Majukumu ya Viongozi na Wafanyakazi (2)

Kwanza tupitie maudhui makuu ya ushirika wetu katika mkutano uliopita. (Wakati uliopita, Uliorodhesha majukumu kumi na tano ya viongozi na wafanyakazi, na hasa ulishiriki juu ya mawili ya kwanza: La kwanza ni kuwaongoza watu kula na kunywa maneno ya Mungu na kuyaelewa, na kuingia katika uhalisi wa maneno ya Mungu; la pili ni kufahamu hali za kila aina ya mtu, na kusuluhisha matatizo mbalimbali yanayohusiana na kuingia katika uzima wanayokumbana nayo katika maisha yao halisi. Kulingana na vipengele hivi viwili, Ulichanganua udhihirisho husika wa viongozi wa uongo.) Je, mmewahi kutafakari kuhusu ni majukumu gani kati ya haya mawili ambayo mngeweza kutekeleza kama mngekuwa viongozi? Watu wengi huhisi kila mara kwamba wana ubora kiasi wa tabia, akili, na hisia ya mzigo kiasi fulani, na hivyo hutamani kugombea nafasi ya kuwa viongozi, na hawataki kuwa wafuasi wa kawaida. Kwa hivyo, kwanza angalia kama unaweza kutekeleza majukumu haya mawili, na ni lipi ambalo unaweza zaidi wa kutekeleza, na una uwezo wa kulichukua. Tusizungumzie kwa sasa kuhusu kama wewe una ubora wa tabia wa kuwa kiongozi, au kama una uwezo wa kazi hii au hisia ya mzigo, na kwanza uangalie iwapo unaweza kutekeleza majukumu haya mawili vizuri. Je, umewahi kutafakari swali hili? Wengine wanaweza kusema, “Sipangi kuwa kiongozi, kwa hivyo kwa nini nitafakari? Ninahitaji tu kufanya kazi yangu vizuri—swali hili halinihusu mimi. Katika maisha haya, sitaki kamwe kuwa kiongozi, na sitaki kamwe kuchukua majukumu ya kiongozi au mfanyakazi, kwa hivyo sihitaji kamwe kutafakari maswali kama hayo.” Je, kauli hii ni sahihi? (Hapana.) Hata kama hutaki kuwa kiongozi, je, bado huhitaji kujua jinsi mtu anayekuongoza anavyotekeleza majukumu haya mawili, iwapo ametimiza majukumu yake, iwapo ana ubora wa tabia unao, uwezo, na hisia ya mzigo inaohitajika, na iwapo anafikia mahitaji haya mawili? Kama huelewi au huwezi kung’amua mambo haya, na akuongoze utumbukie kwenye shimo, je, utajua? Ukimfuata tu kwa njia iliyochanganyikiwa na uwe tu mpumbavu, kama hujui kwamba yeye ni kiongozi wa uongo, au kwamba anakupotosha au hujui anakokuelekeza, basi wewe utakuwa hatarini. Kwa sababu huelewi mawanda ya majukumu ya viongozi na wafanyakazi, na huna utambuzi wa viongozi wa uongo, utamfuata kwa njia ya kuchanganyikiwa, na kufanya chochote anachokwaomba ufanye, bila kujua kama anachoshiriki na wewe kinapatana na ukweli katika maneno ya Mungu, au kama ni ukweli. Utafikiri kwamba kwa sababu ana shauku, kwa sababu anajishughulisha kufanya kazi kwa bidii kuanzia alfajiri hadi jioni na anaweza kulipa gharama, na kwa sababu, mtu anapokuwa katika shida, ananyoosha mkono wa msaada kumsaidia, na hamwonyeshi kutojali, kwamba yuko anafikia kiwango kinachohitajika kama kiongozi. Hujui kwamba viongozi wa uongo hawana uwezo wa kuelewa maneno ya Mungu, kwamba haijalishi wanafanya kazi kwa muda gani, hawataelewa nia za Mungu au kujua mahitaji ya Mungu ni nini, hawataweza hata kutambua mafundisho ni nini na ukweli ni nini, hawatajua jinsi ya kuelewa maneno ya Mungu na ukweli kwa njia safi, wala hawatajua jinsi ya kula na kunywa maneno ya Mungu—hili linaonyesha wazi kwamba wao ni viongozi wa uongo. Viongozi wa uongo hawapati matokeo yoyote katika kazi wanayofanya. Watashiriki na wewe na kufanya mambo kwa njia isiyo ya dhati, lakini hawatajua vizuri kuhusu hali uliyomo, ni magumu gani mnayokabiliana nayo, na kama yametatuliwa kweli, na wewe mwenyewe hutajua mambo haya pia. Kwa nje, watakuwa wamesoma maneno ya Mungu na kushiriki kuhusu ukweli na wewe, lakini wewe bado utaishi katika hali ya makosa bila uwezo wa kugeuza hayo. Haijalishi ni magumu gani unayokumbana nayo, wataonekana kutekeleza majukumu yao, lakini hakuna matatizo yako yoyote yatakayotatuliwa kupitia ushirika au usaidizi wao, na matatizo hayo yataendelea. Je, kiongozi wa aina hii anafikia kiwango kinachohitajika? (Hapana.) Kwa hivyo, ni ukweli upi unaohitaji kuelewa ili kutambua mambo haya? Unahitaji kuelewa iwapo viongozi na wafanyakazi hufanya kila kazi na kushughulikia kila tatizo kulingana na mahitaji ya maneno ya Mungu, kama kila neno wanalonena ni la vitendo na linalingana na ukweli katika maneno ya Mungu. Zaidi ya hayo, unahitaji kuelewa iwapo, unapokabiliwa na matatizo mbalimbali, mbinu yao ya kutatua masuala inakuongoza kuelewa maneno ya Mungu na kupata njia ya kutenda, au wanazungumza tu maneno na mafundisho, wanapaza tu sauti wakisema kauli mbiu, au kukuonya. Baadhi ya viongozi na wafanyakazi hupenda kuwasaidia watu kupitia katika kuwasihi, wengine kupitia kutia motisha, na wengine kupitia kufichua, kushutumu, na kupogoa. Bila kujali njia wanayotumia, ikiwa inaweza kukuongoza wewe uingie katika ukweli halisi, utatue matatizo yako halisi, ikufanye uelewe nia za Mungu ni zipi na hivyo kukuwezesha ujijue na kupata njia ya utendaji, basi unapokabiliwa na hali kama hizo katika siku zijazo, utakuwa na njia ya kufuata. Kwa hivyo, kiwango cha msingi zaidi cha kupima kama kiongozi au mfanyakazi anafikia kiwango kinachohitajika ni kama anaweza kutumia ukweli kutatua shida na matatizo ya watu, akiwawezesha kuelewa ukweli na kupata njia ya utendaji.

Wakati uliopita, tulishiriki kwa kiasi fulani kuhusu majukumu ya kwanza na ya pili ya viongozi na wafanyakazi, na tukachanganua baadhi ya udhihirisho wa viongozi wa uongo kuhusiana na majukumu haya mawili. Udhihirisho wao wa msingi ni uelewa wa kina kifupi na wa juujuu wa maneno ya Mungu na kushindwa kuelewa ukweli. Ni dhahiri kwamba kwa sababu hiyo hawawezi kuwaongoza wengine kuelewa maneno ya Mungu na kuelewa nia Zake. Watu wanapokabiliwa na ugumu, viongozi wa uongo hawawezi kutumia ujuzi wao wa uzoefu kuwaongoza watu hao kuelewa ukweli na kuingia katika uhalisi, ili wawe na njia ya kufuata, wala hawawezi kuwafanya watafakari na kujijua katikati ya matatizo mbalimbali, na kutatua matatizo haya kwa wakati mmoja. Kwa hivyo leo, hebu kwanza tushiriki kuhusu ugumu wa kuingia katika uzima ni upi, na ni matatizo gani mbalimbali ya kawaida yanayohusiana na kuingia katika uzima ambayo watu hukutana nayo mara nyingi katika maisha yao ya kila siku. Hebu tufanye muhtasari maalum wa mambo haya. Je, hili linahitaji tulifanyie ushirika? (Ndiyo.) Ninyi mnavutiwa kwa kiasi fulani na mada hizi zinazohusiana na kuingia katika uzima sasa, sivyo? Nilipokutana nanyi kwa mara ya kwanza na kuzungumza nanyi, bila kujali kilichosemwa, mlikuwa ganzi na msio wachangamfu, wavivu, na msio na mjibizo wa haraka. Ilionekana kama kwamba nyinyi hamkuelewa chochote, na hamkuwa na kimo chochote, sembuse kuingia katika uzima. Sasa, tunapozungumzia mambo yanayohusu kubadilisha tabia ya mtu maishani, wengi wenu mnavutiwa na mada hii, na mna maoni fulani kuhusu hilo. Hili ni jambo chanya. Kama nyinyi hamngekuwa mkifanya wajibu wenu, je, mngeweza kufikia mambo haya? (Hapana, hatungeweza.) Hii ni neema ya Mungu; yote yanatokana na neema Yake.

Kipengele cha Pili: Kufahamu hali za kila aina ya mtu, na kusuluhisha matatizo mbalimbali yanayohusiana na kuingia katika uzima wanayokumbana nayo katika maisha yao halisi (Sehemu ya Pili)

Aina Nane za Matatizo ya Kuingia Katika Uzima

I. Matatizo Yanayohusiana na Kutimiza Wajibu wa Mtu

Kuhusu ugumu wa kuingia katika uzima, hebu kwanza tuangalie kwa upana zaidi ugumu unaohusiana na kutekeleza wajibu wa mtu. Unapokabiliana na matatizo yanayohusisha kutenda ukweli katika kutekeleza wajibu wako, na huwezi kushughulikia mambo kulingana na kanuni, je, huu si ugumu katika kuingia katika uzima? (Ndiyo, ni ugumu.) Kwa maneno rahisi, ni hali, mawazo, mitazamo mbalimbali, na njia fulani zisizo sahihi za kufikiri zinazotokea wakati wa kutekeleza wajibu wa mtu. Kwa hivyo, ni matatizo gani maalum yaliyopo katika suala hili? Kwa mfano, kila mara kuna kujaribu kutotenda kwa dhati, kuwa mjanja, na wa kuzembea wakati wa kutekeleza wajibu wa mtu—je, hii si hali ambayo hudhihirika na kufunuliwa kwa kawaida wakati wa utekelezaji wa wajibu? Pia kuna kutoijali kazi yako sahihi, na kujilinganisha na wengine kila mara unapotekeleza wajibu wako, kuchukulia mahali ambapo mtu hufanya wajibu wake kama uwanja wa michezo au uwanja wa mapambano, na kufikiria kuhusu kupata “kigezo” wakati wowote mtu anapotekeleza wajibu wake, ukisema kwa ndani: “Nitaona ni nani aliye bora kuniliko mimi na ni nani anayeweza kuchochea roho yangu ya kupambana, kisha nitashindana na yeye, nigombee na yeye na kujilinganisha na yeye, ili nione ni nani anayepata matokeo bora na ufanisi wa hali ya juu katika kutekeleza wajibu wake, na ni nani aliye bora katika kushinda mioyo ya watu.” Kisha kuna kuelewa kanuni za kutekeleza wajibu wako lakini kutotaka kuzifuata, au kutenda kulingana na ukweli katika maneno ya Mungu au mahitaji ya nyumba ya Mungu, na kila mara kupendelea kuchafua utendaji wa wajibu wa mtu na mapendeleo ya mtu binafsi, ukisema, “Ninapenda kufanya namna hii, napenda kufanya namna ile; Niko tayari kufanya hivi, nataka kufanya namna hiyo.” Huu ni ukaidi, kutaka kufuata mapenzi yako mwenyewe kila wakati, na kutenda jinsi unavyotaka kulingana na mapendeleo yako mwenyewe, kupuuza mahitaji yote ya nyumba ya Mungu, na kupendelea kupotoka kutoka kwenye njia sahihi. Je, haya si maonyesho halisi ambayo watu wengi huonyesha wanapotekeleza wajibu wao? Ni wazi kwamba masuala haya yote yanahusisha ugumu katika kutekeleza wajibu wako. Tafadhali ongeza juu ya haya. (Kushindwa kushirikiana kwa upatano na wengine unapotekeleza wajibu wako, na Kutenda kwa njia yako mwenyewe kila wakati.) Hili pia linahesabiwa kama ugumu. Kushindwa kushirikiana kwa upatano na wengine unapotekeleza wajibu wako, na kutaka kufanya mambo kwa njia yako mwenyewe kila wakati na kuwa na uamuzi wa mwisho; kutaka kujinyenyekeza kutafuta ushauri na kusikiliza maoni ya wengine unapokabiliwa na matatizo, lakini kutoweza Kutenda hili, na kuhisi vibaya mtu anapojaribu kufanya hivi—hili ni tatizo. (Daima kulinda maslahi yako mwenyewe unapotekeleza wajibu, kuwa mbinafsi na mchafu, na kujua jinsi ya kutatua tatizo linapotokea, lakini kuhisi kwamba halikuhusu wewe, kuogopa kuchukua jukumu ikiwa litaenda vibaya, na hivyo kutothubutu kusonga mbele.) Kutotatua tatizo unapoliona, kulichukulia kuwa halihusiani na wewe mwenyewe, na kulipuuza—hili pia linahesabiwa kama kutekeleza wajibu wako bila uaminifu. Bila kujali kama wewe unawajibika kwa kazi au la, ikiwa unaweza kuona na kutatua tatizo, unapaswa kutekeleza jukumu hili. Huu ni wajibu wako na kazi inayokuhusu. Ikiwa msimamizi anaweza kulitatua, wewe unaweza kuliacha, lakini ikiwa hawezi, wewe unapaswa kusonga mbele na kulitatua. Msigawanye masuala kulingana na upo katika upeo wa majukumu ya nani—huku ni kutokuwa mwaminifu kwa Mungu. Kuna kitu kingine? (Kutegemea akili na vipawa vya mtu kufanya kazi huku akitekeleza wajibu wake, na kutotafuta ukweli.) Kuna watu wengi ambao wako hivi. Daima wanafikiri kwamba wana akili na ubora mzuri wa tabia, na hawajali kila kitu kinachowapata; hawatafuti ukweli hata kidogo, na hutenda kulingana na mapenzi yao wenyewe, na kwa sababu hiyo, hawawezi kutekeleza wajibu wowote ipasavyo. Haya yote ni matatizo ambayo watu hukabiliana nayo wanapotekeleza wajibu wao.

II. Masuala Yanayohusiana na Jinsi Mtu Anavyoshughulikia Matarajio na Hatima Yake

Jinsi mtu anavyoyachukulia matarajio na hatima yake pia ni suala muhimu linalohusiana na kuingia katika uzima. Baadhi ya watu wako tayari kulipa gharama ikiwa wanaamini wana tumaini la kuokolewa, na wanakuwa hasi wakifikiri kwamba hakuna tumaini. Nyumba ya Mungu isipowastawisha na kuwakuza, hawataki kulipa gharama, na wao hufanya wajibu wao kwa njia isiyo ya dhati tu bila kuchukua jukumu. Bila kujali wanachofanya, wao hufikiria matarajio na hatima yao kila wakati, wakijiuliza, “Je, kweli nitakuwa na hatima nzuri? Je, ahadi za Mungu zimetaja matarajio na hatima ya mtu kama mimi itakuwaje?” Wasipopata jibu sahihi, hawatakuwa na shauku ya kufanya chochote. Wakistawishwa na kukuzwa na nyumba ya Mungu, wanajawa nguvu, na katika kila kitu wanachofanya wao ni waangalifu hasa. Hata hivyo, wakishindwa kufanya wajibu wao vizuri na wafukuzwe, wao huwa hasi mara moja na wanaacha wajibu wao, wanakosa matumaini yote. Wanapokabiliwa na upogoaji, wao huwaza, “Je, Mungu hanipendi tena? Kama ni hivyo, Angesema hivyo mapema, badala ya kuzuia ufuatiliaji wangu wa dunia!” Wakitimuliwa, wao huwaza, “Je, hawanidharau? Ni nani aliyeniripoti? Je, ninaondolewa? Kama ni hivyo, wangesema hivyo mapema!” Zaidi ya hayo, mioyo yao imejaa miamala, madai, na maombi yasiyo na msingi kutoka kwa Mungu. Haijalishi kanisa linawapangia wafanye nini, wanaona kwamba wao kuwa na matarajio mema na hatima njema, pamoja na baraka za Mungu, ndiyo masharti ya kufanya hivyo. Angalau, kuchukuliwa kwa sura na mtazamo mzuri, na kukubaliwa, ni masharti yao ya kukubali na kutii. Je, haya si maonyesho ya jinsi wanavyoshughulikia matarajio na hatima yao? Ongeza kwenye haya. (Kupotoka au masuala yakiibuka wakati wa kufanya wajibu wa mtu na apogolewe, yeye hulalamika kumhusu Mungu na kujilinda; anaogopa kufunuliwa na kuondolewa, na kila mara wanajiachia njia ya kutokea.) Wanahisi kuogopa kufunuliwa na kuondolewa, na kila mara wanaacha njia ya kutokea—huu pia ni udhihirisho wa jinsi wanavyoshughulikia matarajio na hatima yao. (Mtu anapoona kwamba maneno ya Mungu ya kufichua na kuonyeshwa sifa yanalingana na yeye, au anapokabiliwa na kupogolewa na ahisi aibu, anahitimisha kwamba yeye ni mwenye kuboronga, ibilisi na Shetani, na kwamba hawezi kukubali ukweli. Anaamua kwamba hana tumaini la kuokolewa na hivyo anakuwa hasi.) Linapokuja suala la matarajio na hatima yao, watu hawawezi kuacha kabisa nia na matamanio yao wenyewe. Wanayachukulia kila mara kama vitu muhimu zaidi na kuyafuatilia ipasavyo, wakivichukulia kama nguvu inayowasukuma na sharti la kila kitu wanachofuatilia. Wanapokabiliwa na hukumu, kuadibu, majaribu, kusafishwa, au kufunuliwa, au wanapokutana na hali hatari, mara moja wanawaza, “Je, Mungu hanitaki tena? Je, Ananisukuma mbali? Sauti Anayozungumza nami ni kali sana; je, Hataki kuniokoa? Je, Anataka kuniondoa? Ikiwa Anataka kuniondoa, Anapaswa kusema hivyo haraka iwezekanavyo, nikiwa bado mchanga, ili asizuie harakati zangu za ulimwengu.” Hili husababisha uhasi, upinzani, ukinzani, na uzembe ndani yao. Hizi ni baadhi ya hali na dhihirisho zinazohusisha jinsi watu wanavyochukulia matarajio na hatima yao. Huu ni ugumu mkubwa unaohusiana na kuingia katika uzima.

III. Matatizo Yanayohusiana na Mahusiano Kati ya Watu

Hebu tuangalie kipengele kingine—mahusiano kati ya watu. Hili pia ni tatizo kubwa linalohusiana na kuingia katika uzima. Jinsi unavyowatendea watu usiowapenda, watu ambao maoni yao yanatofautiana na yako, watu unaowafahamu, watu walio na uhusiano wa kifamilia na wewe au ambao wamekusaidia, na watu ambao hukupa maonyo ya haraka kila wakati, na kukwambia maneno ya kweli, na kukusaidia, na kama wewe unaweza kumtendea kila mtu kwa haki, pamoja na jinsi unavyotenda migogoro inapotokea na kati yako na watu wengine, pamoja na wivu na migogoro inayotokea miongoni mwenu, na kutoweza kuingiliana kwa usawa, au hata kushirikiana kwa usawa katika mchakato wa kufanya wajibu wako—hizi ni baadhi ya hali na dhihirisho zinazohusiana na mahusiano kati ya watu. Je, kuna zingine? (Kuwa mtu anayewafurahisha watu na kutothubutu kusema anapogundua matatizo ya mtu mwingine, kwa kuogopa kumuudhi.) Hii ni hali inayotokea wakati mtu anaogopa kuwaudhi wengine. (Pia, jinsi mtu anavyowatendea viongozi na wafanyakazi, na wale wenye mamlaka na hadhi.) Jinsi unavyowatendea viongozi na wafanyakazi, au watu wenye mamlaka na hadhi—iwe kwa kusifu mno na kujipendekeza, au kwa kuwatendea ipasavyo—huu ni udhihirisho maalum wa jinsi unavyowatendea wale wenye mamlaka na ushawishi. Haya kwa ujumla ni matatizo ya mahusiano kati ya watu.

IV. Masuala Yanayohusiana na Hisia za Kibinadamu

Hebu tuzungumzie kidogo kuhusu hisia za kibinadamu. Ni masuala yapi yanayohusiana na hisia? Kwanza ni jinsi unavyowatathmini wanafamilia wako, na jinsi unavyoyachukulia mambo wanayofanya. “Mambo wanayofanya” hapa kwa kawaida yanajumuisha wanapovuruga na kusumbua kazi ya kanisa, wanapowahukumu watu bila wao kujua, wanaposhiriki katika baadhi ya matendo ya wasioamini, na kadhalika. Je, unaweza kuyashughulikia mambo haya bila upendeleo? Inapokulazimu uandike tathmini ya wanafamilia wako, je, unaweza kufanya hivyo bila upendeleo na bila kuegemea upande wowote, mkiweka hisia zenu kando? Hii inahusiana na jinsi unavyowachukulia wanafamilia wako. Zaidi ya hayo, je, mna hisia kuelekea wale mnaoelewana nao au waliokusaidia hapo awali? Je, unaweza kuona matendo na mwenendo wao kwa njia isiyo ya upendeleo, isiyoegemea upande wowote, na iliyo sahihi? Ikiwa watavuruga na kuisumbua kazi ya kanisa, je, utaweza kuwaripoti au kuwafichua mara moja baada ya wewe kujua kuhusu jambo hilo? Pia, je, una hisia kuelekea wale walio karibu na wewe kwa ulinganisho, au wanaoshiriki maslahi sawa na wewe? Je, unayo tathmini, ufafanuzi, na njia ya kushughulika na matendo na tabia zao bila upendeleo na bila kuegemea upande wowote? Tuseme kwamba watu hawa, ambao una uhusiano wa kihisia nao, wanashughulikiwa na kanisa kulingana na kanuni, na matokeo ya hili hayalingani na mawazo yako mwenyewe—unawezaje kukabiliana na jambo hili? Je, utaweza kutii? Je, bado utaendelea kuingiliana nao kwa siri, na, je, utapotoshwa nao na hata kuchochewa nao kutoa udhuru kwa ajili yao, kuwahalalishia, na kuwatetea? Je, utawasaidia na kuwatetea wale waliokusaidia, huku ukipuuza kanuni za ukweli na kupuuza maslahi ya nyumba ya Mungu? Je, haya si masuala mbalimbali yanayohusiana na hisia? Baadhi ya watu husema, “Je, hisia hazihusiani na jamaa na wanafamilia pekee? Je, upeo wa hisia si wazazi wako, kaka na dada zako tu, na wanafamilia wengine?” Hapana, hisia zinajumuisha watu wengi. Achia mbali kuwatathmini wanafamilia wao bila upendeleo—baadhi ya watu hawawezi hata kuwatathmini marafiki na wandani wao wa karibu bila upendeleo, na hupotosha ukweli wanapozungumza kuhusu watu hawa. Kwa mfano, ikiwa rafiki yake hashughulikii kazi yake inayofaa na kila mara hujihusisha na matendo yaliyopotoka na maovu katika wajibu wake, atamtaja kama mcheshi sana, na kusema kwamba ubinadamu wake haujakomaa na bado haujatulia. Je, hakuna hisia ndani ya maneno haya? Haya ni maneno yaliyojaa hisia. Mtu ambaye hana uhusiano na yeye asipoghulikia kazi yake inayofaa na ajihusishe na matendo yaliyopotoka na maovu, atakuwa na mambo makali zaidi ya kusema kumhusu mtu huyo, na anaweza hata kumlaani. Je, huu si udhihirisho wa kuzungumza na kutenda kulingana na hisia? Je, watu wanaoishi kulingana na hisia zao hawana upendeleo? Je, ni waadilifu? (Hapana.) Kuna ubaya gani kwa watu wanaozungumza kulingana na hisia zao? Kwa nini hawawezi kuwatendea wengine kwa haki? Kwa nini hawawezi kuzungumza kulingana na kanuni za ukweli? Watu ambao ni wenye ndimi mbili na ambao hawategemezi maneno yao kamwe kwenye ukweli ni waovu. Kutokuwa na upendeleo mtu anapozungumza, kila mara hunena kulingana na hisia zake na kwa ajili yake mwenyewe, na si kulingana na kanuni za ukweli, kutofikiria kazi ya nyumba ya Mungu, na kulinda tu hisia zake binafsi, umaarufu, faida, na hadhi—hii ndiyo tabia ya wapinga Kristo. Hivi ndivyo wapinga Kristo wanavyosema; kila kitu wanachosema ni kiovu, kinasumbua, na kinavuruga. Watu wanaoishi Katikati ya mapendeleo na maslahi ya mwili huishi miongoni mwa hisia zao. Watu wanaoishi kulingana na hisia zao ni wale ambao hawakubali au kutenda ukweli hata kidogo. Wale wanaozungumza na kutenda kulingana na hisia zao hawana uhalisi wa kweli hata kidogo. Ikiwa watu kama hao watakuwa viongozi, bila shaka watakuwa viongozi wa uongo au wapinga Kristo. Si tu kwamba hawawezi kufanya kazi halisi, wanaweza pia kushiriki katika matendo mbalimbali maovu. Hakika wataondolewa na kuadhibiwa.

V. Masuala Yanayohusiana na Kutamani Faraja za Mwili

Kutamani starehe za mwili pia ni suala zito. Je, mnaona baadhi ya dhihirisho za kutamani starehe za mwili ni zipi? Ni mifano gani mnayoweza kutoa kutokana na yale mliyoyaona katika uzoefu wenu wenyewe? Je, kufurahia faida za hadhi kuna umuhimu? (Ndiyo.) Kitu kingine chochote? (Kupendelea kazi rahisi kuliko zile ngumu mnapofanya majukumu yenu, na kutaka kuchagua kazi nyepesi kila wakati.) Wakati wa kufanya wajibu, watu huchagua kazi nyepesi kila wakati, kazi ambayo haichoshi, na hiyo haihusishi kustahimili hali ya anga nje ya nyumba. Huku ni kuchagua kazi rahisi na kuepuka zile ngumu, na ni dhihirisho la kutamani starehe za mwili. Ni kitu kipi kingine? (Daima hulalamika wakati wajibu wao ni mgumu kidogo, unachosha kidogo, unapohusisha kulipa gharama.) (Kujishughulisha na chakula na mavazi, na raha za mwili.) Hizi zote ni dhihirisho za kutamani starehe za mwili. Mtu kama huyo anapoona kwamba kazi ni ngumu sana au ni hatari, huilazimishia mtu mwingine; yeye mwenyewe hufanya kazi ya starehe tu, na hutoa visingizio, akisema kwamba yeye ni mwenye ubora duni wa tabia, kwamba hana uwezo wa kufanya kazi, na hawezi kuichukua kama mzigo wake—ila kwa kweli, ni kwa sababu anatamani starehe za mwili. Hataki kuteseka, bila kujali kazi anavyofanya au wajibu anaofanya. Akiambiwa kwamba mara tu atakapomaliza kazi hiyo kutakuwa na nyama ya nguruwe iliyochomwa ili kula, anafanya haraka na kwa ufanisi, na huwezi kuwa na haja ya kumharakisha, kumsukuma, au kumwaangalia; lakini ikiwa hakuna nyama ya nguruwe iliyochomwa ili yeye aile, na anapaswa kufanya wajibu wake kwa muda wa ziada, anaahirisha mambo, na kutafuta sababu na visingizio vya kila aina vya kuiahirisha, na baada ya kufanya kwa muda, anasema, “Ninahisi kizunguzungu, mguu wangu umekufa ganzi, nimechoka! Kila sehemu ya mwili wangu inauma, naweza kupumzika kwa muda?” Tatizo ni lipi hapa? Anatamani starehe za mwili. Pia kuna wakati ambapo watu hulalamika kila mara kuhusu matatizo wanapotimiza wajibu wao, wakati hawataki kuweka juhudi yoyote, wakati, mara tu wanapopata muda kidogo wa kupumzika, wao hupumzika, hupiga kelele bila kufanya kazi, au kushiriki katika burudani. Na kazi inapoanza na kubadili mwendo na utaratibu wa maisha yao, hawafurahii na hawaridhiki nayo. Wananung’unika na kulalamika, na wanakuwa wazembe katika kutekeleza wajibu wao. Huku ni kutamani starehe za mwili, sivyo? Kwa mfano, ili kudumisha umbo lao, baadhi ya wanawake hufanya mazoezi na kulala usingizi wa kurejesha urembo wao kila siku katika nyakati maalum. Hata hivyo, mara tu kazi inapoanza kuwa na shughuli nyingi na utaratibu huu kuathiriwa, wao hukosa furaha, wakisema, “Hili si jambo zuri; kufanya kazi hii kunachelewesha mambo sana. Siwezi kuiruhusu iathiri mambo yangu binafsi. Sitamjali mtu yeyote anayejaribu kunisukuma; nitafuata mwendo wangu mwenyewe. Wakati wa yoga ukifika, nitafanya yoga. Wakati wa kulala kwa usingizi wa urembo wangu ukifika, nitalala. Nitaendelea kufanya mambo haya kama nilivyofanya hapo awali. Mimi si mjinga na mchapakazi kama nyinyi nyote. Katika miaka michache, nyote mtageuka kuwa wanawake wazee, wenye sura ya kawaida, miili yenu itanyauka, na hamtakuwa wembamba tena. Hakuna atakayetaka kuwaangalia, na hamtakuwa na Imani yoyote maishani.” Kwa ajili ya kuridhisha starehe zao za kimwili, kwa ajili ya uzuri, kupendwa na wengine, na kuishi kwa kujiamini zaidi, wanakataa kuacha raha na mapendeleo ya miili yao, haijalishi wana shughuli nyingi za wajibu wao kiasi. Huku ni kujiingiza katika starehe za mwili. Baadhi yao husema, “Mungu ana wasiwasi, nasi tunapaswa kuzingatia nia za Mungu.” Lakini wanawake hawa husema, “Sijaona kwamba Mungu ana wasiwasi; mimi ni mwema mradi tu nisiwe na wasiwasi. Nikizingatia nia za Mungu, ni nani atakayejali yangu?” Je, wanawake kama hao wana ubinadamu wowote? Je, wao si mashetani? Pia kuna watu fulani ambao, bila kujali jinsi kazi yao ilivyo na shughuli nyingi, hawataruhusu iathiri jinsi wanavyovaa na kile wanachovaa. Wanatumia saa nyingi kila siku kwenye vipodozi, na wanakumbuka vizuri sana kama milango ya nyumba zao ni nguo gani za kuvaa kila siku zinazolingana na jozi fulani za viatu, na wakati wa kufanya matibabu ya urembo na masaji, bila kuchanganyikiwa kuhusu mambo haya hata kidogo. Hata hivyo, linapokuja suala la kiasi gani cha ukweli wanachoelewa, ni ukweli gani ambao bado hawaelewi au hawajaingia katika, ni mambo gani ambayo bado wanashughulikia kwa njia ya uzembe na bila uaminifu, ni tabia gani potovu walizofichua, na masuala mengine yanayohusiana na ukweli unaohusisha kuingia katika uzima, hawajui chochote kuhusu mambo haya hata kidogo. Wanapoulizwa kuyahusu, hawajui chochote kuhusu mambo haya hata kidogo. Wanapoulizwa kuyahusu, hawajui kabisa. Hata hivyo, linapokuja suala la mada zinazohusiana na raha za mwili—kula, kunywa, na burudani—wanaweza kuzungumza bila kikomo, haiwezekani kuwazuia. Haijalishi kazi ya kanisa ina shughuli nyingi kiasi gani au majukumu yao yana shughuli nyingi kiasi gani, utaratibu na hali ya kawaida ya maisha yao haivurugwi kamwe. Hawawi wasiojali kamwe kuhusu mambo madogo madogo ya maisha ya mwili na kuyadhibiti kikamilifu, wakiwa wakali sana na wasiocheka. Lakini, wanapoishughulikia kazi ya nyumba ya Mungu, haijalishi jambo hilo ni kubwa kiasi gani na hata kama linaweza kuhusisha usalama wa akina ndugu, wanalishughulikia kwa uzembe. Hawajali hata kuhusu mambo yanayohusisha agizo la Mungu au wajibu wanaopaswa kufanya. Hawachukui jukumu lolote. Huku ni kujiingiza katika starehe za mwili, au sio? Je, watu wanaojiingiza katika starehe za mwili wanafaa kufanya wajibu? Mara tu mtu anapozungumzia suala la kufanya wajibu wake, au anapozungumzia kulipa gharama na kupitia shida, wanaendelea kutikisa vichwa vyao. Wana matatizo mengi sana, wamejaa malalamiko, na wamejaa uhasi. Watu kama hao hawana maana, hawastahili kufanya wajibu wao, na wanapaswa kuondolewa. Kuhusu kutamani starehe za mwili, tutakomea hapo.

VI. Matatizo Yanayohusiana na Kujijua Mwenyewe

Kujijua mwenyewe ni kipengele muhimu zaidi cha kuingia katika uzima. Lakini kwa watu wengi, kwa sababu hawapendi ukweli au kuufuatilia, kujijua linakuwa ugumu mkubwa kwao. Kwa hivyo, ni hakika kwamba wale wasiopenda ukweli hawawezi kujijua kikweli. Ni vipengele gani vilivyopo katika kujijua? Cha kwanza ni kujua ni tabia gani potovu zinazofichuliwa katika usemi na matendo ya mtu. Wakati mwingine, ni kiburi, wakati mwingine ni udanganyifu, au labda uovu, kutokubadilika, au usaliti, na kadhalika. Zaidi ya hayo, jambo linapompata mtu, anapaswa kujichunguza ili kuona kama ana nia au matilaba yoyote ambayo hayalingani na ukweli. Anapaswa pia kuchunguza kama kuna kitu chochote katika usemi au matendo yake kinachompinga au kumwasi Mungu. Hasa, anapaswa kuchunguza kama ana hisia ya kubeba mzigo na ni mwaminifu linapokuja suala la wajibu wake, kama anajitumia kwa dhati kwa ajili ya Mungu, na kama ni shughuli za muamala au za kijuujuu. Kujijua pia kunamaanisha kujua kama mtu ana dhana na mawazo, madai ya kupita kiasi, au suitafahamu na malalamiko kumhusu Mungu, na kama mtu ana akili ya kutii. Kunamaanisha kujua kama mtu anaweza kutafuta ukweli, kukubali kutoka kwa Mungu na kuwa na moyo wa kumtii Mungu anapokabili hali, watu, matukio, na mambo ambayo Anapanga. Kunamaanisha kujua kama mtu ana dhamiri na akili na kama mtu ni mpenda ukweli. Kunamaanisha kujua kama mtu anatii au anajaribu kubishana anapokumbana na mambo, na kama mtu hutegemea dhana na mawazo au kutafuta ukweli katika mtazamo wake kwa mambo haya. Haya yote ni mawanda ya kujijua. Mtu anapaswa kutafakari kama anapenda ukweli na ana imani ya kweli kwa Mungu kulingana na mtazamo wake kuelekea hali na watu, matukio, na mambo mambalimbali. Ikiwa mtu anaweza kujua tabia yake potovu na kuona jinsi uasi wake ulivyo mkubwa dhidi ya Mungu, basi atakuwa amekua. Zaidi ya hayo, linapokuja suala la mambo yanayohusisha jinsi anavyomtendea Mungu, mtu anapaswa kutafakari kama ana dhana, hofu, au utii katika jinsi anavyolitendea jina la Mungu na mwili Wake, na hasa mtazamo wake kuhusu ukweli ukoje. Mtu anapaswa pia kujua mapungufu yake, kimo chake, na kama ana ukweli halisi, na pia kama harakati zake na njia anayotembea ni sahihi na inalingana na nia za Mungu. Haya yote ni mambo ambayo watu wanapaswa kujua. Kwa muhtasari, vipengele mbalimbali vya kujijua binafsi kimsingi vinajumuisha yafuatayo: ufahamu wa kama ubora wa tabia ya mtu ni wa juu au wa chini, ufahamu wa tabia yake, ufahamu wa nia na matilaba ambayo mtu anayo katika matendo yake, ufahamu wa tabia potovu na kiini cha asili ambacho mtu hufichua, ufahamu wa mapendeleo na harakati zake, ufahamu wa njia anayotembea, ufahamu wa mitazamo yake kuhusu mambo, ufahamu wa mtazamo wake kuhusu maisha na maadili, na ufahamu wa mtazamo wake kwa Mungu na ukweli. Kujijua binafsi kunajumuisha vipengele hivi.

VII. Maonyesho Mbalimbali ya Watu katika Jinsi Wanavyomtendea Mungu

Sehemu inayofuata ya maudhui kuhusu kuingia katika uzima inahusu udhihirisho mbalimbali wa watu katika jinsi wanavyomtendea Mungu. Kwa mfano, kuna kuwa na mawazo kuhusu Mungu, kukuza suitafahamu kumhusu na kujichunga dhidi yake, kutoa madai yasiyo na msingi kwake, kutaka kumkwepa kila wakati, kutopenda maneno Anayosema, na kutafuta kumchunguza kila mara. Pia kuna kutoweza kuona au kutambua uweza wa Mungu, na pia kuwa na mtazamo wa shaka kuhusu ukuu, mipango, na mamlaka ya Mungu, na kukosa maarifa kabisa ya mambo haya. Zaidi ya hayo, si tu kushindwa kuepuka au kukataa kashfa na kufuru ambayo wasioamini na ulimwengu huleta dhidi ya Mungu, lakini kinyume chake, kutaka kuuliza kama ni kweli au ukweli. Je, huku si kumtilia shaka Mungu? Mbali na udhihirisho huu, kuna mengine yapi? (Kumtilia Mungu shaka na kumjaribu Mungu.) (Kujaribu kujipendekeza kwa Mungu.) (Kutotaka kukubali uchunguzi wa Mungu.) Kuna kutotaka kukubali uchunguzi wa Mungu huku wakati huo huo ukitilia shaka kwamba Mungu anaweza kuchunguza mioyo ya ndani ya watu. (Pia kuna kumpinga Mungu.) Huu pia ni udhihirisho—kumpinga Mungu na kumpigia kelele. Kuna kutumia mtazamo wa kutweza na dharau katika kumtendea Mungu, kuzungumza na Yeye na kushirikiana na Yeye. Kuna kitu kingine chochote? (Kutomfanyia Mungu mambo kwa dhati na kumdanganya.) (Kulalamika kuhusu Mungu.) Pia kuna kutotii au kutafuta ukweli kamwe unapokabiliwa na matatizo, na kila mara kubishana kwa niaba yako mwenyewe na kulalamika. (Pia kuna kutoa hukumu na kumkufuru Mungu.) (Kushindana na Mungu kwa ajili ya hadhi.) (Kubishana na kumnyonya Mungu.) (Kumkana Mungu, kumkataa Mungu, na kumsaliti Mungu.) Haya yote ni masuala muhimu; ni hali mbalimbali na tabia potovu zinazojitokeza katika jinsi watu wanavyomtendea Mungu. Kimsingi, huu ndio udhihirisho mbalimbali wa jinsi watu wanavyomtendea Mungu.

VIII. Mitazamo na Udhihirisho Mbalimbali ya Watu katika Utendeaji Wao wa Ukweli

Kipengele kingine cha maudhui kuhusu kuingia katika uzima ni jinsi watu wanavyouchukulia ukweli. Kuna dhihirisho gani katika kipengele hiki? Kuna kuuchukulia ukweli kama nadharia au kauli mbiu, kama kanuni, au kama mtaji wa kuishi kwa kutulitegemea kanisa na kufurahia faida za hadhi. Tafadhali ongeza juu ya hili. (Kuuchukulia ukweli kama riziki ya kiroho.) Kuna kuuchukulia ukweli kama riziki ya kiroho ili kukidhi mahitaji ya mtu ya kiroho. (Kutokubali ukweli na kuuchukia.) Huu ni mtazamo kuelekea ukweli. (Kufikiri kwamba maneno ya Mungu yanalenga kuwafichua wengine, kwamba hayahusiani na mtu binafsi, na kujiona kama bwana wa ukweli.) Umeelezea dhihirisho hili ipasavyo. Watu wenye dhihirisho hili wanaamini kwamba wanaelewa ukweli wote unaonenwa na Mungu, na kwamba tabia na kiini potovu cha mwanadamu ambacho Yeye hufichua kinarejelea wengine, na si wao. Wanajiona kama mabwana wa ukweli, mara nyingi wakitumia maneno ya Mungu kuwafundisha wengine, kana kwamba wao wenyewe hawana tabia potovu, wanajiona tayari wao ni mfano halisi wa ukweli na wasemaji wa ukweli. Wao ni takataka ya aina gani? Wanataka kuwa mfano halisi wa ukweli—je, wao si kama Paulo tu? Paulo alikana kwamba Bwana Yesu hakuwa Kristo na Mungu; yeye mwenyewe alitaka kuwa Kristo na Mwana wa Mungu. Watu hawa ni kama Paulo, wao ni wa aina moja na yeye, wao ni wapinga Kristo. Kuna kitu kingine? (Kuyachukulia maneno ya Mungu kama yale ya mtu wa kawaida, si kama ukweli unaopaswa kutekelezwa, na kuwa na mtazamo wa kupuuza na wa juu juu tu kuelekea maneno ya Mungu.) Kutoyachukulia maneno ya Mungu kama ukweli unaopaswa kukubaliwa na kutekelezwa, lakini kuyachukulia kama maneno ya kibinadamu—hili ni jambo moja. (Kuyahusisha maneno ya Mungu na falsafa na nadharia za wasioamini.) Kuna kuyahusisha maneno ya Mungu na falsafa, kuyachukulia maneno ya Mungu kama mapambo au maneno matupu huku ukizingatia misemo inayojulikana ya watu maarufu na wakubwa kama ukweli, na kuyachukulia maarifa, desturi za kitamaduni, na mila kama ukweli na kuyabadilisha maneno ya Mungu na mambo hayo. Watu wanaoonyesha udhihirisho huu huzungumza bila kukoma kuhusu kutaka kutenda ukweli na kushuhudia na kueneza maneno ya Mungu wanapokabiliwa na hali mbalimbali, lakini mioyoni mwao, huwapenda watu hao maarufu na wakubwa kutoka katika ulimwengu wa kidunia, na hata humsifu Bao Gong wa Nasaba ya Song ya kale, wakisema, “Kwa kweli alikuwa mwamuzi mkali na asiyependelea upande wowote. Hakuwahi kutoa uamuzi usio wa haki, hakukuwahi kutokea upotoshaji wowote wa haki kwa mujibu wake, au roho zozote zilizodhulumiwa na upanga wake wa uuaji kisheria!” Je, huku si kumsifu na kumstahi mtu maarufu na mwenye hekima? Kujaribu kuyachukulia kimakosa matendo ya watu maarufu kama ukweli ni kukashifu na kuukufuru ukweli! Kanisani, watu kama hawa huzungumza sana kuhusu kutaka kutenda ukweli na kueneza maneno ya Mungu, lakini wanachofikiria akilini mwao na wanachosema kwa kawaida ni misemo na methali za kitamaduni tu, ambazo wao huonyesh kwa njia waliyoifanyia mazoezi na kwa ufasaha. Mambo haya huwa midomoni mwao na hutoka kwa urahisi kutoka kwenye ndimi zao. Hawajawahi kusema neno lolote kuhusu uelewa wao wa uzoefu wa maneno ya Mungu, na bado hawajasema ni lipi kati ya maneno ya Mungu ambalo ni kigezo au msingi wa matendo na mwenendo wao. Wanachosema ni makosa tu, kama vile, “Mtu huacha jina lake nyuma popote akaapo, kama vile bata bukini hujitangaza popote arukapo,” “Uuaji kisheria hufanya vichwa vibiringie,” “Daima kuna kitu cha kudharauliwa kuhusu watu wenye kusikitisha,” “Daima jiachie nafasi ya kugaagaa,” “Hata kama sijapata mafanikio yoyote, nimevumilia magumu; kama si magumu, basi uchovu,” “Usivunje daraja baada ya kuvuka mto; usimwue punda baada ya kushusha mzigo,” “Mwadhibu mtu vikali ili awe mfano kwa wengine, mfanye awe onyo kwa wengine,” na “Maafisa wapya wana hamu ya kuvutia,” miongoni mwa mengine—hakuna hata moja kati ya yale wanayosema ambayo ni kweli. Baadhi ya watu wanakariri maneno ya washairi wa kisasa na hata kuyachapisha katika sehemu ya maoni ya video za nyumba ya Mungu. Je, hili si dhihirisho la ukosefu wa uelewa wa kiroho? Je, maneno hayo ni kweli? Je, yanahusiana na ukweli? Baadhi ya watu mara nyingi husema mambo kama “Kuna mungu futi tatu juu yako,” na “Mema na maovu yatalipwa mwishowe; ni suala la muda tu.” Je, kauli hizi ni kweli? (Hapana.) Zinatoka wapi? Je, zinapatikana katika maneno ya Mungu? Zinatoka katika utamaduni wa Kibuddha na hazina uhusiano wowote na kumwamini Mungu. Licha ya haya, watu mara nyingi hujaribu kuwavuta hadi kiwango cha ukweli; hili ni dhihirisho la ukosefu wa uelewa wa kiroho. Baadhi ya watu wana azimio kidogo la kujitoa kwa ajili ya Mungu, na wanasema, “Nyumba ya Mungu imenistawisha, Mungu ameniinua, kwa hivyo lazima niishi kulingana na msemo, ‘Muungwana atajitolea maisha yake kwa ajili ya wale wanaomwelewa.’ “Wewe si muungwana, na Mungu hajakwambua uyatoe maisha yako. Je, ni muhimu kuwa na ujasiri wa hali ya juu unapofanya wajibu? Huwezi hata kutimiza wajibu wako sasa ukiwa uko hai, je, kuna tumaini lolote la wewe kufanya hivyo katika kifo? Utafanyaje wajibu wako basi? Wengine husema, “Mimi ni mwaminifu kiasili, mimi ni mtu jasiri na mwenye shauku. Ninapenda kujitolea kitu kwa ajili ya marafiki zangu. Ni vile vile na Mungu: Kwa kuwa Mungu amenichagua, amenistawisha, na kuniinua, lazima niilipe neema ya Mungu. Hakika nitajitolea kila kitu kwa ajili ya Mungu, hata mpaka kifo changu!” Je, huu ni ukweli? (Hapana.) Mungu amenena maneno mengi sana, kwa nini hawajakumbuka hata moja kati ya hayo? Wakati wote, wanachoshiriki ni: “Hakuna haja ya kusema kitu kingine chochote. Muungwana atajitolea maisha yake kwa ajili ya wale wanaomwelewa, na mtu lazima ajitolee kila kitu kwa ajili ya marafiki zake na kuwa mwaminifu.” Hawawezi hata kutamka msemo “kulipa upendo wa Mungu.” Baada ya kusikiliza mahubiri na kusoma maneno ya Mungu kwa miaka mingi, hawajui ukweli hata mmoja, na hawawezi hata kusema maneno machache ya kiroho—huu ndio uelewa wao wa ndani na ufafanuzi wa ukweli. Hebu Niambie, je, hili si jambo la kusikitisha? Je, si la kuchekesha? Je, hili si dhihirisho la ukosefu wa uelewa wa kiroho? Baada ya kusikiliza mahubiri mengi, hawaelewi ukweli na hawajui ukweli ni nini, lakini wanayatumia maneno hayo ya kishetani, ya dhihaka, ya kipuuzi, na ya kuchekesha sana kwa ushupavu kuchukua nafasi ya ukweli. Mbali na mawazo na ufahamu wao wa ndani kuwa namba hii, pia wao hueneza na kuwafundisha wengine hili kila mara, na kuwafanya wengine wawe na uelewa sawa na wao. Je, hili halibebi ndani yake kwa kiasi fulani asili ya kusababisha vurugu na usumbufu? Inaonekana kwamba watu hawa ambao hawaelewi ukweli na hawana uelewa wa kiroho ni hatari, wana uwezo wa kusababisha vurugu na usumbufu na kufanya mambo ya dhihaka na ya kipuuzi wakati wowote na mahali popote. Udhihirisho mwingine wa jinsi watu wanavyouchukulia ukweli ni upi? (Kudharau ukweli, kukubali tu kile kinacholingana na mawazo yako mwenyewe, na kukana na kukataa kufanya kile kisicholingana.) Kukubali na kufanya tu kile kinacholingana na mawazo yako mwenyewe na kupinga na kulaani kwa usawa kile kisicholingana—huu ni mtazamo. (Kutoamini kwamba ukweli unaweza kutatua tabia potovu za mtu au kumbadilisha.) Kutokukubali au kuamini ukweli pia ni mtazamo. Udhihirisho mwingine ni kwamba mwelekeo na mtazamo wa mtu kuelekea ukweli hubadilika kulingana na hisia, mazingira, na mhemko wake. Kwa watu hawa, wanapohisi vizuri na wakiwa na furaha siku moja, wanawaza, “Ukweli ni bora! Ukweli ni uhalisi wa mambo yote chanya, jambo linalostahili zaidi kwa wanadamu kutenda na kueneza.” Wakati hisia zao ni mbaya, wao huwaza, “Ukweli ni nini? Kuna manufaa gani ya kutenda ukweli? Je, unaweza kukupatia pesa? Ukweli unaweza kubadili nini? Ni nini kinachoweza kutokea ukitenda ukweli? Sitautenda—unaleta tofauti gani?” Asili yao ya kishetani hujitokeza. Udhihirisho huu ni tabia na hali mbalimbali ambazo watu hufichua jinsi wanavyoutendea ukweli. Ni udhihirisho gani mwingine maalum? (Kutoyachukulia maneno ya Mungu kama ukweli au uzima bali kuyachambua na kuyachunguza.) Kuna kuyachukulia maneno ya Mungu kwa mtazamo wa kitaaluma, kila mara ukichambua na kuuchunguza ukweli kulingana na ujuzi wa mtu, bila mtazamo wowote wa kukubali na kutii. Haya ndiyo matatizo ya jinsi watu wanavyouchukulia ukweli ambayo yanaweza kufafanuliwa na kufanywa kuwa vichwa vya muhtasari.

Kuna vipengele nane kwa jumla katika maudhui yetu kuhusu ugumu wa kuingia katika uzima, na hivyo ndivyo vipengele vikuu vinavyohusiana na kuingia katika uzima na kufikia wokovu. Hali na tabia zinazofunuliwa na watu ndani ya vipengele hivi nane zote zimefichuliwa katika maneno ya Mungu; Mungu ameweka mahitaji kwa watu na kuwaonyesha njia ya kutenda. Watu wakiweza kuweka juhudi katika maneno ya Mungu, wachukue mtazamo wa uzito, mtazamo wa kutamani, na kubeba mzigo kwa ajili ya kuingia katika uzima wao wenyewe, basi ndani maneno ya Mungu, wanaweza kupata ukweli unaofaa ili kutatua aina hizi nane za matatizo, na kuna njia za kutenda kwa kila mojawapo. Hakuna hata kimoja kati ya hivyo ambacho ni changamoto zisizoweza kutatuliwa au ni fumbo la aina yoyote. Hata hivyo, ikiwa hubebi mzigo wowote kwa ajili ya kuingia katika uzima wako mwenyewe, na hupendelei ukweli hata kidogo au kubadilisha tabia yako, basi haijalishi maneno ya Mungu yalivyo wazi na sahihi kiasi gani, yatabaki kuwa maandishi na mafundisho tu kwako (maandiko na mafundisho yako). Usipofuatilia na kutenda ukweli, basi haijalishi una matatizo gani, hutaweza kupata suluhisho, jambo ambalo litafanya iwe vigumu sana kwako kupata wokovu. Labda utabaki milele katika hatua ya kuwa mfanyakazi; labda utabaki milele katika hatua ya kutoweza kupata wokovu na kukataliwa na kuondolewa na Mungu.

Athari na Matokeo Mabaya ya Kazi ya Viongozi wa Uongo

Linapokuja suala la matatizo yote ambayo watu hukumbana nayo katika kuingia kwao uzimani, viongozi wa uongo hufanya nini? Watu wanapokabiliwa na aina yoyote ya hali inayoangukia ndani ya mojawapo ya aina hizi nane za matatizo, je, viongozi wa uongo wanaweza kutambua hili, na kutumia maneno ya Mungu na ujuzi wao wenyewe wa uzoefu kutatua matatizo ya watu hawa? Kwa bahati mbaya, watu wanapokumbana na matatizo, viongozi hawa wa uongo hushiriki tu katika juhudi za juu juu, wakitoa tu baadhi ya maneno yasiyo na maana, yanayolenga nje, na yasiyo na umuhimu ambayo hayana uhusiano wowote na tabia zao na matatizo halisi, ili kushughulikia masuala yao. Kwa mfano, viongozi wa uongo mara nyingi husema, “We hupendi tu ukweli!” Hivi ndivyo wanavyojaribu kutatua matatizo halisi ya watu na kuainisha kiini chao. Hawawezi kuwasaidia watu kupata majibu katika maneno ya Mungu hata kwa suala au hali ndogo, wala hawawezi kulitatua kwa kushiriki katika ukweli. Badala yake, wanatoa baadhi ya maneno ya mafundisho na yasiyohusiana, au wanalifanya tatizo dogo liwe kubwa sana ili kuwapuuzilia watu mbali kabisa bila kuwapa fursa ya kutubu. Kwa kweli, ikiwa mtu ana uwezo wa kuelewa maneno ya Mungu na ana uelewa wa kiroho, ataweza kupata ufichuzi wa Mungu wa vipengele hivi nane vya hali kutoka katika maneno Yake, si vigumu. Hata hivyo, kwa sababu viongozi wa uongo hawana uelewa wa kiroho, wana ubora duni wa tabia, na hawana uwezo wa kuelewa, pamoja na ukweli kwamba baadhi yao wana shauku tu, wana hamu ya kutenda, ni wanafiki, na wanajifanya kama watu wa kiroho, hawawezi kutatua masuala ya watu wengine hata kidogo. Linapokuja suala la masuala mbalimbali ambayo watu hukumbana nayo, viongozi wa uongo watawashauri, wakisema, “Kazi ya Mungu imeendelea hadi hapa; kwa nini wewe bado una wivu na kubishana na wengine? Je, una muda wa kufanya hivyo? Kuna faida gani ya kupigana juu ya hilo? Huwezi kuendelea bila kupigana juu yake?” “Kazi ya Mungu imefika hapa, lakini bado una hisia nyingi, na huwezi kuachilia. Hivi karibuni, hisia hizi zitakuangamiza!” “Kazi ya Mungu imefikia hapa, kwa nini bado unajali chakula na mavazi? Huwezi kuishi bila kuvaa gauni moja? Huwezi kuishi bila kununua viatu vya ngozi? Unapaswa kuwaza zaidi kuhusu maneno ya Mungu na wajibu wako!” “Jambo linapokupata, mwombe Mungu zaidi. Bila kujali kinachokupata, kuna funzo moja: kujifunza kumtii Mungu na kuelewa mamlaka na mpangilio Wake.” Je, ushauri huu unaweza kutatua matatizo halisi? Hauwezi hata kidogo. Vinginevyo wanasema, “Watu wamepotoshwa sana na Shetani. Kwa kuwa na hisia, je, humuasi Mungu? Kwa kutojijua, je, humuasi Mungu?” Bila kujali tatizo lililopo, viongozi wa uongo hawajui jinsi ya kushiriki ukweli ili kuchanganua kiini au hali ya mtu, hawawezi kuona jinsi hali za watu zinavyotokea, na kisha, kulingana na hali zao, washiriki ukweli ili kutatua masuala yao, watoe msaada na riziki inayofaa. Badala yake, wao kila wakati husema mambo yaleyale: “Mpende Mungu! Fanya kazi kwa bidii katika kufanya wajibu wako, lazima uwe mwaminifu kwa Mungu, na uombe zaidi unapokumbana na matatizo!” “Kila kitu kiko ndani ya mamlaka na mpangilio wa Mungu. Kila kitu kiko mikononi mwa Mungu!” “Usipotafuta ukweli, hilo halitafaa. Lazima usome maneno ya Mungu zaidi. Maneno ya Mungu yanaweka kila kitu wazi, lakini watu hawapendi ukweli!” “Majanga yamekaribia, matokeo ya kila kitu yamekaribia, na kazi ya Mungu inakaribia mwisho, lakini wewe huna wasiwasi. Je, mwanadamu ana siku ngapi zilizosalia? Ufalme wa Mungu umefika!” Viongozi wa uongo hutamka tu misemo hii isiyolenga jambo lolote muhimu, hawachambui na kuchanganua matatizo mbalimbali mahususi, au kutoa huduma halisi au usaidizi kwa watu. Wanawatafutia watu vifungu kadhaa kutoka katika maneno ya Mungu vya kusoma, au wanatoa ushauri usiofaa ili kuwashughulikia. Ni kitu gani kinachotokea mwishoni? Katika madhara ya viongozi wa uongo, kando na watu kutojua tabia zao potovu, wao pia hawajui tabia zao ni za aina gani, hawajui wao ni watu wa aina gani, na kiini cha asili waliyo nayo; hawajui ubora wao wa tabia ukoje, hawajui kama wana uwezo wa kuelewa au la, au wako kwenye njia gani. Bado wanashikilia vitu vya kidunia na vya mtindo wanavyopenda na kuvithamini mioyoni mwao, na hakuna mtu anayewasaidia kuelewa, kuchanganua, na kuchambua mambo haya. Haya ni matokeo ya kazi ya viongozi wa uongo. Matatizo yanapotokea, wao huwakaripia watu, wakiwashutumu kiholela na kuwashtaki kimakosa, au huwapa watu ushauri na masomo mengi, au wao hutumia maneno ya Mungu kufanya ulinganisho wa kulazimishwa na usio sahihi. Wale wanaowasikia huwaza, “Ninahisi ni kama ninaelewa, lakini pia kama sielewi—ni kama niliweza kuelewa walichosema, lakini pia huenda sikuelewa. Mbona hili liko hivyo? Kila kitu ambacho kiongozi anasema ni sahihi, lakini kwa nini siwezi kuondoa suala hili moyoni mwangu? Kwa nini siwezi kupata suluhisho la ugumu huu? Kwa nini bado nafikiri namna hii na kutaka kufanya mambo haya? Kwa nini siwezi kuelewa kiini na msingi wa suala hilo uko wapi? Kiongozi anasema kwamba sipendi ukweli, na ninakubali kwamba sipendi, lakini kwa nini siwezi kutoka katika hali hii?” Je, viongozi hawa wamekuwa na matokeo yoyote? Ingawa wamezungumza na kufanya kazi, yote ni mkanganyiko mkubwa, na haujawa na athari kama inavyopaswa kuwa. Hawajawawezesha watu kuelewa nia za Mungu, kujilinganisha na maneno ya Mungu, kuelewa kwa usahihi hali zao, au kutatua matatizo yao wenyewe. Kuhusu wale watu wasiorudika, wasio na haya ambao hawakubali ukweli hata kidogo, wanapowasikia viongozi hawa wakiwaonya kwa bidii na kwa uvumilivu, wanahisi wamekata tamaa sana. Wakati huo huo, wanarudia maneno ambayo viongozi hawa husema—baada ya viongozi kumaliza sehemu ya kwanza, watu hawa wanaweza kuendelea na ile inayofuata, na wakose Subira haraka, wakisema, “Msiendelee. Tayari nimeelewa kila kitu mnachosema. Mkiendelea, nitahisi kichefuchefu na kutaka kutapika!” Viongozi wanaendelea kusema, “Wewe hupendi ukweli. Kama ungependa ukweli, ungeelewa kila kitu ninachosema.” Wao hujibu kwa ukali, “Haijalishi kama ninapenda ukweli au la, umerudia maneno haya mara nyingi, hakuna kitu kipya ndani yake, na nimechoka kuyasikia!” Viongozi wa uongo hufanya kazi kwa njia hii, wakishikilia kanuni kwa ukali na kuzingatia misemo fulani, wakishindwa kabisa kutatua matatizo halisi ya watu. Mtu akiwa na mawazo kuhusu Mungu, viongozi wa uongo husema mtu huyo hajijui. Mtu akiwa na ubinadamu duni, asiyeweza kuelewana na watu, na asiye na mahusiano ya kawaida kati ya watu, viongozi wa uongo husema kwamba yeye na mtu mwingine anayehusika wana makosa, wakiwahutubia wote wawili, wakiwalaumu wote wawili, wakisema, “Sawa, nyinyi wawili mko sawa sasa. Tunahitaji kuwa wenye haki na wenye busara katika matendo yetu, tukimtendea kila mmoja sawa bila upendeleo wowote. Yeyote anayesema kwa busara anapenda ukweli, huku wale wanaosema bila ukweli wanapaswa kunyamaza, wazungumze kidogo na kufanya zaidi katika siku zijazo. Yeyote anayesema kitu sahihi anapaswa kusikilizwa zaidi.” Je, huku ni kutatua tatizo? Je, huku ni kufanya kazi? Je, huku si kama kuwatuliza watoto na kuwadanganya watu? Viongozi wa uongo wanaweza kuonekana kama walio na shughuli nyingi, lakini hawawezi kutatua matatizo ya mtu yeyote. Je, kazi yao ina ufanisi kiasi gani? Haina thamani na ni upuuzi! Haya ni matendo ya wasioamini.

Katika uzoefu wa watu katika kumwamini Mungu, mara nyingi hukumbana na matatizo fulani, na viongozi wa uongo hawawezi kuyatatua yoyote kati ya hayo. Viongozi wa uongo hawawezi hata kutatua matatizo fulani dhahiri ambayo yanaweza kutatuliwa kwa maneno machache tu, na pia huyafanyia mzaha mkubwa na kugeuza kila suala dogo kuwa jambo kubwa. Watu wengine si waovu, ni kwamba tu katika ubinadamu wao, wanakosa adabu kidogo, hawaelewi adabu ya msingi, na ni wabaya kidogo. Viongozi wa uongo huchukua masuala haya madogo na kuyafanyia mzaha mkubwa, wakiwafanya akina ndugu wayajadili, wayakosoe, na kuyalaani, yote kwa lengo la kuacha taswira ya kudumu kwa watu hao, ili wasithubutu kuendelea kutenda hivyo. Je, hili ni jambo muhimu? Je, hii ni njia ya kutatua matatizo? Je, huku ni kutumia ukweli kutatua masuala? (Hapana.) Mradi tu hakuna masuala makubwa katika ubinadamu wa mtu, na mtu huyo si mwovu na anaweza kujitumia kwa dhati, basi, katika hali ambapo anakubali, inatosha kuendelea kufanya kazi juu yake, kumpa kumbusho, msaada, ushirika, na usaidizi. Watu wakiendelea kutenda hivi kwa uthabiti, basi wana tatizo katika tabia zao au tabia mbovu sana, na hivyo upogoaji na kutiwa adabu kwa ukali ni lazima. Wakikataa kukubali hili, basi wajibu wao usitishwe, au wanapaswa kuondolewa. Viongozi wa uongo hawawezi kunga’mua hili, wala hawatatenda hivi; wanapokutana na watu waovu kama hao, wanawatendea kama ndugu, wakiwapa msaada na usaidizi. Je, huku ni kufanya kazi? Je, ni kutumia ukweli kutatua masuala? (Hapana.) Kazi ya viongozi wa uongo ni ya kipuuzi, ya kitoto, na ya kuchekesha, na hakuna chochote ndani yake kinacholingana na nia za Mungu. Katika kila kitu wanachofanya, unaweza kuona kwamba wao ni watu wa kawaida, hawana uelewa wa kiroho, na hutenda kwa njia ya kutojali na bila kanuni. Vile vile, hawawezi kung’amua au kuelewa kwa usahihi matatizo mbalimbali ambayo watu hukumbana nayo katika kuingia kwao uzimani. Kwa hivyo, majaribio yao ya utatuzi yanaonekana kuwa ya kijinga, ya kipumbavu, na kama yale ya mtu wa kawaida. Wale wanaokubali msaada wao pia huhisi wasiwasi na waliozimwa. Baada ya muda, baadhi yao hata hupoteza imani, wakisema, “Kiongozi amefanya ushirika nami mara nyingi, kwa nini sijabadilika? Kwa nini ninaendelea kurudia hali hiyo? Je, ni kweli kwamba ubinadamu wangu ni duni sana, na siwezi kuokolewa?” Baadhi hata wana mashaka, wakisema, “Je, kuna tatizo katika roho yangu? Je, roho wabaya wanafanya kazi ndani yangu? Je, Mungu hataniokoa? Je, hiyo haimaanishi kwamba sina tumaini?” Haya ndiyo matokeo ya kazi ya viongozi wa uongo. Katika kazi yao, wanachanganya jambo moja na jingine, na wanatenda kwa njia ya dhihaka, ya kipuuzi, ya kijinga, na ya kipumbavu, ambayo hatimaye husababisha kutotatuliwa kwa haraka kwa matatizo mbalimbali yanayowakabili baadhi ya watu ambao kwa kweli hufuatilia ukweli. Kama matokeo, hili husababisha ubaya na udhaifu kutokea ndani ya watu hao, pamoja na dhana fulani na suitafahamu kuhusu Mungu na kazi Yake. Wao husema, “Nimesoma maneno mengi ya Mungu, kwa nini tatizo langu haliwezi kutatuliwa? Je, maneno ya Mungu yanaweza kuwaokoa na kuwabadilisha watu kweli?” Mioyo yao husababisha shaka, na wananaswa katika mkanganyiko. Kwa hivyo, viongozi wa uongo wanapofanya kazi, hawazalishi matokeo mengi chanya, lakini wao husababisha mambo mengi hasi. Mbali na kazi yao kushindwa kuondoa mawazo, mashaka, na hukumu za watu kuhusu Mungu, pia hiyo huongeza suitafahamu yao na kujihadhari kwao na Mungu. Hata baada ya miaka mingi ya imani, masuala ya watu hawa bado hayajatatuliwa. Huku wakipotoshwa na kuelekezwa vibaya na viongozi wa uongo, suitafahamu yao na kujihadhari kwao na Mungu huongezeka. Kwa hivyo, je, wanaweza kupata kuingia katika uzima?

Ufahamu wa viongozi wa uongo kuhusu mambo chanya kama vile ukweli na mabadiliko ya tabia ya mwanadamu unaweza kushawishi maoni na mitazamo ya watu wengi kuhusu mambo chanya. Ni jambo moja viongozi wa uongo wasipofanya kazi yoyote—mara tu wanapoanza kufanya kazi, mkengeuko hujitokeza na matokeo mabaya hutokea. Mazingira yasiyofaa hutokea katika makanisa haya, yaani, baadhi ya misemo potovu na ya kipuuzi mara nyingi huzalishwa, na watu hapo hawaelewi maneno ya kiroho ambayo hutajwa mara nyingi katika maneno ya Mungu au kujua jinsi ya kuyatumia, huku maneno yanayoitwa maneno ya kiroho na misemo ambayo mara nyingi huzungumzwa na viongozi hawa wa uongo yakienea sana katika makanisa haya. Athari ya mambo haya kwa watu si ndogo: Mbali na kutowasaidia watu kupata maarifa ya vitendo na sahihi zaidi ya maneno ya Mungu na ukweli, au kuwawezesha kupata njia sahihi ya utendaji katika maneno Yake, kinyume chake, kwa kweli yanawafanya watu wawe na maarifa yaliyopotoka zaidi, ya kinadharia, na ya mafundisho kuhusu ukweli, na wakati huo huo, yanawafanya watu wasiwe na ufahamu wa wazi kuhusu njia ya utendaji. Kwa kufanya hivyo, viongozi wa uongo huingilia mtazamo wa watu na kuathiri uelewa wao safi wa ukweli. Viongozi wa uongo wana athari gani katika kufanya mambo haya? Wao hufanya jukumu gani? Ingawa kuwaainisha kama wavurugaji na wasumbufu kunaweza kuwa kupita kiasi, kuwaita wapumbavu wanaozunguka huku na kule si kuzidisha hata kidogo. Nilipokuwa Nimeanza tu hatua hii ya kazi, Nilikutana na baadhi ya watu, na Nilipokuwa nikiwasikiliza wakizungumza, mmoja wao aliuliza kuhusu hali ya mtu, na mtu ghafla akamaka maneno, “Ameungua hadi kuwa majivu.” Nilipouliza, “Ameungua hadi kuwa majivu? Hiyo ina maana gani?” Alijibu, “Kuungua hadi kuwa majivu kunamaanisha kwamba mtu ametimuliwa na labda ameacha kuamini.” Nikasema, “Hii kauli ni katili sana—haimpi mtu huyo uhuru wowote. Je, Nimewahi kusema jambo kama hilo? Sikujuaje kuhusu neno hili? Sijawahi kumuainisha mtu yeyote hivi, au kusema kwamba mtu akiacha kufanya wajibu wake au kumwacha Mungu, ‘anaungua hadi kuwa majivu.’ Kauli hii itatokeaje?” Baadaye, Niligundua kwamba kifungu hiki kilitoka kwa muumini mzee, mzee wa kushikilia sana elimu ya vitabu. Alikuwa msomi sana, alikuwa amemwamini Mungu kwa muda mrefu, na alikuwa na cheo. Aliponena kifungu hiki, kundi hilo la watu waliochanganyikiwa halikutumia utambuzi na kujifunza kutoka kwake, na kikawa kifungu maarufu. Je, mnafikiri kifungu hiki ni sahihi? Je, kina msingi? Je, ni sahihi? (Hapana, si sahihi.) Tunapaswa kukichukuliaje? Je, kinapaswa kuruhusiwa kuendelea kanisani? (Hapana, hakipaswi.) Kinapaswa kufichuliwa na kukosolewa, na kutatuliwa kutoka kwenye msingi wake. Baadaye, kupitia ukosoaji na uchanganuzi, watu hawa waliochanganyikiwa hawakuthubutu kuendelea kukisema, lakini watu wachache wasio na taarifa bado wanaweza kuwa wanakitumia kwa siri faraghani. Watu hao wanaweza kudhani kwamba ni kifungu cha kiroho sana kinachotokana na “mtu anayejulikana sana” na kuamini kinapaswa kuendelea kutumika. Je, viongozi wenu wamejihusisha na vitendo kama hivyo? Je, wameathiri vibaya kuingia kwenu katika uzima, mabadiliko ya tabia, au njia ambayo ninyi mnaitembea? (Zamani, alipokuwa akihubiri injili, kiongozi wa uongo aliwahi kusema, “Mungu hutushinda kupitia hukumu na kuadibu, kwa hivyo tunapohubiri injili kwa watu wa dini, tunahitaji kuzungumza nao kwa sauti kali, na kuwakaripia; ni hapo tu ndipo wanaweza kushindwa.”) Kauli hii inaweza kusikika kuwa ya busara, lakini, je, inalingana na kanuni za ukweli? Je, Mungu aliwaagiza watu kufanya hivi? Je, neno la Mungu linasema, “Mnapohubiri injili kila mahali, lazima uinuke na kuwatawala watu kwa ukatili, mkitumia hukumu na kuadibu kuhubiri injili kila pahali”? (Hapana.) Kwa hivyo, kauli hii ilitoka wapi? Ni wazi kwamba, ni nadharia inayofikiriwa kutoka kichwani mwa kiongozi wa uongo ambaye hana uelewa wa kiroho. Kwa juujuu, kauli hii inaweza kuonekana kama haina tatizo: “Wanadamu wote lazima wapitie hukumu na kuadibu kwa Mungu. Ikiwa hawawezi kuipokea moja kwa moja kutoka kwa maneno ya Mungu, je, hawawezi kuipokea kwa njia isiyo ya moja kwa moja? Kwa vyovyote vile, hiyo ndiyo athari ambayo maneno ya Mungu yanakusudiwa kufikia—kuwashinda wanadamu wote. Je, haingekuwa bora kwao kupokea hili hivi karibuni? Kabla Mungu hajachukua hatua, tutachukua hatua hii ya kinga, ili watu waweze kukuza kinga ya aina fulani. Kisha Mungu anapowahukumu na kuwaadibu kweli, watu hao hawataasi, hawatampinga, au kumsaliti Mungu. Hili litazuia hisia za Mungu kuumizwa. Je, si hilo ni jambo zuri?” Kwa juujuu, kila sentensi inaonekana kuwa sahihi, na kusema kimafundisho, inaonekana kuwa na mantiki. Hata hivyo, je, hii ni kanuni ya ukweli? Je, nyumba ya Mungu ina masharti gani kwa ajili ya kuhubiri injili? Je, inawahitaji watu kufanya hivi? (Hapana.) Kwa hivyo, nadharia hii si halali, na mtu aliyeipendekeza ni kiongozi wa uongo.

Viongozi wa uwongo mara nyingi hujifanya kuwa wa kiroho, wakitamka uwongo wa kuhadaa ili kuwapotosha na kuwalekeza watu vibaya. Ingawa uongo huu unaweza kuonekana kuwa usio na tatizo kijuujuu, una athiri vibaya kuingia kwa watu katika uzima, ukiwasumbua, kuwapotosha, na kuwazuia watu kutembea katika njia ya kufuatilia ukweli. Kwa sababu ya maneno haya ya kiroho ya uwongo, watu wengine huanza kuwa na mashaka na upinzani dhidi ya maneno ya Mungu, wanakuza fikira, na hata suitafahamu kumhusu Mungu na kujihadhari dhidi Yake, na kisha kuenda pepe kutoka Kwake. Hii ndiyo athari ambayo kauli za kiroho za uwongo za viongozi wa uwongo huwa nazo kwa watu. Washiriki wa kanisa wanapokuwa wakipotoshwa na kuathiriwa na kiongozi wa uwongo, kanisa hilo hugeuka kuwa dini, kama vile Ukristo au Ukatoliki, ambapo watu huzingatia tu kauli na mafundisho ya mwanadamu. Wote huabudu mafundisho ya Paulo, wakifikia hata kiwango cha kutumia maneno yake mahali pa yale ya Bwana Yesu, badala ya kuifuata njia ya Mungu. Matokeo yake, wote hugeuka kuwa Mafarisayo wanafiki na wapinga Kristo. Hivyo basi, wanalaaniwa na kuhukumiwa na Mungu. Kama vile Paulo, viongozi wa uwongo hujikweza na kujishuhudia wenyewe, wao huwapotosha na kuwasumbua watu. Huwapotosha na kuwaingiza katika desturi za kidini, na namna watu hawa wanavyomwamini Mungu inakuwa sawa kabisa na ile ya watu wa kidini, jambo ambalo huchelewesha kuingia kwao katika njia sahihi ya imani yao katika Mungu. Viongozi wa uwongo huwapotosha na kuwasumbua watu daima, na kisha watu hao hubuni nadharia na kauli nyingi za roho za uwongo. Nadharia, kauli, na matendo haya ni kinyume kabisa na ukweli, na hayana uhusiano wowote nao. Lakini viongozi wa uwongo wanapowapotosha na kuwaelekeza vibaya watu, wao huyachukulia mambo haya kama vitu chanya, kama ukweli. Wao huamini kimakosa kwamba mambo haya ni ukweli, na kufikiri kwamba maadamu wanaamini mambo haya mioyoni mwao na wanaweza kuyasema kwa ufasaha, na maadamu mambo hayo yanakubaliwa na kila mtu, basi wameupata ukweli. Wakipotoshwa na mawazo na mitazamo hii, mbali na watu kutoweza kuuelewa ukweli, wao pia hawawezi kutenda au kupitia maneno ya Mungu, sembuse kuingia katika uhalisi wa ukweli. Badala yake, wanazidi kuwa mbali na maneno ya Mungu na mbali hata zaidi na kuingia katika uhalisi wa ukweli. Kinadharia, hakuna ubaya wowote na maneno ambayo viongozi wa uwongo husema na kauli mbiu wanazopaza sauti, yote ni sahihi. Basi, kwa nini hayatimizi chochote kabisa? Hii ni kwa sababu kile ambacho viongozi wa uwongo huelewa na kufahamu ni cha juu juu mno. Hayo yote ni mambo ya mafundisho, ambayo hayahusiani na uhalisi wa ukweli katika maneno ya Mungu, mahitaji ya Mungu au nia Zake. Ukweli ni kwamba, mafundisho yote ambayo viongozi wa uwongo huhubiri hayafikii kabisa uhalisi wa ukweli—kwa usahihi zaidi, hayana uhusiano wowote na ukweli wala na maneno ya Mungu. Basi, viongozi wa uwongo wanapozungumzia maneno na mafundisho haya mara kwa mara, yanahusiana na nini? Kwa nini wao hushindwa daima kuingia katika uhalisi wa ukweli? Hili linahusiana moja kwa moja na ubora wa tabia wa viongozi wa uwongo. Ni hakika kabisa kwamba viongozi wa uwongo wana ubora duni wa tabia na hawana uwezo wa kufahamu ukweli. Haijalishi wanaamini katika Mungu kwa miaka mingapi, hawataelewa ukweli wala kuwa na uingiaji katika uzima, na inaweza pia kusemwa kwamba haijalishi wanaamini katika Mungu kwa miaka mingapi, haitakuwa rahisi kwao kuingia katika uhalisi wa ukweli. Ikiwa kiongozi wa uwongo hatatimuliwa, na badala yake aruhusiwe kuendelea na wadhifa wake, ni matokeo ya aina gani yatakayofuata? Uongozi wake utawavuta watu wengi zaidi na zaidi katika desturi na kanuni za kidini, katika maneno na mafundisho, na katika fikira potovu zisizo wazi na mawazo ya kubuni. Tofauti na wapinga Kristo, viongozi wa uwongo hawawaongozi watu kuja mbele yao au mbele ya Shetani, lakini ikiwa hawawezi kuwaongoza watu wateule wa Mungu kuingia katika uhalisi wa ukweli wa maneno Yake, je, watu wateule wa Mungu wataweza kupata wokovu Wake? Je, wataweza kukamilishwa na Mungu? La hasha. Ikiwa watu wateule wa Mungu hawawezi kuingia katika uhalisi wa ukweli, je, si bado wanaishi chini ya nguvu za Shetani? Je, si bado wao ni wapotovu wanaoshikiliwa chini ya nguvu za Shetani? Je, si hili linamaanisha kwamba wataangamia mikononi mwa viongozi wa uwongo? Ndiyo maana matokeo ya kazi ya viongozi wa uwongo na wapinga Kristo kimsingi ni sawa. Wote wawili hawawezi kuwafanya watu wateule wa Mungu waelewe ukweli, waingie katika uhalisi, na wapate wokovu. Wote wawili huwadhuru watu wateule wa Mungu na kuwaangamiza. Matokeo ni sawa kabisa.

Baadhi ya uzushi na uwongo wa viongozi wa uwongo ni upi? Yafupisheni ninyi wenyewe baadaye. Ninawaachia kazi hii ili Nione kama mnaweza kuyatambua. Je, viongozi walio karibu nanyi wamewahi kusema maneno fulani ambayo ni ya kiroho au yanapatana na hisia za kibinadamu na, kijuujuu, yanaonekana kuwa sahihi na yanalingana na ukweli lakini yanashindwa kukimu kuingia kwako katika uzima na kutatua matatizo yako halisi? Ikiwa huna utambuzi wa maneno haya na hata unayathamini na kuyaweka moyoni, ukiyaruhusu yakutawale na kukuongoza kila wakati, na yayayumbishe mawazo na mwenendo wako kila wakati, je, si matokeo ya hili ni mazito sana? (Ndiyo.) Basi ni muhimu sana kwenu kuchimba kwenye mzizi wa masuala haya, ili mpate ni mambo gani ambayo ni uzushi na uwongo yanayoweza kuwafanya watu washuke hadhi hadi kufikia kiwango ambapo imani yao katika Mungu hugeuka kuwa imani ya kidini, ikiwasababisha wampinge Mungu na kukataliwa na Mungu. Kwa mfano, tuseme mtu anasema, “Usijitahidi kuwa kiongozi. Ukitimuliwa au kuondoshwa baada ya kuwa kiongozi, hutapata hata fursa ya kuwa muumini wa kawaida.” Je, mazungumzo ya aina hii ni uzushi na uwongo wa viongozi wa uwongo? (Ndiyo.) Hakika? Uzushi na uwongo wa viongozi wa uwongo lazima vitofautishwe na vile vya wapinga Kristo; msivichanganye pamoja. Mtu huyo anamaanisha nini kwa kusema mambo kama hayo? Ni nia gani zilizofichwa katika maneno haya? Je, kuna kitu cha kutiliwa shaka ndani ya maneno hayo? Ni wazi, yana hila inayokusudiwa kuwapotosha watu, yanamaanisha kwamba watu wengine wanapaswa kuepuka kujitahidi kuwa viongozi, kwamba kufanya hivyo hakutaleta matokeo mazuri. Lengo lao la kusema hivi ni kuwafanya watu waachane na wazo la kuwa kiongozi ili kusiwe na mtu atakayeshindana nao kwa ajili ya sifa na hadhi, na hivyo kuwaruhusu wajisikie huru kuwa viongozi milele. Wakati huo huo, wanawaambia watu, “Hivi ndivyo nyumba ya Mungu inavyowatendea viongozi na wafanyakazi, inakupandisha cheo inapokuhitaji na isipokuhitaji, inakushusha chini kabisa, na kukuacha bila fursa hata ya kuwa muumini wa kawaida.” Asili ya maneno haya ni ipi? (Kumkufuru Mungu.) Ni mtu wa aina gani anayesema maneno ya kufuru dhidi ya Mungu? (Mpinga Kristo.) Ndani ya maneno haya, kuna nia mbili za uovu zinazoweza kusababisha matokeo mawili: Moja ni kuwaambia wengine wasigombee hadhi kabisa, jambo ambalo huhakikisha hadhi yao wenyewe inabaki salama; nyingine ni kukufanya umwelewe Mungu visivyo, uache kumwamini Mungu na badala yake uanze kuwaamini wao. Huyu ndiye mpinga Kristo aliye dhahiri kabisa. Inaonekana ninyi hamna uwezo wa kufahamu; Nimezungumza kuhusu mifano ya hili hapo awali. Ninyi sio tu wazembe na mna kumbukumbu duni, bali uwezo wenu wa kufahamu pia ni haba. Hamwezi hata kumtambua mpinga Kristo aliye dhahiri kama huyo. Je, viongozi wa uwongo wangesema mambo kama hayo? Je, wao wangewapotosha watu na kumpinga Mungu waziwazi na kwa kujua? (La.) Ingawa mambo ambayo viongozi wa uwongo husema na kufanya yanaweza kuonekana kuwa yasiyo na tatizo kijuujuu, kazi yao haina kanuni na haiwezi kupata matokeo. Viongozi wa uwongo hawawezi kutatua tatizo lolote la watu, kuwaleta katika njia sahihi ya imani katika Mungu, au kuwaongoza kwenda mbele za Mungu. Kila kitu wanachosema ni sahihi, hawajapunguza bidii katika kazi yao hata kidogo, wana bidii na shauku, na kijuujuu wanaonekana kuwa na imani, kuwa na azimio, na kuwa tayari kuvumilia ugumu na kulipa gharama. Zaidi ya hayo, wanaonekana kuwa na uvumilivu wa ajabu na kuweza kuvumilia uchovu na ugumu wa kila aina. Ni kwamba tu ubora wao wa tabia na uwezo wa kufahamu ni duni, na hawana ufahamu sahihi wa ukweli. Wanafanya nini kuhusu huu upungufu wa uwezo wa kufahamu? Wanatumia kanuni na mafundisho, na pia nadharia za kiroho wanazozizungumzia mara kwa mara, kutatua tatizo hili. Baada ya miaka michache chini ya uongozi wao, mafundisho, kanuni, na matendo ya nje ya kila aina huibuka miongoni mwa watu. Watu hushikilia mafundisho, kanuni, na matendo haya, na kuamini kwamba wanatenda ukweli na wanaingia katika uhalisi wa ukweli, lakini kwa kweli, bado wako mbali sana na uhalisi wa ukweli! Punde tu mioyo ya watu inapojazwa, kutawaliwa, na kuongozwa na mambo haya, utatuzi huwa wa taabu. Kila jambo lazima lichanganuliwe na kuchambuliwa moja baada ya lingine ili watu wayaelewe. Kisha, watu lazima waambiwe ukweli, mafundisho, kauli mbiu, na kanuni ni nini, na ufahamu sahihi wa ukweli, kauli sahihi, na kanuni za ukweli ni nini. Yote haya yanahitaji kutatuliwa moja baada ya lingine; la sivyo, wale walio na tabia njema kiasi, wanaotii sheria, na wanaofuatilia mambo ya kiroho watapotoshwa na kuangamizwa na viongozi wa uwongo. Watu hawa wanaweza kuonekana kuwa wa moyo, wanaoweza kuvumilia ugumu na kulipa gharama, na wanaoweza kuomba mambo yanapowapata. Hata hivyo, kama tu ilivyo kwa watu wa kidini, Mungu anaporudi, hakuna hata mmoja wao anayemtambua Yeye, hakuna hata mmoja wao anayekiri kwamba Mungu anafanya kazi mpya tena, na wote wanampinga Yeye. Kwa nini iko hivi? Ni kwa sababu viongozi wa uwongo na wapinga Kristo wamewapotosha—wamewadhuru na kuwaangamiza waumini wengi wa dhati katika Mungu.

Viongozi wa uwongo huzungumza tu maneno na mafundisho—kile wanachowafanya watu waelewe ni mafundisho tu na si ukweli, na kile wanachowafanya watu waone ni mambo ya roho ya uongo. Matokeo ya kuzungumza maneno na mafundisho ni yapi? Kiroho cha uwongo, ufahamu wa uwongo, maarifa ya uwongo, utendaji wa uwongo, na utii wa uwongo—yote ni ya uwongo. Huu “uwongo” hutokeaje? Huo husababishwa na viongozi wa uwongo kuwa na ufahamu uliopotoka, wa upande mmoja, na wa juu juu wa ukweli, na kushindwa kabisa kufahamu kiini cha ukweli. Viongozi wa uwongo huwaletea watu kanuni, maneno na mafundisho mengi, pamoja na baadhi ya kauli mbiu na nadharia. Watu hao hawaelewi nia za kweli za Mungu hata kidogo, na wanapokumbana na hali mbalimbali ngumu, hawajui jinsi ya kuzishughulikia na kuzikabili, au jinsi ya kufahamu nia za Mungu. Je, watu kama hao wanaweza kuja mbele za Mungu? Je, wanaweza kumkubali Mungu na kuacha kumpinga Yeye? La, hawawezi. Kwa hivyo, ni muhimu sana na ni lazima kwenu kufanya muhtasari wa uzushi na uwongo wa viongozi wa uwongo na kupata utambuzi kuwahusu. Mnapofanya muhtasari, ni muhimu sana kuvitofautisha na uwongo unaotumiwa na wapinga Kristo kuwapotosha watu. Kuhusu jukumu la pili la viongozi na wafanyakazi—kufahamu hali za kila aina ya mtu, na kusuluhisha matatizo mbalimbali yanayohusiana na kuingia katika uzima wanayokumbana nayo katika maisha yao halisi—tutahitimisha hapa ushirika wetu wa kuchanganua matendo mbalimbali ya viongozi wa uwongo na kiini cha masuala yanayowahusu viongozi wa uwongo.

Kipengele cha Tatu: Kushiriki Kanuni za Ukweli Zinazopaswa Kueleweka Ili Kutekeleza Kila Wajibu Ipasavyo (Sehemu ya Kwanza)

Viongozi wa Uwongo Wanaweza Tu Kunena Maneno na Mafundisho ili Kuwahimiza Watu

La kufuata, tutashiriki juu ya jukumu la tatu la viongozi na wafanyakazi—kushiriki kanuni za ukweli zinazopaswa kueleweka ili kutekeleza kila wajibu ipasavyo. Hii ni kazi muhimu na ya msingi ya viongozi na wafanyakazi, na tutashiriki na kuchanganua udhihirisho wa viongozi wa uwongo kwa kuzingatia jukumu hili. Uwezo wa kiongozi au mfanyakazi wa kushiriki waziwazi juu ya kanuni za ukweli ambazo watu wanapaswa kuelewa ili kutekeleza wajibu wao vizuri ndicho kielelezo bora zaidi cha iwapo wanamiliki uhalisi wa ukweli, na ndicho ufunguo wa kubaini iwapo wanaweza kufanya kazi halisi vizuri. Sasa, hebu tuangalie jinsi viongozi wa uwongo wanavyoishughulikia kazi hii. Sifa moja ya viongozi wa uwongo ni kutokuwa na uwezo kwao wa kueleza kikamilifu au kufafanua suala lolote linalohusisha kanuni za ukweli. Mtu anapotafuta kutoka kwao, wanaweza tu kumwambia maneno matupu na mafundisho. Wanapokabiliwa na matatizo yanayohitaji utatuzi, wao hujibu mara kwa mara kwa kauli kama, “Ninyi nyote ni wataalamu katika kutekeleza wajibu huu. Mkiwa na matatizo, mnapaswa kuyatatua ninyi wenyewe. Msiniulize mimi; mimi si mtaalamu, na sielewi. Lishughulikieni ninyi wenyewe.” Watu wengine wanaweza kujibu, “Tunakuuliza kwa sababu hatuwezi kutatua tatizo; tusingekuuliza kama tungeweza. Hatuelewi tatizo hili linalohusisha kanuni za ukweli.” Viongozi wa uwongo hujibu, “Je, si nimekwisha kukuambia kanuni? Tekeleza wajibu wako vizuri, na usisababishe usumbufu au vurugu. Bado unauliza nini? Lishughulikie jinsi unavyoona inafaa! Maneno ya Mungu yamekwisha nenwa: Tangulizeni masilahi ya nyumba ya Mungu.” Watu hao huachwa wakiwa wamechanganyikiwa kabisa, wakiwaza, “Hili si suluhisho la tatizo!” Hivi ndivyo viongozi wa uwongo huichukulia kazi; wao huikagua tu, hufanya mambo kwa njia isiyo ya dhati, na hawashughulikii matatizo kamwe. Bila kujali masuala ambayo watu huibua, viongozi wa uwongo huwaambia watafute ukweli wao wenyewe. Wao huwauliza watu mara kwa mara, “Mna matatizo yoyote? Kuingia kwenu katika uzima kuko vipi? Je, mnatekeleza wajibu wenu kwa njia ya kijuujuu?” Watu hao hujibu, wakisema, “Mara kwa mara, mimi hujipata katika hali ya kutenda kwa namna isiyo ya dhati, na kupitia maombi, huitatua na kujirekebisha, lakini bado sielewi kanuni za ukweli za kutekeleza wajibu wangu.” Viongozi wa uwongo husema, “Je, sikushiriki kanuni maalum na wewe katika mkutano uliopita? Hata nilikupa vifungu kadhaa vya maneno ya Mungu. Je, hupaswi kuwa umeelewa sasa?” Kwa kweli, wanaelewa mafundisho yote, lakini bado hawawezi kutatua matatizo yao. Viongozi wa uwongo hata husema maneno makuu, “Kwa nini huwezi kulitatua? Ni kwamba tu hujasoma maneno ya Mungu kwa kina cha kutosha. Ukiomba zaidi na ukisoma maneno ya Mungu zaidi, basi matatizo yako yote yatatatuliwa. Ninyi mnahitaji kujifunza kujadiliana na kutafuta njia pamoja, kisha matatizo yenu hatimaye yatatatuliwa. Kuhusu masuala ya kitaaluma, msiniulize Mimi; jukumu langu ni kukagua kazi. Nimekamilisha kazi yangu, na yaliyosalia yanahusisha mambo ya kitaaluma, ambayo sielewi.” Viongozi wa uwongo mara nyingi hutumia sababu na visingizio kama “Sielewi, sijawahi kujifunza, mimi si mtaalamu” ili kuwapuuza watu na kukwepa maswali. Wanaweza kuonekana wanyenyekevu sana; hata hivyo, hili hufichua suala zito kuhusu viongozi wa uwongo—hawana ufahamu wowote wa matatizo yanayohusisha maarifa ya kitaaluma katika kazi fulani, wanahisi wasiokuwa na uwezo na huonekana wenye aibu na fedheha sana. Basi wanafanya nini? Wanaweza tu kukusanya vifungu kadhaa vya maneno ya Mungu ili kushiriki na kila mtu wakati wa mikutano, wakizungumzia baadhi ya mafundisho ili kuwahimiza watu. Viongozi wenye ukarimu kiasi wanaweza kuonyesha kuwajali watu na kuwauliza mara kwa mara, “Je, mmekumbana na matatizo yoyote maishani mwenu hivi karibuni? Mna nguo za kutosha kuvaa? Je, kumekuwa na yeyote miongoni mwenu anayetenda kwa namna isiyofaa?” Ikiwa kila mtu anasema hana masuala hayo, wao hujibu, “Basi hakuna tatizo. Endeleeni na kazi yenu; nina mambo mengine ya kushughulikia,” na huondoka kwa haraka, wakihofia kwamba mtu anaweza kuibua maswali na kuwaomba wayashughulikie, na kuwaweka katika hali ya aibu. Hivi ndivyo viongozi wa uwongo hufanya kazi—hawawezi kutatua matatizo yoyote halisi. Wanawezaje kutekeleza kazi ya kanisa kwa ufanisi? Matokeo yake, mlundikano wa masuala yasiyotatuliwa hatimaye huzuia kazi ya kanisa. Hii ni sifa na udhihirisho mkuu wa jinsi viongozi wa uwongo hufanya kazi.

Katika kazi yao, viongozi wa uwongo wana shauku ya kuhubiri tu, na wanapenda zaidi kuzungumza maneno na mafundisho, na kusema maneno ya kuwahimiza na kuwafariji watu, wakifikiri kwamba maadamu wanawafanya watu wawe na nguvu na shughuli nyingi katika utendaji wa wajibu wao, ni sawa na wao kuwa wamefanya kazi nzuri. Zaidi ya hayo, viongozi wa uwongo wana shauku kubwa kuhusu kujali hali ya maisha ya kila siku ya kila mtu. Wao huwauliza watu mara kwa mara kama wanakumbana na matatizo yoyote kuhusu suala hilo, na ikiwa kweli kuna yeyote anayekumbana na tatizo, wako tayari kusaidia kutatua matatizo haya. Wao hujishughulisha kweli na mambo haya ya jumla, wakati mwingine hata wao huahirisha milo, na mara nyingi hukesha na kuamka mapema. Kwa kuzingatia shughuli zao nyingi na bidii yao, kwa nini matatizo katika kazi ya kanisa na magumu yanayowakabili watu wateule wa Mungu katika kutekeleza wajibu wao hubaki bila kutatuliwa? Hii ni kwa sababu viongozi wa uwongo hawawezi kamwe kueleza waziwazi kanuni za ukweli zinazohusiana na kutekeleza wajibu. Maneno na mafundisho, na mahimizo wanayosema hayana ufanisi kabisa na hayawezi kutatua masuala halisi hata kidogo. Bila kujali wanasema kiasi gani au wana shughuli nyingi au wamechoka kiasi gani, kazi ya kanisa haipigi hatua kamwe. Ingawa kila mtu anaonekana kutekeleza wajibu wake kwa nje, hapati matokeo mengi halisi, kwa sababu viongozi wa uwongo hawawezi kushiriki kanuni za ukweli zinazohusiana na kutekeleza wajibu, au kutumia ukweli kutatua masuala halisi—kwa hivyo hawawezi kutatua masuala mengi yaliyo katika utendaji wa wajibu. Kwa mfano, wakati mmoja nyumba ya Mungu ilihitaji kuchapisha vitabu vya maneno ya Mungu, na kiongozi alilazimika kuwachagua watu wawili ili wasimamie kazi hii. Viwango vya kuwachagua watu ni vipi? Ubinadamu wao unapaswa kuwa mzuri kiasi, wanapaswa kuwa wa kutegemewa, na wenye uwezo wa kukabiliana na hatari. Baada ya watu hao kuchaguliwa, kiongozi huyu aliwaambia, “Leo, nimewaita ninyi wawili ili niwakabidhi jambo: Nyumba ya Mungu ina kitabu kinachohitaji kuchapishwa, na ninahitaji mtafute kiwanda cha uchapishaji, na baada ya nakala zote kuchapishwa, lazima mzisambaze mara moja mikononi mwa watu wateule wa Mungu, ili waweze kula na kunywa maneno ya Mungu bila kuchelewa. Je, mmeazimia kutekeleza kazi hii? Je, mko tayari kubeba mzigo huu na hatari hii?” Watu hao wawili waliamini kwamba huku kulikuwa ni Mungu kuwainua, kwa hivyo wakakubali. Kisha kiongozi akawauliza, “Je, mna azimio la kutimiza agizo la Mungu? Mko tayari kuapa?” Kisha watu hao wawili wakaapa, wakisema, “Ikiwa hatuwezi kutimiza agizo la Mungu na tuivuruge kazi hii, na kusababisha kazi ya nyumba ya Mungu ipate hasara, basi na tupigwe na radi na ngurumo kutoka mbinguni. Amina!” Kiongozi akasema, “Pia, tunahitaji kushiriki juu ya ukweli. Katika kufanya kazi hii sasa, je, mnafanya biashara? Je, mnaombwa kufanya kazi kama wafanyakazi?” Watu hao wawili wakajibu, “La, huu ni wajibu wetu.” Kiongozi akasema, “Kwa kuwa ni wajibu wenu, lazima mlipe upendo wa Mungu. Hamwezi kumhuzunisha Mungu au kumfanya Awe na wasiwasi. Kuwa tayari kukabiliana na hatari haitoshi; mnahitaji kutekeleza wajibu wenu kwa uaminifu. Mnapokumbana na masuala, mnapaswa kuomba zaidi na kushauriana. Msiwe wakaidi au kutenda kwa hiari yenu. Kwa nini niliwafanya ninyi wawili mshirikiane? Ni ili muweze kujadiliana mambo yanapotokea, na kurahisisha ninyi kuchukua hatua. Ikiwa hamwezi kufikia makubaliano, basi ombeni. Kila mtu anapaswa kuachilia maoni yake, na mtende tu mnapokuwa mmefikia makubaliano. Natumai ninyi wawili mnaweza kuikamilisha kazi hii kwa mafanikio!” Mwishowe, kiongozi huyu alitafuta kifungu cha maneno ya Mungu kuhusu jinsi ya kutekeleza wajibu vizuri, na wote watatu wakaomba kwa kukisoma mara kadhaa. Baada ya hayo, jambo hilo lilionekana kuwa limekabidhiwa kwao, na wajibu wa kiongozi ulionekana kuwa umetimizwa. Utendaji wa kiongozi katika kazi hii ulikuwaje? Kiongozi aliridhika kabisa, kama walivyoridhika watu hao wawili. Watazamaji walitoa maoni, “Kiongozi huyu kwa kweli anajua jinsi ya kufanya kazi; usemi wake umepangwa vizuri na una msingi imara, na anafanya mambo hatua kwa hatua. Kwanza, aliwagawia kazi hao wawili, kisha akatatua masuala yao yanayohusisha mawazo na mitazamo, na mwishowe, akasema maneno makali, akiwafanya waape na kutoa ahadi. Kwa kweli aliifanya kazi hii kwa utaratibu, na kweli anastahili cheo cha kiongozi—yeye ni mwenye uzoefu na anabeba mzigo.” Mwishowe, kiongozi aliwaambia, “Kumbukeni hili: Kuchapisha vitabu si kazi rahisi, si jambo ambalo mtu wa kawaida anaweza kulifanya. Kazi hii hamkukabidhiwa na mimi au nyumba ya Mungu; ni agizo kutoka kwa Mungu. Hampaswi kumwangusha Yeye. Maadamu mtaikamilisha kazi hii vizuri, maisha yenu yatapiga hatua, na mtakuwa na uhalisi.” Kimsingi, hapakuwa na masuala yoyote ya kanuni katika maneno haya; yaliweza kuonekana kuwa sahihi kwa kiasi fulani. Basi, hebu tuchanganue jambo hili na tuone ule “uwongo” ulidhihirika wapi katika huyu kiongozi wa uwongo. Je, kiongozi alitoa maagizo yoyote kuhusu masuala mbalimbali ya kina, kama vile vipengele vya kitaaluma na kiufundi vinavyohusiana na kazi hii? Je, alishiriki kanuni zozote maalum za ukweli au viwango vinavyohitajika? (Hapana.) Alisema tu maneno matupu na yasiyo na maana—maneno ambayo watu wengi husema mara kwa mara, maneno yasiyo na uzito wowote. Kwa sababu kiongozi alikuwa akizungumza yeye mwenyewe na kutoa maagizo, watu waliyachukulia maneno haya kuwa na uzito zaidi kuliko kawaida, lakini kwa kweli, yalikuwa ni mazungumzo yasiyohusika na hayakuwa na athari yoyote katika kutatua masuala halisi yanayohusiana na uchapishaji wa vitabu. Basi, ni masuala gani maalum yanayohusika katika uchapishaji wa vitabu? Tunapaswa kuyajadili na tuone kama kazi aliyoifanya kiongozi huyu ilikuwa ni ya kiongozi wa uwongo.

Kwanza, uchapishaji wa vitabu unahusisha upagaji, na kisha kuna usahihishaji wa maandishi, upangiliaji wa orodha ya yaliyomo na maandishi makuu, na pia uzito, rangi, na ubora wa karatasi. Pia kuna nyenzo ya jalada, kama linapaswa kuwa laini au gumu, na muundo, rangi, mchoro, na fonti ya jalada. Mwishowe, kuna ujalidishaji, kama kutumia gundi au kushona. Haya yote ni masuala yaliyo ndani ya mawanda ya uchapishaji wa vitabu. Je, kiongozi alijadili lolote kati ya haya? (La.) Suala lingine ni kutafuta kiwanda cha uchapishaji: kama mashine za uchapishaji na ujalidishaji ni za kisasa, ubora wa uchapishaji na ujalidishaji ukoje, na bei—je, hawakupaswa kutoa maagizo kwa mambo haya yote, na pia kanuni na mawanda? Ikiwa kiongozi angesema, “Sielewi mambo haya; tafuteni tu chochote,” je, angekuwa kiongozi wa maana? Je, maneno yasiyohusika aliyoyasema yanaweza kuchukua nafasi ya masuala mbalimbali ya kina yanayohusika katika uchapishaji wa vitabu? (La.) Na bado, kiongozi huyu wa uwongo aliamini kwamba yalihusika. Alifikiri, “Nimekwisha shiriki ukweli mwingi sana, na nimewaambia kanuni zote. Wanapaswa kuelewa mambo haya!” Hili “wanapaswa” ndiyo mantiki na njia ya kutatua matatizo ya huyu kiongozi wa uwongo. Mwishowe, vitabu vilipochapishwa, kwa sababu karatasi ilikuwa ya ubora duni sana na nyembamba sana, maandishi yalionekana pande zote mbili, jambo ambalo lilifanya iwe ya kuchosha sana na vigumu kwa watu wazee na wale wenye macho hafifu kusoma vitabu hivyo. Pia kulikuwa na suala la hatua ya mwisho, mchakato wa ujalidishaji—ujalidishaji kufikia kiwango kinachostahili au la huathiri ubora wa jumla na muda wa kudumu wa kitabu. Kwa sababu kiongozi hakutoa maagizo, na wale walioitekeleza kazi hii walikosa kanuni na uzoefu, na wakajihusisha na kujadiliana bei bila kuwajibika, kiwanda cha uchapishaji kilifanya kazi duni na kutumia nyenzo duni ili wasipate hasara, na mwishowe vitabu viliposambazwa kwa akina ndugu na dada vikaanza kubomoka ndani ya miezi miwili. Majalada na kurasa zilianguka, na kazi yote ya uchapishaji ilikuwa bure. Huu ulikuwa wajibu wa nani? Ikiwa mtu angewajibishwa, wajibu wa moja kwa moja ungekuwa wa watu wawili waliosimamia uchapishaji wa vitabu, na wajibu usio wa moja kwa moja ungekuwa wa kiongozi wa uwongo. Kiongozi wa uwongo hata alikuwa na kisingizio, akisema: “Huwezi kunilaumu kwa kazi hii kuharibika; mimi pia sielewi! Sijawahi kuchapisha vitabu, na similiki kiwanda cha uchapishaji. Nitajuaje kuhusu mambo haya?” Je, kisingizio hiki kinakubalika? Kama kiongozi, kazi hii iko ndani ya mawanda ya majukumu yako. Bila kujali kama ni kazi inayohusiana na taaluma, ustadi, aina ya maarifa, au ukweli, huhitaji kuelewa kila sehemu yake, lakini, je, umejitahidi kujifunza kuhusu kile usichokijua? Je, umetimiza majukumu yako kwa umakini na kwa dhati? Watu wengine wanaweza kusema, “Ninataka kutimiza majukumu yangu, lakini sielewi hili pia. Haijalishi ninavyojaribu kujifunza kwa bidii, siwezi tu kulielewa!” Hili linamaanisha kwamba, kama kiongozi, hufikii kiwango kinachostahili; wewe ni kiongozi wa uwongo halisi. Ndugu na dada walihisi kinyongo kiasi kwa sababu ya ubora duni wa vitabu, wakisema, “Ingawa vitabu hivi havitugharimu pesa, ubora wake ni duni sana! Kiongozi huyu alifanyaje kazi yake? Aliitekelezaje kazi hii?” Kiongozi aliposikia hili, alijibu, “Mnaweza kunilaumu kwa hilo? Similiki kiwanda cha uchapishaji, na si mimi ndiye mwamuzi. Zaidi ya hayo, je, huku si kuokoa fedha kwa ajili ya nyumba ya Mungu? Je, ni makosa kuiokolea nyumba ya Mungu fedha?” Maneno ya kiongozi yalikuwa sahihi, hayakuwa na makosa; kiongozi hakuhitaji kuwajibika kisheria. Hata hivyo, kulikuwa na tatizo moja, ambalo ni kwamba pesa zilizotumika kuchapisha vitabu zilipotea bure. Vitabu walivyosambaziwa akina ndugu na dada vilianza kubomoka na kupoteza kurasa ndani ya miezi miwili. Ni nani anayepaswa kuwajibikia hili? Je, huu haukuwa wajibu wa kiongozi? Hili lilitokea ndani ya mawanda wa kazi yako, wakati ulipokuwa ukihudumu kama kiongozi, kwa hivyo, je, hupaswi kuwajibika? Lazima ubebe lawama; huwezi kukataa wajibu wako! Watu wengine wanaweza hata kuzungumza kwa njia isiyo na mantiki, wakisema, “Sijawahi kufanya kazi hii hapo awali. Je, siruhusiwi kufanya makosa katika kazi ambayo sijawahi kuifanya?” Kwa kuzingatia tu kauli hii, hufai kwa kazi yako, na unapaswa kutimuliwa. Huna sifa za kuwa kiongozi; wewe ni kiongozi wa uwongo asilia. Kusema maneno mengi matamu, lakini bila kufanya kazi yoyote halisi—huu ndio udhihirisho dhahiri zaidi wa kiongozi wa uwongo.

Baadhi ya viongozi wa uwongo hawawezi kufanya kila kipengele cha kazi halisi ipasavyo na kwa vitendo. Wanaweza tu kushughulikia baadhi ya mambo ya jumla, na kisha wanaamini kwamba wanafikia kiwango kinachostahili kama viongozi, kwamba wao ni wa ajabu, na mara nyingi wao hujisifu, wakisema, “Lazima nihangaike na kila kitu kanisani, na lazima nishughulikie kila tatizo. Je, kanisa linaweza kuendelea bila mimi? Kama singewaandalia mikutano, je, hamngekuwa kama mchanga usioshikamana? Kama singefuatilia na kusaidia kuidumisha kazi ya utengenezaji filamu, je, kusingekuwa na watu wanaoisumbua kila wakati? Je, kazi ya utengenezaji filamu ingeweza kuendelea vizuri? Ingawa mimi si mtaalamu wa kazi ya nyimbo za sifa, kama singekuja mara kwa mara kukagua kazi yenu, kuwasimamia, na kuwaandalia mikutano, je, mngeweza kutunga nyimbo hizo za sifa? Ingewachukua muda gani kuelewa mambo?” Kauli hizi zinaweza kuonekana za busara na sahihi, lakini ukiangalia kwa makini, je, vipengele mbalimbali vya kazi ya kitaaluma vinavyosimamiwa na viongozi hawa wa uwongo vinaendeleaje? Je, wanaweza kushiriki kanuni za ukweli waziwazi? (La.) Wakati mmoja, timu ya utengenezaji filamu ilitafuta ushauri kuhusu suala la rangi za mavazi. Walipiga picha kadhaa, na mandhari na watu katika picha hizo walikuwa tofauti, lakini rangi za mavazi kimsingi zilikuwa katika mpangilio mmoja wa rangi—zote zilikuwa rangi za kijivu na njano zinazofanana na udongo. Niliuliza, “Kuna nini? Kwa nini wamevaa rangi hizi?” Walisema kwamba rangi hizi zilichaguliwa kimakusudi, kwamba walizipata sokoni kwa taabu na juhudi kubwa. Nikasema, “Kwa nini mlichagua rangi hizi? Je, Aliye juu aliwapa maagizo kuhusu hilo? Je, Aliye juu hakuwaagiza mtumie rangi mbalimbali, na kwamba rangi ziwe za heshima na za adabu? Matokeo haya yalitokeaje?” Mwishowe, baada ya kuuliza, watu wengine walisema, “Rangi nyingine hazionekani za heshima na za adabu vya kutosha, au kama zile zinazovaliwa na waumini katika Mungu au watakatifu. Ni mpangilio huu tu wa rangi ndio unaonekana zaidi kama kile ambacho waumini wanapaswa kuvaa. Kwa hivyo, kila mtu alikubaliana na maoni kwamba kuvaa nguo za rangi ya aina hii ndiko kunakomtukuza Mungu zaidi na kunawakilisha vyema zaidi sura ya nyumba ya Mungu.” Nikasema, “Sikuwahi kamwe kuwaambia ninyi nyote mvae nguo za rangi hizi. Kuna rangi nyingi za heshima na za adabu. Fikirieni jinsi upinde wa mvua ulivyo mzuri ambao Mungu aliuweka kama ishara ya agano Lake na wanadamu. Kuna nyekundu, rangi ya machungwa, njano, kijani, bluu, nili, zambarau—kila rangi inawakilishwa, isipokuwa zile mnazovaa. Kwa nini mlichagua rangi hizo?” Je, kiongozi wao alifanya kazi halisi ya kufanya uhakiki kuhusu mambo haya? Ninathubutu kusema kwamba hakufanya hivyo kabisa. Ikiwa kiongozi angekuwa na ufahamu safi na angeelewa kweli ukweli na mahitaji ya Mungu, washiriki wa timu ya utengenezaji filamu wasingechagua mavazi kama hayo na kushauriana na Aliye juu kuyahusu. Suala la mavazi lingeweza kutatuliwa katika ngazi ya chini, lakini kiongozi wa uwongo hakuwa na uwezo wa kulishughulikia. Badala yake, bila aibu akamuuliza Aliye juu kulihusu. Je, mtu kama huyu hapaswi kupogolewa? Huyu kiongozi wa uwongo hakuweza hata kutatua tatizo hili rahisi kabisa—ana faida gani? Wewe ni takataka tu! Uliulizwa kumtukuza Mungu na kumshuhudia Yeye, lakini uliishia kumwaibisha Mungu. Je, huelewi mengi sana? Je, huwezi kueleza kwa ufasaha wingi wa maarifa na mafundisho? Basi kwa nini mafundisho hayo yote na maarifa hayo yote hayakuwa na ufanisi katika hali hii? Ungewezaje hata kushindwa kutatua na kufanya uhakiki kuhusu suala la mavazi? Je, umekuwa na athari unayopaswa kuwa nayo kama kiongozi? Je, umetimiza majukumu unayopaswa kutimiza kama kiongozi? Huu ni udhihirisho wa kiongozi wa uwongo. Katika kazi yoyote maalum, viongozi wa uwongo hawana ufahamu wa kanuni. Hawawezi kutoa marekebisho na utatuzi wa wakati unaofaa kwa masuala yoyote ya ufahamu uliopotoka wa ukweli, na kuwawezesha watu kupata mwelekeo na njia kupitia hili. Viongozi wa uwongo husema tu maneno na mafundisho na kupaza sauti za kauli mbiu; hawawezi kufanya kazi yoyote halisi.

Viongozi wa Uwongo Hawafanyi Kazi Halisi wala Hawashughulikii Kazi Yao Inayowapasa

Baadhi ya viongozi wa uwongo hawawezi kufanya kazi yoyote halisi, lakini wao hushughulikia mambo fulani ya jumla yasiyo na maana, na wanafikiri kwamba huku ni kufanya kazi halisi, kwamba iko ndani ya upeo wa majukumu yao. Zaidi ya hayo, wanashughulikia mambo haya kwa uzito sana na kwa kweli wanatia bidii nyingi, wakiyatekeleza kwa namna nzuri sana. Kwa mfano, kulikuwa na mtu kanisani ambaye hapo awali alikuwa amefanya kazi kama mwoka vitobosha. Siku moja, aliamua kutokana na wema wa moyo wake kwamba ilimpasa tu Aniokee vitobosha, na akajitayarisha kufanya hivyo bila kunijulisha kulihusu. Aliwauliza viongozi wake kama iliruhusiwa, nao wakasema, “Endelea. Vikiwa na ladha nzuri, tutampa Mungu. Kama sivyo, sote tunaweza kuvila.” Alikuwa amepata idhini ya viongozi, jambo ambalo lilifanya kazi hii kuwa halali na inayofaa, kwa hivyo alikusanya haraka viungo na akaoka bechi moja, akisema, “Sijui kama vitakuwa na ladha nzuri, au kama vitaweza kumridhisha Mungu, au kama vitapatana na ladha Yake.” Viongozi wakajibu, “Ni sawa. Tutajitolea muda na afya yetu kiasi, na tujiweke katika hatari kidogo kwa ajili ya Mungu. Tutavionja kwanza na tuvikague kwa niaba ya Mungu. Visipokuwa na ladha nzuri kweli na tumwombe Mungu avile, Atahisi kukasirika na kusikitishwa sana na sisi. Kwa hivyo, kama viongozi, tuna jukumu na wajibu wa kufanya ukaguzi kuhusu jambo hili. Huku ni kufanya kazi halisi.” Baadaye, kila kiongozi wa kikundi aliyekuwa na “hisia ya uwajibikaji” kiasi alionja vitobosha hivyo. Baada ya kuvionja, walitoa tathmini, wakisema, “Jiko lilikuwa na joto sana katika bechi hii, halijoto ilikuwa juu sana, na kuna uwezekano wa kusababisha joto la ndani—pia ni chungu kiasi. Hizo hazifai! Tunahitaji kuwa na mtazamo wa kuwajibika na tuoke bechi nyingine na tuionje tena!” Baada ya kuionja bechi hii, walisema, “Hii inakaribia kuwa sawa sawa. Ina ladha ya siagi, ladha ya yai, na ufuta pia. Kwa kweli inastahili kutoka kwa mwoka vitobisha! Kwa kuwa kuna nyingi sana, na Mungu hawezi kumaliza hizi zote peke Yake, hebu tuweke 10 au 20 katika gudulia, na tumpe Mungu ili Aonje kama sampuli. Mungu akiziona ni tamu, tunaweza kuendelea kuzioka kwa bechi kubwa zaidi.” Walinikabidhi gudulia na Mimi nikaonja viwili. Nilidhani vilifaa kama kitu kipya tu, lakini si kama mlo kamili, kwa hivyo Niliacha kuvila. Watu wengine hata walidhani vilitengenezwa nyumbani na mshiriki wa nyumba ya Mungu, kwamba vilijaa upendo, uaminifu, na hofu, na vilikuwa na maana kubwa ingawa ladha yake ilikuwa ya kawaida tu. Baadaye, Mimi nililirudisha lile gudulia la vitobosha. Sivutiwi na mambo kama hayo na Sina hamu navyo. Zaidi ya hayo, Nikiwa natamani vitobosha, Mimi ninaweza kuvinunua vya ladha mbalimbali na kutoka nchi tofauti sokoni bila kutumia pesa nyingi. Baadaye, Niliwaambia, “Naishukuru nia yenu, lakini tafadhali msiniokee tena. Sitavila, na Nikitaka, nitanunua Mwenyewe. Ikiwa haja itatokea, basi vitengeneze tu Nitakapowaomba; Nisipowaambia mvitengeneze, basi hamhitaji kuvioka tena.” Je, hili halikuwa rahisi kueleweka? Kama wangekuwa wenye tabia njema na watiifu, wangeyakumbuka maneno Yangu na wajizuie kuvioka tena. Mungu anaponena, ndiyo humaanisha ndiyo, la humaanisha la, na “msioke” humaanisha “msioke”. Hata hivyo, baada ya muda kupita, waliniletea magudulia mengine mawili ya vitobosha. Niliwaambia, “Sikuwaambia msioke tena?” Wakajibu, “Hivi ni tofauti na vya wakati uliopita.” Nikajibu, “Hata kama ni tofauti, bado ni vitobosha. Hakuna haja ya kuoka vitobosha vyovyote. Sijaribu kuwa na mpole—Nikitaka, nitawaambia. Je, huwezi kuelewa lugha ya binadamu? Msioke tena.” Je, maneno haya yanaeleweka? (Ndiyo.) Lakini kwa nini yule mtu aliyekuwa akivioka alionekana kusahau kila mara? Ikiwa viongozi wake wangeweza kumkagua, wasishirikiane naye kwa dhati au kumtia moyo kufanya hivi, na wangeweza kumzuia mara moja, je, yule mtu aliyekuwa akioka vitobosha bado angethubutu kufanya hivyo? Angalau, hangelifanya hivyo kwa ujasiri na bila kujali. Kwa hivyo, viongozi hao walikuwa na athari gani katika hali hii? Walijihusisha na kila jambo dogo, wakajiingiza katika kila kitu, na wakajichukulia jukumu la kunifanyia ukaguzi. Walikuwa na “upendo” mwingi kiasi kwamba maneno hayawezi kuuelezea. Je, hii ndiyo kazi waliyopaswa kuwa wakifanya? Hapakuwa na maagizo ya kufanya hivi ndani ya kanuni za kazi za nyumba ya Mungu, na Mimi sikuwakabidhi jukumu hili; lilianzishwa na watu, Mimi sikuliomba. Basi kwa nini viongozi hawa walitekeleza jukumu hili kwa bidii hivyo? Huu ni udhihirisho wa viongozi wa uwongo: kutoshughulikia kazi yao inayofaa. Kulikuwa na kazi nyingi sana kanisani zilizohitaji kufuatiliwa, kukaguliwa, na kuhimizwa na wao, na matatizo mengi halisi yaliyohitaji kutatuliwa na wao kwa kufanya ushirika juu ya ukweli, lakini hawakufanya kazi yoyote kati ya hizo. Badala yake, walikuwa wazembe kiasi cha kunionjea Mimi vitobosha jikoni. Katika jambo hili, walikuwa makini sana na walitia bidii nyingi. Je, si hivi ndivyo viongozi wa uwongo hufanya? Je, tayari si jambo la kuchukiza sana? Sikutarajia kamwe kwamba, baada ya muda kupita, jambo hili lingeibuka tena. Yule mtu aliyeoka vitobosha alitaka kuanza kuniokea tena. Nilimwambia kiongozi mmoja mahususi, “Wewe nenda ukatatue hili. Unahitaji kumwelezea hili waziwazi. Akifanya tena, Nitakuwajibisha wewe!” Kukiwa na kazi nyingi sana za kufanya kanisani, kazi yoyote ingewafanya wawe na shughuli kwa muda. Kwa nini walikuwa wazembe kiasi hicho? Walikuja hapa kujinenepesha au kushiriki katika porojo tupu? Hapa si mahali pa mambo hayo. Baadaye, hapakuwa na habari zaidi kuhusu jambo hili. Mara tu baada ya Mimi kutoa agizo hilo, kiongozi huyo hakutoa ripoti zozote. Kwa vyovyote vile, hakuna mtu aliyeniletea vitobosha hivyo vidogo tena, jambo ambalo lilikuwa nafuu kubwa. Kulingana na tukio hili, je, tunaweza kusema viongozi hawa hawakuwa wakishughulikia kazi yao inayofaa? (Ndiyo.) Jambo hili si zito sana; kuna mengine mabaya zaidi.

Mara nyingi Mimi hutembelea makanisa fulani ili kuangalia huku na kule, kukutana na viongozi, kutoa maelekezo kwa ajili ya kazi fulani, na kutatua masuala fulani. Wakati mwingine, inanilazimu Nile chakula cha mchana katika makanisa haya, jambo ambalo huibua swali la ni nani atatayarisha mlo. Viongozi walikuwa wawajibikaji sana kiasi kwamba walimchagua mtu aliyedai kuwa mpishi. Nikasema, “Kama yeye ni mpishi au la si muhimu; cha muhimu ni kwamba Mimi hupendelea chakula cha kawaida. Ninapenda kuonja ladha halisi ya viungo. Chakula hakipaswi kuwa na chumvi nyingi, mafuta mengi, au cha kusisimua sana. Wakati wa baridi, Ninahitaji kula kitu kilicho na joto joto. Pia, chakula lazima kiive vizuri, kisiwe kibichi, na kiwe rahisi kumeng’enywa.” Je, Sikueleza kanuni hizi waziwazi? Je, zilikuwa rahisi kutimiza? Zilikuwa rahisi kukumbuka na rahisi kutenda. Mke afanyaye kazi nyumbani ambaye amepika kwa miaka mitatu hadi mitano angeweza kufahamu kanuni hizi na kuzitimiza. Kwa hivyo, hapakuwa na haja ya kusisitiza juu ya kumpata mpishi wa kunitayarishia mlo Wangu; mtu anayeweza kupika milo ya nyumbani angetosha. Hata hivyo, viongozi hawa walikuwa na “upendo” mwingi sana kiasi kwamba walisisitiza kumtafuta “mpishi” ili aandae mlo walipokuwa wakinikaribisha Mimi. Kabla ya mpishi kunipikia rasmi, viongozi walilazimika kufanya ukaguzi. Walifanyaje hili? Walimwagiza mpishi atengeneze bechi ya andazi la kinyunya na tambi zenye rojo, na wakamfanya akaange baadhi ya vyakula. Viongozi wote na wakuu wa vikundi mbalimbali walivionja, na wakaviona vyakula vyote kuwa vizuri kabisa. Mwishowe, walimwomba mpishi achukue kazi ya kunipikia. Tukiacha kando matokeo ya kuonja kwa viongozi na asili ya masuala yaliyohusika, hebu kwanza tuzungumzie chakula kilichotayarishwa na mpishi huyu. Mara ya kwanza Nilipoenda, mpishi alikaanga vyakula vichache, na kila mtu aliridhika kabisa. Mara ya pili, mpishi alitengeneza bechi ya maandazi ya kinyunya. Baada ya kuila ya kwanza, Nilihisi kuna kitu hakikuwa sawa—yalikuwa na ukali kiasi. Wengine walionizunguka pia walisema kwamba maandazi hayo ya kinyunya yalikuwa na ukali kiasi, na walihisi ndimi zao zilianza kuvimba. Hata hivyo, kwa kuwa maandazi ya kinyunya ndiyo yalikuwa chakula kikuu pekee, ilibidi niyamalize ingawa yalikuwa na ukali. Hakuna pilipili iliyoonekana kwenye kujazo, kwa hivyo Nilipuuza tu chochote kilichosababisha ukali huo na Nikamaliza mlo. Matokeo yake, mwili Wangu ulianza kupata mzio jioni hiyo. Sehemu nyingi kote mwilini Mwangu zilianza kuwasha bila kukoma, na ilibidi Niendelee kujikuna; Nilijikuna hadi Nilipotoa damu ndipo Nikahisi afueni. Niliwashwa kwa siku tatu kabla ya hisia hiyo kupungua polepole. Baada ya mzio huu, Niligundua kuwa pilipili ilikuwa imeongezwa bila shaka kwenye maandazi ya kinyunya; la sivyo, yasingekuwa na ukali kiasi hicho. Nilikuwa nimewajulisha wasiweke viungo vyenye ukali kama pilipili kwa kuwa Sikuweza kuvivumilia. Hata hivyo, waliongeza kiasi kikubwa ili kuridhisha ladha zao wenyewe, ambacho kilizidi kiwango cha kawaida; kulikuwa na hisia ya ukali ulipokuwa ukila maandazi ya kinyunya hizo. Mpishi hakuweza hata kupata uwiano sawa katika upishi wake, aliongeza pilipili ya kutosha kumpa mtu mzio. Baadaye, Nilimwambia, “Kamwe usiongeze tena viungo hivyo vyenye ukali. Siwezi kuvivumilia. Ikiwa kweli una ubinadamu wowote, usifanye hivyo tena. Ukijipikia mwenyewe, Sitaingilia kile unachokula. Hata hivyo, ukiwa unanipikia Mimi, basi usiongeze chochote. Fuata viwango Vyangu.” Je, angeweza kufanya hivyo? Je, viongozi hawakupaswa kushughulikia kazi hii? Kwa bahati mbaya, hakuna aliyejali, na hawakufanya kazi yoyote waliyopaswa kufanya. Wakati mmoja, mpishi alipokuwa karibu kupika tena, alichukua pilipili ili aiongeze kwenye chakula, na mtu aliyekuwa karibu alimwona na kumzuia. Chini ya usimamizi wake mkali, hakupata fursa ya kuiongeza. Viongozi hawakuweza kutatua tatizo dogo kama hili—wangeweza kufanya nini, basi? Mpishi alipokuwa akipika, walikuwa wepesi sana kukionja. Watu kadhaa walienda kukionja. Kilikuwa ni mlo wa kawaida tu wa nyumbani; kulikuwa na nini cha kuonja? Je, ninyi nyote ni wataalamu wa vyakula? Je, mnaelewa kila kitu ghafla baada ya kuwa viongozi? Je, mnaelewa kanuni za afya? Je, nyumba ya Mungu iliwapanga ninyi kufanya hivi? Ni lini Niliwakabidhi au kuwaagiza ninyi kuonja chakula kwa niaba Yangu? Ninyi mmekosa busara mno, hamna aibu hata kidogo! Mtu yeyote mwenye aibu kiasi hangelifanya jambo la waziwazi, la kuchukiza, na lisilo na busara kiasi hicho. Inaonyesha kwamba watu hawa hawana aibu hata kidogo—walinionjea Mimi chakula! Hamfuati wala hamtimizi kanuni zozote Nilizowaambia. Chochote kilicho na ladha nzuri kwenu na kinachopatana na ladha zenu, mnamwomba mpishi akipike. Je, huko ni kunipikia Mimi? Je, si ni kujipikia wenyewe? Je, hivi ndivyo mnavyotenda kama viongozi? Mkitumia kila fursa kujinufaisha, kutafuta njia za mkato, na kujaribu kujipendekeza Kwangu—ikiwa mnataka kujipendekeza Kwangu, msinidhuru! Je, huku si kukosa maadili? Je, si ni kuwa na nia zisizofaa? Hawana aibu na wana nia zisizofaa, lakini bado walidhani kwamba walikuwa waaminifu sana! Je, jambo lolote kati ya haya waliyofanya ndilo viongozi wanapaswa kufanya kweli? (Hapana.) Hakuna walichofanya kilichokuwa na viwango vyovyote. Hawakujua hata ni chakula gani chenye afya au kisicho na afya, lakini walidhani wangeweza kuja hapa na kufanya kazi ya wataalamu wa afya na chakula kwa ajili Yangu! Ni nani aliweka sharti kwamba ni lazima mfanye ukaguzi linapokuja suala la kunipikia? Je, kanisa lina agizo hili? Je, nyumba ya Mungu ilifanya mpango huu? Mianya mingi sana ilijitokeza katika vipengele mbalimbali vya kazi ya kanisa, watu wengi sana walikuwa na kutoelewa kumhusu Mungu na hawakuelewa ukweli hata kidogo, lakini hamkushughulikia mambo hayo. Badala yake, mliweka juhudi zenu katika eneo dogo kama jikoni, mkitimiza “wajibu” wenu. Ninyi ni viongozi wa uwongo hasa, ninyi ni wanafiki! Mlikuwa mbele Yangu kabisa mkikagua mambo—mlielewa nini? Mliuliza maoni Yangu? Mlikuwa mkieleza wazo lenu au Langu? Kama mngekuwa mkieleza wazo Langu, na Ningewaomba ninyi mliwasilishe, basi kile mnachokuwa mkifanya kingekuwa sahihi. Lingekuwa ni jukumu lenu. Ikiwa mngekuwa mkieleza wazo lenu na si Langu, na mkasisitiza kuwalazimisha wengine wasikilize na kulikubali, asili ya jambo hili ni ipi? Niambieni, je, Mimi Singechukizwa na hili? Nilikuwa pale pale, nao hawakutumia neno hata moja kuniuliza ni vitu gani Ninavyokula au mahitaji Yangu ni yapi—walifanya tu maamuzi bila idhini Yangu, na wakatoa amri kiholela bila Mimi kujua. Je, walikuwa wakijaribu kuniwakilisha Mimi? Hawa ni viongozi wa uwongo wanaofanya mambo maovu ovyoovyo, wakijifanya kuwa wa kiroho, wakijifanya kuzingatia mzigo wa Mungu, na wakijifanya kuelewa ukweli, na wakifanya tu mambo ya kinafiki. Je, huku si kupita kiasi vya kutosha? Je, tayari si ni jambo la kuchukiza na la kudharaulika sana? (Ndiyo.) Je, mmepata utambuzi wowote? Mmejifunza masomo yoyote kutokana na hili? Kila mojawapo ya mambo haya ni la kuchukiza zaidi kuliko lililopita, na kuna lingine ambalo ni la kuchukiza hata zaidi.

Wakati huu wa baridi, mtu mwenye moyo mwema alinunulia koti “zuri” la manyoya ya bukin. Uzuri wake haukuwa katika rangi au mtindo wa koti bali katika bei yake ya juu na ubora wa hali ya juu; lilikuwa ni kitu cha thamani. Kuna msemo miongoni mwa wasioamini, “Unyoya wa bukini uliotumwa kutoka umbali wa maili elfu: zawadi inaweza kuwa ndogo, lakini hisia ni kubwa.” Siyo tu kwamba koti hili lilibeba hisia, bali kwa kweli lilikuwa ghali sana. Kabla ya kuliona koti, tayari Nilikuwa nimesikia kwamba lilikuwa zuri na jekundu, lenye muundo mzuri, na lilikuwa nene lilipoguswa. Nilikuwa nimesikia kulihusu, kwa hivyo bila shaka baadhi ya watu walikuwa wameliona tayari—yaani, watu wengi walikuwa wameliona, wakalikadiria ukubwa, na kulichunguza kwa karibu, wakisema mambo kama, “Ninaijua chapa hii,” “Rangi ni nzuri, ni zuri kweli!” “Baada ya wewe kuliona, lilete nilitazame,” na hivyo tu habari zilienea. Sijui ilichukua muda gani kwa habari hizi kufika masikioni Mwangu, na Mimi kupata habari kidogo kulihusu. Je, ninyi mnaweza kuona tatizo hapa? Bila Mimi kuliona koti, tayari lilikuwa limeonwa, likapitishwa huku na kule, na kuonyeshwa na watu wengine wengi. Je, hili si tatizo? Je, watu wanaweza kutazama, kugusa, na kuonyesha vitu Vyangu kiholela? (Hapana.) Je, ni vitu vya nani ambavyo watu wanaweza kugusa na kutazama kiholela? (Hakuna mtu angetaka hili litokee, na hakuna anayepaswa kufanya hivi.) Basi, je, Vyangu havipaswi kuwa na mipaka hata zaidi? Watu wengine husema, “Kwa nini viwe na mipaka? Wewe ni mtu mashuhuri. Je, maisha ya faragha ya watu mashuhuri na maarufu hayafichuliwi kila wakati? Wanapocheza michezo, wanapopata matibabu ya urembo, wanaposhirikiana na nani, wanapovaa chapa gani—je, mambo haya yote hayaanikwi? Kwa nini Vyako visianikwe?” Je, Mimi ni mtu mashuhuri? Mimi si mtu mashuhuri, na wewe si shabiki Wangu. Wewe ni nani? Wewe ni mtu wa kawaida, kiumbe aliyeumbwa, na mwanadamu mpotovu. Mimi ni nani? (Mungu.) Mimi si mtu wa umma; Sina wajibu wa kukufichulia kila kitu, kukuripotia kila kitu, au kukujulisha kuhusu kila kitu. Basi, kwa nini unagusa kitu kilicho Changu? Je, si kufanya hivyo si jambo la kuchukiza? Je, Nilikuagiza wewe kutazama na kufanya ukaguzi wa kitu hiki Changu? Hapana. Lakini watu wengine walithubutu kukichukua na kukitazama kiholela kwa namna hii ya ujasiri, na hata kukipitisha huku na huko. Nani alikupa haki ya kukipitisha? Je, huu ni wajibu wako? Ikiwa humwamini Mungu, basi sisi hatujuani. Ni kwa sababu unamwamini Mungu ndiyo maana Ninajua wewe ni nani, lakini Sijui hali ya familia yako, maisha ya kila siku, au hali yako ya kifedha ikoje, na Sijali kujua. Je, sisi ni wandani wa karibu? Mimi si rafiki yako wa karibu, mwandani, au mwenzako. Hatufahamiani, na hatujafikia hatua ambapo kila kitu Changu kinapaswa kuwa wazi ili ukitazame. Je, wewe ungeniruhusu Mimi nitazame vitu vyako vyote, na kuvionyesha kwa kila mtu avione na aviguse? Hata unapoleta kitu nyumbani kutoka sokoni, kinahitaji kuoshwa mara kadhaa ili kuua viini! Je, vitu ambavyo watu wengine wamevigusa kiholela si vya kuchukiza? Kwa nini hujioni kama mtu wa nje? Ni nani aliyekuagiza kukagua koti Langu? Je, Ninakuamini? Je, umeosha mikono yako iwe safi kabla ya kuligusa koti Langu kiholela? Je, Sitachukizwa na wewe? Je, unaelewa hili wazi? Kwa nini huna aibu kiasi hicho? Umekosa busara sana! Umemwamini Mungu kwa miaka kadhaa na umesikia mahubiri mengi sana; imekuwaje ukose hata busara kidogo? Kufungua kiholela matoleo ya Mungu, kugusa kiholela nguo Zake, vitu vilivyokuwa Vyake—hili ni tatizo la aina gani? Ninapoona kwamba vifungashio vya vitu hivi vimefunguliwa na kutupwa, Nitakosaje kukasirika? Ninachukizwa na mambo haya, na Ninawachukia sana watu hawa. Sitaki kuwaona tena, na kwa hakika Sitaki kushirikiana na watu hawa ambao ni wabaya kuliko nguruwe na mbwa! Kumbukeni, kila mtu ana heshima yake, na Mimi nina heshima zaidi. Usijihusishe na vitu vilivyo Vyangu; la sivyo, Nitakukirihi na kukuchukia sana!

Kwa nje, viongozi wa uwongo huenda wasitende maovu makubwa au kuwa wahalifu waovu waziwazi. Hata hivyo, jambo la kuchukiza zaidi kuwahusu ni kwamba wanaweza kuona kuna kazi halisi ya kufanywa lakini hawaifanyi, wanajua vizuri sana kwamba hawawezi kutatua masuala lakini hawatafuti ukweli, wanawaona watu waovu wakisababisha usumbufu lakini hawawashughulikii, na badala yake wanashughulikia tu mambo ya jumla ya nje. Wanafuatilia kwa karibu na kushughulikia kwa umakini mkubwa masuala ya kando na mambo madogo, lakini hawafanyi kazi yoyote inayohusiana na kuingia katika uzima kwa watu wateule wa Mungu, au kujali kuhusu mambo mbalimbali yanayopingana na kanuni za ukweli. Badala yake, wanafanya tu kazi isiyohusiana na ukweli. Hawa ni viongozi wa uwongo hasa. Viongozi wa uwongo hawajui kabisa kanuni za ukweli zinazohusika katika vipengele mbalimbali vya kazi ya kanisa. Wakipimwa dhidi ya kanuni na viwango vya viongozi na wafanyakazi, viongozi wa uwongo ni wajinga na wapumbavu. Haijalishi mazito yanayotokea katika kazi ya kanisa ni mazito vipi, viongozi wa uwongo hawawezi kuyaona au kuyatatua hata yakitokea mbele ya macho yao, na walio juu wanapaswa kuja na kutatua matatizo hayo wenyewe. Je, si watu hawa ni viongozi wa uwongo? (Ndiyo.) Kwa kweli wao ni viongozi wa uwongo. Kwa mfano, katika kazi ya maandishi ya kanisa, ni vitabu vipi vinavyopaswa kusahihishwa na vipi vinavyopaswa kutafsiriwa—hizi ni kazi muhimu kwa kanisa. Je, kuna kanuni zozote kuhusu jinsi ya kusahihisha na kutafsiri vitabu? Kazi hii ina kanuni kabisa, imejikita sana katika kanuni, na inahitaji sana ushirika na mwongozo maalum; lakini viongozi wa uwongo hawawezi kufanya kazi hii. Wanapowaona ndugu na dada wakiwa na shughuli na wajibu wao, wao husema kwa unafiki, “Kazi ya maandishi na kazi ya kutafsiri ni muhimu hasa. Mnapaswa kuweka mioyo yenu katika kufanya kazi hii vizuri, na nitatatua masuala yoyote mliyo nayo.” Mtu anapouliza swali kwa kweli, viongozi hawa wa uwongo husema, “Sielewi jambo hili. Mimi ni mlei katika kutafsiri lugha za kigeni. Mwombeni Mungu na mtafuteni Yeye.” Mtu anapouliza swali lingine, akiuliza, “Hatuwezi kupata watu wanaofaa kutafsiri lugha fulani, tufanye nini kulihusu?” viongozi wa uwongo hujibu, “Mimi ni mlei katika jambo hili. Lishughulikieni ninyi wenyewe.” Je, kusema hivi kunaweza kutatua tatizo? Wanatafuta kisingizio na kufunika ukweli kwamba hawafanyi kazi yao, wakisema, “Mimi ni mlei; sielewi taaluma hii,” na hivyo wanakwepa tatizo wanalopaswa kulitatua. Hivi ndivyo viongozi wa uwongo hufanya kazi. Mtu anapouliza swali, viongozi wa uwongo husema, “Mwombeni Mungu na mtafute kutoka Kwake; sielewi taaluma hii, lakini ninyi mnaelewa.” Hili linaweza kuonekana kama unyenyekevu, kwani wanakiri kwamba hawawezi na hawaielewi taaluma, lakini kwa kweli, hawawezi kutekeleza kazi ya uongozi hata kidogo. Bila shaka, kuwa kiongozi si lazima kumaanishe kwamba anahitaji kuelewa taaluma ya kila aina, lakini anapaswa kushiriki waziwazi kanuni za ukweli zinazohitajika kutatua matatizo, bila kujali matatizo hayo yanahusiana na taaluma ya aina gani. Maadamu watu wanaelewa kanuni za ukweli, matatizo yanaweza kutatuliwa ipasavyo. Viongozi wa uwongo hutumia “Mimi si mtaalamu katika hili; sielewi taaluma hii” kama sababu ya kuepuka kushiriki kanuni za ukweli za kutatua matatizo. Huku si kufanya kazi halisi. Ikiwa viongozi wa uwongo daima wanatumia “Mimi si mtaalamu katika hili; sielewi taaluma hii” kama sababu ya kuepuka kutatua matatizo, basi hawafai kwa kazi ya uongozi. Jambo bora wanalopaswa kufanya ni kujiuzulu na kumwacha mtu mwingine achukue nafasi yao. Lakini, je, viongozi wa uwongo wana busara ya aina hii? Je, wataweza kujiuzulu? Hawataweza. Hata wanafikiri, “Kwa nini wanasema sifanyi kazi yoyote? Ninafanya mikutano kila siku, na nina shughuli nyingi kiasi kwamba siwezi hata kula kwa wakati, na ninapata usingizi mchache. Ni nani anayesema matatizo hayatatuliwi? Ninafanya mikutano na kushiriki nao, na ninawatafutia vifungu vya maneno ya Mungu.” Tuchukulie kwamba unamwuliza, “Mtu alisema hawezi kupata watafsiri wanaofaa katika baadhi ya lugha. Unatatua vipi tatizo hili maalum?” Atasema, “Niliwaambia kwamba sielewi taaluma, na nikawaambia wajadiliane na kulishughulikia wenyewe.” Kisha unamwuliza, “Tatizo hili linahusisha matumizi ya matoleo na maendeleo ya kazi ya kanisa. Hawawezi kufanya maamuzi wenyewe, wanakuhitaji wewe utoe mwelekeo na utafute kanuni za ukweli ili kulitatua. Je, ulifanya hivi?” Atajibu: “Sikufanyaje? Sijachelewesha kazi yoyote. Ikiwa hakuna mtu wa kutafsiri lugha hiyo, basi watafsiri tu lugha nyingine!” Unaona, viongozi wa uwongo hawawezi kufanya kazi halisi na bado wanatoa visingizio chungu nzima. Ni jambo la aibu na la kuchukiza kweli! Ubora wako wa tabia ni duni sana, huelewi taaluma zozote, na unakosa ufahamu wa kanuni za ukweli zinazohusika katika kila kipengele cha kazi ya kitaaluma—kuna faida gani ya kuwa nawe kama kiongozi? Wewe ni mjinga tu na mtu asiyefaa! Kwa kuwa huwezi kufanya kazi yoyote halisi, kwa nini bado unatumika kama kiongozi wa kanisa? Umekosa busara kabisa. Kwa kuwa unakosa kujielewa, unapaswa kusikiliza maoni kutoka kwa watu wateule wa Mungu na utathmini kama unafikia viwango vya kuwa kiongozi. Na bado, viongozi wa uwongo hawafikirii kamwe mambo haya. Bila kujali ni kiasi gani cha kazi ya kanisa imecheleweshwa, na ni hasara kiasi gani imesababishwa kwa kuingia katika uzima kwa watu wateule wa Mungu wakati wa miaka yao mingi ya kutumika kama viongozi, hawajali. Hii ndiyo sura mbovu ya viongozi wa uwongo hasa.

Fikirieni jinsi viongozi na wafanyakazi wanavyoshughulikia kazi yao—je, inalingana na kile ambacho Nimewaambia hivi punde? Je, kuna wowote wasiofanya kazi halisi, na, je, unaweza kuwatambua kuwa ni viongozi wa uwongo? Ukiwatambua kuwa ni viongozi wa uwongo, kuanzia leo na kuendelea hupaswi kuwachukulia tena kama viongozi; unapaswa kuwachukulia kama mtu mwingine yeyote. Hii ndiyo kanuni sahihi ya utendaji. Wengine wanaweza kujiuliza, “Je, hili linamaanisha kuwabagua, kuwadharau, au kuwatenga kwa sababu wao ni viongozi wa uwongo?” Hapana, haimaanishi hivyo. Hawawezi kufanya kazi halisi, na wanaweza tu kusema maneno na mafundisho fulani na maneno matupu fulani ili kukudangaya usipate kitu cha thamani. Hili linakuambia ukweli mmoja, ambao ni kwamba wao si viongozi wako. Huhitaji kuomba maelekezo yao kwa tatizo au ugumu wowote unaokumbana nao katika kazi yako. Ikilazimu, ninyi mnaweza kuwaruka kwa kuliripoti kwa walio juu na kushauriana na walio juu jinsi ya kulishughulikia na kulitatua. Nimewafundisha ninyi njia ya utendaji, lakini jinsi mnavyotenda ni juu yenu. Sikuwahi kusema kwamba viongozi wote wameamriwa kimbele na Mungu, kwamba ni lazima uwasikilize na kuwatii, na kwamba ni lazima uwasikilize hata kama unawatambua kuwa ni viongozi wa uwongo. Sikuwahi kukuambia hivyo. Ninachoshiriki sasa ni jinsi ya kuwatambua viongozi wa uwongo. Unapomtambua mtu kuwa ni kiongozi wa uwongo, unaweza kukubali na kutii kile anachosema ikiwa ni sahihi na kinalingana na ukweli. Hata hivyo, ikiwa hawezi kutatua tatizo, na anaongopa na kukudangaya usipate thamani kamili, na kuathiri maendeleo ya kazi, basi si lazima ukubali uongozi wake. Ikiwa ninyi wenyewe mnaweza kufahamu kanuni, basi mnapaswa kutenda kulingana nazo. Mkiwa hamwezi kufahamu, mna mashaka, au hamna uhakika wa kanuni, basi mnapaswa kutafuta ukweli na kujadiliana ili kushughulikia tatizo. Mkiwa bado hamwezi kufanya uamuzi baada ya kujadiliana, liripotini tatizo kwa Walio juu na mshauriane nao kulihusu. Hizi zote ni njia nzuri za kushughulikia matatizo—hakuna magumu yasiyoweza kutatuliwa.

Tumalizie ushirika wetu hapa leo. Kwaherini!

Januari 16, 2021

Inayofuata: Majukumu ya Viongozi na Wafanyakazi (4)

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp