Utendaji (5)

Wakati wa Enzi ya Neema, Yesu alinena maneno fulani na Akatekeleza hatua moja ya kazi. Yote yalikuwa na muktadha, na yote yalikuwa ya kufaa kwa hali za watu wa wakati huo; Yesu alinena na kufanya kazi kama ilivyostahili muktadha wa wakati huo. Pia Alinena unabii kiasi. Alitabiri kwamba Roho wa ukweli angekuja katika siku za mwisho na angetekeleza hatua fulani ya kazi. Ambalo ni kusema, Hakuelewa chochote zaidi ya kazi ambayo Yeye Mwenyewe alipasa Afanye wakati wa enzi hiyo; kwa maneno mengine, kazi iliyoletwa na Mungu mwenye mwili ni yenye mipaka. Hivyo, Yeye hufanya tu kazi ya enzi ambayo Yeye yumo na Hafanyi kazi nyingine ambayo haihusiani na Yeye. Wakati huo, Yesu hakufanya kazi kulingana na hisia au maono, bali ilivyostahili wakati na muktadha. Hakuna aliyemwongoza au kumwelekeza Yeye. Kazi Yake nzima ilikuwa nafsi Yake—ilikuwa ni kazi iliyopaswa kutekelezwa na Roho wa Mungu mwenye mwili, ambayo ilikuwa kazi yote iliyokaribishwa na kupata mwili. Yesu alifanya kazi tu kulingana na kile ambacho Yeye Mwenyewe aliona na kusikia. Kwa maneno mengine, Roho alifanya kazi moja kwa moja; hakukuwa na haja ya wajumbe kumwonekania na kumpa ndoto, wala kwa nuru yoyote kubwa kumwangazia na kumkubalia Aone. Alifanya kazi kwa uhuru na bila vizuizi, ambayo ilikuwa kwa sababu kazi Yake haikutegemea hisia. Kwa maneno mengine, Alipofanya kazi, Hakutafuta kwa kupapasa na kubahatisha, lakini Alitimiza mambo kwa urahisi, Akifanya kazi na kunena kulingana na mawazo Yake mwenyewe na kile Alichoona kwa macho Yake mwenyewe, Akitoa riziki ya papo hapo kwa kila mwanafunzi aliyemfuata Yeye. Hii ndiyo tofauti kati ya kazi ya Mungu na kazi ya watu: Watu wanapofanya kazi, wao hutafuta na kupapasa huku na kule, kila mara wakiiga na kufikiria sana kwa kutegemea msingi uliowekwa na wengine ili kutimiza kuingia kwa ndani zaidi. Kazi ya Mungu ni utoaji wa kile Alicho, na Yeye hufanya kazi ambayo Yeye Mwenyewe anapaswa kufanya. Hatoi riziki kwa kanisa kwa kutumia ufahamu kutoka katika kazi ya mwanadamu yeyote. Badala yake, Yeye hufanya kazi ya sasa kwa kutegemea hali za watu. Hivyo, kufanya kazi kwa njia hii ni mara elfu huru zaidi kuliko kazi ambayo watu hufanya. Kwa watu, inaweza hata kuonekana kwamba Mungu hazingatii wajibu Wake na Hufanya kazi kwa namna yoyote Apendayo—lakini kazi yote ambayo Yeye hufanya ni mpya. Lakini, unapaswa kujua kwamba kazi ya Mungu mwenye mwili kamwe haitegemezwi kwa hisia. Wakati huo, baada ya Yesu kumaliza kazi Yake ya kusulubiwa, mara ambapo wanafunzi waliomfuata Yesu walikuwa wamefikia hatua fulani katika kupata kwao uzoefu, walihisi kwamba siku ya Mungu ilikuwa inakuja, na kwamba wangekutana na Bwana hivi karibuni. Hiyo ilikuwa hisia waliyokuwa nayo, na kwao, hisia hii ilikuwa yenye umuhimu mkubwa kabisa. Lakini kwa kweli, hisia zilizo ndani ya watu si za kutegemewa. Walihisi kwamba labda walikuwa wanakaribia kufika mwisho wa njia, au kwamba yote waliyofanya na kuteseka kuliamuliwa na Mungu. Vivyo hivyo, Paulo alisema kwamba alikuwa amemaliza mwendo wake, kwamba alikuwa amevipiga vita, na alikuwa amewekewa taji la haki. Hivyo ndivyo alivyohisi, na aliandika haya katika nyaraka na kuzituma kwa makanisa. Vitendo kama hivyo vilitokana na mzigo alioubeba kwa ajili ya makanisa, na hivyo vilipuuzwa na Roho Mtakatifu. Paulo aliposema maneno hayo, hakuwa na hisia ya mashaka, wala hakuhisi shutuma yoyote, na kwa hiyo aliamini kwamba mambo kama hayo yalikuwa ya kawaida sana na sahihi kabisa na kwamba yalikuwa yametoka kwa Roho Mtakatifu. Lakini yakitazamwa kutoka leo, haya hayakutoka kwa Roho Mtakatifu hata kidogo. Zilikuwa tu njozi za mwanadamu. Kuna njozi nyingi ndani ya wanadamu, na Mungu hazitilii maanani au kutoa maoni yoyote zinapotokea. Kazi nyingi ya Roho Mtakatifu haitekelezwi kupitia kwa hisia za watu—Roho Mtakatifu hafanyi kazi ndani ya hisia za watu kando na nyakati ngumu, za giza kabla ya Mungu kuwa mwili, au kipindi ambapo hakuna mitume au wafanyakazi. Wakati wa hatua hiyo, kazi ya Roho Mtakatifu huwapa watu hisia fulani maalumu. Kwa mfano: Wakati ambapo watu hawana mwongozo wa maneno ya Mungu, wanakuwa na hisia isiyoelezeka ya furaha wanapoomba; wanakuwa na hisia ya furaha mioyoni mwao, na wanakuwa na amani na utulivu. Mara wanapokuwa na mwongozo wa maneno, watu huhisi uchangamfu ndani ya roho zao, wana njia ya kutenda katika vitendo vyao na kwa kawaida pia wana hisia za amani na utulivu. Watu wanapokumbana na hatari, au Mungu anapowazuia kufanya mambo fulani, mioyoni mwao wanahisi kufadhaishwa na kutahayari. Hizi ni hisia anazopewa mwanadamu na Roho Mtakatifu kabisa. Hata hiyo, ikiwa mazingira mabaya yanaibua hali ya hofu, ikiwasababisha watu kuwa na wasiwasi mkuu na wenye uoga, huo ni udhihirisho wa kawaida wa ubinadamu na hauhusiani na kazi ya Roho Mtakatifu.

Watu kila mara huishi katikati ya hisia zao wenyewe, na wamefanya hivyo kwa miaka mingi sana. Wakiwa na amani mioyoni mwao, wao hutenda (wakiamini kwamba kuwa radhi kwao ni hisia ya amani), na wakati ambapo hawana amani ndani ya mioyo yao, wao hawatendi (wakiamini kutopenda au kutotaka kwao kuwa hisia ya wasiwasi). Mambo yakiendelea kwa urahisi, wao hudhani kwamba ni mapenzi ya Mungu. (Kwa kweli, ni jambo ambalo lilipaswa kufanyika kwa urahisi sana, hii ikiwa ndiyo sheria asili ya mambo.) Mambo yasipoenda kwa urahisi, wao hudhani kwamba siyo mapenzi ya Mungu. Wanapokumbana na kitu kisichoendelea kwa urahisi, wao hukoma. Hisia kama hizo si sahihi, na kutenda kulingana nazo kutasababisha kuchelewa kwingi. Kwa mfano, bila shaka kutakuwa na ugumu katika kuweka ukweli katika vitendo na hata zaidi katika kufanya mapenzi ya Mungu. Mambo mengi mazuri yatakuwa magumu kutimiza. Jinsi tu msemo usemavyo, “Utambuzi wa mambo mazuri kawaida hutanguliwa na wakati mgumu.” Watu wana hisia nyingi sana katika maisha yao halisi, zikiwaacha wasijue cha kufanya kila mara na wasiwe na uhakika kuhusu mambo mengi. Hakuna kilicho dhahiri kwa watu wasipoweza kuelewa ukweli. Lakini kwa ujumla, wanapotenda ama kunena kulingana na hisia zao, mradi tu si jambo ambalo hukiuka kanuni za msingi, Roho Mtakatifu hajibu hata kidogo. Ni kama “taji la haki” aliyohisi Paulo: Kwa miaka mingi, hakuna yeyote aliyeamini kwamba hisia zake zilikuwa zenye makosa, wala Paulo mwenyewe hakuhisi kamwe kwamba hisia zake zilikuwa na makosa. Hisia za watu hutoka wapi? Hizo, bila shaka, ni mijibizo itokayo katika akili zao. Hisia tofauti husababishwa kulingana na mazingira tofauti, na mambo tofauti. Wakati mwingi, watu hufanya uamuzi kwa kutumia mantiki ya binadamu ambayo kupitia kwayo hupata seti ya fomyula, jambo ambalo husababisha uundaji wa hisia nyingi za binadamu. Bila kujua, watu huingia katika uamuzi wao wenyewe wenye mantiki, na kwa njia hii, hisia hizi hugeuka kuwa kile ambacho watu hutegemea katika maisha yao; hizo huwa gongo la hisia katika maisha yao, kama vile taji la haki la Paulo au “kukutana na Bwana hewani” kwa Witness Lee. Mungu takribani hana njia ya kuingilia katika hisia za mwanadamu, na lazima Azikubalie zikue kama zitakavyokua. Leo, Nimenena nawe wazi wazi kuhusu vipengele mbalimbali vya ukweli. Ukiendelea kufuata hisia zako, je, wewe bado huishi katika mambo yasiyo dhahiri? Wewe huyakubali maneno ambayo yameonyeshwa kwa dhahiri kwako, na kila mara wewe hutegemea hisia zako binafsi. Katika hili, je, wewe si kama kipofu anayegusa ndovu? Na ni nini ambacho utapata hatimaye?

Kazi yote inayofanywa na Mungu mwenye mwili leo ni halisi. Hiki si kitu ambacho unaweza kuhisi, au kitu unachoweza kufikiria, sembuse kuwa kitu ambacho unaweza kufahamu—ni kitu tu ambacho utaweza kuelewa wakati ambapo ukweli utadhihirika kwako. Wakati mwingine, hata yanapokujia, bado huwezi kuona kwa dhahiri, na watu hawataelewa hadi Mungu mwenyewe achukue hatua kuleta uwazi mkuu kwa mambo ya ukweli kuhusu kile kinachotokea. Wakati huo, kulikuwa na njozi nyingi miongoni mwa wanafunzi waliomfuata Yesu. Waliamini kwamba siku ya Mungu ilikuwa karibu kufika na wao wangekufa kwa ajili ya Bwana hivi karibuni na waweze kukutana na Bwana Yesu. Petro alingoja miaka saba mizima kwa sababu ya hisia hii—lakini bado haikufika. Walihisi kwamba maisha yao yalikuwa yamekomaa; hisia zilizokuwa ndani yao zilizidi mara dufu na hisia hizi zikawa kali zaidi, lakini walipitia kushindwa kwingi na hawakuweza kufanikiwa. Wao wenyewe hawakujua kilichokuwa kikiendelea. Je, kile ambacho kwa kweli kilitoka kwa Roho Mtakatifu hakingeweza kutimizwa? Hisia za watu si za kutegemewa. Hili sababu watu wana njia zao za kufikiria na mawazo yao wenyewe, wao hujenga ushirikiano mwingikutegemea muktadha na hali za wakati huo. Hasa, wakati ambapo jambo huwatendekea watu ambao njia za mawazo yao ni safi, wao huwa wenye kusisimuka mno na hawawezi kujizuia kuunda ushirikiano mwingi. Hili hasa linahusisha “mabingwa” wenye maarifa na nadharia ya fahari sana, ambao uhusiano wao huwa hata mwingi zaidi baada ya miaka mingi ya kushughulika na ulimwengu; bila wao kujua, huo hutwaa mioyo yao na kugeuka kuwa hisia zao zenye nguvu kabisa, na wao huridhika nao. Watu wanapotaka kufanya jambo, hisia na mawazo yatatokea ndani yao na watadhani kwamba yako sahihi. Baadaye, wanapoona kwamba hayajatimia, watu hawawezi kuelewa kilichoenda mrama. Labda wao huamini kwamba Mungu ameubadilisha mpango Wake.

Haizuiliki kwamba watu wote wana hisia. Wakati wa Enzi ya Sheria watu wengi pia walikuwa na hisia fulani, lakini makosa katika hisia zao yalikuwa machache zaidi kuliko ya watu wa leo. Hilo ni kwa sababu hapo awali, watu waliweza kutazama kuonekana kwa Yehova; wangeweza kuona wenye ujumbe na walikuwa na ndoto. Watu wa leo hawawezi kuona maono au wajumbe, na hivyo makosa katika hisia zao yamekua mara dufu. Wakati ambapo watu wa leo huhisi kwamba jambo fulani ni sahihi hasa na kwenda kulitia katika vitendo, Roho Mtakatifu hawashutumu na wana amani sana ndani yao. Baada ya ukweli huo, ni kupitia tu kwa ushirika au kusoma maneno ya Mungu ndipo wao hugundua walikuwa wamekosea. Kipengele kimoja cha hili ni kwamba hakuna wajumbe wanaoonekana kwa watu, ndoto ni haba sana, na watu hawaoni chochote kuhusu maono angani. Kipengele kingine ni kwamba Roho Mtakatifu haongezi shutuma Zake na kufundisha nidhamu Kwake ndani ya watu; kuna kazi ya Roho Mtakatifu ndani yao kwa nadra sana. Hivyo, kama watu hawali na kunywa maneno ya Mungu, hawatafuti ukweli kwa njia ya vitendo, na hawaelewi njia ya kutenda, basi hawatavuna chochote. Kanuni za kazi ya Roho Mtakatifu ni kama zifuatazo: Hazingatii kile ambacho hakihusu kazi Yake; ikiwa jambo haliko ndani ya mawanda ya mamlaka Yake, Yeye haingilii kati wala kuhisi kamwe, Akiwakubalia watu wasababishe matatizo yoyote wapendayo. Unaweza kutenda vyovyote utakavyo, lakini siku itakuja ambapo utajipata ukiwa mwenye kushikwa na wahaka na usijue la kufanya. Mungu hufanya kazi kwa lengo moja tu katika mwili Wake mwenyewe, Yeye haingilii kati kamwe katika kazi ya mwanadamu. Badala yake, Anajiepusha kabisa na ulimwengu wa mwanadamu, na Hufanya kazi ambayo Anapaswa kuifanya. Hutashutumiwa ukifanya kitu kibaya leo, wala hutatuzwa ukifanya kitu kizuri kesho. Haya ni mambo ya binadamu, na hayana uhusiano hata kidogo na kazi ya Roho Mtakatifu—hili haliko ndani ya mawanda ya kazi Yangu hata kidogo.

Katika wakati ambao Petro alikuwa akifanya kazi, alinena maneno mengi na kufanya kazi nyingi. Yawezekana kwamba hakuna kati ya kazi hiyo iliyotoka kwa mawazo ya binadamu? Kwa hiyo kuweza kutoka kabisa kwa Roho Mtakatifu haiwezekani. Petro alikuwa tu kiumbe wa Mungu, alikuwa mfuasi, alikuwa Petro, sio Yesu, na viini vyao havikuwa sawa. Ingawa Petro alitumwa na Roho Mtakatifu, si kila kitu alichofanya kilitoka kwa Roho Mtakatifu, kwani hata hivyo, alikuwa mwanadamu. Paulo pia alinena maneno mengi na aliandika nyaraka zisizo chache kwa makanisa, ambazo baadhi yake zimekusanywa katika Biblia. Roho Mtakatifu hakuonyesha maoni yoyote, kwani huo ndio wakati ambao Paulo alikuwa akitumiwa na Roho Mtakatifu. Alipata uzoefu na maarifa fulani, na kuyaandika chini na kuyapisha kwa ndugu zake katika Bwana. Yesu hakuwa na mjibizo wowote. Kwa nini Roho Mtakatifu hakumkomesha wakati huo? Ilikuwa kwa sababu kuna baadhi ya uchafu unaoibuka kutoka katika namna ya kufikiri ya watu; hili haliepukiki. Aidha, vitendo vyake havikufikia kiwango cha kuwa ukatizaji au usumbufu. Wakati ambapo kuna kazi ya aina fulani kama hiyo ya ubinadamu, watu huona ikiwa rahisi zaidi kuikubali. Mradi uchafu wa namna ya kufikiri ya kawaida ya mwanadamu haujiingizi katika chochote, unachukuliwa kama kawaida. Kwa maneno mengine, watu wote wenye namna ya kufikiri ya kawaida wana uwezo wa kufikiria kwa njia hiyo. Wakati ambapo watu wanaishi katika mwili, wao huwa na namna yao wenyewe ya kufikiri, lakini hakuna njia ya kuondoa vitu hivi. Hata hivyo, baada ya kuipitia kazi ya Mungu kwa muda na kuelewa ukweli fulani, kutakuwa na namna hizi za kufikiri chache zaidi hizi ndani ya akili za watu. Wakati ambapo wamepitia mambo mengi, wataweza kuona kwa dhahiri na hivyo watapinga mambo kidogo zaidi. Kwa maneno mengine, wakati ambapo fikira za watu na uamuzi wenye mantiki hukanushwa, hisia zao zisizo za kawaida zitakuwa chache zaidi. Wale wote wanaoishi katika mwili huwanamna yao wenyewe ya kufikiri, lakini mwishowe, Mungu atawashughulikia hadi kwa kiwango ambapo namna yao wenyewe ya kufikiri hazitaweza kuwasumbua, hawatategemea tena hisia maishani mwao, kimo chao halisi kitakua, na watakuwa na uwezo wa kuishi kwa kufuata maneno ya Mungu ndani ya uhalisi, na hawatafanya tena mambo ambayo si dhahiri au yaliyo tupu, na kisha hawatafanya mambo mbayo yanasababisha usumbufu Kwa njia hii, njozi zao hazitakuwepo tena, na kuanzia wakati huu kuendelea mbele vitendo vyao vitakuwa kimo chao halisi.

Iliyotangulia: Utendaji (4)

Inayofuata: Ukweli wa Ndani wa Kazi ya Ushindi (1)

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp