28. Jinsi ya Kuuchukulia Wajibu Wako

Na Zhongcheng, Uchina

Mwenyezi Mungu anasema, “Mahitaji ya msingi ya imani ya mtu kwa Mungu ni kuwa ni sharti awe na moyo mwaminifu, na kwamba ajitolee mwenyewe, na kutii kwa kweli. Kile kigumu sana kwa mwanadamu ni kupeana mwili wake ili abadilishe na imani ya kweli, ambapo kupitia hii anaweza kupata ukweli mzima, na kutimiza wajibu wake kama kiumbe wa Mungu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Mafanikio au Kushindwa Kunategemea Njia Ambayo Mwanadamu Hutembea). “Wajibu ni kazi ambayo Mungu amewaaminia watu; ni misheni za watu kukamilisha. Hata hivyo, hakika wajibu si biashara yako unayoiendesha mwenyewe, wala si kitu kinachokusaidia ujitokeze katika umati. Watu wengine hutumia wajibu wao kama fursa za kujishughulisha na usimamizi wao wenyewe na kuunda vikundi; wengine kuridhisha matamanio yao; wengine kujaza utupu wanaohisi ndani yao; na wengine kuridhisha akili yao ya kuamini kwamba watabahatika, wakidhani kwamba mradi wanatimiza wajibu wao, watakuwa na sehemu katika nyumba ya Mungu na katika hatima nzuri ambayo Mungu amempangia mwanadamu. Mitazamo kama hiyo kuhusu wajibu si sahihi; inamchukiza Mungu na lazima itatuliwe kwa haraka(Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Baada ya kusoma haya, ningependa kushiriki kuhusu uzoefu wangu.

Mnamo 2017, wajibu wangu kanisani ulikuwa wa uandishi. Baadaye, kiongozi wa kanisa alipanga kwamba Ndugu Lin afanye kazi nami na akaniambia nihakikishe kwamba nitamsaidia. Nilikubali kwa furaha, nikiwaza, “Nimesikia kwamba Ndugu Lin anapenda sana kuandika makala na yeye ni hodari sana. Ikiwa anaweza kuelewa kanuni haraka, hakika tutazidi kupata mafanikio katika kazi ya timu yetu. Kiongozi atadhani kwamba nina uwezo na atanithamini sana, kwa hivyo sina budi kumsaidia kadri niwezavyo.” Nilimpa Ndugu Lin kanuni na vifaa vyote husika ambavyo nilikuwa nimemkusanyia ili avisome ili apate kuelewa kila kitu alichohitaji kujua haraka iwezekanavyo. Alipogonga mwamba katika kazi yake nilimsaidia kuchambua msururu wa mawazo, huku nikimpa mifano na marejeo kiasi. Baada ya muda kidogo, alielewa baadhi ya kanuni, na hati ambazo aliziandika zilikuwa bayana na za vitendo. Kumwona akifanya maendeleo ya haraka sana kulinifurahisha sana. Alikuwa ameyaelewa mambo haraka sana, nilifikiri kwamba alikuwa na uwezo! Timu yetu ilianza kuwa na ufanisi zaidi na kazi yangu ilipunguka sana. Nilifikiria kwamba baada ya Ndugu Lin kupata mafunzo kwa muda zaidi, tutapata matokeo bora zaidi katika wajibu wetu.

Siku moja, kiongozi alisema kwamba kulikuwa na kanisa lililohitaji kwa haraka mtu atakayeandika hati, na kwa kuwa Ndugu Lin alikuwa hodari wa kufanya hivyo na mwaminifu katika kazi yake, alitakiwa kuhamishwa katika kanisa hilo ili kuchukua kazi yao ya uandishi. Nilishtuka niliposikia hayo, nikiwaza, “Ati nini? Unamhamisha? Huwezi kufanya hivyo. Nimetia juhudi nyingi katika kumfahamisha kazi na kanuni, na ndiyo kwanza ameanza kuonyesha matumaini kiasi tu kakatika timu. Akihamishwa hivi sasa, kazi yetu bila shaka itaathirika. Kisha watu watanionaje? Je, watasema kwamba sina uwezo? Nilikasirika zaidi nilipokuwa nikifikiri kuhusu hayo. Kiongozi alisema kwamba baada ya Ndugu Lin kuhamishwa, nitaweza kumfundisha mtu mwingine. Sikusema lolote, lakini nilikuwa nikipinga wazo hilo. Niliwaza, “Unasema hivyo kana kwamba si kitu. Unafikiri kumfundisha mtu ni rahisi sana? Kunahitaji muda mwingi sana na bidii! Zaidi ya hayo, baada ya Ndugu Lin kuhamishwa, jukumu lote litakuwa langu tena. Kuna shughuli nyingi kwa sasa, kwa hivyo mtu mmoja hodari akiondoka, kazi yetu bila shaka itaathirika sana.” Kadiri nilivyozidi kufikiria hilo, ndivyo nilivyozidi kupinga jambo hilo. Siku mbili baadaye, kiongozi aliniagiza niandike tathmini ya Ndugu Lin. Niliwaza, “Nafaa kuzingatia udhaifu wake na jinsi anavyoonyesha upotovu badala ya sifa zake nzuri. Labda kiongozi hatamhamisha, basi.” Nilihisi mwenye hatia kidogo baada ya kumaliza tathmini yangu, na nikajiuliza iwapo nilikuwa mdanganyifu. Lakini baadaye niliwaza kwamba nilikuwa nikifikiria tu kazi ya timu. Kwa hivyo, nilimkabidhi kiongozi tathmini yangu. Siku chache zilipita bila majibu yoyote kutoka kwa kiongozi, na nilianza kuhisi wasiwasi, nikifikiri, “Je, labda hajaiona na bado atamhamisha Ndugu Lin? Hapana, siwezi kukaa tu. Lazima nifikirie njia ya kumzuia.” Nilijaribu kujua maoni yake vizuri, kwa kumuuliza Ndugu Lin, "Je, unaonaje ukiambiwa uchukue wajibu wa uandishi wa kanisa lingine?” Alisema bila kusita, “Nitatii mipango ya kanisa. Niko tayari kwenda.” Nilijibu upesi, “Unapowajibikia kazi ya uandishi, ni muhimu kuelewa kanuni na kuwa na uwezo. Bila hayo, maendeleo ya kazi hakika yatazuiwa. Naona ni bora uendelee kufanya wajibu wako hapa.” Kwa mshangao wangu, Ndugu Lin hakuathirika hata kidogo, lakini alisema tu kwa matumaini, “Nafasi ikijitokeza, niko tayari kwenda na kumtegemea Mungu.” Nilisikitika kwamba sikuwa nimefanikisha lengo langu, na nilihisi kwamba alinivunja moyo. Wakati mmoja niliona kwamba hati aliyoshughulikia ilikuwa na matatizo, na sikuweza kujizuia kumkasirikia na kumkaripia. Wakati huo, kila nilipofikiri kuhusu Ndugu Lin kuhamishwa, nilihangaika sana. Sikuweza kuhisi utulivu wowote katika kazi yangu na nilikanganyikiwa. Sikuwa pia na utambuzi wa maswala yoyote katika kazi. Nilikuwa kila mara nikitunduwaa. Niliteseka sana. Nilimwomba Mungu na kumsihi Aniongoze ili nijijue.

Kisha nikasoma maneno haya kutoka kwa Mungu: “Watu mara nyingi hawautii ukweli katika vitendo, mara nyingi wao huupuuza ukweli, na mara nyingi wanaishi ndani ya tabia potovu ya kishetani yenye ubinafsi na ya aibu, wakilinda heshimu yao, sifa zao, hadhi yao, na masilahi yao binafsi. Hawajapata ukweli. Kwa sababu hii, wewe umefadhaika sana, umesumbuka sana, na umejizuia sana(“Uingiaji Katika Uzima Lazima Uanze na Uzoefu wa Kutenda Wajibu wa Mtu” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). “Ni kiwango kipi ambacho kulingana nacho matendo ya mtu yanaonwa kuwa mema au mabaya? Inategemea na iwapo katika fikira, maonyesho, na matendo yako, una ushuhuda wa kutia ukweli katika vitendo na wa kuishi kwa kudhihirisha uhalisi wa ukweli au la. Ikiwa huna uhalisi huu au huishi kwa kudhihirisha hili, basi bila shaka wewe ni mtenda maovu. Je, Mungu anawatazamaje watenda maovu? Fikira zako na matendo ya nje hayashuhudii kwa Mungu, wala hayamwaibishi Shetani au kumshinda; badala yake, yanamwaibisha Mungu, na katika kila kitu ni ishara za kumfanya Mungu aibike. Humshuhudii Mungu, hujitumii kwa ajili ya Mungu, na hutimizi jukumu na wajibu wako kwa Mungu lakini badala yake unatenda kwa ajili yako. Ni nini maana ya ‘kwa ajili yako’? Kwa ajili ya Shetani. Kwa hiyo, mwishowe Mungu atasema, ‘Tokeni Kwangu, ninyi ambao hutenda udhalimu.’ Machoni pa Mungu, matendo yako hayajakuwa mema lakini badala yake yamekuwa matendo mabaya. Hakuna thawabu. Mungu hakukumbuki. Je, huu si utupu?(“Mpe Mungu Moyo Wako wa Kweli, Na Unaweza Kupata Ukweli” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Nilipokuwa nikitafakari maneno ya Mungu, niligundua kwamba Mungu huamua ikiwa watu wanafanya mema au mabaya si kwa kuzingatia iwapo wanajitumia kijuujuu, wanateseka kiasi gani, au wanalipa gharama kiasi gani, lakini hasa kwa kuangalia nia za watu na ikiwa matendo yao ni kwa ajili ya Mungu, au kwa ajili yao wenyewe, na ikiwa wanatenda ukweli. Kweli. Nilitafakari juu ya hali yangu kwa kipindi hicho na nikaona kwamba juhudi yangu ya kumsaidia Ndugu Lin kufahamu kanuni haraka haikuwa kwa ajili ya kazi ya kanisa. Nilitaka tu kuboresha ufanisi wa timu kupitia kwake, ili nionekane kuwa mzuri. Nilipoona kwamba alikuwa karibu kuhamishwa, nilihofia kwamba kazi ya timu itaathirika, kwamba sifa na hadhi yangu vitapata madhara, kwa hivyo nilipoandika tathmini yangu nilisisitiza kwa makusudi makosa yake, na kujaribu kumpotosha kiongozi. Nilisema hata mambo fulani hasi ili kukomesha shauku yake ya wajibu. Je, huko kulikuwaje kutenda ukweli na kufanya wajibu wangu? Nilikuwa nikifanya wajibu wangu kwa ubinafsi, bila kuzingatia kazi ya kanisa kwa ujumla, lakini nilizingatia tu matokeo ya kazi ambayo niliwajibika, na ikiwa sifa na hadhi yangu vitaathirika. Nilikuwa pia mdanganyifu na nilizuia kazi ya kanisa ambayo kiongozi alikuwa amepanga. Ni mimi niliyekuwa nikikatiza kazi ya nyumba ya Mungu, na kutenda maovu na kumpinga Mungu! Nilipoona jinsi nilivyokuwa katika hali hatari, nilimwomba Mungu, “Ee Mungu, mimi ni mbinafsi sana na mwenye kustahili dharau. Nimekatiza kazi ya nyumba ya Mungu kwa ajili ya masilahi yangu. Mungu, ningependa kutubu Kwako.”

Kisha nikasoma haya katika maneno ya Mungu: “Usifanye mambo kwa ajili yako daima na usiyafikirie masilahi, hadhi na sifa yako mwenyewe kila wakati. Pia usiyafikirie masilahi ya mwanadamu. Lazima kwanza uyafikirie masilahi ya nyumba ya Mungu, na uyape kipaumbele. Unapaswa kuyafikiria mapenzi ya Mungu na uanze kwa kutafakari kama umekuwa mwenye najisi katika utimizaji wa wajibu wako au la, kama umefanya kila uwezalo kuwa mwaminifu, kama umefanya kila uwezalo kutimiza majukumu yako, na kufanya kadiri uwezavyo au la, na vile vile kama umefikiria wajibu wako na kazi ya nyumba ya Mungu kwa moyo wote au la. Lazima uyazingatie mambo haya. Yafikirie mara kwa mara, na itakuwa rahisi kwako kutekeleza wajibu wako(“Mpe Mungu Moyo Wako wa Kweli, Na Unaweza Kupata Ukweli” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Nilipata njia ya utendaji ndani ya maneno ya Mungu. Sikuwa na budi kurekebisha nia zangu katika wajibu wangu, kukubali uchunguzi wa Mungu, kuacha masilahi yangu, na kutetea kazi ya nyumba ya Mungu. Ndugu Lin alikuwa mwenye ubora mzuri wa tabia, na alitafuta ukweli alipokabiliwa na matatizo, kwa hivyo kama angekubali kazi katika kanisa lingine, hilo lingefaidi kazi ya nyumba ya Mungu. Angeweza pia kupata utendaji zaidi kwa njia hiyo, kwa hivyo nilipaswa kumuunga mkono. Baadaye, nilimtafuta kiongozi na nikamwambia kuhusu nia zangu za ubinafsi na za hila na nikatoa tathmini ya Ndugu Lin kwa haki na bila upendeleo. Aliishia kuhamishiwa katika kanisa lingine, na mwishowe nilihisi amani kidogo ndani yangu. Kutenda ukweli hutupa amani.

Wakati huo, nilidhani kwamba nilikuwa nimebadilika kidogo. Sikuwahi kufikiri kwamba nitakapokutana na hali kama hii, asili yangu ya kishetani ya ubinafsi na ya kustahili dharau ingejitokeza tena.

Msimu wa baridi wa mwaka wa 2018, mimi na Ndugu Chen tulikuwa tukifanya kazi pamoja kama viongozi wa timu. Tulifidiana udhaifu wetu, na kwa mwongozo wa Mungu, tulizidi kupata matokeo bora katika kazi yetu. Nilifurahia sana kufanya kazi na Ndugu Chen. Wakati mmoja baada ya mkutano, kiongozi alizungumza nami akasema kwamba timu nyingine ilihitaji msaada, na kwamba Ndugu Chen labda atahamishiwa. Nilihisi kwamba Ndugu Chen alikuwa na ubora mzuri wa tabia, alielewa ukweli haraka, na alikuwa na mwaminifu katika wajibu wake, kwa hivyo alisaidia sana katika kusogeza mbele kazi ya timu yetu. Iwapo ataondoka na kazi yetu iathirike, kiongozi atanionaje? Je, atafikiria kwamba sikuwa na uwezo katika kazi yangu? Sikutaka kabisa kumwona Ndugu Chen akiondoka, lakini kwa kuzingatia kazi ya kanisa, ilibidi nikubali. Kwa mshangao wangu, kiongozi huyo aliendelea kusema kwamba kulikuwa na hitaji lingine la haraka kanisani na alitaka Dada Lu, mshiriki mwingine wa timu, aende kusaidia. Nilipigwa na bumbuazi niliposikia hayo. Niliwaza, “Unamwondoa Dada Lu? Ndugu Chen anahamishwa, na sasa Dada Lu anaenda pia. Watu wawili muhimu katika timu yetu wataondoka, kwa hivyo kazi yetu hakika itaathirika. Haiwezekani! Siwezi kukuacha umchukue dada Lu.” Lakini baadaye wazo lilinijia akilini “Nikikataa katakata, je, kiongozi hatasema kuwa mimi ni mbinafsi?” Baadaye nilipendekeza dada mwingine ambaye hakuwa na ubora mzuri sana wa tabia. Baada ya kukagua kila kitu, kiongozi bado alihisi kuwa Dada Lu ndiye aliyekuwa chaguo bora, na akanisihi nishiriki na dada Lu juu ya mabadiliko haya ya wajibu. Nilisema kwamba nitafanya hivyo, lakini moyoni mwangu nilipinga wazo hilo kabisa. Baada ya hapo nilimweleza ndugu mwingine maoni yangu, nikilalamika juu ya kiongozi kutozingatia shida zangu, kuhamisha watu wawili muhimu kwa ghafla. Je, nlipaswa kufanyaje kazi yangu kama kiongozi wa timu? Niliongea kwa urefu, kisha ghafla nikagundua yale niliyokuwa nikiyasema hayakuwa sahihi. Je, sikuwa nikijaribu kumfanya ndugu huyu aniunge mkono na kutoa malalamiko yangu? Jambo hilo lilimkosea Mungu. Kadiri nilivyozidi kufikiria hayo, ndivyo nilivyozidi kuhisi vibaya. Nilikuja mbele za Mungu upesi katika maombi na nikatafakari juu yangu. Baada ya kuomba, nilifikiria ni kwa nini kila mara mtu aliye chini yangu alipohitaji kuhamishwa, nilipinga vikali, nikijaribu kila niwezalo kuzuia. Je, asili ya kweli iliyonisababisha mimi kutenda kwa njia hiyo ilikuwa gani?

Nilisoma maneno haya ya Mungu: “Wajibu ni kazi ambayo Mungu amewaaminia watu; ni misheni za watu kukamilisha. Hata hivyo, hakika wajibu si biashara yako unayoiendesha mwenyewe, wala si kitu kinachokusaidia ujitokeze katika umati. Watu wengine hutumia wajibu wao kama fursa za kujishughulisha na usimamizi wao wenyewe na kuunda vikundi; wengine kuridhisha matamanio yao; … Mitazamo kama hiyo kuhusu wajibu si sahihi; inamchukiza Mungu na lazima itatuliwe kwa haraka(Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). “Katika muktadha wa kazi leo, watu bado watafanya aina sawa ya mambo kama yale ya ‘hekalu kuwa kuu kuliko Mungu’. Kwa mfano, watu huona kutimiza wajibu wao kama kazi yao; wanaona kutoa ushuhuda kwa Mungu na kupigana na joka kubwa jekundu kama harakati ya kisiasa ya kulinda haki za kibinadamu, kwa ajili ya demokrasia na uhuru; wao hugeuza wajibu wao ili kutumia weledi wao kuwa ajira, lakini wanachukulia kumcha Mungu na kujiepusha na maovu tu kama kipande cha kanuni ya kidini ya kufuatwa; na kadhalika. Je, maonyesho haya kwa upande wa binadamu hasa hayako sawa na ‘hekalu ni kuu kumliko Mungu’? Isipokuwa tu kwamba miaka elfu mbili iliyopita, watu walikuwa wakiendeleza shughuli zao za kibinafsi katika hekalu linaloshikika, lakini leo, watu wanaendeleza shughuli zao za kibinafsi katika mahekalu yasiyogusika. Wale watu wanaothamini masharti huona masharti kuwa kuu zaidi kuliko Mungu, wale watu wanaopenda hadhi huona hadhi kuu zaidi kuliko Mungu, wale watu wanaopenda ajira zao huziona ajira hizo kuwa kuu zaidi kuliko Mungu na kadhalika—maonyesho yao yote yananifanya Mimi kusema: ‘Watu humsifu Mungu kuwa ndiye mkuu zaidi kupitia kwa maneno yao, lakini kwa macho yao kila kitu ni kikuu zaidi kuliko Mungu.’ Hii ni kwa sababu punde tu watu wanapopata fursa katika njia yao ya kumfuata Mungu ili kuonyesha vipaji vyao, au kuendelea na shughuli zao binafsi za kibiashara au ajira yao binafsi, wanakuwa mbali na Mungu na kufanya kwa bidii ajira wanayoipenda. Kuhusiana na kile ambacho Mungu amewaaminia, na mapenzi Yake, mambo hayo yote yametupiliwa mbali kitambo. Katika hali hii, ni nini tofauti baina ya watu hawa na wale wanaoendesha biashara zao katika hekalu miaka elfu mbili iliyopita?(Neno, Vol. 2. Kuhusu Kumjua Mungu. Kazi ya Mungu, Tabia ya Mungu, na Mungu Mwenyewe III).

Nilipokuwa nikizingatia maneno ya Mungu, nilipata ubayana zaidi juu ya kiini cha vitendo vyangu. Nilikuwa mpinzani na nilizuia kila wakati kiongozi alipomhamisha mtu kutoka katika timu yangu, hasa kwa sababu nilichukulia wajibu wangu kama biashara yangu. Kila mara niliwaona wale ndugu kama watu ambao nilikuwa nimewafundisha, kwa hivyo walipaswa kufanya wajibu wao ndani ya eneo la madaraka yangu, wakisogeza mbele kazi katika timu yangu, na hawakupaswa kuhamishwa. Mawazo yangu hayakuwa ya busara kabisa na yalikuwa upuuzi mtupu. Bila kujali wale ndugu walikuwa na ubora upi wa tabia au uwezo kiasi gani yote yaliamuliwa na Mungu kabla kwa ajili ya kazi Yake. Walipaswa kuwekwa mahali popote ambapo walihitajika katika nyumba ya Mungu. Hilo ni jambo lililoamuliwa. Lakini nilikuwa nikijaribu kuwadhibiti, na kuwachukulia kama zana za kunitumikia na kunifanyia kazi. Nilimpinga kila mtu ambaye alitaka kumhamisha mtu mwingine, na hata nilifanya uamuzi na kujaribu kuunda vikundi sirini. Je, nilikuwa na tofauti gani na Mafarisayo ambao walimpinga Bwana Yesu? Mafarisayo walichukulia hekalu kama eneo lao la mamlaka na hawakuwakubalia waumini waliache ili kumfuata Bwana Yesu. Walifanya juu chini kuwadhibiti waumini ili waweze kuhifadhi hadhi na mapato yao, na wakadai bila aibu kwamba waumini hao walikuwa wao. Kwa mintarafu yangu, nilikuwa nimewazuia kina ndugu chini ya udhibiti wangu, na sikutaka nyumba ya Mungu iwahamishe. Je, sikuwa nikitumia eneo langu la mamlaka kumpinga Mungu? Nilikuwa nikichukua njia ya mpinga Kristo, kumpinga Mungu, na nilikuwa nimeikosea tabia Yake! Wazo hili liliniogofya, na nilianza kuchukia tabia yangu ya kishetani ya ubinafsi na ya kustahili dharau. Nilifanya hima kumwomba Mungu kwa kutubu. Baada ya hapo nilienda kuongea na Dada Lu juu ya uhamishwaji wake, halafu nikazungumza na huyo ndugu niliyekuwa nimemdanganya, nikafanya ushirika na kuchambua asili na matokeo ya kile nilichokuwa nimesema ili kwamba awe na utambuzi fulani. Mwishowe nilipata amani kidogo.

Baada ya Dada Lu na Ndugu Chen kuhamishwa, Dada Li alifika kwenye timu. Alikuwa na ubora mzuri wa tabia na alikuwa mwepesi wa kuelewa mambo. Kazi ya timu haikucheleweshwa. Niliona kwa kweli kwamba kutekeleza wajibu wangu kwa manufaa ya nyumba ya Mungu, si kwa manufaa yangu, ndiyo njia halisi ya kupata baraka za Mungu. Mungu atapanga watu wanaofaa kwa kazi hiyo. Ataitetea kazi Yake. Siku moja, miezi mitatu baadaye, dada Lin aliporudi kutoka kwenye mkutano, aliniambia kuwa kanisa lililokuwa karibu lilikuwa likifanya kazi ya injili vizuri, na walihitaji sana watu wa kuwanyunyizia wageni. Kiongozi yule alipendekeza kwamba Dada Li achukue wajibu wa kunyunyizia. Nilihisi kutoridhika tena kidogo, lakini niligundua mara moja kuwa hali yangu ilikuwa mbaya. Nilikumbuka nyakati zote hapo awali ambapo nilikuwa nimepuuza masilahi ya nyumba ya Mungu kwa ajili ya sifa na hadhi yangu. Nilihisi vibaya sana, na mwenye hatia sana, na kisha nikakumbuka maneno haya ya Mungu: “Wajibu si shughuli yako ya faragha, na kwa kuutimiza hujifanyii jambo au kusimamia biashara yako ya kibinafsi. Katika nyumba ya Mungu, haijalishi unachokifanya, hushughulikii biashara yako mwenyewe; ni kazi ya nyumba ya Mungu, ni kazi ya Mungu. Lazima ukumbuke maarifa haya kila wakati na useme, ‘Hii siyo shughuli yangu mwenyewe; ninafanya wajibu wangu na kutimiza jukumu langu. Ninafanya kazi ya nyumba ya Mungu. Hii ni kazi ambayo Mungu aliniaminia na ninamfanyia Yeye. Hii siyo shughuli yangu ya faragha.’ Ikiwa unafikiri kwamba ni shughuli yako ya faragha, na uufanye kulingana na dhamira, kanuni na nia zako mwenyewe, basi utakuwa mashakani(Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Maneno ya Mungu yalieleza waziwazi hata zaidi kwamba wajibu wangu ni agizo la Mungu kwangu, si biashara yangu ya binafsi. Siwezi tu kufanya nitakavyo ili kukidhi masilahi yangu. Napaswa kuzingatia masilahi ya nyumba ya Mungu, kutafuta ukweli, na kufanya kile ambacho Mungu anahitaji. Huo pekee ndio mtazamo na mantiki ambayo kiumbe anapaswa kuwa nayo katika wajibu wake. Nilikuwa nikifikiria kila wakati juu ya masilahi yangu, na nilifanya mambo mengi yaliyohasiri masilahi ya nyumba ya Mungu na kumpinga Mungu. Nilijua kwamba sikufaa kuishi hivyo tena. Sikuwa na budi kuacha tamaa zangu za ubinafsi na kutenda ukweli. Nilipofikiria hili, nilihisi utulivu. Nilimwambia Dada Lin, “Kiongozi amepanga haya ili kufaidi kazi ya nyumba ya Mungu. Tunapaswa kuzungumza na Dada Li mara moja kuhusu mabadiliko haya katika wajibu wake. Hatuwezi kuathiri kazi ya nyumba ya Mungu.”

Kujifunza kuacha masilahi yangu mwenyewe katika wajibu wangu, kufikiria kazi ya nyumba ya Mungu, kujua nafasi yangu, na kuwa na dhamiri na mantiki kidogo yote yalitokana na kupitia hukumu na kuadibu kwa maneno ya Mungu.

Iliyotangulia: 27. Jinsi Mtu Anavyopaswa Kuchukulia Wajibu Wake

Inayofuata: 29. Toba ya Afisa

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp