Njia … (7)

Katika yale tunayoyapitia kwa vitendo, tunaona kwamba kuna nyakati nyingi ambapo Mungu ametufungulia njia yeye binafsi, ili njia tunayoitembea iweze kuwa thabiti zaidi na halisi zaidi. Kwani hii ndiyo njia ambayo Mungu ametufungulia tangu zamani za kale, na ambayo kizazi chetu kimepitishwa baada ya miaka mingi sana. Kwa hiyo tumeishika njia ya wale waliotutangulia, ambao hawakuitembea mpaka mwisho. Tumechaguliwa na Mungu kutembea hatua yake ya mwisho. Na kwa hiyo, tuliandaliwa njia hii hasa na Mungu, na bila kujali iwapo tumebarikiwa ama kukabiliwa na msiba, hakuna mtu mwingine anayeweza kuitembea njia hii. Ningependa kuongeza ufahamu Wangu mwenyewe kwa jambo hili: Usifikirie kujaribu kutorokea kwingine, ama kujaribu kupata njia nyingine, na usitamani hadhi, ama kujaribu kuanzisha ufalme wako mwenyewe—hizi zote ni njozi. Unaweza kuwa na fikira fulani za awali kuhusu maneno Yangu, na hali ikiwa hivyo, Ningependekeza kwamba uache kukanganyika sana. Itakuwa bora ukilifikiria hili zaidi; usijaribu kuwa mjanja, na usiyachanganye mabaya na mema. Utajuta hilo mara tu mpango wa Mungu unapotimia. Ninachosema ni kuwa, ufalme wa Mungu utakapofika, mataifa yote ya dunia yatavunjwa vipande vipande. Wakati huo utaona kwamba mipango yako mwenyewe pia imeharibika, na kwamba wale ambao wanaadibiwa wataangamizwa, na Mungu atadhihirisha tabia Yake kikamilifu kupitia hili. Nadhani kwamba kwa kuwa mambo haya ni dhahiri sana Kwangu, napaswa kukuambia kuyahusu, ili usinilaumu baadaye. Kwamba tumeweza kuitembea njia hii hadi leo kuliamuliwa na Mungu, kwa hiyo usifikiri kwamba wewe ni mtu wa kipekee, wala kuwa huna bahati—hakuna anayeruhusiwa kutoa maoni kuhusu kazi ya sasa ya Mungu asije akavunjwa vipande vipande. Nimetiwa nuru na kazi ya Mungu: Hali iweje, Mungu atalikamilisha kundi hili la watu, kazi Yake haitawahi kubadilika tena, na Atalichukua kundi hili la watu hadi mwisho wa njia, na kukamilisha kazi Yake duniani. Sote tunapaswa kuelewa hili. Watu wengi wanapenda “kutazamia mbele,” na tamaa zao haziishi. Hakuna yeyote kati yao anayeelewa mapenzi ya Mungu ya leo yaliyo dharura, na kwa hiyo wote wanafikiri kuhusu kutoroka. Wao ni kama farasi waliotoroka wanaotaka tu kuzurura mwituni; ni wachache wanaotaka kuishi katika nchi nzuri ya Kanaani ili kutafuta njia ya maisha ya binadamu. Watu wasipofurahia nchi iliyojaa maziwa na asali baada ya kuiingia, ni nini zaidi wanachotaka basi? Kusema ukweli, kuna mwitu tu nje ya nchi nzuri ya Kanaani. Hata baada ya watu kuingia mahali pa pumziko, hawawezi kufanya wajibu wao; je, si wao ni makahaba tu? Ukipoteza nafasi ya kukamilishwa na Mungu hapa, utajuta milele, majuto yako hayatakuwa na kikomo. Utakuwa kama Musa aliyeiona nchi ya Kanaani lakini hakuweza kuifurahia, makonde yake yakiwa yamekazwa sana, na kifo chake kujaa majuto—hudhani hili kuwa jambo la haya? Hulioni kuwa jambo la aibu, la kukejeliwa na wengine? Je, uko tayari kufedheheshwa na wengine? Je, hutaki kuwa na maisha mazuri? Je, hutaki kuwa mtu mwenye heshima na mwadilifu anayekamilishwa na Mungu? Je, kweli huna hamu ya kufanikisha chochote? Huko tayari kuzichukua zile njia nyingine; je, pia hutaki kuichukua njia ambayo Mungu amekuamulia? Je, unathubutu kuyapinga mapenzi ya Mbinguni? Bila kujali jinsi “ustadi” wako ulivyo wa juu, kweli unaweza kuikosea Mbingu? Naamini kwamba ni heri tujaribu kujijua vyema. Neno moja kutoka kwa Mungu linaweza kubadili mbingu na dunia, sembuse mtu mdogo dhaifu machoni pa Mungu?

Katika yale niliyoyapitia Mimi mwenyewe, Nimeona kwamba kadiri unavyozidi kumpinga Mungu, ndivyo Mungu atakavyoonyesha tabia Yake adhimu zaidi, na ndivyo Atakavyokuadibu vikali zaidi; kadiri unavyozidi kumtii, ndivyo Atakavyokupenda na kukulinda zaidi. Tabia ya Mungu ni kama chombo cha adhabu: Ukitii utakuwa salama salimini; wakati hutii—wakati unajaribu kujiringa kila wakati, na kucheza shere kila wakati—tabia ya Mungu inabadilika mara moja. Yeye ni kama jua katika siku yenye mawingu mengi, Atajificha kutoka kwako na kukuonyesha hasira Yake. Tabia Yake pia ni kama hali ya hewa ya mwezi wa Juni, ambapo anga ni shwari kwa mwendo mrefu na maji yako matulivu, mpaka wakati ambapo mkondo unaenda kwa kasi ghafla, na maji yanaanza kuwa na msukosuko wa mawimbi. Je, unaweza kuthubutu kutojali kiasi hiki ukiwa umekabiliwa na tabia kama hii ya Mungu? Katika uzoefu wenu, wengi wenu ndugu mmeona kwamba Roho Mtakatifu anapofanya kazi mchana, mnajawa na imani—lakini bila kutarajia, Roho wa Mungu anakutelekeza ghafla, na unasumbuka sana kiasi kwamba huwezi kulala usiku, ukitafuta huku na kule mahali ambapo Roho Wake ametoweka. Bila kujali unachofanya, huwezi kupata alikoenda Roho Wake—lakini ghafla, Anakuonekania tena, na unafurahi sana kama wakati Petro kwa ghafla alimtazama Bwana wake Yesu mara nyingine, unafurahi sana kiasi kwamba karibu ulie. Kweli umesahau hili baada ya kulipitia mara nyingi sana? Bwana Yesu Kristo, aliyepata mwili, aliyetundikwa msalabani, na kisha akafufuka na kupaa mbinguni, daima amejificha kutoka kwako kwa muda fulani, na kisha Anakuonekania kwa muda fulani. Anajifichua kwako kwa sababu ya haki yako, na Anakasirika na kuondoka kutoka kwako kwa sababu ya dhambi zako, kwa hiyo mbona huombi Kwake zaidi? Je, hukujua kwamba baada ya Pentekoste, Bwana Yesu Kristo ana agizo jingine duniani? Unajua tu ukweli kwamba Bwana Yesu Kristo alipata mwili, Akaja duniani, na kutundikwa msalabani. Hujawahi kutambua kwamba Yesu uliyemwamini awali amemwaminia mtu mwingine kazi Yake kitambo, na kwamba ilikamilishwa zamani, kwa hiyo Roho wa Bwana Yesu Kristo amekuja duniani tena katika mwili ili kufanya sehemu nyingine ya kazi Yake. Ningependa kusema kitu hapa—licha ya ukweli kwamba kwa sasa mko katika mkondo huu, Ninaweza kusema kwamba wachache kati yenu wanamwamini mtu huyu kuwa Yule mliyepewa na Bwana Yesu Kristo. Mnajua tu kumfurahia; hamkiri kwamba Roho wa Mungu amekuja tena duniani, na hamkiri kwamba Mungu wa leo ndiye Yesu Kristo wa miaka mingi iliyopita. Na kwa hiyo Nasema kwamba ninyi nyote mnatembea pasi kuona—mnakubali tu popote mnapoishia—na hampi hili uzito hata kidogo. Kwa hiyo mnamwamini Yesu kwa maneno, lakini mnathubutu kumpinga Yule ambaye Mungu anamshuhudia leo bila kuficha. Je, si wewe ni mpumbavu? Mungu wa leo hajali kuhusu makosa yako. Hakushutumu. Unasema kwamba unamwamini Yesu, kwa hiyo Bwana wako Yesu Kristo anaweza kukuachilia? Je, unadhani kwamba Mungu ni pahali fulani pa wewe kutolea hisia, kudanganya na kusema uongo? Bwana wako Yesu Kristo anapojifichua mara nyingine, Ataamua iwapo wewe ni mwenye haki au iwapo wewe ni mwovu kwa msingi wa jinsi unavyotenda sasa. Watu wengi wanaishia kuwa na fikira kuhusu kile Ninachoita “ndugu Zangu,” na wanaamini kwamba mbinu za Mungu za kufanya kazi zitabadilika. Je, watu kama hawa hawakaribishi kifo? Je, Mungu anaweza kumshuhudia Shetani kama Mungu Mwenyewe? Je, humhukumu Mungu kwa kufanya hili? Je, unaamini kwamba mtu yeyote tu anaweza kuwa Mungu Mwenyewe? Ikiwa kweli ungejua, basi hungekuwa na fikira zozote. Kifungu kifuatacho kiko ndani ya Biblia: Vitu vyote ni kwa ajili Yake na vitu vyote vinatoka Kwake. Atawaleta wana wengi katika utukufu na Yeye ndiye Nahodha wetu…. Kwa hiyo hana aibu atuitapo ndugu. Huenda unaweza kuyakariri maneno haya kwa urahisi, lakini huelewi maana yake halisi. Je, humwamini Mungu pasi kuona?

Naamini kwamba kizazi chetu kimebarikiwa kuweza kuichukua njia ambayo vizazi vya awali havikuweza kukamilisha, na kutazama kuonekana tena kwa Mungu wa miaka mingi iliyopita—Mungu aliye miongoni mwetu, na Aliyejaa katika vitu vyote. Hungewahi kufikiri kwamba ungeitembea njia hii—je, hili ni jambo unaloliweza? Njia hii inaongozwa moja kwa moja na Roho Mtakatifu, inaongozwa na Roho wa Bwana Yesu Kristo aliyeongezwa nguvu mara saba, na ndiyo njia ambayo Mungu wa leo amekufungulia. Hata katika njozi zako zisizowezekana hungewahi kufikiria kwamba Yesu wa miaka mingi iliyopita angeonekana tena mbele yako. Je, huhisi mwenye furaha? Ni nani anayeweza kukutana ana kwa ana na Mungu? Mara nyingi huwa Nakiombea kikundi chetu kipokee baraka kubwa zaidi kutoka kwa Mungu, ili tuweze kufadhiliwa na Mungu na kupatwa na Yeye, lakini pia kumekuwa na nyakati nyingi ambapo Nimelia kwa uchungu kwa sababu yetu, nikimsihi Mungu atupe nuru, ili tuweze kutazama ufunuo mkubwa zaidi. Niwaonapo watu wanaojaribu kumpumbaza Mungu kila wakati na kamwe hawana hamu ya kufanikisha chochote, ama vinginevyo wanaojali mwili, au wanaojitahidi kwa ajili ya masilahi na sifa ili waonekane muhimu, Nawezaje kukosa kuhisi uchungu mkubwa moyoni Mwangu? Watu wanawezaje kuwa wapumbavu kiasi hicho? Kweli kazi Yangu haijakuwa na matokeo? Ikiwa watoto wako wangekuasi na wakose kukupenda kama mzazi, ikiwa wangekosa dhamiri, ikiwa wangejijali tu na kamwe wasizingatie hisia zako, na wakufukuze kutoka nyumbani baada ya wao kukua, ungehisi vipi wakati huo? Je, si machozi yangetiririka usoni pako unapokumbuka damu, jasho na kujitolea ulivyotia katika kuwalea? Hivyo Nimemwomba Mungu mara nyingi na kusema, “Ee Mungu! Ni Wewe tu Ujuaye iwapo Ninaubeba mzigo kwa ajili ya kazi Yako. Mahali ambapo matendo Yangu hayalingani na mapenzi Yako, Unanifundisha nidhamu, Unanikamilisha, na kunifanya Nitambue. Ombi Langu la pekee Kwako ni kwamba Uwaguse watu hawa zaidi, ili Uweze kutukuzwa karibuni na waweze kupatwa na Wewe, ili kazi Yako iweze kutimiza mapenzi Yako, na mpango Wako uweze kukamilika mapema.” Mungu hataki kuwashinda watu kupitia kuwaadibu, Hataki siku zote kuwatawala watu kabisa. Anawataka watu watii maneno Yake na kufanya kazi kwa namna iliyo na nidhamu, na kwa kufanya hili, waridhishe mapenzi Yake. Lakini watu hawana aibu na wanamwasi kila wakati. Naamini kwamba ni bora kwetu kutafuta njia rahisi zaidi ya kumridhisha, yaani, kutii mipango Yake yote. Ikiwa kweli unaweza kutimiza hili, utakamilishwa. Je, hili si jambo rahisi na la furaha? Chukua njia unayopaswa kuchukua; usitilie maanani kile wanachosema wengine, na usifikirie sana. Je, si mustakabali na majaliwa yako viko mikononi mwako mwenyewe? Unajaribu daima kutoroka, ukitaka kuichukua njia ya dunia—lakini mbona huwezi kutoka? Kwa nini unasitasita katika njia panda kwa miaka mingi na kisha unaishia kuichagua njia hii tena? Baada ya kuzurura kwa miaka mingi, kwa nini sasa umerudi kwa hii nyumba bila kutaka? Je, haya ni mapenzi yako? Kwa wale kati yenu mlio katika mkondo huu, ikiwa hamniamini basi sikilizeni hili: Ikiwa umepanga kuondoka, ona kama Mungu atakuruhusu, ona jinsi Roho Mtakatifu anavyokugusa—lipitie mwenyewe. Kusema ukweli, hata ukipitia msiba, lazima uupitie katika mkondo huu, na kama kuna mateso, lazima uteseke hapa, leo; huwezi kuenda pengine. Je, unaelewa hili? Utaenda wapi? Hii ni amri ya Mungu ya utawala. Je, unafikiri kwamba Mungu kulichagua kundi hili la watu hakuna maana? Katika kazi Yake leo, Mungu hakasiriki kwa urahisi—lakini watu wakijaribu kuukatiza mpango Wake, uso Wake unabadilika mara moja, ukiacha kuwa mchangamfu na kugeuka wenye huzuni. Kwa hiyo, Nakushauri utulie na kutii mipango ya Mungu, na umruhusu Akukamilishe. Watu wanaofanya hili tu ndio werevu.

Iliyotangulia: Njia … (6)

Inayofuata: Njia … (8)

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp