Kumpenda Mungu tu Ndiko Kumwamini Mungu Kweli

Mnapotaka kumpenda na kumjua Mungu leo, kwa upande mmoja ni lazima mstahimili mateso, usafishaji, na kwa ule upande mwingine, ni lazima mgharamike. Hakuna funzo lililo kubwa kuliko lile la kumpenda Mungu, na inaweza kusemwa kuwa funzo ambalo watu hujifunza katika maisha yao yote ya imani ni jinsi ya kumpenda Mungu. Hii ni kusema, kama unamwamini Mungu ni lazima umpende Mungu. Ikiwa unamwamini tu Mungu lakini humpendi, hujapata ufahamu wa Mungu, na hujawahi kumpenda Mungu kwa upendo wa kweli utokao moyoni mwako, basi imani yako kwa Mungu ni bure; kama katika imani yako kwa Mungu humpendi Mungu, basi unaishi bure, na maisha yako yote ndiyo ya duni zaidi kwa maisha yote. Ikiwa katika maisha yako yote hujawahi kumpenda au kumtosheleza Mungu, basi kuna haja gani ya kuishi? Kuna haja gani ya imani yako kwa Mungu? Huku si kuharibu nguvu? Hii ni kusema, kama watu wanataka kuamini na kumpenda Mungu, ni sharti wagharamike. Badala ya kujaribu kuenenda kwa namna fulani kwa nje tu, wanapaswa watafute utambuzi wa kweli kutoka ndani ya mioyo yao. Ikiwa unapenda sana kuimba na kucheza lakini huwezi kuonyesha ukweli katika vitendo, unaweza kusemekana kwamba unampenda Mungu? Kumpenda Mungu kunahitaji utafutaji wa mapenzi ya Mungu katika mambo yote, na kwamba ujisaili wewe mwenyewe kwa kina jambo lolote likikutokea, kujaribu kujua mapenzi ya Mungu na kujaribu kuona mapenzi ya Mungu ni yapi katika suala hili, Anataka ufanikishe nini, na ni jinsi gani utayajali mapenzi Yake? Kwa mfano: jambo fulani linafanyika linalokutaka uvumilie hali ngumu, wakati huo unapaswa ufahamu ni nini mapenzi ya Mungu, na ni jinsi gani unapaswa kuyajali mapenzi ya Mungu. Usijiridhishe mwenyewe: Jiweke kando kwanza. Hakuna kitu kilicho duni kuliko mwili. Ni lazima udhamirie kumridhisha Mungu, na ni lazima utekeleze wajibu wako. Katika mawazo kama hayo, Mungu atakupa nuru ya kipekee katika jambo hili, na moyo wako pia utapata faraja. Jambo lolote likikutendekea, liwe dogo au kubwa, ni sharti kwanza ujiweke pembeni na kuuona mwili kama kitu duni zaidi kuliko vitu vyote. Kadiri unavyouridhisha mwili zaidi, ndivyo unavyochukua uhuru zaidi; ukiuridhisha mara hii, wakati mwingine utataka zaidi. Hili linapoendelea, watu wanapata kuupenda mwili hata zaidi. Mwili mara zote una tamaa kupita kiasi, mara zote mwili unakutaka uuridhishe, na kwamba uutosheleze kwa ndani, iwe ni katika chakula unachokula, unachokivaa, au kuwa na hasira katika matendo yako, au kuushawishi udhaifu na uzembe wako… Kadiri unavyouridhisha mwili zaidi, ndivyo tamaa yake inaongezeka, na jinsi mwili unavyopotoka zaidi, hadi kufikia kiwango ambacho miili ya watu inahodhi dhana nzito, na kutomtii Mungu, na kujiinua, na kuanza kuishuku kazi ya Mungu. Kadiri unavyouridhisha mwili zaidi, ndivyo udhaifu wa mwili unavyokuwa mkubwa; daima utahisi kuwa hakuna anayekuonea huruma kwa udhaifu wako, daima utaamini kuwa Mungu amezidi sana, na utasema: Mungu anawezaje kuwa mkali namna hii? Ni kwa nini Hawezi kuwapa watu nafasi? Watu wakiudekeza sana mwili, na kuupenda kupindukia, basi wanajiangamiza wao wenyewe. Ikiwa unampenda Mungu kwa dhati, na huuridhishi mwili, basi utaona kuwa kila anachokifanya Mungu ni chenye haki sana, na kizuri sana, na kwamba laana Yake kwa uasi wako na hukumu ya udhalimu wako ni haki. Zitakuwepo nyakati ambapo Mungu atakurudi na kukufundisha nidhamu, na kuanzisha mazingira ya kukukasirisha, na kukushurutisha uje mbele Zake—na daima utahisi kuwa anachokifanya Mungu ni cha ajabu. Hivyo utahisi kana kwamba hakuna uchungu mwingi, na kwamba Mungu anapendeza. Ukifuata udhaifu wa mwili, na kusema kwamba Mungu amezidi, basi daima utahisi uchungu na daima utahuzunika, na utakosa uwazi kuhusu kazi yote ya Mungu na itaonekana kana kwamba Mungu hana huruma kwa udhaifu wa mwanadamu, na Hatambui shida za mwanadamu. Hivyo utajihisi mnyonge na mpweke, kana kwamba umekumbwa na dhuluma kubwa, na wakati huo utaanza kulalama. Kadiri unavyoutosheleza udhaifu wa mwili, ndivyo unavyohisi kuwa Mungu anazidi, hadi inakuwa mbaya kiasi kwamba unaikana kazi ya Mungu, na kuanza kumpinga Mungu na kujaa uasi. Hivyo unafaa kuuasi mwili na usiutosheleze: “Mume wangu(mke), watoto, matarajio, ndoa, familia—hakuna hata moja kati ya haya ambalo ni la thamani! Moyoni mwangu mna Mungu pekee na nitajaribu kumridhisha Mungu kadiri ya uwezo wangu, na si kuuridhisha mwili.” Lazima uwe na azimio hili. Daima ukiwa na azimio hili, basi ukiuweka ukweli katika vitendo, na kujiweka kando, utaweza kufanya hivyo kwa juhudi kidogo. Inasemekana kuwa kulikuwepo na mkulima aliyeona nyoka barabarani aliyekuwa ameganda. Huyu mkulima alimchukua yule nyoka na kumweka kifuani mwake, na baada ya yule nyoka kuamka alimuuma yule mkulima hadi akafa. Miili ya wanadamu ni kama yule nyoka: asili yake ni kuyadhuru maisha yao—na ikipata mbinu yake kikamilifu, maisha yako yanapotea. Mwili ni wa Shetani. Kuna tamaa kupita kiasi ndani yake, hujithamini wenyewe, unafurahia faraja, na kushangilia burudani, kujiachilia katika uvivu na uzembe, na baada ya kuuridhisha kwa kiwango fulani mwishowe utakuangamiza. Hivi ni kusema, ukiuridhisha sasa, wakati mwingine utakuomba zaidi. Daima mwili una tamaa na matakwa kupita kiasi, na unajinufaisha kutokana na wewe kuutosheleza mwili na kukufanya uufurahie hata zaidi na kuishi katika starehe zake—na ikiwa hutaushinda, mwishowe utajiangamiza mwenyewe. Iwapo utapata uzima mbele za Mungu, na namna hatima yako itakavyokuwa, inategemea uasi wako dhidi ya mwili utakuwa wa namna gani. Mungu amekuokoa, na kukuteua na kukuamulia kabla, bado ikiwa leo hauko radhi kumridhisha, hauko radhi kuuweka ukweli katika vitendo, hauko radhi kuuasi mwili wako kwa moyo umpendao Mungu kwa dhati, hatimaye utajiangamiza mwenyewe, na kwa hivyo utapitia mateso mengi. Ikiwa mara zote unautosheleza mwili, Shetani atakumeza hatua kwa hatua, na kukuacha bila uzima, au upako wa Roho, hadi siku itafika ambayo ndani utakuwa giza. Ukiishi katika giza, utakuwa umetekwa nyara na Shetani, hutakuwa na Mungu tena moyoni mwako, na wakati ule utaukataa uwepo wa Mungu na kumwacha. Kwa hivyo, ikiwa watu wanataka kumpenda Mungu, ni lazima walipe gharama ya uchungu na kupitia shida. Hakuna haja ya hamasa za nje na shida, kusoma zaidi na kuzungukazunguka zaidi; badala yake, wanafaa kuweka kando vitu vilivyomo ndani yao: mawazo kupita kiasi, maslahi ya kibinafsi, na masuala yao binafsi, fikira, na nia. Hayo ndiyo mapenzi ya Mungu.

Ushughulikiaji wa Mungu juu ya tabia za nje za watu ni sehemu moja ya kazi Yake; kwa mfano, kushughulikia ubinadamu wa watu wa nje, usiokuwa wa kawaida, au maisha na tabia zao, njia na desturi zao, na vilevile vitendo vyao vya nje, na hamasa zao. Lakini Anapowataka watu wauweke ukweli katika vitendo na wabadilishe tabia zao, kimsingi kinachoshughulikiwa hapa ni motisha na mawazo yaliyo ndani yao. Kushughulikia tabia zako za nje tu si kugumu; ni sawa na kukukataza kula vitu uvipendavyo, jambo ambalo ni rahisi. Kinachogusia fikira zilizo ndani yako, hata hivyo, si rahisi kukiachia. Inawahitaji wauasi mwili wao, na kulipa gharama, na kuteseka mbele za Mungu. Hii ndiyo hali hasa katika nia za watu. Tangu watu waanze kumwamini Mungu, wamekuwa na nia ambazo si sahihi. Wakati ambapo huweki ukweli katika vitendo, unahisi kuwa motisha zako ni sahihi, lakini jambo likikutokea, utaona kuwa kuna motisha nyingi ndani zisizo sahihi. Hivyo, Mungu akiwafanya watu kuwa wakamilifu, Anawafanya kugundua kuwa kuna dhana nyingi ndani yao ambazo zinawazuia kumfahamu Mungu. Ukitambua kuwa motisha zako zina makosa, kama unaweza kuacha kutenda kulingana na motisha na dhana zako, na unaweza kuwa na ushuhuda wa Mungu na kusimama imara katika msimamo wako kwa kila lifanyikalo kwako, hili linathibitisha kuwa umeuasi mwili wako. Ukiasi dhidi ya mwili wako, bila shaka kutakuwa na vita ndani yako. Shetani atajaribu kufanya watu kuifuata, atajaribu kuwafanya wafuate dhana za kimwili na kutekeleza maslahi ya kimwili—ila maneno ya Mungu yatawapa nuru watu na kuwaangazia kwa ndani, na wakati huu itakuwa juu yako ikiwa utamfuata Mungu au utamfuata Shetani. Mungu anawataka watu kuweka ukweli katika matendo kimsingi kushughulikia mambo yaliyo ndani yao, kushughulikiwa fikira zao, na dhana zao ambazo haziufuati moyo wa Mungu. Roho Mtakatifu huwagusa watu ndani ya mioyo yao, na kuwapa nuru na mwangaza. Kwa hivyo katika tukio lolote katika vita: Kila wakati watu wanapoweka ukweli katika vitendo, au kuweka mapenzi ya Mungu katika vitendo, huwa kuna vita vikali, na japokuwa mambo yanaweza kuonekana shwari katika miili yao, ila ndani ya mioyo yao kutakuwa na vita vya kufa na kupona—na ni baada tu ya hivi vita vikali, baada ya kutafakari kwa kina, ndipo ushindi au kushindwa kunaweza kuamuliwa. Mtu anashindwa kujua ama acheke au alie. Kwa sababu motisha nyingi ndani ya watu zina makosa, ama kwa sababu kazi kubwa ya Mungu inakinzana na dhana zao, watu wakiuweka ukweli katika vitendo vita vikali huzuka kisirisiri. Baada ya kuuweka huu ukweli katika vitendo, kisirisiri watu watakuwa wamemwaga machozi mengi sana ya huzuni kabla ya kuamua kumridhisha Mungu. Ni kwa sababu ya vita hivi watu huvumilia shida na usafishaji; huku ni kuteseka kwa kweli. Vita vikikukabili, kama unaweza kusimama kweli upande wa Mungu, utaweza kumridhisha Mungu. Katika harakati ya kutenda ukweli, hakuepukiki kwamba mtu atateseka kwa ndani; ikiwa, wanapoweka ukweli katika vitendo, kila kitu ndani yao kingekuwa sawa, basi wasingehitaji kufanywa wakamilifu na Mungu, na kusingekuwa na vita, na hawangeteseka. Ni kwa sababu kuna mambo mengi ndani ya watu ndipo hawafai kutumiwa na Mungu, na tabia nyingi za uasi wa mwili, ndipo watu wanapaswa kujifunza funzo la kuasi dhidi ya mwili kwa kina zaidi. Huku ndiko Mungu anaita kuteseka ambako Alimtaka mwanadamu kushiriki Naye. Ukikumbana na shida, fanya hima na umwombe Mungu: Ee Mungu! Ninataka kukuridhisha, ninataka kustahimili mateso ya mwisho ili kuuridhisha moyo Wako, na bila kujali kuwa vikwazo ninavyokumbana navyo ni vikubwa kiasi gani, bado ni sharti nikuridhishe. Hata ikiwa ni kuyatoa maisha yangu yote, bado ni sharti nikuridhishe! Ukiomba na hili azimio utaweza kusimama imara katika ushuhuda wako. Kila wawekapo ukweli katika vitendo, kila wapitiapo usafishaji, kila wanapojaribiwa, na kila wakati kazi ya Mungu inapowashukia, watu wanapitia mateso makubwa. Haya yote ni mtihani wa watu, na kwa hivyo ndani yao wote mna vita. Hii ndiyo gharama hasa wanayolipa. Kusoma zaidi neno la Mungu na kuzungukazunguka zaidi, kwa namna fulani ni gharama. Ndiyo watu wanapaswa kufanya, ndio wajibu wao, na jukumu ambalo ni sharti walitimize, lakini ni lazima watu waweke kando yale yanayofaa kuwekwa kando. Ikiwa hamwezi, basi haijalishi mateso yako yatakuwa makubwa kiasi gani, na utazunguka kiasi gani, yote yatakuwa bure! Hivi ni kusema, ni mabadiliko ndani yako tu yanaweza kuamua iwapo mateso yako ya nje yana thamani. Tabia yako ya ndani ikibadilika na ikiwa umeweka ukweli katika vitendo, basi mateso yako yote ya nje yatapata kibali cha Mungu; ikiwa hakujakuwa na mabadiliko katika tabia yako ya ndani, basi haijalishi unateseka kiasi gani au unazungukazunguka kiasi gani nje, hakutakuwa na kibali kutoka kwa Mungu—na mateso ambayo hayajaidhinishwa na Mungu ni bure! Hivyo, kama gharama ambayo umelipa imedhinishwa na Mungu inaamuliwa na kama umekuwa na mabadiliko ndani yako au la, na kama unatia ukweli katika vitendo na kuasi dhidi ya motisha na dhana zako mwenyewe ili kupata ridhaa ya mapenzi ya Mungu, ufahamu wa Mungu, na uaminifu kwa Mungu. Haijalishi unazungukazunguka kiasi gani, ikiwa hujawahi kujua kuasi dhidi ya motisha zako, unatafuta tu matendo na hamasa za nje, na usitilie maanani maisha yako, basi taabu zako zitakuwa zimepita bure. Ikiwa una kitu unachotaka kusema katika mazingira fulani, ila kwa ndani unahisi kwamba kukisema si sawa, kwamba kukisema hakuna faida kwa ndugu na dada zako, na kinaweza kuwadhuru, basi na usikiseme, uchague kuumia kwa ndani, kwa kuwa haya maneno hayawezi kuridhisha mapenzi ya Mungu. Wakati huu, kutakuwa na vita ndani yako, lakini utakuwa tayari kuumia na kuviacha uvipendavyo, utakuwa radhi kustahimili haya mateso ili kumridhisha Mungu na ingawa utaumia kwa ndani, hutautosheleza mwili, na moyo wa Mungu utakuwa umeridhishwa, hivyo utafarijika kwa ndani. Kwa hakika huku ni kulipa gharama, na ndiyo gharama inayotakiwa na Mungu. Ukitenda kwa njia hii, kwa hakika Mungu atakubariki; ikiwa huwezi kulifanikisha hili, basi haijalishi unaelewa kiasi gani, au unaweza kunena vyema kiasi gani, yote haya hayatafaa kitu! Katika njia ya kumpenda Mungu, ikiwa unaweza kusimama upande wa Mungu anapopigana na Shetani, na usimgeukie Shetani, basi utakuwa umefanikisha mapenzi ya Mungu, na utakuwa umesimama imara katika ushuhuda wako.

Katika kila hatua ya kazi anayoifanya Mungu ndani ya watu, kwa nje inaonekana kama maingiliano kati ya watu, kana kwamba yalizaliwa kwa mipango ya wanadamu au kutokana na kuingilia kwa wanadamu. Ila kisirisiri, hatua ya kazi, na kila kitu kinachotendeka, ni pingamizi la Shetani kwa Mungu, na huhitaji watu kuwa imara katika ushuhuda wao kwa Mungu. Kwa mfano, tazama wakati Ayubu alijaribiwa: kisirisiri, Shetani alikuwa akiwekeana dau na Mungu, na kilichomtokea Ayubu kilikuwa ni matendo ya wanadamu, na kuingilia kwa wanadamu. Kuna pingamizi la Shetani kwa Mungu katika kila hatua ambayo Mungu anatenda ndani yenu—katika kila kitu kuna vita. Kwa mfano, ikiwa unawabagua ndugu na dada zako, utakuwa na maneno ambayo unataka kusema—maneno unayohisi huenda yasimpendeze Mungu—lakini usipoyasema, utahisi kutoridhika ndani, na kwa wakati huu vita vitazuka ndani yako: “Niseme au nisiseme?” Hivi ndivyo vita. Kwa hivyo, katika kila jambo unalopitia kuna vita, na wakati kuna vita ndani yako, kutokana na ushirikiano wako na kuteseka kwako, Mungu anafanya kazi ndani yako. Hatimaye unaweza kuliweka kando jambo lenyewe na ghadhabu yako inazimika. Hiyo ndiyo athari ya ushirika wako na Mungu. Kila kitu wafanyacho watu kinawahitaji kulipa gharama fulani katika juhudi zao. Bila taabu ya kweli, hawawezi kumridhisha Mungu, hata hawakaribii kumridhisha Mungu, na wanarusha tu maneno matupu! Je, haya maneno matupu yaweza kumridhisha Mungu? Wakati Mungu na Shetani wanapigana katika milki ya kiroho, utamridhishaje Mungu, na utasimamaje imara katika ushuhuda wako Kwake? Unapaswa kujua kuwa kila kitu unachokipitia ni majaribu makubwa na ndipo Mungu hukuhitaji kuwa na ushuhuda. Kwa nje yataonekana kama mambo madogo; lakini haya mambo yakitendeka huonyesha kama unampenda Mungu au la. Ikiwa unampenda, utaweza kusimama imara katika ushuhuda wako Kwake, na ikiwa hujaweka upendo Wake katika vitendo, hili linaonyesha kuwa wewe si Mtu ambaye anapenda kuuweka ukweli katika vitendo, kwamba huna ukweli, huna uzima, kuwa wewe ni makapi! Mambo huwatokea watu wakati Mungu anawataka wasimame imara katika ushuhuda wao Kwake. Hakuna kubwa lililokutendekea kwa sasa, na huna ushuhuda mkubwa, lakini kila chembe ya maisha yako ya kila siku inahusiana na ushuhuda kwa Mungu. Ikiwa utawavutia ndugu na dada zako, wanafamilia, na kila aliye karibu nawe; ikiwa siku moja wasioamini watakuja na wavutiwe na yote unenayo na utendayo, na kuona kuwa yote afanyayo Mungu ni ya ajabu, basi utakuwa umekuwa na ushuhuda. Ijapokuwa huna ufahamu na wewe si mwerevu sasa, kupitia kwa kufanywa mkamilifu na Mungu, unaweza kumridhisha na kuzingatia mapenzi Yake, ukiwaoshyesha wengine kazi kubwa Aliyofanya miongoni mwa watu wenye ubora duni wa tabia. Watu wanapokuja kumjua Mungu na kuwa washindi mbele ya Shetani, waaminifu kwa Mungu kwa kiwango kikubwa, basi hakuna aliye na uthabiti kuliko hili kundi la watu, na huu ndio ushuhuda mkubwa zaidi. Ijapokuwa huwezi kufanya kazi kubwa, unaweza kumridhisha Mungu. Wengine hawawezi kuyaacha mawazo yao, ila wewe unaweza; wengine hawawezi kuwa na ushuhuda kwa Mungu wakati wa mapito yao ya kweli, ila unaweza kutumia hadhi na matendo yako ya kweli kulipia mapenzi ya Mungu na kuwa na ushuhuda mkubwa Kwake. Hili ndilo huhesabika kama mapenzi ya kweli kwa Mungu. Ikiwa huliwezi hili, basi hutoi ushuhuda miongoni mwa jamaa zako, miongoni mwa ndugu zako, miongoni mwa dada zako, au mbele ya walimwengu. Ikiwa huwezi kuwa na ushuhuda mbele ya Shetani, Shetani atakucheka, atakuchukulia kama mzaha, mwanasesere, mara kwa mara atakuchezea na kukughadhibisha. Majaribu mengi yatakupata siku za usoni—lakini ikiwa leo unampenda Mungu kwa moyo wa dhati, na ikiwa haijalishi ukubwa wa majaribu yaliyo mbele, bila kujali unachokipitia, unaweza kusimama imara katika ushuhuda wako, na kuweza kumridhisha Mungu, basi moyo wako utafarijiwa, na utakuwa jasiri hata majaribu utakayokabiliana nayo siku za usoni yawe makubwa kiasi gani. Hamwezi kuona ni nini kitatendeka siku za usoni; mnaweza tu kuridhisha Mungu katika hali ya leo. Hamwezi kufanya kazi yoyote kubwa, na unafaa kulenga kumridhisha Mungu kwa kuyapitia maneno yake katika maisha halisi, na kuwa na ushuhuda thabiti na mzito ambao unamtia aibu Shetani. Japo mwili wako hautaridhishwa na utateseka, utakuwa umemridhisha Mungu na kumletea aibu Shetani. Ikiwa daima unatenda hivi, Mungu atakufungulia njia mbele yako. Na siku moja, jaribio kubwa likija, wengine wataanguka chini, ila utaweza kuendelea kusimama imara: kwa sababu ya gharama uliyolipa, Mungu atakulinda ili usimame imara na usianguke. Kwa kawaida, ikiwa unaweza kuweka ukweli katika vitendo na kumridhisha Mungu kwa moyo ambao unampenda kweli, kwa hakika Mungu atakulinda wakati wa majaribu ya siku zijazo. Japokuwa wewe ni mpumbavu na mwenye kimo cha chini na usiye mwerevu, Mungu hatakubagua. Inategemea iwapo motisha zako ni za haki. Unaweza kumridhisha Mungu leo, iwapo uko makini na masuala madogo, unamridhisha Mungu kwa mambo yote, una moyo unaompenda Mungu kwa dhati, unampa Mungu moyo wa dhati, na japokuwa kuna baadhi ya mambo ambayo huwezi kuelewa, unaweza kwenda mbele za Mungu kurekebisha motisha zako, na kuyafuata mapenzi ya Mungu, na kufanya kila lipaswalo kumridhisha Mungu. Pengine ndugu na dada zako wataachana nawe, lakini moyo wako utakuwa unamridhisha Mungu, na hutatamani raha za mwili. Ikiwa daima unatenda kwa namna hii, utalindwa majaribu yakikusibu.

Majaribu haya yanailenga hali gani ya ndani ya watu? Yanalenga tabia ya uasi ndani ya watu ambayo haiwezi kumridhisha Mungu. Kuna mengi ambayo ni machafu ndani ya watu, na mengi ambayo ni ya unafiki, na kwa hivyo Mungu anawatia katika majaribu ili kuwasafisha. Lakini, ikiwa leo unaweza kumridhisha Mungu, basi majaribu ya siku zijazo yatakuwa ukamilifu kwako. Ikiwa leo, huwezi kumridhisha Mungu, basi majaribu ya siku za usoni yatakushawishi, na utaanguka bila kujua, na wakati huo hutaweza kujisaidia mwenyewe, kwani huendani na kazi ya Mungu, na huna kimo halisi. Na kwa hivyo, kama unataka kuweza kusimama imara katika siku za usoni, kumridhisha vyema Mungu, na kumfuata hadi mwisho, unapaswa kujenga msingi thabiti leo, unafaa kumridhisha Mungu kwa kutia ukweli katika vitendo kwa kila jambo, na kuzingatia mapenzi Yake. Iwapo daima unatenda kwa namna hii, kutakuwa na msingi ndani yako, na Mungu atahamasisha ndani yako moyo unaompenda, na Atakupa imani. Siku moja ambapo majaribu yatakuwa yamekukumba kwa kweli, ijapo utaumia, na kuhisi umedhulumiwa kwa kiwango fulani, na kuwa na huzuni kubwa, kana kwamba ulikuwa umekufa—ila mapenzi yako kwa Mungu hayatabadilika, na yataongezeka zaidi. Hizo ni baraka za Mungu. Ikiwa unaweza kumkubali Mungu na yote asemayo na atendayo leo kwa moyo mtiifu, basi kwa hakika utabarikiwa na Mungu, na kwa hivyo utakuwa mtu aliyebarikiwa na Mungu, na anayepokea ahadi Yake. Ikiwa leo hutendi, siku ambayo majaribu yatakukumba utakosa imani au moyo wenye mapenzi, na wakati huo jaribu litakuwa kishawishi; utatoswa ndani ya kishawishi cha Shetani na hutapata namna ya kuponyoka. Leo, unaweza kusimama imara jaribio dogo likikukabili, ila huenda usiweze kusimama imara siku ambayo jaribio kubwa litakukumba. Baadhi ya watu hujivuna, na kufikiri kwamba wako karibu na ukamilifu. Ikiwa huzami zaidi wakati huo, na kuridhika, basi utakuwa hatarini. Leo, Mungu hafanyi kazi ya majaribu makubwa, kwa kuonekana, kila kitu kiko salama, ila Mungu atakapokujaribu, utagundua kuwa umepungukiwa sana, kwani kimo chako ni kidogo mno, na huna uwezo wa kustahimili majaribu mazito. Ukisalia jinsi ulivyo na uko katika hali ya inesha, basi, majaribu yatakapokuja, utaanguka. Mara nyingi inafaa mtazame udogo wa kimo chenu; mtapiga hatua kwa njia hii tu. Ikiwa unauona udogo wa ukomavu wako wakati wa majaribu tu, kwamba kimo chako ni dhaifu, kwamba kuna kidogo sana ndani yako ambacho ni halisi, na kwamba hutoshi kwa mapenzi ya Mungu—na kama utagundua haya wakati wa majaribu tu, utakuwa umechelewa mno.

Ikiwa hujui tabia ya Mungu, bila shaka utaanguka wakati wa majaribu, kwa kuwa hufahamu jinsi Mungu anavyowafanya watu kuwa wakamilifu, na ni kwa njia gani Huwafanya wakamilifu, na majaribu ya Mungu yakikushukia na yasilingane na mawazo yako, utashindwa kusimama imara. Upendo wa kweli wa Mungu ni tabia Yake kamili, na tabia kamili ya Mungu inapoonyeshwa kwa watu, hili linauletea mwili wako nini? Tabia ya haki ya Mungu inapoonyeshwa kwa watu, bila shaka miili yao iapata uchungu mkubwa zaidi. Iwapo hutapata haya maumivu, basi huwezi kufanywa mkamilifu na Mungu, wala huwezi kumpa Mungu mapenzi ya kweli. Mungu akikufanya mkamilifu kwa hakika atakuonyesha tabia Yake kamili. Tangu uumbaji hadi leo, Mungu hajawahi kumwonyesha mwanadamu tabia Yake kamili—ila katika siku za mwisho Anaifichua kwa hili kundi la watu ambao Aliwateua awali na kuwachagua, na kwa kuwafanya watu wakamilifu, Anaiweka wazi tabia Yake, na kupitia kwayo Analifanya kamili kundi la watu. Huo ndio upendo wa kweli wa Mungu kwa watu. Kuyapitia mapenzi ya kweli ya Mungu kunawapasa watu wastahimili uchungu mkali, na kulipa gharama kubwa. Ni baada tu ya hili ndipo watapatikana na Mungu na waweze kutoa tena mapenzi ya kweli kwa Mungu, na ni hapo tu ndipo Moyo wa Mungu utaridhishwa. Ikiwa watu wanataka wafanywe wakamilifu na Mungu, na kama wanataka kufanya na mapenzi Yake, na kumpa Mungu mapenzi yao ya dhati kikamilifu, ni sharti wapitie mateso mengi na maumivu makali kutokana na hali hizo, kupata uchungu mkali kuliko mauti, hatimaye watashurutishwa kuirejesha mioyo yao ya kweli kwa Mungu. Ikiwa mtu anampenda Mungu kwa dhati au la, itafichuliwa wakati wa shida na usafishaji. Mungu hutakasa mapenzi ya watu, na hili vilevile hupatikana tu ndani ya shida na usafishaji.

Iliyotangulia: Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu

Inayofuata: Mazungumzo Mafupi Kuhusu “Ufalme wa Milenia Umefika”

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp