Jinsi ya Kuhudumu kwa Upatanifu na Mapenzi ya Mungu

Mtu anapomwamini Mungu, mtu anapaswa kumtumikiaje, hasa? Ni masharti yapi yanayopaswa kutimizwa na ni ukweli upi unaopaswa kufahamika na wale wanaomhudumia Mungu? Na ni wapi unapoweza kuwa ukikengeuka katika huduma yako? Unapaswa kuwa na majibu ya mambo haya yote. Masuala haya yanagusia jinsi unavyomwamini Mungu, jinsi unavyotembea katika njia ya kuongozwa na Roho Mtakatifu, na jinsi unatii mipango ya Mungu katika mambo yote, na yatakuwezesha kujua kila hatua ya kazi ya Mungu ndani yako. Ukifika mahali hapo utafurahia kujua imani katika Mungu ni nini, namna ya kumwamini Mungu vizuri, na kile unachopaswa kufanya ili kutenda mambo kwa upatanifu na mapenzi ya Mungu. Hili litakufanya utii kikamilifu kazi ya Mungu, na hutakuwa na malalamiko, hutahukumu, au kuchambua, sembuse kutafiti. Zaidi ya hayo, nyote mtakuwa na uwezo wa kumtii Mungu hadi kifo, mkimruhusu Mungu awaongoze na kuwachinja kama kondoo, ili nyote muweze kuwa akina Petro wa miaka ya tisini, na muweze kumpenda Mungu kwa hali ya juu sana hata msalabani, bila malalamiko yoyote. Hivyo ndivyo mtakavyoweza kuishi kama akina Petro wa miaka ya tisini.

Kila mtu ambaye ameamua anaweza kumhudumia Mungu—lakini ni lazima iwe kwamba wale tu ambao wanayashughulikia kwa makini mapenzi ya Mungu na kuyafahamu mapenzi ya Mungu ndio wanaohitimu na walio na haki ya kumhudumia Mungu. Nimegundua hili kati yenu: Watu wengi wanaamini ya kuwa bora tu wanaeneza injili kwa bidii kwa ajili ya Mungu, waende barabarani kwa ajili ya Mungu, wajitumie na kuacha vitu kwa ajili ya Mungu, na kadhalika, basi huku ni kumhudumia Mungu; hata zaidi, watu wa kidini huamini kwamba kumhudumia Mungu kuna maana ya kukimbia hapa na pale wakiwa na Biblia mikononi mwao, wakieneza injili ya ufalme wa mbinguni na kuwaokoa watu kwa kuwafanya watubu na kuungama; kuna wakuu wengi wa kidini wanaofikiri kwamba kumhudumia Mungu ni kuhubiri makanisani baada ya kusoma na kufunzwa katika chuo cha seminari, kuwafunza watu kwa kusoma sura za Biblia; pia kuna watu katika maeneo ya umaskini wanaoamini kwamba kumhudumia Mungu kuna maana ya kupokea uponyaji na kufukuza mapepo, au kuwaombea ndugu, au kuwahudumia; miongoni mwenu, kunao wengi wanaoamini kwamba kumhudumia Mungu kuna maana ya kula na kunywa maneno ya Mungu, kumwomba Mungu kila siku, na pia kutembelea na kufanya kazi katika makanisa kila mahali; kunao ndugu wengine wanaoamini kwamba kumhudumia Mungu kunamaanisha kutoolewa wala kulea familia kamwe, na kutoa nafsi zao zote kwa Mungu. Ilhali watu wachache wanajua maana ya kweli ya kumhudumia Mungu. Ingawa kunao wengi wanaomhudumia Mungu kama nyota angani, idadi ya wale wanaoweza kuhudumu moja kwa moja, na wanaoweza kutumikia kulingana na mapenzi ya Mungu, ni hafifu—ndogo isiyo na maana. Kwa nini Ninasema hivi? Ninasema hivi kwa sababu wewe hufahamu kiini cha fungu la maneno “huduma kwa Mungu,” na unafahamu machache sana kuhusu jinsi ya kutumikia kulingana na mapenzi ya Mungu. Kuna hitaji la haraka kwa watu kuelewa hasa ni aina gani ya huduma kwa Mungu ndiyo inayoweza kulingana na mapenzi Yake.

Ikiwa ungependa kutumikia kulingana na mapenzi ya Mungu, ni lazima kwanza ufahamu ni watu wa aina gani wanamfurahisha Mungu, ni watu wa aina gani wanachukiwa na Mungu, ni watu wa aina gani wanafanywa kuwa kamili na Mungu, na ni watu wa aina gani wana sifa zinazostahili kumhudumia Mungu. Hiki ni kiasi kidogo zaidi unachopaswa kujiandaa nacho. Isitoshe, unapaswa kujua malengo ya kazi ya Mungu, na kazi ambayo Mungu Ataitenda hapa na wakati huu. Baada ya kufahamu haya, na kupitia kwa mwongozo wa maneno ya Mungu, kwanza unafaa kuingia, na kupokea agizo la Mungu kwanza. Unapopata uzoefu wa kweli kwa msingi wa maneno ya Mungu, na unapojua kweli kazi ya Mungu, utakuwa umehitimu kumhudumia Mungu. Na unapomhudumia ndipo Mungu hufungua macho yako ya kiroho, na kukuruhusu kuwa na ufahamu mkubwa zaidi wa kazi Yake na kuiona dhahiri zaidi. Ukiingia katika ukweli huu, uzoefu wako utakuwa wa kina zaidi na wa kweli, na wale wote ambao wamepata uzoefu wa aina hiyo wataweza kutembea miongoni mwa makanisa mengi na kuwatolea ndugu zako, ili muweze kutumia nguvu za kila mmoja kufidia upungufu wako na kupata maarifa mengi zaidi ndani ya roho zenu. Ni baada tu ya kutimiza matokeo haya ndipo utakapoweza kutumikia kulingana na mapenzi ya Mungu na kufanywa mkamilifu na Mungu wakati wa kufanya huduma yako.

Wanaomhudumia Mungu wanapaswa kuwa marafiki wema wa Mungu, wanapaswa kumfurahisha Mungu, na kuwa na uaminifu wa hali ya juu kwa Mungu. Bila kujali iwapo unatenda bila kuonekana na watu, au mbele ya watu, unaweza kupata furaha ya Mungu mbele za Mungu, unaweza kusimama imara mbele za Mungu, na bila kujali jinsi watu wengine wanavyokutendea, wewe huifuata njia yako mwenyewe kila mara, na kuushughulikia kwa makini mzigo wa Mungu. Mtu wa aina hii pekee ndiye rafiki mwema wa Mungu. Marafiki wema wa Mungu wanaweza kumhudumia Yeye moja kwa moja kwa sababu wamepewa agizo kuu la Mungu, na mzigo wa Mungu, wao wanaweza kuuchukulia moyo wa Mungu kama moyo wao wenyewe, na mzigo wa Mungu kama mzigo wao wenyewe, na hawazingatii iwapo watafaidi au watapoteza matarajio: Hata wasipokuwa na matarajio, na hawatafaidi chochote, watamwamini Mungu daima kwa moyo wa upendo. Kwa hivyo, mtu wa aina hii ni rafiki mwema wa Mungu. Marafiki wema wa Mungu ni wasiri Wake pia; ni wasiri wa Mungu pekee ndio wanaoweza kushiriki katika kutotulia Kwake, matamanio Yake, na ingawa mwili wao una uchungu na ni mdhaifu, wanaweza kuvumilia uchungu na kuacha kile wanachokipenda ili kumridhisha Mungu. Mungu huwapa watu wa aina hii mizigo mingi, na kile ambacho Mungu anataka kufanya kinathibitishwa katika ushuhuda wa watu kama hawa. Yaani, watu hawa wanapendwa na Mungu, wao ni watumishi wa Mungu wanaoupendeza moyo Wake, na ni watu wa aina hii pekee ndio wanaoweza kutawala pamoja na Mungu. Ukishakuwa rafiki mwema wa Mungu ndipo utakapoweza kabisa kutawala pamoja na Mungu.

Yesu aliweza kukamilisha agizo la Mungu—kazi ya ukombozi wa wanadamu wote—kwa sababu alikabidhi kila tatizo kwa mapenzi ya Mungu, bila kufuata mipango na fikira Zake binafsi. Basi pia, Yeye Alikuwa rafiki mwema wa Mungu—Mungu Mwenyewe, jambo ambalo nyote mnalielewa vizuri sana. (Kwa kweli, alikuwa Mungu Mwenyewe aliyetolewa ushahidi na Mungu; Ninataja jambo hili hapa kwa kuutumia ukweli wa Yesu ili kuonyesha mfano wa suala hili.) Aliweza kuuweka mpango wa usimamizi wa Mungu katika kiini cha mambo yote, na kila mara alimwomba Baba wa mbinguni na kuyatafuta mapenzi ya Baba wa mbinguni. Aliomba, na kusema: “Mungu Baba! Timiza kile ambacho ni mapenzi Yako, na usitende kulingana na nia Zangu; ingekuwa heri ukitenda kulingana na mpango Wako. Mwanadamu anaweza kuwa dhaifu, lakini kwa nini unapaswa kumshughulikia? Ni vipi ambavyo mwanadamu anaweza kustahili kukuhangaisha, mwanadamu ambaye ni kama chungu mkononi Mwako? Ndani ya moyo Wangu, Ninatamani tu kutimiza mapenzi Yako, na Ninatamani Utende Unachotaka kutenda ndani Yangu kulingana na makusudio Yako mwenyewe.” Alipokuwa njiani kuelekea Yerusalemu, Yesu alihisi maumivu makali, kama kwamba kisu kilikuwa kimedungwa ndani ya moyo Wake, ilhali hakuwa na nia yoyote ya kwenda kinyume cha Neno lake; kila mara kulikuwa na nguvu zenye uwezo mkuu zilizomvutia Yeye kuelekea mahali ambapo Angesulubiwa. Mwishowe, alipigiliwa misumari juu ya msalaba na akawa mfano wa mwili wenye dhambi, akiikamilisha kazi hiyo ya ukombozi wa wanadamu, na kufufuka kutoka kwa pingu za kifo na Kuzimu. Mbele Yake, kifo, jehanamu, na Kuzimu vilipoteza nguvu zao, na vilishindwa Naye. Aliishi miaka thelathini na tatu, na katika miaka hiyo yote daima Alifanya kila Alichoweza kutimiza mapenzi ya Mungu kulingana na kazi ya Mungu wakati huo, bila kuzingatia atakachofaidi au kupoteza Yeye binafsi, na kila mara akiwaza kuhusu mapenzi ya Mungu Baba. Hivyo, baada ya Yeye kubatizwa, Mungu alisema: “Huyu ni Mwana wangu Mpendwa, ambaye Ninapendezwa naye.” Kwa sababu ya huduma Yake mbele ya Mungu, iliyokuwa na upatanifu na mapenzi ya Mungu, Mungu aliuweka mzigo mzito wa kuwakomboa wanadamu wote juu ya mabega yake na akamfanya ajitolee kuutimiza, na Alikuwa na ujuzi na ustahiki wa kuikamilisha kazi hii muhimu. Katika maisha Yake yote, alivumilia mateso yasiyokuwa na kipimo kwa ajili ya Mungu, na alijaribiwa na Shetani mara nyingi, lakini hakufa moyo. Mungu alimpa kazi ya aina hiyo kwa sababu Alimwamini Yeye, na kumpenda Yeye, na hivyo basi Mungu mwenyewe alisema: “Huyu ni Mwana wangu Mpendwa, ambaye Ninapendezwa naye.” Wakati huo, ni Yesu pekee ambaye angeweza kutimiza agizo hili, na hii ilikuwa sehemu moja ya Mungu kutimiza kazi Yake ya kuwakomboa wanadamu wote katika Enzi ya Neema.

Ikiwa, kama Yesu, unaweza kuushughulikia kwa makini mzigo wa Mungu, na kuyakataa mambo ya mwili wako, Mungu atakuaminia kazi Zake muhimu, ili uweze kufikia masharti ya kumhudumia Mungu. Ni katika hali hizo pekee ndipo utakapothubutu kusema kwamba unafanya mapenzi ya Mungu na kukamilisha agizo Lake, hapo ndipo utakapothubutu kusema unamhudumia Mungu kweli. Ukilinganishwa na mfano wa Yesu, unaweza kuthubutu kusema kwamba wewe ni mwandani wa Mungu? Je, unaweza kuthubutu kusema kwamba unafanya mapenzi ya Mungu? Je, unaweza kuthubutu kusema kwamba kweli unamhudumia Mungu? Leo, hufahamu aina hii ya huduma kwa Mungu, unaweza kuthubutu kusema kwamba wewe ni rafiki mwema wa Mungu? Ukisema kwamba unamhudumia Mungu, humkufuru Yeye? Fikiria kuhusu hilo: Je, unamhudumia Mungu, au unajihudumia wewe mwenyewe? Unamhudumia Shetani, ilhali kwa ukaidi unasema kwamba unamhudumia Mungu—katika jambo hili humkufuru Mungu? Watu wengi walio nyuma Yangu wanatamani baraka ya cheo, wana ulafi wa chakula, wanapenda kulala na kuushughulikia mwili kwa makini, kila mara wakiogopa kwamba hakuna njia ya kuondoka ndani ya mwili. Hawaifanyi kazi yao ya kawaida kanisani, lakini wanalitumia kanisa vibaya, au wanawaonya ndugu zao kwa maneno Yangu, wanasimama juu na kuwatawala wengine. Watu hawa huendelea kusema kwamba wanafanya mapenzi ya Mungu, wao husema kila mara kwamba ni marafiki wema wa Mungu—huu si upuuzi? Ikiwa una motisha iliyo sahihi, lakini huwezi kutumikia kulingana na mapenzi ya Mungu, basi wewe unakuwa mpumbavu; lakini ikiwa motisha yako si sahihi, na bado unasema kwamba unamhudumia Mungu, basi wewe ni mtu anayempinga Mungu, na unastahili kuadhibiwa na Mungu! Sina huruma kwa watu wa aina hiyo! Wao ni doezi katika nyumba ya Mungu, na kila mara wao hutamani raha za mwili, na hawazingatii mambo ambayo Mungu anayapenda; kila mara wao hutafuta mambo yaliyo mazuri kwao, wala hawatilii maanani mapenzi ya Mungu, mambo yote wanayoyafanya hayaongozwi na Roho wa Mungu, kila mara wao hufanya hila dhidi ya ndugu zao na kuwadanganya, na kuwa ndumakuwili, kama mbweha ndani ya shamba la mizabibu, akiiba mizabibu kila mara na kulikanyaga na kuliharibu shamba la mizabibu. Je, watu wa aina hiyo wanaweza kuwa marafiki wema wa Mungu? Je, unastahili kupokea baraka za Mungu? Wewe huwajibiki kuhusu maisha yako na kanisa, unastahili kupokea agizo la Mungu? Ni nani anayeweza kuthubutu kumwamini mtu kama wewe? Unapohudumu kwa njia hii, je, Mungu anaweza kuthubutu kukuaminia kazi kubwa zaidi? Je, si wewe unachelewesha mambo?

Nasema hivi ili uweze kujua masharti yanayohitajika kutimizwa ili kuhudumu kwa upatanifu na mapenzi ya Mungu. Usipoutoa moyo wako kwa Mungu, usipoyashughulikia kwa makini mapenzi ya Mungu kama alivyofanya Yesu, basi huwezi kuaminiwa na Mungu, na mwishowe utahukumiwa na Mungu. Labda leo, katika huduma yako kwa Mungu, kila mara wewe huficha kusudi la kumdanganya Mungu na kila mara wewe humtendea kwa njia isiyo ya dhati. Kwa ufupi, bila kujali chochote kingine, ukimdanganya Mungu, hukumu isiyo ya huruma itakujia. Unapaswa kutumia vizuri nafasi ya kuwa umeingia katika njia sahihi ya kumhudumia Mungu kwa kumpa Mungu moyo wako kwanza, bila kugawanya uaminifu wako. Bila kujali iwapo uko mbele za Mungu, au mbele ya watu wengine, moyo wako unapaswa kuelekezwa kwa Mungu kila wakati, na unapaswa kufanya uamuzi wa kumpenda Mungu kama Yesu. Kwa kufanya hivi, Mungu atakufanya uwe mkamilifu, ili uwe mtumishi wa Mungu anayempendeza Mungu. Ikiwa ungependa kweli kufanywa mkamilifu na Mungu, na huduma yako iwe katika upatanifu na mapenzi Yake, basi unapaswa kubadilisha maoni yako ya awali kuhusu imani kwa Mungu, na kubadilisha jinsi ulivyokuwa ukimhudumia Mungu, ili nafsi yako yote iweze kufanywa kuwa kamilifu na Mungu; kwa kufanya hivi, Mungu hatakuacha, na, kama Petro, utakuwa katika kikosi cha mbele cha wale wanaompenda Mungu. Ukibaki kuwa mtu asiyetubu, basi utakutana na mwisho kama wa Yuda. Hii inapaswa kufahamika na watu wote wanaomwamini Mungu.

Iliyotangulia: Jinsi ya Kuingia Katika Hali ya Kawaida

Inayofuata: Jinsi ya Kujua Uhalisi

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp