Mungu Huwafanya Kuwa Watimilifu Wale Wanaolingana na Nia Zake
Sasa Mungu anataka kupata kikundi fulani cha watu, kikundi kinachojumuisha wale wanaofanya juu chini kushirikiana na Yeye, wanaoweza kuitii kazi Yake, wanaoamini maneno ambayo Mungu ananena kuwa ya kweli, na wanaoweza kutia matakwa ya Mungu katika vitendo; wao ndio wale walio na uelewa wa kweli mioyoni mwao, wao ndio wale wanaoweza kufanywa kuwa watimilifu, na bila shaka wataweza kuitembea njia ya utimilifu. Wale wasioweza kufanywa kuwa watimilifu ni watu wasio na uelewa wazi wa kazi ya Mungu, wasiokula na kunywa maneno ya Mungu, wasiotilia maanani maneno Yake, na wasio na mioyo yoyote impendayo Mungu. Wale wanaomtilia shaka Mungu mwenye mwili, ambao daima hawana uhakika kumhusu Yeye, ambao hawachukulii maneno Yake kwa uzito kamwe na daima hujaribu kumdanganya, ni watu wanaompinga Mungu na ni wa Shetani; hakuna namna ya kuwafanya watu kama hao kuwa watimilifu.
Ikiwa unataka kufanywa kuwa mtimilifu, basi ni lazima kwanza upate fadhila machoni pa Mungu, kwa maana Yeye huwafanya kuwa watimilifu wale Anaowatazama kwa upendeleo na wanaolingana na nia Zake. Ukitaka kulingana na nia za Mungu, basi ni lazima uwe na moyo unaoitii kazi Yake, ni lazima ufanye juu chini kufuatilia ukweli, na ni lazima ukubali uchunguzi wa Mungu katika mambo yote. Je, yote unayofanya yamepita chini ya uchunguzi wa Mungu? Je, nia yako ni sahihi? Ikiwa nia yako ni sahihi, basi Mungu atakukubali; ikiwa nia yako si sahihi, hili linaonyesha kwamba kile ambacho moyo wako unapenda si Mungu, bali ni mwili na Shetani. Kwa hivyo, ni lazima utumie maombi kama njia ya kukubali uchunguzi wa Mungu katika mambo yote. Unapoomba, ingawa Sijasimama mbele yako binafsi, Roho Mtakatifu yuko pamoja na wewe, na ni Mimi Mwenyewe na Roho wa Mungu ambao unawaomba. Kwa nini unaamini katika mwili huu? Unaamini kwa sababu Yeye ana Roho wa Mungu. Je, ungemwamini mtu huyu Asingekuwa na Roho wa Mungu? Unapomwamini mtu huyu, unamwamini Roho wa Mungu. Kukufanya umche mtu huyu ni kukufanya umche Roho wa Mungu. Imani katika Roho wa Mungu ni imani katika mtu huyu, na imani katika mtu huyu pia ni imani katika Roho wa Mungu. Unapoomba, unahisi Roho wa Mungu yuko pamoja na wewe na kwamba Mungu yuko mbele yako, na kwa hivyo unamwomba Roho Wake. Leo, watu wengi wanaogopa kuleta matendo yao mbele za Mungu; ingawa unaweza kuudanganya mwili Wake, huwezi kumdanganya Roho Wake. Jambo lolote ambalo haliwezi kustahimili uchunguzi wa Mungu halikubaliani na ukweli, na linapaswa kuwekwa kando; kufanya vinginevyo ni kumkosea Mungu. Kwa hivyo, iwe unaomba, unazungumza na kufanya ushirika na akina ndugu, au unatekeleza wajibu wako na kufanya mambo, ni lazima uweke moyo wako mbele za Mungu. Unapotimiza wajibu wako, Mungu yuko pamoja na wewe, na mradi nia yako ni sahihi na ni kwa ajili ya kazi ya nyumba ya Mungu, Atakubali yote unayofanya; unapaswa kutimiza wajibu wako kwa dhati. Unapoomba, unapaswa kuwa na moyo umpendao Mungu na kutafuta utunzaji, ulinzi, na uchunguzi wa Mungu. Ikiwa hizi ndizo nia zako, maombi yako yatakuwa na matokeo. Kwa mfano, unapoomba katika mikutano, ukiufungua moyo wako na umwombe Mungu na umwambie yaliyo moyoni mwako bila kusema uwongo, basi maombi yako hakika yatakuwa na matokeo. Ukiwa na moyo wa dhati umpendao Mungu, basi weka kiapo kwa Mungu: "Mungu, uliye mbinguni na duniani na kati ya vitu vyote, ninaapa Kwako: Roho Wako na achunguze yote ninayofanya na anilinde na anitunze nyakati zote, ili kila kitu ninachofanya kiweze kusimama imara mbele Yako. Ikitukia moyo wangu usikupende Wewe au uwahi kukusaliti, basi niadibu na unilaani vikali. Usinisamehe katika maisha haya wala katika dunia ijayo!" Je, unathubutu kuweka kiapo kama hicho? Ikiwa huthubutu, hili linaonyesha kwamba wewe ni mwoga, na kwamba bado unajipenda mwenyewe. Je, ninyi mna azimio hili? Ikiwa hili kweli ndilo azimio lenu, mnapaswa kuweka kiapo hiki. Ukiwa na azimio na uweke kiapo kama hicho, basi Mungu atatimiza azimio lako. Unapoweka kiapo kwa Mungu, Yeye husikiliza. Mungu huamua iwapo wewe ni mwenye dhambi au mwenye haki kulingana na maombi yako na utendaji wako. Sasa ninyi mko katika mchakato wa kufanywa kuwa watimilifu, na ikiwa kwa kweli una imani ya kufanywa kuwa mtimilifu, basi utaleta yote unayofanya mbele za Mungu na ukubali uchunguzi Wake. Ukifanya jambo la uasi uliokithiri au ukimsaliti Mungu, basi Yeye atakitimiza kiapo chako; katika wakati huo, iwe unakabiliwa na upotevu au unakabiliwa na kuadibiwa, litakuwa ni kosa lako mwenyewe. Wewe uliweka kiapo, kwa hivyo unapaswa kukitii. Ukiweka kiapo, lakini usikitii, utaingia katika mateso ya milele. Kwa kuwa kiapo kilikuwa chako, Mungu atakitimiza kiapo chako. Wengine huogopa baada ya kuomba, na kusema, "Yote yamekwisha! Fursa yangu ya kuwa mpotovu imekwisha; fursa yangu ya kufanya mambo mabaya imekwisha; fursa yangu ya kujiingiza katika matamanio yangu ya kidunia imekwisha!" Watu hawa bado wanapenda dunia na dhambi, na hakika wataingia katika mateso ya milele.
Kama muumini wa Mungu, ni lazima uweze kuleta matendo na vitendo vyako vyote mbele Zake na ukubali uchunguzi Wake. Ikiwa kile unachofanya kinaweza kuletwa mbele ya Roho wa Mungu lakini si mbele ya mwili wa Mungu, hili linaonyesha kwamba hujakubali uchunguzi wa Roho Wake. Roho wa Mungu ni nani? Mtu ambaye Mungu anamshuhudia ni nani? Je, Wao si kitu kimoja? Wengi huwaona kama viumbe wawili tofauti, wakiamini Roho wa Mungu ni Roho wa Mungu, na mtu ambaye Mungu anamshuhudia ni mwanadamu tu. Lakini, je, wewe hujakosea? Mtu huyu anafanya kazi kwa niaba ya nani? Wale wasiomjua Mungu mwenye mwili hawana ufahamu wa kiroho. Roho wa Mungu na mwili Wake ni kitu kimoja, kwa sababu Roho wa Mungu amefanywa halisi katika mwili. Ikiwa mtu huyu si mwema kwako, je, Roho wa Mungu atakuwa mwema? Je, wewe hujachanganyikiwa? Leo, wote wasioweza kukubali uchunguzi wa Mungu hawawezi kupokea kibali Chake, na wale wasiomjua Mungu mwenye mwili hawawezi kufanywa kuwa watimilifu. Angalia yote unayofanya, na uone kama yanaweza kuletwa mbele za Mungu. Ikiwa huwezi kuleta yote unayofanya mbele za Mungu, hili linaonyesha kwamba wewe ni mtenda maovu. Je, watenda maovu wanaweza kufanywa kuwa watimilifu? Yote unayofanya, kila kitendo, kila nia, na kila mwitikio vinapaswa kuletwa mbele za Mungu. Hili linamaanisha kwamba kila kitu kuanzia maisha yako ya kiroho ya kila siku—kuomba, kumkaribia Mungu, kula na kunywa maneno ya Mungu, kushiriki na akina ndugu zako, na kuishi maisha ya kanisa—hadi huduma yako ya ushirikiano na wengine, kinapaswa kuletwa mbele za Mungu ili Yeye avichunguze. Ni utendaji kama huo ndio utakaokusaidia kufikia ukuaji katika maisha. Mchakato wa kukubali uchunguzi wa Mungu ni mchakato wa utakaso. Kadiri unavyoweza kukubali uchunguzi wa Mungu, ndivyo unavyozidi kutakaswa na ndivyo unavyozidi kulingana na nia za Mungu, ili usiingie katika upotovu, na moyo wako utaweza kuishi katika uwepo Wake. Kadiri unavyokubali uchunguzi Wake, ndivyo Shetani anavyozidi kuaibishwa na ndivyo uwezo wako wa kuasi mwili unavyozidi kuwa mkubwa. Kwa hivyo, kukubali uchunguzi wa Mungu ni njia ya utendaji ambayo watu wanapaswa kuifuata. Haijalishi kile unachofanya, hata unaposhiriki na akina ndugu zako, unapaswa kuleta matendo yako mbele za Mungu na kutafuta uchunguzi Wake, na unapaswa kukusudia kumtii Mungu Mwenyewe; hili litafanya utendaji wako uwe sahihi zaidi. Ikiwa tu unaleta yote unayofanya mbele za Mungu na ukubali uchunguzi wa Mungu ndiyo unaweza kuwa mtu anayeishi katika uwepo wa Mungu.
Wale wasio na uelewa wa Mungu hawawezi kamwe kumtii Mungu kikamilifu. Watu kama hawa ni wana wa uasi. Wana tamaa ya makuu sana, na kuna uasi mwingi sana ndani yao, kwa hivyo wanajitenga na Mungu na hawako tayari kukubali uchunguzi Wake. Watu kama hawa hawawezi kufanywa kuwa watimilifu kwa urahisi. Watu wengine ni wenye kujagua kuhusu jinsi wanavyokula na kunywa maneno ya Mungu na katika kuyakubali kwao. Wanakubali sehemu fulani za maneno ya Mungu zinazolingana na mawazo yao huku wakikataa zile ambazo hazilingani. Je, huu si uasi na upinzani wa wazi kabisa dhidi ya Mungu? Mtu akimwamini Mungu kwa miaka mingi bila kupata hata uelewa kidogo kumhusu Yeye, basi yeye ni asiyeamini. Wale walio tayari kukubali uchunguzi wa Mungu ndio wale wanaofuatilia uelewa kumhusu Yeye, walio tayari kukubali maneno Yake. Wao ndio watakaopokea urithi na baraka za Mungu, na wao ndio waliobarikiwa zaidi. Mungu huwalaani wale wasio na nafasi kwa ajili Yake mioyoni mwao, na Yeye huwaadibu na kuwatelekeza watu kama hao. Ikiwa humpendi Mungu basi Atakutelekeza, na ikiwa husikilizi kile Ninachosema, basi Ninaahidi kwamba Roho wa Mungu atakutelekeza. Jaribu ikiwa huamini! Leo Ninakufafanulia njia ya utendaji, lakini kama utaitia katika vitendo ni juu yako wewe mwenyewe. Ikiwa huamini, ikiwa huitii katika vitendo, utajionea mwenyewe kama Roho Mtakatifu anafanya kazi ndani yako au la! Ikiwa hufuatilii uelewa wa Mungu, basi Roho Mtakatifu hatafanya kazi ndani yako. Mungu hufanya kazi ndani ya wale wanaofuatilia na kuthamini maneno Yake. Kadiri unavyothamini maneno ya Mungu zaidi, ndivyo Roho Wake atafanya kazi zaidi ndani yako. Kadiri mtu anavyothamini maneno ya Mungu zaidi, ndivyo atakavyopata fursa nyingi zaidi za kufanywa kuwa mtimilifu na Mungu. Mungu huwafanya kuwa watimilifu wale wanaompenda Yeye kwa kweli, na Yeye huwafanya kuwa watimilifu wale ambao mioyo yao imetulia mbele Zake. Unapaswa kuthamini kazi yote ya Mungu, kuthamini nuru ya Mungu, kuthamini uwepo wa Mungu, kuthamini utunzaji na ulinzi wa Mungu, na kuthamini jinsi maneno ya Mungu yanavyokuwa uhalisi wako na kutoa ruzuku kwa maisha yako—hili linalingana vyema zaidi na nia za Mungu. Ikiwa unathamini kazi ya Mungu, yaani, ikiwa unathamini kazi yote ambayo Yeye amefanya ndani yako, basi Yeye atakubariki na kusababisha yote yaliyo yako yaongezeke. Usipoyathamini maneno ya Mungu, Yeye hatafanya kazi ndani yako; Atakupa tu neema kidogo kwa ajili ya imani yako, akikuruhusu uwe na baraka kidogo ya kimwili au kuipa familia yako usalama kidogo. Unapaswa kutafuta kuyafanya maneno ya Mungu kuwa uhalisi wako, kuweza kumridhisha Yeye, na kulingana na nia Zake; hupaswi kutafuta tu kufurahia neema Yake. Hakuna kitu muhimu zaidi kwa waumini kuliko kupokea kazi ya Mungu, kupata ukamilisho, na kuwa wale wanaofuata mapenzi ya Mungu. Hili ndilo lengo unalopaswa kufuatilia.
Yote ambayo mwanadamu alifuatilia katika Enzi ya Neema sasa yamepitwa na wakati, kwa sababu kwa sasa kuna kiwango cha juu zaidi cha ufuatiliaji; kile kinachofuatiliwa ni cha juu zaidi na cha vitendo zaidi, kile kinachofuatiliwa kinaweza kuridhisha vyema zaidi kile ambacho mwanadamu anataka kwa ndani. Katika enzi zilizopita, Mungu hakufanya kazi juu ya watu kama Anavyofanya leo; Yeye hakuzungumza nao sana kama Anavyofanya leo, wala matakwa Yake kwao hayakuwa ya juu kama matakwa Yake ya leo. Ukweli kwamba Mungu ana matakwa haya kwenu sasa kunaonyesha kwamba nia kuu ya Mungu inawalenga ninyi, kwenye kikundi hiki cha watu. Ikiwa kwa kweli unataka kufanywa kuwa mtimilifu na Mungu, basi lifuatilie hilo kama lengo lako kuu. Haijalishi kama unakimbia huku na huko, unajitumia, unatimiza wajibu, au unakubali agizo la Mungu, daima lenga kufanywa kuwa mtimilifu na kuridhisha nia za Mungu, ili kufikia lengo hili. Mtu akisema hafuatilii kufanywa kuwa mtimilifu na Mungu au kuingia katika uzima, bali anafuatilia tu amani na furaha ya mwili, basi yeye ni kipofu zaidi kati ya watu. Wale wasiofuatilia uhalisi wa maisha, bali wanafuatilia tu uzima wa milele katika dunia ijayo na usalama katika maisha haya, ndio vipofu zaidi kati ya watu. Kwa hivyo, yote unayofanya yanapaswa kufanywa kwa madhumuni ya kufanywa kuwa mtimilifu na kupatwa na Mungu.
Kazi ambayo Mungu anafanya juu ya watu ni kuwaruzuku kulingana na mahitaji yao tofauti. Kadiri maisha ya mtu yalivyo ya juu, ndivyo anavyohitaji zaidi na ndivyo anavyofuatilia zaidi. Ikiwa katika awamu hii huna ufuatiliaji, hili linathibitisha kwamba Roho Mtakatifu amekutelekeza. Wale wote wanaofuatilia maisha hawatatelekezwa kamwe na Roho Mtakatifu; watu kama hao daima wana kitu cha kufuatilia, na daima wana shauku mioyoni mwao. Watu kama hao hawatosheki kamwe na hali yao ya sasa. Kila awamu ya kazi ya Roho Mtakatifu inalenga kufikia matokeo ndani yako, lakini ukiridhika na hali yako ya sasa, ikiwa huna mahitaji tena, ikiwa hukubali tena kazi ya Roho Mtakatifu, basi Atakutelekeza. Watu wanahitaji uchunguzi wa Mungu kila siku; wanahitaji ruzuku tele kutoka kwa Mungu kila siku. Je, watu wanaweza kumudu bila kula na kunywa neno la Mungu kila siku? Ikiwa mtu daima anahisi kana kwamba hawezi kula au kunywa neno la Mungu kwa namna ya kutosha, ikiwa daima anatafuta na daima ana njaa na kiu ya haki, Roho Mtakatifu daima atafanya kazi ndani yake. Kadiri mtu anavyokuwa na njaa na kiu ya haki, ndivyo anavyoweza kufanya ushirika kuhusu mambo ya vitendo. Kadiri mtu anavyozingatia kutafuta ukweli, ndivyo anavyofikia ukuaji katika maisha yake kwa haraka zaidi, na kumfanya awe mwenye uzoefu mwingi na awe tajiri wa nyumba ya Mungu.