongea kwa uhakika. Hata hivyo, maneno haya yaliyozungumzwa kwa uhakika ni shambulio, ni kufuru na ni upinzani kwa Yehova Mungu, kwa Mungu Mwenyewe. Mnahisi vipi mnapomsikia? Mnahisi chuki? Mnaweza kuona nia zake? Kwanza kabisa, anakataa kabisa tathmini ya Yehova ya Ayubu—yule anayemwogopa Mungu na kuepuka maovu. Kisha anakataa kabisa kila kitu anachosema na kufanya Ayubu, yaani, anakataa kumcha Yehova. Je, yeye anashitaki? Shetani anashitaki, anakataa na anashuku kila anachofanya na kusema Yehova. Haamini, akisema, “Ukisema mambo yako namna hii, mbona sijaiona? Umempa baraka nyingi, anawezaje kukosa kukucha?” Je, huku si kukataa kabisa kila anachofanya Mungu? Kushitaki, kukataa, kufuru—maneno yake si ya ugomvi? Si ni maonyesho ya ukweli ya kile anachofikiria Shetani ndani ya moyo wake? Haya maneno hakika si sawa na maneno tuliyoyasoma hivi sasa: “Natoka katika kuenda hapa na pale duniani, na katika kutembea juu chini humo.” Ni tofauti sana na hayo. Kupitia maneno haya, Shetani anaweka wazi mtazamo wake kwa Mungu na kuchukizwa na kumcha Mungu kwa Ayubu ambako kuko katika moyo wake. Haya yakifanyika, ubaya wake na asili yake mbovu inafichuliwa kabisa. Anawachukia wale wanaomcha Mungu, anawachukia wale wanaoepukana na maovu, na hata zaidi anamchukia Yehova kwa sababu ya kumpa mwanadamu baraka. Anataka kutumia fursa hii kumwangamiza Ayubu ambaye Mungu alimwinua na mkono Wake mwenyewe, kumwangamiza, akisema: “Unasema Ayubu anakuogopa na kuepukana na maovu. Naiona vingine.” Anatumia mbinu mbalimbali kumchochea na kumjaribu Yehova, na kutumia mbinu mbalimbali ili Yehova Mungu amkabidhi Ayubu kwa Shetani ili atawaliwe, adhuriwe na ashughulikiwe kwa ukatili. Anataka kutumia fursa hii ili kumwangamiza mtu huyu ambaye ni mwenye haki na mtimilifu katika macho ya Mungu. Yeye kuwa na moyo wa aina hii ni msukumo wa muda mfupi? La, siyo. Imekuwa ikiundwa kwa muda mrefu. Mungu anafanya kazi, Mungu anamtunza mtu, anamwangalia mtu, na Shetani anafuata hatua Yake yote. Yeyote anayefadhiliwa na Mungu, Shetani pia anatazama, akifuata nyuma. Iwapo Mungu anamtaka mtu huyu, Shetani atafanya kila kitu kwa uwezo wake kumzuia Mungu, akitumia mbinu mbalimbali mbovu kujaribu, kusumbua na kuharibu kazi anayofanya Mungu ili kufikia lengo lake lililofichwa. Lengo lake ni nini? Hataki Mungu awe na mtu yeyote; anataka wale wote ambao Mungu anataka, kuwamiliki, kuwatawala, kuwaelekeza ili wamwabudu, ili watende maovu pamoja naye. Je, hii siyo nia ya husuda ya Shetani? Kwa kawaida, ninyi husema mara nyingi kwamba Shetani ni mwovu sana, mbaya sana, lakini umemwona? Mnaweza kuona tu jinsi ambavyo mwanadamu ni mbaya na hamjaona kwa uhakika jinsi ambavyo Shetani ni mbaya sana. Lakini mmemwona kwa hili swala linalohusiana na Ayubu? (Ndiyo.) Swala hili limeufanya uso wenye sura mbaya wa Shetani na kiini chake kuwa wazi kabisa. Shetani yuko vitani na Mungu, akifuata nyuma Yake. Lengo lake ni kubomoa kazi yote ambayo Mungu anataka Kufanya, kuwamiliki na kudhibiti wale wote ambao Mungu anawataka, kuwafisha kabisa wale ambao Mungu anataka. Kama hawajafishwa, basi wanakuja kwa milki ya Shetani kutumiwa naye—hili ndilo lengo lake. Na Mungu anafanya nini? Mungu anasema tu sentensi rahisi katika kifungu hiki; hakuna rekodi ya chochote zaidi ambacho Mungu anafanya, lakini tunaona kwamba kuna rekodi nyingi zaidi za kile ambacho Shetani anafanya na kusema. Katika kifungu cha maandishi hapa chini, Yehova alimwuliza Shetani, “Ni wapi umetoka?” Jibu la Shetani ni nini? (Bado ni “Natoka katika kuenda hapa na pale duniani, na katika kutembea juu chini humo.”) Bado ni sentensi hiyo. Imekuwaje wito wa Shetani, kazi ya Shetani ya ujuzi wa juu? Si Shetani ni wa kuchukia? Kusema sentensi hii inayochafua moyo mara moja inatosha. Kwa nini Shetani daima anarejelea Sentensi hii? Hii inadhihirisha kitu kimoja: asili ya Shetani haibadiliki. Shetani hawezi kutumia visingizio kuficha uso wake mbaya. Mungu anamwuliza swali na anajibu kwa njia kama hiyo, sembuse anavyotendea watu! Hamwogopi Mungu, hamchi Mungu, na hamtii Mungu. Hivyo anathubutu kuwa na kiburi kwa ukaidi mbele ya Mungu, kutumia haya maneno ili kujaribu kupuuza swali la Mungu, kutumia jibu hili moja kwa kurudia rudia kujibu swali la Mungu, kujaribu kutumia jibu hili kumshangaza Mungu—huu ndio uso usiopendeza wa Shetani. Haamini uweza wa Mungu, haamini mamlaka ya Mungu, na hakika hayuko tayari kujinyenyekeza chini ya mamlaka ya Mungu. Daima anampinga Mungu, daima anashambulia yote anayofanya Mungu, akijaribu kuharibu yote ambayo Mungu anafanya—hili ndilo lengo lake ovu.

Katika mpango wa Mungu wa usimamizi wa miaka elfu sita, vifungu hivi viwili ambavyo Shetani anasema na mambo ambayo Shetani anafanya katika kitabu cha Ayubu yanawakilisha upinzani wake kwa Mungu, na hivi ndivyo Shetani akidhihirisha alivyo kwa kweli. Umeyaona maneno na matendo ya Shetani katika maisha halisi? Utakapoyaona, unaweza kutoyafikiria kuwa vitu vilivyoongelewa na Shetani, lakini badala yake kuyafikiria kuwa vitu vilivyoongelewa na mwanadamu. Kipi kilichowakilishwa, wakati mambo kama hayo yanazungumzwa na mwanadamu? Shetani anawakilishwa? Hata kama utamtambua, bado huwezi kuona kwamba ukweli unazungumzwa na Shetani. Lakini hapa na sasa umeona bila shaka kile ambacho Shetani mwenyewe amesema. Sasa una uelewa usio na shaka na ulio wazi kabisa wa uso wenye sura mbaya na uovu wa Shetani. Hivyo hivi vifungu viwili vilivyozungumzwa na Shetani ni vya thamani kwa watu wa leo kuweza kujua asili ya Shetani? Hivi vifungu viwili vinastahili kukusanywa ili binadamu leo aweze kutambua uso wenye sura mbaya wa Shetani, kutambua uso wa asili na wa kweli wa Shetani? Ingawa kusema jambo hili hakuonekani kufaa sana, kulieleza kwa njia hii bado kunaweza kuchukuliwa kuwa sahihi. Naweza tu kuliweka kwa njia hii na iwapo mnalielewa, basi imetosha. Tena na tena, Shetani anayashambulia mambo ambayo Yehova anafanya, akitoa mashtaka kuhusu kumcha Yehova kwa Ayubu. Anajaribu kumchochea Yehova kwa kutumia mbinu mbalimbali, kumfanya Yehova Mungu kumkubali kumjaribu Ayubu. Maneno yake basi yanachochea sana. Basi Niambieni, baada ya Shetani kuzungumza maneno haya, Mungu anaweza kuona wazi kile ambacho Shetani anataka kufanya? (Ndiyo.) Katika moyo wa Mungu, huyu mtu Ayubu ambaye Mungu anamwangalia—huyu mtumishi wa Mungu, ambaye Mungu anamchukulia kuwa mwenye haki, mtu mtimilifu—anaweza kuyahimili majaribio ya aina hii? (Ndiyo.) Kwa nini Mungu ana uhakika sana kuhusu hilo? Mungu huchunguza moyo wa binadamu daima? (Ndiyo.) Kwa hivyo Shetani anaweza kuchunguza moyo wa binadamu? Shetani hawezi. Hata kama Shetani anaweza kuona moyo wa mwanadamu, asili yake mbovu haiwezi kuamini kwamba utakatifu ni utakatifu, ama kwamba uchafu ni uchafu. Shetani mwovu hawezi kuthamini chochote kilicho takatifu, chenye haki ama chenye kung’aa. Shetani hawezi kuepuka kuumiza kwa kutenda kupitia asili yake, uovu wake, na kupitia mbinu hizi anazotumia. Hata kwa hatari ya yeye kuadhibiwa na kuangamizwa na Mungu, hasiti kumpinga Mungu kwa ukaidi—huu ni uovu, hii ni asili ya Shetani. Kwa hivyo katika kifungu hiki, Shetani anasema: “Ngozi kwa ngozi, ndiyo, yote ambayo mtu anayo atayatoa kwa sababu ya uhai wake. Lakini nyosha mbele mkono wako sasa, na uguse mfupa wake na nyama yake, na yeye atakulaani mbele ya uso Wako.” Shetani anafikiri kwamba kumcha Mungu kwa mwanadamu ni kwa sababu mwanadamu amepata manufaa mengi kutoka kwa Mungu. Mwanadamu hupata manufaa mengi kutoka kwa Mungu, kwa hivyo anasema Mungu ni mwema. Lakini si kwa sababu Mungu ni mwema, ni kwa sababu tu mwanadamu amepata manufaa mengi na hivyo anaweza kumcha Mungu kwa njia hii: Punde Mungu anapomnyima manufaa haya, basi anaachana na Mungu. Katika asili yake mbovu, Shetani haamini kwamba moyo wa mwanadamu kwa kweli unaweza kumcha Mungu. Kwa sababu ya asili yake mbovu hajui utakatifu ni nini, na hata chini zaidi hajui heshima ya kuogopa ni nini. Hajui ni nini kumtii Mungu ama ni nini kumcha Mungu. Kwa sababu yeye mwenyewe hazijui, anafikiri mwanadamu hawezi kumcha Mungu pia. Niambieni, si Shetani ni mwovu? Isipokuwa kanisa letu, hakuna kati ya makundi ya kidini na madhehebu mbalimbali, ama makundi ya kidini na ya kijamii, yanayoamini uwepo wa Mungu, sembuse wao kuamini kwamba Mungu amekuwa mwili na Anafanya kazi ya hukumu, hivyo wanafikiri kwamba kile unachoamini si Mungu. Mwanamume mzinzi huangalia huku na kule na kumwona kila mtu mwingine kama mzinzi, kama alivyo yeye. Mwanadamu anayedanganya kila wakati anaangalia na kuona hakuna mtu mwaminifu, anawaona wote wakidanganya. Mtu mwovu anawaona watu wote wakiwa waovu na anataka kupigana na kila mtu anayemwona. Wakati wale watu ambao walio na uaminifu kwa kulinganisha wanawaona wote kuwa waaminifu, na hivyo daima wanalaghaiwa, wanadanganywa, na hakuna wanachoweza kufanya kuhusu hilo. Nasema mifano hii michache ili kuwafanya kuwa na uhakika zaidi: asili mbovu ya Shetani si msukumo wa muda mfupi ama kitu kinachosababishwa na mazingira yake, wala si udhihirisho wa muda ulioletwa na sababu yoyote ama usuli wowote. Sivyo kabisa! Hana namna ila kuwa hivyo! Hawezi kufanya chochote chema! Hata anaposema kitu kinachofurahisha kusikia, anakushawishi tu. Kadiri maneno yake yanavyofurahisha, yenye busara zaidi, uungwana zaidi, ndivyo nia zake za husuda zinakuwa za kijicho zaidi nyuma ya maneno haya. Shetani anaonyesha uso na asili ya aina gani katika vifungu hivi viwili? (Ya kudhuru kwa siri, yenye kijicho, na mbovu.) Tabia yake ya msingi ni mbovu, hasa mbovu na yenye kijicho.

Kwa sababu sasa tumemaliza kuzungumza kuhusu Shetani, hebu turudie kuzungumza kuhusu Mungu wetu. Wakati wa mpango wa usimamizi wa miaka elfu sita wa Mungu, matamshi machache sana ya moja kwa moja ya Mungu yamerekodiwa katika Biblia, na yale yaliyorekodiwa ni rahisi sana. Hivyo acha tuanzie mwanzoni. Mungu alimuumba mwanadamu na tangu hapo daima Ameongoza maisha ya binadamu. Iwe kwa kuwapa wanadamu baraka, kuwapa sheria na amri Zake, ama kuweka masharti kanuni mbalimbali za maisha, mnajua lengo analonuia Mungu kwa kufanya mambo haya ni nini? Kwanza, mnaweza kusema kwa uhakika kwamba yote anayofanya Mungu ni kwa wema wa binadamu? Mnaweza kufikiria kwamba sentensi hii kwa kulinganishwa ni pana na tupu, lakini kuzungumza hasa, si kila kitu anachofanya Mungu ni cha kumwongoza na kumwelekeza mwanadamu kuishi maisha ya kawaida? Iwe ili mwanadamu ashike kanuni Zake ama ashike sheria Zake, lengo la Mungu ni kwa mwanadamu kutomwabudu Shetani, kutodhuriwa na Shetani; hili ndilo la msingi zaidi, na hili ndilo lililofanywa mwanzoni kabisa. Mwanzoni kabisa, wakati mwanadamu hakuelewa mapenzi ya Mungu, Alichukua baadhi ya sheria na kanuni rahisi na kuweka masharti yaliyoshughulikia vipengele vyote vinavyoweza kufikiriwa. Masharti haya ni rahisi, lakini ndani yake kuna mapenzi ya Mungu. Mungu anamthamini, Anamtunza na kwa hakika Anampenda mwanadamu. Kwa hivyo tunaweza kusema kwamba moyo Wake ni mtakatifu? Tunaweza kusema kwamba moyo wake ni safi? (Ndiyo.) Je, Mungu anazo nia zilizofichwa? (La.) Kwa hivyo hili lengo Lake ni sahihi na halisi? Haijalishi masharti aliyoweka Mungu, katika kazi Yake yote yana athari halisi kwa mwanadamu, na yanaongoza njia. Kwa hivyo kuna fikira zozote za kibinafsi katika akili ya Mungu? Je, Mungu anayo malengo zaidi kuhusiana na mwanadamu, ama Anataka kumtumia mwanadamu kwa jinsi fulani? La hasha. Mungu anafanya Asemavyo, na pia Anafikiria namna hii moyoni Mwake. Hakuna mchanganyiko wa madhumuni, hakuna fikira za kibinafsi. Hajifanyii chochote, lakini Anamfanyia mwanadamu kila kitu kabisa, bila malengo yoyote ya kibinafsi. Ingawa Ana mipango na nia kwa mwanadamu, Hajifanyii chochote. Kila kitu Anachofanya kinafanyiwa mwanadamu tu, kumlinda mwanadamu, kumhifadhi mwanadamu dhidi ya kupotezwa. Hivyo si moyo huu Wake ni wenye thamani? Unaweza kuona hata ishara kidogo zaidi ya moyo wenye thamani kama huu ndani ya Shetani? (La.) Huwezi kuliona dokezo moja la moyo huu kwa Shetani. Kila kitu anachofanya Mungu kinafichuliwa kiasili. Sasa, hebu tutazame jinsi ambavyo Mungu anafanya kazi; Anafanyaje kazi kazi Yake? Je, Mungu anazichukua sheria hizi na maneno Yake na kuyafunga pamoja kwa kukaza juu ya kichwa cha kila mtu, kama kama laana inayofungwa na ukanda[a], Akizilazimisha kwa kila mwanadamu? Je, Anafanya kazi namna hii? (La.) Kwa hivyo Mungu anafanya kazi Yake namna gani? Je, Anatishia? Je, Yeye huwazungumzia kwa njia isiyo ya moja kwa moja? (La.) Wakati huelewi ukweli, Mungu hukuongoza vipi? Anakuangazia, akikwambia wazi kwamba kufanya haya hakuambatani na ukweli, na kisha Anakuambia kile unachofaa kufanya. Kutoka kwa njia hizi ambazo Mungu anafanya kazi, unahisi kwamba una uhusiano wa aina gani na Mungu? Je, unahisi kwamba Mungu si mwenye kufikiwa? (La.) Hivyo unahisije unapoona njia hizi ambazo kwazo Mungu hufanya kazi? Maneno ya Mungu ni halisi hasa, na uhusiano Wake na mwanadamu ni wa kawaida hasa. Mungu yuko karibu nawe kwa njia ya pekee; hakuna umbali kati yako na Mungu. Wakati Mungu anakuongoza, Anapokukimu, Anapokusaidia na kukufadhili, unahisi jinsi Mungu alivyo mpole, uchaji Anaoleta; unahisi jinsi Anavyopendeza, unahisi joto Lake. Lakini Mungu anaposhutumu upotovu wako, ama Anapokuhukumu na kukufundisha nidhamu kwa sababu ya kuasi dhidi Yake, Mungu anatumia njia gani? Anakushutumu kwa kutumia maneno? Anakufundisha nidhamu kupitia mazingira yako na kupitia kwa watu, masuala na mambo? (Ndiyo.) Nidhamu hii inafika kiwango kipi? Je, inafikia mahali sawa ambapo Shetani anamdhuru mwanadamu? (La, inafika kiwango ambacho mwanadamu anaweza kuvumilia.) Mungu anafanya kazi kwa njia ya upole, laini, yenye upendo na ya kujali, kwa njia iliyopimwa kwa namna ya ajabu na sahihi. Njia Yake haikufanyi uhisi hisia kali ya mhemuko kama vile; “Mungu lazima aniache nifanye hivi” ama “Lazima Mungu aniache nifanye vile.” Mungu kamwe hakupi mawazo hisia kali zinazofanya mambo yawe yenye kutovumilika. Sivyo? Hata unapoyakubali maneno ya Mungu ya hukumu na kuadibu, unahisi vipi basi? Unapohisi mamlaka ya Mungu na nguvu ya Mungu, unahisi vipi basi? Unahisi kwamba Mungu ni mtakatifu na asiyekosewa? Je, wewe huhisi umbali kati yako na Mungu katika nyakati hizi? Je, wewe huhisi hofu ya Mungu? La—badala yake, unahisi uchaji wenye hofu kwa Mungu. Je, si kwa sababu ya kazi ya Mungu kwamba watu huhisi mambo haya yote? Je, wangekuwa na hisia hizi ikiwa Shetani ndiye aliyekuwa akifanya kazi? La hasha. Mungu hutumia maneno Yake, ukweli Wake na uhai Wake kuendelea bila kusita kumkimu mwanadamu, kumfadhili mwanadamu. Wakati mwanadamu ni mnyonge, wakati mwanadamu anahisi huzuni, Mungu kwa hakika hazungumzi kwa ukali, akisema: “Usihisi mwenye kukata tamaa? Kwa nini wewe ni dhaifu? Kuna sababu gani ya kuwa dhaifu? Wewe huwa dhaifu sana daima, na wewe daima huwa hasi! Kuna haja gani ya wewe kuwa hai? Kufa tu!” Je, Mungu anafanya kazi hivi? (La.) Je, Mungu ana mamlaka ya kutenda kwa namna hii? Ndiyo, Anayo. Lakini Mungu hatendi kwa namna hii. Mungu hatendi hivi kwa sababu ya kiini Chake, kiini cha utakatifu wa Mungu. Upendo Wake kwa mwanadamu, kuthamini na utunzaji Wake wa mwanadamu haviwezi kuelezwa wazi kwa sentensi moja au mbili. Si kitu kinacholetwa na kujisifu kwa mwanadamu lakini ni kitu ambacho Mungu analeta kupitia kwa vitendo halisi; ni ufunuo wa kiini cha Mungu. Je, hizi njia zote ambazo Mungu anafanya kazi zinaweza kumruhusu mwanadamu kuona utakatifu wa Mungu? Kwa hizi njia zote ambazo Mungu anafanya kazi, zikiwemo nia nzuri za Mungu, zikiwemo athari ambazo Mungu anataka kutimiza kwa mwanadamu, zikiwemo njia mbalimbali ambazo Mungu anatumia kufanya kazi kwa mwanadamu, aina ya kazi Anayofanya, kile Anachotaka mwanadamu kuelewa—umeona uovu ama ujanja wowote katika nia nzuri za Mungu? (La.) Hivyo, katika kila kitu ambacho Mungu anafanya, kila kitu ambacho Mungu anasema, kila kitu anachofikiria katika moyo Wake, na pia kiini chote cha Mungu anachofichua—tunaweza kumwita Mungu mtakatifu? (Ndiyo.) Mwanadamu yeyote amewahi kuona utakatifu huu duniani, ama kwake mwenyewe? Mbali na Mungu, umewahi kuuona ndani ya mtu yeyote ama ndani Shetani? (La.) Kutoka kwa yale tuliyoyazungumzia hadi sasa, tunaweza kumwita Mungu wa kipekee, Mungu mtakatifu Mwenyewe? (Ndiyo.) Yote ambayo Mungu anampa mwanadamu, yakiwemo maneno ya Mungu, njia tofauti ambazo kwazo Mungu anafanya kazi kwa mwanadamu, kile ambacho Mungu anamwambia mwanadamu, kile ambacho Mungu anamkumbusha mwanadamu kuhusu, kile ambacho Anashauri na kutia moyo, vyote vimetoka kwa kiini kimoja: Vyote vimetoka kwa utakatifu wa Mungu. Iwapo hakungekuwa na Mungu mtakatifu kama huyu, hakuna mwanadamu ambaye angechukua nafasi Yake kufanya kazi Anayofanya. Iwapo Mungu angewachukua watu hawa na kuwakabidhi kabisa kwa Shetani, mmewahi kuzingatia mngekuwa katika hali ya aina gani leo? Nyinyi nyote mngekuwa mmeketi hapa, kamili na wasioharibika? Pia mngesema: “Natoka katika kuenda hapa na pale duniani, na katika kutembea juu chini humo”? Je, ungekuwa mshupavu sana, mwenye uhakika sana na mjeuri kupindukia kiasi cha kusema maneno kama hayo na kujigamba bila haya mbele za Mungu? Hakika ungefanya, bila shaka yoyote! Mtazamo wa Shetani kwa mwanadamu unawaruhusu kuona kwamba asili na kiini cha Shetani ni tofauti kabisa na cha Mungu. Kiini kipi cha Shetani ni kinyume cha utakatifu wa Mungu? (Uovu wake.) Asili ya uovu ya Shetani ni kinyume na utakatifu wa Mungu. Watu wengi zaidi hawatambui maonyesho haya ya Mungu na kiini hiki cha utakatifu wa Mungu ni kwa sababu wanaishi chini ya umiliki wa Shetani, ndani ya upotovu wa Shetani na ndani ya boma anamoishi Shetani. Hawajui utakatifu ni nini ama jinsi ya kufafanua utakatifu. Hata unapoona utakatifu wa Mungu, bado huwezi kuufafanua kuwa utakatifu wa Mungu kwa uhakika wowote. Hii ni tofauti katika maarifa ya mwanadamu ya utakatifu wa Mungu.

Ni sifa ya uwakilishi ya aina gani inayoonyeshwa na kazi ya Shetani kwa mwanadamu? Mnapaswa kuweza kujifunza hii kupitia uzoefu wenu wenyewe—ndiyo sifa ya uwakilishi zaidi ya Shetani, kitu ambacho anafanya zaidi, kitu ambacho anajaribu kufanya na kila mtu. Pengine hamwezi kuona sifa hii, kwa hivyo hamhisi kwamba Shetani ni wa kutisha na wa kuchukia sana. Kuna mtu anayejua sifa hii ni nini? (Kila kitu anachofanya, anafanya ili kumdhuru mwanadamu.) Anamdhuru mwanadamu vipi? Mnaweza kuniambia hasa zaidi na kwa kina? (Anamshawishi, anamlaghai na kumjaribu mwanadamu.) Hii ni sahihi, hii inaonyesha vipengele kadhaa. Pia anamdanganya kumshambulia na kumtuhumu mwanadamu—haya yote. Kuna mengine zaidi? (Anasema uwongo.) Udanganyifu na uongo hujitokeza kiasili kabisa kwa Shetani. Anafanya hivi mara nyingi hadi uongo unabubujika kutoka kwa mdomo wake bila yeye hata kuhitaji kufikiria. Mengine zaidi? (Anapanda mfarakano.) Hii si muhimu sana. Nitawaelezea kitu ambacho kitawatisha, lakini Sifanyi hivyo ili kuwaogopesha. Mungu anafanya kazi kwa mwanadamu na mwanadamu anathaminiwa katika mtazamo wa Mungu na moyo Wake. Kinyume na hayo, je, Shetani anamthamini mwanadamu? Hamthamini mwanadamu. Anachofikiria tu ni kumdhuru mwanadamu. Hii si sahihi? Wakati anafikiria kumdhuru mwanadamu, anafanya hivyo katika hali ya dharura ya akili? (Ndiyo.) Kwa hivyo inapokuja kwa kazi ya Shetani kwa mwanadamu, hapa Nina virai viwili vinayoweza kuelezea vizuri asili yenye nia mbaya na ovu ya Shetani, vinavyoweza kuwaruhusu kujua chuki ya Shetani: Katika mtazamo wa Shetani kwa mwanadamu, daima anataka kumiliki na kumtawala kwa nguvu, kila mmoja wao, ili aweze kufika mahali ambapo anaweza kumdhibiti mwanadamu kabisa, kumdhuru mwanadamu, ili aweze kutimiza lengo hili na tamaa isiyowezekana. “Umiliki wa nguvu” unamaanisha nini? Unafanyika na kibali chako, ama bila kibali chako? Unafanyika na kujua kwako, ama bila kujua kwako? Ni bila kujua kwako kabisa! Katika hali ambazo huna ufahamu, pengine wakati hajasema chochote ama pengine wakati hajafanya chochote, wakati hakuna kauli kigezo, hakuna muktadha, yuko hapo karibu nawe, akikuzunguka. Anatafuta fursa ya kukunyonya, kisha anakumiliki kwa nguvu, anakutawala, akitimiza lengo lake la kukudhibiti kikamilifu na kukudhuru. Hii ni nia na tabia ya kawaida zaidi katika mapambano ya Shetani dhidi ya Mungu kwa ajili ya mwanadamu. Mnahisi vipi mnaposikia haya? (Tuna hofu na woga katika mioyo yetu.) Mnahisi kuchukizwa? (Ndiyo.) Mnapohisi kuchukizwa, mnafikiria Shetani hana haya? Mnapofikiria Shetani hana haya, mnahisi kuchukizwa na wale watu walio karibu nanyi ambao daima wanataka kuwatawala, wale walio na matarajio yasiyowezekana ya hadhi na maslahi yao? (Ndiyo.) Hivyo ni mbinu gani anazotumia Shetani kumtawala kwa nguvu na kummiliki mwanadamu? Mnaelewa hili vizuri? Mnaposikia maneno haya mawili “umiliki wa nguvu” na “utawala,” mnahisi chukizo na mnaweza kuhisi uovu ulio katika maneno haya. Bila kibali ama maarifa yako, Shetani anakutawala, anakumiliki kwa nguvu, na kukupotosha. Unaweza kuonja nini kwa moyo wako? Je, unahisi chuki na maudhi? (Ndiyo.) Wakati unahisi hii chuki na maudhi kwa njia hii ya Shetani, una hisia gani kwa Mungu? (Shukrani.) Shukrani kwa Mungu kwa kukuokoa. Kwa hivyo sasa, wakati huu, unayo hamu ama matakwa ya kumwacha Mungu aongoze kila kitu chako na kutawala kila kitu chako? (Ndiyo.) Kwa muktadha upi? Unasema ndiyo kwa sababu unaogopa kumilikiwa kwa nguvu na kutawaliwa na Shetani? (Ndiyo.) Huwezi kuwa na mawazo kama haya, siyo sahihi. Usiwe na hofu, Mungu yuko hapa. Hakuna chochote cha kuhofia. Ukishaelewa asili mbovu ya Shetani, unapaswa kuwa na uelewa sahihi zaidi ama upendo wa kina wa mapenzi ya Mungu, nia nzuri za Mungu, huruma ya Mungu na stahamala kwa mwanadamu na tabia Yake ya haki. Shetani ni wa kuchukia sana, lakini ikiwa hili bado haliutii moyo upendo wako kwa Mungu na utegemezi na uaminifu wako kwa Mungu, basi wewe ni mtu wa aina gani? Uko tayari kumwacha Shetani akudhuru hivyo? Baada ya kuona uovu na ubaya wa Shetani, tunageuka na kisha kumwangalia Mungu. Maarifa yako ya Mungu sasa yamepitia mabadiliko yoyote? Tunaweza kusema Mungu ni mtakatifu? Tunaweza kusema Mungu hana dosari? “Mungu ni utakatifu wa kipekee”—Mungu anaweza kuvumilia jina hili? (Ndiyo.) Hivyo duniani na miongoni mwa mambo yote, ni Mungu Mwenyewe pekee anayeweza kuvumilia huu uelewa wa mwanadamu? Kuna wengine? (La.) Hivyo, ni nini hasa ambacho Mungu anampa mwanadamu? Je, Anakupa tu utunzaji mdogo, wasiwasi na kukutia maanani kidogo wakati huko makini? Mungu amempa nini mwanadamu? Mungu amempa mwanadamu uhai, Amempa mwanadamu kila kitu, na amempa mwanadamu bila masharti bila kudai chochote, bila nia zozote za siri. Anatumia ukweli, Anatumia maneno Yake, Anatumia uhai Wake kumwongoza na kumwelekeza mwanadamu, kumtoa mwanadamu mbali na madhara ya Shetani, mbali na majaribio ya Shetani, mbali na ushawishi wa Shetani na kumruhusu mwanadamu aone wazi asili mbovu ya Shetani na uso wake unaotisha. Je, upendo na wasiwasi wa Mungu kwa binadamu ni wa kweli? Ni kitu ambacho kila mmoja wenu anaweza kupitia? (Ndiyo.)

Kumbuka maisha yenu hadi sasa kwa yote ambayo Mungu amekufanyia katika miaka yote ya imani yako. Iwapo unaihisi kwa kina au la, haikuwa ya umuhimu sana? Haikuwa kile ulichohitaji zaidi kupata? (Ndiyo.) Huu si ukweli? Huu si uhai? (Ndiyo.) Je, Mungu amewahi kukupa nuru, na kisha akuulize umpe Yeye chochote kama malipo ya yale yote Aliyokupa wewe? (La.) Kwa hivyo madhumuni ya Mungu ni yapi? Mbona Mungu anafanya hivi? Mungu pia ana lengo la kukumiliki? (La.) Je, Mungu anataka kuwa mfalme katika moyo wa mwanadamu? (Ndiyo.) Kwa hivyo ni nini tofauti kati ya Mungu kuwa mfalme na umiliki wa nguvu wa Shetani? Mungu anataka kupata moyo wa wanadamu, Anataka kumiliki moyo wa mwanadamu—hii inamaanisha nini? Je, inamaanisha kwamba Mungu anataka mwanadamu kuwa vikaragosi Vyake? Mashine Yake? (La.) Kwa hivyo madhumuni ya Mungu ni nini? Kuna tofauti kati ya Mungu kutaka kumiliki moyo wa mwanadamu na umiliki wa nguvu wa Shetani na utawala wa mwanadamu? (Ndiyo.) Tofauti ni nini? Mnaweza kuniambia waziwazi? (Shetani anafanya hivyo kwa nguvu ilhali Mungu anamwacha mwanadamu ajitolee.) Je, hii ndiyo tofauti? Mungu anautaka moyo wako Afanyie nini? Na zaidi ya hayo, kwa nini Mungu anataka kukumiliki? Mnaelewa vipi ndani ya mioyo yenu “Mungu anamiliki moyo wa mwanadamu”? Ni lazima tuwe na haki kwa Mungu hapa, vinginevyo watu daima hawataelewa, na kufikiri: “Mungu daima anataka kunimiliki. Anataka kunimiliki kwa nini? Sitaki kumilikiwa, nataka tu kuwa mimi mwenyewe. Mnasema Shetani anawamiliki watu, lakini Mungu pia anawamiliki watu: Haya si sawa? Sitaki kumwacha yeyote kunimiliki. Mimi ni mimi mwenyewe!” Tofauti hapa ni nini? Chukua dakika kuifikiria. Nawauliza, je “Mungu hummiliki mwanadamu” ni kirai tupu? Umiliki wa Mungu wa mwanadamu unamaanisha kwamba Anaishi katika moyo wako na anatawala kila neno na kusonga kwako? Akikwambia uketi, huthubutu kusimama? Akikwambia uende Mashariki, huthubutu kwenda Magharibi? Je, ni umiliki unaomaanisha kiti kama hiki? (La, siyo. Mungu anamtaka mwanadamu kuishi kwa kudhihirisha kile Mungu anacho na alicho.) Kwa miaka hii yote Mungu amemsimamia mwanadamu, kwa kazi Yake kwa mwanadamu hadi sasa kwa hatua hii ya mwisho, ni athari ipi imekusudiwa kwa mwanadamu kuhusu maneno yote ambayo Amesema? Je, ni kwamba mwanadamu anaishi kulingana na kile anacho Mungu na alicho? Kwa kuangalia maana halisi ya “Mungu humiliki moyo wa mwanadamu,” inaonekana kama Mungu anachukua moyo wa mwanadamu na kuumiliki, Anaishi ndani yake na Hatoki nje tena; Anakuwa bwana wa moyo wa mwanadamu na anaweza kutawala na kupanga moyo wa mwanadamu atakavyo, ili mwanadamu lazima atende asemayo Mungu atende. Hali ikiwa hivi, ingeonekana kana kwamba kila mtu anaweza kuwa Mungu na awe na kiini na tabia Yake. Kwa hivyo hapa, mwanadamu pia angeweza kufanya matendo ya Mungu? Je, “umiliki” unaweza kuelezewa kwa njia hii? (La.) Kwa hivyo ni nini? Nawauliza hili: Je, maneno na ukweli wote Mungu anampa mwanadamu ni ufunuo wa kiini cha Mungu na kile Anacho na alicho? (Ndiyo.) Hii ni ya uhakika. Lakini je, maneno yote Mungu anampa mwanadamu ni ya Mungu Mwenyewe kuweka katika vitendo, ya Mungu Mwenyewe kumiliki? Chukua dakika moja kuifikiria? Wakati Mungu anamhukumu mwanadamu, Anafanya hivi kwa sababu ya nini? Maneno haya yalitoka wapi? Ni nini yaliyomo katika maneno haya ambayo Mungu anazungumza Anapomhukumu mwanadamu? Ni nini msingi wake? Msingi wake ni tabia potovu ya mwanadamu? (Ndiyo.) Kwa hivyo athari iliyofikiwa na hukumu ya Mungu ya mwanadamu imetokana na kiini cha Mungu? (Ndiyo.) Kwa hivyo umiliki wa Mungu wa mwanadamu ni kirai tupu? Kwa hakika sicho. Kwa hivyo mbona Mungu anasema maneno haya kwa mwanadamu? Ni nini madhumuni Yake ya kusema maneno haya? Anataka kutumia maneno haya kutumika kama maisha ya mwanadamu? (Ndiyo.) Mungu anataka kutumia ukweli wote huu ambao amezungumza katika maneno haya kutumika kama maisha ya mwanadamu. Wakati mwanadamu anauchukua ukweli huu wote na neno la Mungu na kuyabadilisha katika maisha yake, mwanadamu basi anaweza kumtii Mungu? Mwanadamu basi anaweza kumcha Mungu? Mwanadamu basi anaweza kuepuka maovu? Wakati mwanadamu amefika hapa, anaweza basi kutii ukuu na mipango ya Mungu? Mwanadamu sasa yuko katika nafasi ya kutii mamlaka ya Mungu? Wakati watu kama Ayubu, ama kama Petro wanafika mwisho wa barabara yao, wakati maisha yao yanaweza kufikiriwa kuwa yamekomaa, wakati wako na uelewa halisi wa Mungu—Shetani bado anaweza kuwapoteza? Shetani bado anaweza kuwamiliki? Shetani bado anaweza kuwatawala kwa nguvu? (La.) Kwa hivyo huyu ni mtu wa aina gani? Huyu ni mtu ambaye amepatwa kabisa na Mungu? (Ndiyo.) Katika kiwango hiki cha maana, unamwonaje mtu huyu ambaye amepatwa kabisa na Mungu? Kwa Mungu, katika hali hii tayari Amemiliki moyo wa mtu huyu. Lakini mtu huyu anahisi nini? Je, ni kwamba neno la Mungu, mamlaka ya Mungu, na njia ya Mungu yamekuwa uhai ndani ya mwanadamu, basi uhai huu unamiliki utu wote wa mwanadamu, na unafanya yote anayozidi pamoja na kiini chake kutosha kumridhisha Mungu? Kwa Mungu, moyo wa binadamu wakati huu umemilikiwa na Yeye? (Ndiyo.) Mnaelewaje kiwango hiki cha maana sasa? Je, ni Roho wa Mungu anayekumiliki? (La, ni neno la Mungu ambalo linatumiliki.) Ni njia ya Mungu na neno la Mungu ambalo limekuwa maisha yako, na ni ukweli ambao umekuwa maisha yako. Wakati huu, mwanadamu basi ana maisha yanayotoka kwa Mungu, lakini hatuwezi kusema kwamba haya maisha ni maisha ya Mungu. Kwa maneno mengine, hatuwezi kusema kwamba maisha ambayo mwanadamu anapaswa kupata kutoka kwa neno la Mungu ni maisha ya Mungu. Hivyo, licha ya muda ambao mwanadamu anamfuata Mungu, licha ya idadi ya maneno ambayo mwanadamu anapata kutoka kwa Mungu, mwanadamu hawezi kuwa Mungu. Hata kama siku moja Mungu aseme, “Nimemiliki moyo wako, sasa unamiliki maisha Yangu,” utahisi basi kwamba wewe ni Mungu? (La.) Utakuwa nini basi? Hutakuwa na utii kabisa wa Mungu? Moyo wako hautajawa na maisha ambayo Mungu amekupa? Huu utakuwa udhihirisho wa kawaida kabisa wa kile kinachofanyika wakati Mungu anamiliki moyo wa mwanadamu. Huu ni ukweli. Kwa hivyo kuuangalia kutoka kipengele hiki, mwanadamu anaweza kuwa Mungu? Mwanadamu anapoweza kuishi kwa kudhihirisha uhalisi wa maneno ya Mungu, na kuwa mtu anayemcha Mungu nakuepuka maovu ndipo mwanadamu anaweza kiini cha uzima na utakatifu wa Mungu? Licha ya kile kitakachofanyika, mwanadamu bado ni mwanadamu wakati yote yamesemwa na kufanywa. Wewe ni kiumbe aliyeumbwa; wakati umepokea neno la Mungu kutoka kwa Mungu na kupokea njia ya Mungu, unamiliki tu maisha ambayo yanatoka katika maneno ya Mungu, unakuwa mtu anayesifiwa na Mungu, lakini kamwe hutakuwa na kiini cha uzima wa Mungu, sembuse utakatifu wa Mungu.

Tukirudia mada yetu hivi sasa, Niliwauliza swali—je, Ibrahimu ni mtakatifu? Ayubu ni mtakatifu? (La.) “Utakatifu” huu unawakilisha kiini na tabia ya Mungu, na mwanadamu amepungukiwa mno. Mwanadamu hana kiini cha Mungu ama tabia ya Mungu. Hata wakati mwanadamu amepitia maneno yote ya Mungu na amejitayarisha na uhalisi wake, mwanadamu bado hawezi kamwe kuwa na kiini kitakatifu cha Mungu; mwanadamu ni mwanadamu. Mnaelewa, sivyo? Kwa hivyo mnakielewaje kirai hiki “Mungu anakaa katika moyo ya mwanadamu” sasa? (Ni maneno ya Mungu, njia ya Mungu na ukweli Wake yanayokuwa maisha ya mwanadamu.) Umekariri maneno haya. Natumai mtakuwa na uelewa wa kina. Watu wengine wanaweza kuuliza, “Kwa hivyo mbona useme kwamba wajumbe na malaika wa Mungu si watakatifu?” Mnafikiria nini kuhusu swali hili? Labda hamjalifikiria mbeleni. Nitatumia mfano rahisi: Unapowasha roboti, inaweza kucheza ngoma na kuongea, na unaweza kuelewa inachosema. Unaweza kuiita nzuri na yenye uhai, lakini haitaelewa kwa sababu haina uhai. Unapozima uletaji wake wa umeme, bado inaweza kusongasonga? Wakati roboti hii inaamshwa, unaweza kuona ina uhai na ni nzuri. Unaitathmini, iwe ya kina au ya juujuu, lakini iwe vipi macho, unaweza kuiona ikisonga. Lakini unapozima uletaji wake wa umeme, unaona tabia ya aina yoyote kwake? Unaona ikiwa na kiini cha aina yoyote? Unaelewa maana ya kile ninachosema? Hivyo ni kusema, ingawaje roboti hii inaweza kusonga na inaweza kuacha, kamwe hungeweza kuielezea kama kuwa na aina yoyote ya kiini. Huu si ukweli? Hatutazungumzia haya zaidi. Yametosha kwenu kuwa na uelewa wa jumla wa maana. Hebu tutamatishe ushirika wetu hapa. Kwaheri!

Desemba 17, 2013

Tanbihi:

a. “laana inayofungwa na ukanda” ni laana inayotumiwa na mtawa Tang Sanzang katika riwaya ya Kichina Safari ya Magharibi. Anatumia laana hii kumdhibiti Sun Wukong kwa kufunga ukanda wa chuma kwenye kichwa cha Sun Wukong, ukimfanya aumwe na kichwa sana, na hivyo kumfanya aweze kudhibitiwa. Imekuwa istiara ya kueleza kitu kinachomfunga mtu.

Iliyotangulia: Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee III

Inayofuata: Mungu Mwenyewe, Yule wa Kipekee V

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp