Kutanafusi kwa Mwenye Uweza

Kunayo siri kubwa moyoni mwako, ambayo hujawahi kuifahamu kamwe, kwa sababu umekuwa ukiishi katika ulimwengu bila mwanga. Moyo wako na roho yako vimepokonywa na yule mwovu. Macho yako yamezuiwa kwa giza yasione, na huwezi kuliona jua angani wala nyota ikimetameta wakati wa usiku. Masikio yako yamezibwa na maneno ya udanganyifu, na husikii sauti ya Yehova ingurumayo kama radi, wala sauti ya maji yakitiririka kutoka katika kiti cha enzi. Umepoteza kila kitu ambacho kilipaswa kuwa chako kwa haki, kila kitu ambacho Mwenye uweza alikupa. Umeingia katika bahari ya mateso isiyokuwa na mwisho, bila nguvu ya kukuokoa, bila matumaini ya kurudi ukiwa hai, na yote unayofanya ni kupambana na kusonga kila siku.… Tokea wakati huo, hungeweza kuepuka kuteswa na yule mwovu, uliwekwa mbali na baraka za mwenye Uweza, mbali na kukimu kwa mwenye Uweza, unatembea katika njia ambayo huwezi kurejea nyuma tena. Kuitwa mara milioni hakuwezi kusisimua moyo wako na roho yako. Unalala fofofo mikononi mwa yule mwovu, ambaye amekushawishi katika ulimwengu usio na mipaka, bila mwelekeo na bila alama za barabarani. Tokea hapo, umepoteza hali yako ya asili ya kutokuwa na hatia na utakatifu wako, na kuanza kujificha kutokana na utunzaji wa mwenye Uweza. Ndani ya moyo wako, yule mwovu anakuelekeza katika kila jambo na anakuwa uhai wako. Humwogopi tena, kumwepuka, au kumshuku; badala yake, unamchukulia kama Mungu aliye moyoni mwako. Unaanza kumtukuza na kumwabudu, na nyinyi wawili mnakuwa msiotengana kama mwili na kivuli chake, kila akitoa nafsi yake kwa mwingine katika uzima na mauti. Hujui lolote kabisa kuhusu mahali ulikotoka, kwa nini ulizaliwa, au kwa nini utakufa. Unamtazama Mwenye uweza kama mgeni; hujui mwanzo Wake, sembuse yale yote ambayo Amekutendea. Kila kitu kitokacho Kwake kimekuwa cha kuchukiza kwako. Huvitunzi wala kujua thamani yavyo. Unatembea kando na yule mwovu, kuanzia siku ile ulipoanza Mwenye uweza alianza kukukimu. Wewe na yule mwovu mmepitia maelfu ya miaka ya dhoruba na tufani pamoja, na pamoja naye, mnampinga Mungu ambaye alikuwa chanzo cha uhai wako. Hujui lolote kuhusu kutubu, sembuse kwamba umefikia ukingo wa kuangamia. Unasahau kwamba yule mwovu amekujaribu na kukutesa; umesahau asili yako. Kwa njia hii, yule mwovu amekuwa akikuharibu, hatua baada ya hatua, hata mpaka leo. Moyo wako na roho yako vimekufa ganzi na vimeoza. Umeacha kulalamika juu ya maudhi ya dunia ya wanadamu, na huamini tena kwamba dunia si ya haki. Bado hujali sana kama Mwenye uweza yupo. Hii ni kwa sababu ulimchukulia yule mwovu kuwa baba yako wa kweli kitambo, na huwezi tena kutengana naye. Hii ndiyo siri iliyo moyoni mwako.

Alfajiri inapofika, nyota ya asubuhi inaanza kuangaza mashariki. Hii ni nyota ambayo haijawahi kuwepo hapo awali. Inaliangaza anga lililo bado na nyota, ikikuwasha nuru iliyozimwa katika mioyo ya wanadamu. Binadamu si wapweke tena, kwa sababu ya mwanga huu, ambao hukuangazia wewe sawia na wengine. Lakini ni wewe tu unayebaki ukiwa umelala fofofo katika usiku wa giza. Huwezi kuisikia sauti, wala kuiona nuru, hujui kuhusu ujio wa mbingu mpya na nchi mpya, enzi mpya, kwa sababu baba yako hukwambia, “Mwanangu, usiamke, bado ni mapema. Hali ya anga ni baridi, kwa hivyo usiende nje, usije ukachomwa machoni kwa mkuki na upanga.” Unaamini maonyo ya baba yako pekee, maana unaamini kwamba baba yako tu ndiye yuko sahihi, kwa sababu baba yako ana umri mkubwa kuliko wewe na kwamba baba yako anakupenda sana. Maonyo kama hayo na upendo kama huo unakufanya uwache kuamini hekaya kwamba kuna nuru ulimwenguni, na uwache kujali kama ukweli bado upo ulimwenguni humu. Huthubutu tena kutumainia ukombozi kutoka kwa mwenye Uweza. Umeridhika kuwa katika hali hiyo, hutumainii tena ujio wa nuru, na hutazamii tena kuja kwa Mwenye uweza kama ilivyo katika hekaya. Inavyokuhusu wewe, yote yaliyo mazuri hayawezi kufufuliwa tena, wala hayawezi kuendelea kuwepo. Kesho ya wanadamu, siku za baadaye za wanadamu zinapotea, zinaharibika kabisa machoni pako. Unayashika sana mavazi ya baba yako kwa nguvu zako zote, ukifurahia kushiriki taabu zake, ukihofu sana kumpoteza mwenzako wa kusafiri na mwelekeo wa safari yako ya mbali. Ulimwengu huu mkubwa na wenye giza wa binadamu umewaunda wengi wenu, kuwa majasiri na watu wa kujitahidi sana katika kutekeleza majukumu mbalimbali ya ulimwengu huu. Umewaunda “mashujaa” wengi ambao hawaogopi kifo kabisa. Zaidi ya hayo, umetengeneza kundi baada ya kundi la watu waliokufa ganzi na wanadamu waliopooza ambao hawajui makusudi ya kuumbwa kwao. Macho ya Mwenye uweza hukagua kila mmoja wa jamii ya wanadamu walio katika mateso makali. Anachosikia ni vilio vya wale wanaoteseka, Anachoona ni kutokua kwa aibu kwa wale wanaoteseka, na Anachohisi ni kutojiweza na hofu ya jamii ya wanadamu ambayo imepoteza neema ya wokovu. Wanadamu wanakataa utunzaji Wake, wakichagua kutembea katika njia yao wenyewe, na wakijaribu kukwepa macho Yake yanayochunguza kwa karibu, wakiona ni afadhali waonje uchungu wa kilindi cha bahari hadi mwisho, pamoja na adui. Kutanafusi kwa Mwenye uweza hakusikiki tena na binadamu. Mikono ya Mwenye uweza haiko tayari kuwapapasa tena wanadamu hawa wenye huzuni. Anarudia kazi Yake, mara kwa mara akikamata tena, na mara kwa mara akipoteza tena, na kutoka wakati huo, Yeye anaanza kuchoka, kujihisi mchovu, na hivyo Anasitisha kazi inayofanyika, na kuwacha kutembea kati ya wanadamu…. Wanadamu hawana ufahamu kabisa kuhusu mabadiliko haya, hawajui kuhusu kuja na kuondoka, huzuni na ghamu ya Mwenye uweza.

Yote yaliyo duniani humu yanabadilika haraka sawasawa na mawazo ya Mwenye uweza, na chini ya macho Yake. Mambo ambayo wanadamu hawajawahi kuyasikia yanaweza kuja kwa ghafla, ilhali vitu ambavyo wanadamu wamemiliki kwa muda mrefu vinaweza kutoweka bila wao kujua. Hakuna anayeweza kutambua mahali alipo Mwenye uweza sembuse yeyote kuweza kuhisi kuzidi uwezo wa mwanadamu na ukuu wa nguvu za uzima za Mwenye uweza. Anazidi uwezo wa mwanadamu kwa vile Anavyoweza kufahamu yale ambayo wanadamu hawawezi. Yeye ni mkuu kwa vile ni Yeye anayekataliwa na wanadamu na bado Anawaokoa wanadamu. Yeye anajua maana ya maisha na mauti na, isitoshe, Anajua ni kanuni gani zinazofaa katika kuongoza uwepo wa wanadamu Aliowaumba. Yeye ndiye msingi ambao kwao uwepo wa wanadamu hutegemea, na ndiye Mkombozi ambaye hufufua wanadamu tena. Yeye huilemea mioyo yenye furaha kwa huzuni na kuiinua mioyo yenye huzuni kwa furaha, yote kwa ajili ya kazi Yake, na kwa ajili ya mpango Wake.

Wanadamu, baada ya kuuwacha utoaji wa uzima kutoka kwa Mwenye uweza, hawajui azma ya kuishi, lakini hata hivyo wanaogopa kifo. Hawana usaidizi wala msaada, lakini bado wanasita kufumba macho yao, na wanajitayarisha kuendeleza uwepo wa aibu ulimwenguni humu, magunia ya miili wasio na hisia za roho zao wenyewe. Unaishi hivi, bila matumaini, kama vile wafanyavyo wengine, bila lengo. Kuna aliye Mtakatifu tu katika hekaya atakayekuja kuwaokoa watu ambao, wakiwa wanapiga kite katika mateso yao, wanatamani sana kufika Kwake. Hadi sasa, imani hii haijafikiwa kwa wale ambao hawana fahamu. Hata hivyo, watu bado wanaitaka sana. Mwenye uweza ana rehema kwa watu hawa ambao wameteseka sana. Wakati uo huo, Amechoshwa na watu hawa wasio na fahamu, maana imembidi Asubiri sana kupata jibu kutoka kwa wanadamu. Anatamani kutafuta, kuutafuta moyo wako na roho yako, kukuletea chakula na maji na kukuzindua, ili usione kiu na kuhisi njaa tena. Unapokuwa umechoka na unapoanza kuhisi huzuni kubwa ya ulimwengu huu, usipotoke, usilie. Mwenyezi Mungu, Mlinzi, atakaribisha kuwasili kwako wakati wowote. Yuko kandokando yako akiangalia, akikusubiri urudi. Anasubiri siku ambayo utarudisha ghafla kumbukumbu yako: ukitambua ukweli kwamba ulitoka kwa Mungu, lakini wakati fulani usiojulikana ukapoteza mwelekeo wako, wakati fulani usiojulikana ukaanguka barabarani ukiwa hujitambui na tena wakati fulani usiojulikana ukampata “baba.” Isitoshe, unagundua kuwa Mwenye uweza amekuwa hapo muda huo wote, akiangalia, akisubiri kurejea kwako, kwa muda mrefu sana. Amekuwa akitazama na tamanio kubwa, Akingoja itiko pasipo jibu. Kusubiri Kwake kunazidi thamani, na ni kwa ajili ya moyo na roho ya wanadamu. Pengine kusubiri huku hakuna mwisho, na pengine kumefikia mwisho. Lakini unapaswa kujua moyo wako na roho yako hasa viko wapi sasa hivi.

Mei 28, 2003

Iliyotangulia: Mungu Ndiye Chanzo cha Uhai wa Mwanadamu

Inayofuata: Amri Kumi za Utawala Ambazo Lazima Wateule wa Mungu katika Enzi ya Ufalme Wazitii

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp