Naja Kutofautisha Waziwazi kati ya Upendo na Chuki kwa Kupitia Uchungu wa Mateso

26/01/2021

Na Zhao Zhi, Jimbo la Hebei

Jina langu ni Zhao Zhi na mwaka huu nina umri wa miaka 52. Nimekuwa mfuasi wa Mwenyezi Mungu kwa muda wa miaka 14. Kabla ya kupata imani yangu nilifanya biashara; mara nyingi nilikuwa na shughuli za kuburudisha, kuwatumia watu zawadi, na kujuana. Kila mara nilikwenda katika sehemu za burudani kama sehemu za karaoke na kumbi za kamari. Mke wangu alikuwa akibishana nami kila mara juu ya hili na mwishowe aliishia kunitishia kuwa angenitaliki na kuondoka nyumbani kwetu. Wakati huo, nilikuwa nimenaswa kabisa kwenye tatizo hili na sikuweza kujinasua, na hata ingawa nilijitahidi kutunza familia yangu vizuri, singeweza kujinasua. Nilihisi kama maisha yalikuwa yenye taabu sana; nilikuwa mchovu. Mnamo Juni mwaka wa 1999, neema ya wokovu wa Mwenyezi Mungu ulitujia, na kupitia kusoma maneno ya Mungu na kuwa na ushirika na ndugu, mke wangu aligundua kuwa uovu wa ulimwengu na upotovu wa wanadamu ni hasa kwa sababu ya Shetani kutudhuru na kutuchezea. Alionyesha kuelewa hali yangu na alifungua moyo wake katika ushirika nami. Kupitia mwongozo wa maneno ya Mungu, pia niliona kwamba nilikuwa nikizamia katika jungu kuu la dhambi, na kwamba Mungu alikirihishwa na jambo hilo na kulichukia. Hata zaidi ya haya, niliona kwamba sikuwa nikitenda kama mwanadamu hata kidogo. Nilijuta na kuhisi mwenye hatia, na kwa hivyo niliamua mbele za Mungu kuwa mtu mpya. Kuanzia wakati huo, mimi na mke wangu tulimwomba Mungu na kusoma maneno Yake kila siku, na mara kwa mara tulikusanyika na ndugu kwa ajili ya ushirika. Muda si muda, mizozo kati yetu na dhiki ambayo tulikuwa tukihisi ilitawanyika kama wingu la moshi, na maisha yetu yakajaa amani na furaha. Nilikuwa nikifahamu kwa kina kuwa Mwenyezi Mungu alikuwa ameiokoa familia yetu wakati ilipokuwa karibu kuvunjika, na alikuwa ametuletea maisha mapya kabisa. Zaidi ya kujisikia mwenye shukrani nyingi, pia niliamua kimoyomoyo kudhabihu nafsi yangu nzima kulipiza neema ya Mungu. Baada ya hapo nilianza kutekeleza wajibu wangu na kushiriki injili kwa shauku ili watu zaidi waweze kupata wokovu ambao Mungu ametuletea katika siku za mwisho. Hata hivyo, serikali ya Chama cha Kikomunisti cha China inayomkana Mungu haiwaruhusu watu kumwabudu Mungu au kuchukua njia sahihi, na hasa haiwaruhusu watu kueneza injili au kuwa na ushuhuda kwa Mungu. Kwa sababu nilimwamini Mungu na kueneza injili, nilikamatwa na kuteswa na serikali ya CCP.

Ilikuwa siku ya majira ya kuchipua mnamo mwaka wa 2002. Mimi na ndugu mmoja tuliripotiwa kwa polisi na mtu mwenye nia mbaya tulipokuwa tukishiriki injili kijijini. Polisi walikuja mara moja na, bila kuhakikisha hali hiyo hata kidogo, walinitia pingu, wakanivuta hadi katika gari la polisi, na kunipeleka hadi kwenye kituo. Mara tu tulipoingia katika chumba cha mahojiano, kabla hata sijapata nafasi ya kujibu, afisa mmoja alinishambulia, akashika kola yangu, na kunizaba makofi kwa nguvu mara nyingi. Nilipatwa na kizunguzungu mara moja na kuanza kuona vimulimuli, na sikuweza kujizuia kujikwaa na kuanguka sakafuni kwa kutanguliza kichwa. Nilikuwa nikitokwa na damu mdomoni na kwenye pua na uso wangu ulikuwa ukiuma kwa uchungu. Alipogundua haya, polisi huyo mwovu alinipiga teke kwa ukali na kunighadhibikia kwa meno yaliyokerezwa, “Wewe baradhuli, usithubutu kujisingizia kwangu. Inuka!” Maafisa wengine wawili walikuja, waliniinua kwa mikono, na kunitupa upande mmoja, kisha wao watatu walianza kupiga makonde na mateke. Nilikuwa na maumivu yasiyoweza kuvumilika kote mwilini mwangu; Nilianguka sakafuni na sikuweza kuinuka. Walinitazama kwa sura katili, wakinikodolea macho jinsi chui-milia hutazama windo lake. Mmoja wao alinifokea, “Jina lako ni nani? Unatoka wapi? Kwa nini ulikuwa nyumbani kwa mtu huyo? Usipozungumza, utapata adhabu kali kutoka kwangu!” Nilimwomba Mungu kisirisiri, nikimwomba Aulinde moyo wangu ili niweze kukaa kimya mbele za Mungu, na kunipa imani na ujasiri, nisitishwe na vitisho vyao. Walipoona kwamba sikuwa nikizungumza, afisa mwenye sura ya kikatili alichukua kirungu cha umeme na kukipapatisha huko na huko usoni mwangu, na kukifanya kimakusudi kuchakarika. Kisha alinielekezea na kusema kwa kutisha, “Je, utazungumza au la? Ikiwa hutazungumza, nitakupitishia umeme hadi ufe.” Nilishtushwa kidogo na haya na kumwomba Mungu haraka. “Ee Mungu! Vitu vyote viko mikononi Mwako, pamoja na kundi hili la maafisa waovu. Bila kujali jinsi wanavyonitendea, ni kwa idhini Yako. Niko tayari kujisalimisha kwa maagizo na mipangilio Yako. Ni kwamba tu kimo changu ni kidogo sana na ninahisi dhaifu na mwepesi kutishwa. Tafadhali nipe imani na nguvu na unilinde ili nisije kuwa Yuda. Usiniruhusu nipoteze ushuhuda wangu mbele ya Shetani.” Baada ya kusali, kifungu cha maneno ya Mungu kilinijia akilini mwangu: “Ndani yetu tuna uzima wa Kristo Aliyefufuka. Bila shaka, hatuna imani mbele ya Mungu: Na iwe kwamba Mungu Atie imani ya kweli ndani yetu. Neno la Mungu ni tamu kweli! Neno la Mungu ni dawa yenye nguvu! Tilia aibu mapepo na Shetani! Kama sisi tutafahamu neno la Mungu tutakuwa na msaada na neno Lake litaokoa mioyo yetu kwa haraka! Linaondoa vitu vyote na kuweka yote kwa amani. Imani ni kama daraja moja la gogo la mti, wale ambao hushikilia maisha kwa unyonge watakuwa na ugumu katika kulivuka, lakini wale ambao wako tayari kujitolea wenyewe wanaweza kulivuka bila wasiwasi. Kama mtu ana mawazo ya uoga na ya kuogofya, wao wanadanganywa na Shetani. Ina hofu kwamba tutavuka daraja la imani ili kuingia katika Mungu(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 6). “Ni kweli!” Niliwaza. “Ninahisi hofu sana kwa sababu nimedanganywa na ujanja wa Shetani. Licha ya sura za kikatili za maafisa, kila kitu kiko mikononi mwa Mungu na Mungu ndiye tegemeo langu. Lazima nitegemee imani yangu na niegemee maneno ya Mungu ili kumshinda Shetani!” Kwa hivyo, nilikaa kimya, na alipoona kwamba sikuwa nikitamka hata neno moja, afisa huyo aliinua kirungu chake na kukidukua kwangu. Nilifunga macho yangu na kukereza meno yangu nikijiandaa kwa mateso ya maumivu makali, lakini cha kushangaza, ingawa kirungu kilidukuliwa kwangu tena na tena, sikuhisi chochote. Wote walidhani kuwa hilo lilikuwa jambo lisilo la kawaida na wakasema, kwa kukanganyikiwa, “Je, kwa nini hiki hakifanyi kazi leo? Lazima kimeharibika—jaribu kingine.” Kisha walileta kingine wanipitishie umeme nacho, lakini hicho pia hakikufanya kazi. Nilikuwa nikiguta kila mara moyoni mwangu, “Ee Mungu, asante! Umesikia maombi yangu na Unanilinda kisiri. Wewe ni mzuri sana, mwaminifu sana! Mungu, bila kujali nitakabili mateso ya kikatili ya aina gani siku zijazo, niko tayari Kukutegemea kwa moyo wangu wote. Nimeazimia kusimama kidete katika ushuhuda wangu!” Walipoona kuwa kidude chao cha umeme hakileti matokeo yoyote kwangu, bado hawakuwa tayari kuachia hapo, kwa hivyo walinitia pingu na kunifunga silisili, wakanivuta hadi katika gari la polisi, na kunipeleka hadi katika jengo la ghorofa mbili mbali na kijiji.

Tulipoingia ndani, afisa alitabasamu kwa ubaya na kusema kwa kutisha, “Unaweza kuona kwamba hakuna kitu hapa na hakuna mtu atakayegundua kamwe jengo hili. Sasa kwa kuwa uko hapa, ikiwa bado hutazungumza, itakuwa kifo chako. Utazikwa hapa, na hakuna mtu atakayejua. Fikiria mwenyewe—ikiwa wewe ni mwerevu, utatuambia kile tunachohitaji kukijua.” Nilijawa na hofu sana niliposikia hivyo. Kwa kweli sikuweza kufikiri ni nini hawa “Polisi wa watu” wenye sura za kuua waliosimama mbele yangu, ambao walitenda kama tu majambazi wa kuzimu, wangeweza kunitendea. Nilimwomba Mungu haraka moyoni mwangu, nikimwomba Anipe nguvu na azimio la kustahimili mateso ili niweze kuvumilia mateso ya ukatili ambayo yangekuja. Walipoona kwamba bado nilikataa kuzungumza, maafisa wawili kati yao walinivamia na kunivua nguo zangu zote, kisha wakanisimamisha upande mmoja. Mmoja wao alinielekezea kwenye pua yangu na kusema kwa kejeli, “Angalia hayo—kwa kweli hujui aibu.” Mwingine alianza kupekua nguo zangu ndani na nje kama mbwa mwenye njaa anayetafuta chakula. Aliishia kupata yuani 30 tu, kisha akazungusha kichwa chake na kufoka “Wewe ni maskini tu!” Huku akibimbirisha pesa hizo kwenye mfuko wake mwenyewe. Hili lilinifanya nighadhabike na nihisi chuki. Niliwaza, “Je, polisi hawa ‘wanawahudumia watu vipi’? Wao tu ni kikundi cha walaghai na majambazi ambao huwadhulumu watu na kuwanyanyasa watu wa kawaida. Kama leo singeyaona haya kwa macho yangu mwenyewe, sijui ni muda gani ningeendelea kudanganywa na uwongo wa CCP.” Kisha niligundua kuwa mapenzi mema ya Mungu yalikuwa chanzo cha kukamatwa kwangu siku hiyo; Mungu hakuwa akinifanya niteseke kwa kusudi, lakini badala yake haya yalikuwa yakifanyika ili niweze kuona waziwazi sura ya uovu ya CCP. Baada ya muda wa kama dakika nyingine 10, afisa mwingine alikuja na nyaya mbili za umeme na akiwa na tabasamu la kikatili usoni mwake, aliniashiria kwa kutishia na kusema, “Umetishika? Mwaka kabla ya uliopita kulikuwepo na mhalifu mwingine ambaye hakutaka kuzungumza, lakini hakuweza kuvumilia kupitishwa nguvu shoti ya umeme. Aliishia kutoboa siri zote. Nina uhakika kuwa tutakifungua wazi hicho kinywa chako!” Nilipoona kwamba wangenipitishia shoti za umeme, nilihisi chuki na hofu. Ikiwa aina hiyo ya mateso ingeendelea kwa muda mrefu, nilikuwa na uhakika kuwa ningekufa. Nilimwomba Mungu haraka: “Mungu, maafisa hawa waovu ni wakatili sana—ninaogopa kuwa sitaweza kushinda haya. Tafadhali nilinde na Unipe nguvu ili nisije kuwa Yuda na kukusaliti kwa sababu ya udhaifu wa mwili wangu.” Baada ya kusali, Mungu alinipa nuru ya kufikiria wimbo huu wa kanisa: “Kichwa changu kinaweza kupasuka na damu itiririke, lakini ujasiri wa watu wa Mungu hauwezi kupotea. Ushawishi wa Mungu umo moyoni, naamua kumwaibisha Shetani Ibilisi. Maumivu na shida vimeamuliwa kabla na Mungu, nitastahimili aibu ili kuwa mwaminifu Kwake. Kamwe sitamsababisha Mungu alie au kusumbuka” (“Natamani Kuiona Siku ya Utukufu wa Mungu” katika Mfuateni Mwanakondoo na Kuimba Nyimbo Mpya). “Ni kweli,” niliwaza. “Watu wa ufalme ni sharti wawe na uadilifu na uvumilivu wa mtu wa ufalme—kuwa na tamaa ya maisha na kuogopa kifo ni woga. Shetani anafikiria kipumbavu kwamba anaweza kunifanya nimsaliti Mungu kupitia mateso na kwa kufanya hivyo niharibu nafasi yangu ya kupata wokovu. Siwezi kabisa kuruhusu njama yake itimie, na siwezi kabisa kuruhusu jina la Mungu liweze kuaibishwa kwa sababu yangu.” Mara tu nilipofikiria haya yote, nilihisi mlipuko wa nguvu ndani yangu na nikapata ujasiri wa kukabiliana na mateso hayo.

Nilipokuwa tu nikiwaza haya yote, maafisa wawili walinishambulia, wakanigandamiza chini hadi kwenye sakafu kwa tumbo langu, kisha wakangandamiza kiti chini juu yangu. Maafisa wengine wawili walikuja, mmoja kwa kila upande wangu, kila mmoja akiponda wayo kwenye mojawapo ya mikono yangu. Ilisikika kama mikono yangu ilikuwa imepigiliwa msumari sakafuni—sikuweza kusonga hata kidogo. Polisi aliyekuwa na nyaya za umeme alitoa nyaya mbili kutoka katika kisanduku cha saketi na kufungia moja kwenye kidole cha mkono wangu wa kushoto, moja kwenye kidole cha mkono wangu wa kulia, kisha akawasha umeme katika kisanduku cha saketi. Wimbi la mkondo wa umeme papo hapo lilipitia katika kila neva mwilini mwangu; lilikuwa la kutia ganzi na la kuumiza na sikuweza kujizuia kupatwa na mkazo wa ghafla wa misuli katika mwili mzima. Ilikuwa ya kuumiza sana hadi nikapiga mayowe. Polisi waovu walisukuma ndara la sponji mdomoni mwangu. Walinitia mshtuo wa umeme mara nyingi kwa namna hiyo, na kusababisha maumivu kama hayo kiasi kwamba nilikuwa nimerowa jasho kabisa, na kabla ya muda mrefu lilikuwa likil0wa kwenye mavazi yangu yote, kana kwamba nilikuwa nimemwagiwa maji. Walipokuwa wakinitia mshtuo wa umeme, afisa aliendelea kuniambia kwa sauti kubwa, “Je, utazungumza au la? Nitakupitishia mshtuo wa umeme hadi ufe ikiwa hutazungumza! Haya ndiyo unayoyapata kwa ajili ya kutozungumza!” Nilikereza meno yangu kwa nguvu na kujilazimisha kuvumilia uchungu bila kutoa sauti. Walipoona haya, walianza kuendeleza umeme kwa muda mrefu zaidi. Mwishowe, nilihisi kuwa siwezi kustahimili tena na nilitaka tu kufa. Nilitumia kila wakia wa nguvu iliyosalia mwilini mwangu kuwasukuma maafisa hao wawili waliogandamiza kiti juu yangu kisha nikakigongesha kwa nguvu kichwa changu dhidi ya sakafu. Lakini kwa namna ya pekee, sakafu hiyo ngumu ya saruji ghafla ilisikika laini kama pamba, na bila kujali niligongesha kichwa changu kwa nguvu kiasi gani hapo, hakukuwa na athari. Wakati huo huo, mistari kadhaa kutoka kwa maneno ya Mungu ambayo ilikuwa imejitokeza mara nyingi katika ushirika awali ilinijia akilini: “Kuteseka kwa watu wengine hufikia kiwango fulani, na fikira zao hugeukia kifo. Huu si upendo wa kweli kwa Mungu; watu kama hao ni waoga, hawana ustahamilivu, wao ni wadhaifu na wasio na nguvu!(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Ni kwa Kupitia tu Majaribio ya Kuumiza Ndiyo Mnaweza Kujua Kupendeza kwa Mungu). “Hata ingawa miili yenu inateseka, mna neno la Mungu na mna baraka ya Mungu. Huwezi kufariki hata ukitaka: Je, unaweza kukubali bila malalamiko kutomjua Mungu na kutopata ukweli ukifa?(“Ni Kwa Kufuatilia Ukweli Tu Ndiyo Unaweza Kupata Mabadiliko Katika Tabia Yako” katika Kumbukumbu za Hotuba za Kristo). Maneno ya Mungu yalifanya kazi ya kumbusho njema kwangu kwamba nilitaka nife kwa sababu sikuweza kuvumilia mateso, na kwamba singekuwa nikimshuhudia Mungu, lakini ningekuwa nikimwaibisha na kumsaliti Mungu. Ingekuwa kukosa ujasiri, woga, na haingemwaibisha Shetani hata kidogo. Nuru ya Mungu iliniwezesha kugundua kuwa sakafu ghafla kusikika laini ilikuwa Mungu ananikomesha kisirisiri, ananilinda, na kutoniruhusu nife, kwa tumaini kwamba ningeweza kuwa shahidi katikati ya hali hii mbaya, na hivyo kumwaibisha Shetani na kuleta utukufu kwa Mungu. Kuona upendo wa Mungu na ulinzi Wake kulinitia moyo sana na nilifanya azimio kimoyomoyo: Bila kujali hawa polisi wabaya watanitesa jinsi gani, nitastahimili, na hata kama niko katika wakati wa kukaribia kufa, nitautumia vizuri na kuwa shahidi kwa Mungu, na sitamtamausha. Mwili wangu wote ulijawa na nguvu—nilikereza meno yangu na kujiandaa kupokea mateso zaidi ya kikatili ya umeme.

Walipoona kwamba bado sikuwa nikijisalimisha, maafisa walikasirika sana mpaka mishipa yao ilikuwa ikivimba. Walikuwa na mitazamo katili machoni mwao, walikuwa wakikereza meno yao na kufumba ngumi zao, wakionekana kana kwamba walikuwa wakitamani kuniangamiza. Mmoja wao, akiwa ameghadhibika kwelikweli, alinijia kwa vishindo na kukamata nywele zangu chache, akainua kichwa changu kwa nguvu, akaenda upande wa uso wangu na kunifokea kwa sura katili, “Wewe baradhuli, utazungumza au la? Ikiwa hutazungumza, nitachuna ngozi yako na kukuacha katika hali mahututi. Hilo ndilo utakalolipata kwa kutozungumza!” Kisha akaacha nywele zangu, na kumfokea polisi mwingine mwovu, “Mpe volteji ya kudhuru ya umeme!” Kwa ajili ya kutoweza kuhimili umeme huu wa volteji ya juu zaidi, nilizimia. Walinirushia maji baridi ili kunifufua, kisha wakaendelea na mateso yao. Baada ya mishtuo kadhaa zaidi nilikuwa kwenye maumivu yasiyovumilika mwilini mwangu mwote. Kwa kweli sikuweza kuvumilia zaidi na nilihisi kama ningeweza kufa wakati wowote. Katika shida hii, Mungu alinielekeza kufikiria wimbo huu wa kanisa: “Katika shida, uongozi wamaneno ya Mungu huupa nguvu moyo wangu; siwezi kushikilia jembe na kutazama nyuma. Ni nadra sana kuweza kukubali mafunzo ya ufalme na siwezi kabisa kukosa fursa hii ya kukamilishwa. Nikimwangusha Mungu, nitajuta maisha yangu yote. Nikimwacha Mungu nitahukumiwa na historia. … Moyo wangu unathamini ukweli tu na umejitolea kwa Mungu, kamwe sitaasi tena na kumfadhaisha Mungu. Nimeamua kumpenda Mungu na kuendelea kujitolea kabisa kwa Mungu na hakuna chochote au yeyote anayeweza kunizuia. Nami nitakuwa na ushuhuda wa kumtukuza Mungu bila kujali jinsi majaribu na dhiki yalivyo. Nitaishi maisha yenye maana kwa kuupata ukweli na ukamilishaji wa Mungu” (“Nimeamua Kujitolea Kabisa Kwa Mungu” katika Mfuateni Mwanakondoo na Kuimba Nyimbo Mpya). Niliwaza pia haya maneno ya Mungu: “Kama unayo pumzi moja tu, Mungu hatakuacha ufariki(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 6). Nilipoongozwa na maneno ya Mungu, moyo wangu dhaifu uliimarishwa tena. Nilijiambia, “Bila kujali ninyi kikundi cha pepo ni wakatili kiasi gani, mnaweza tu kuutesa mwili wangu na kufanya maisha yangu kuwa mabaya kuliko kifo, lakini hamuwezi kamwe, kubadilisha kabisa hamu yangu ya kumfuata Mungu. Kadiri mnavyozidi kunitesa, ndivyo ninavyozidi kufahamu waziwazi nyuso zenu za uovu, na ndivyo ninavyozidi kuwa thabiti katika azimio langu la kumfuata Mungu. Msithubutu kufikiria kuwa mnaweza kunifanya nimsaliti ndugu hata mmoja—hata ikiwa itamaanisha nitakufa leo, nitamridhisha Mungu mara hii moja!” Mara tu nilipokuwa tayari kudhabihu maisha yangu, mara nyingine tena nilishuhudia uweza wa Mungu na rehema Zake na utunzaji kwangu. Walinipitishia mshtuo wa umeme mara nyingi zaidi, na walipoona kwamba nilikuwa nikipatwa na mikazo hatari ya ghafla ya misuli mwilini mwote, hawakuthubutu kuendelea, wakiogopa kwamba ningekufa na wangelaumiwa. Lakini bado hawakuacha—waliniinua tena kutoka chini, wakiigeuza mikono yangu kwa nguvu nyuma ya mgongo wangu na kuifunga kwa kamba kwa kukaza. Ilikuwa imekazwa sana kiasi kwamba vifundo vya mikono yangu vilikuwa katika maumivu makali, na baada ya muda mfupi mikono yangu ikawa baridi na kuvimba; ilikuwa yenye ganzi sana hadi nikapoteza hisia zote ndani. Polisi waovu walitaka kuninyonga ili wanitese zaidi, lakini kila wakati walipovuta kambu juu ilifunguka. Walijaribu kufanya hivi mara nyingi, lakini kila wakati uliishia kwa kushindwa. Wakishangazwa, walisema, “Kuna nini leo? Kamba ni ngumu sana kugusa—si jambo la kawaida hata! Labda ni ishara kwamba hatupaswi kumuua mtu huyu?” Mmoja wao akasema, “Haidhuru! Hayo yametosha kwa leo. Usiku unakaribia.” Afisa huyo mwovu ambaye alitaka kuninyonga hakuwa na lingine la kufanya ila kusalimu amri, lakini akanielekezea na kuniambia kwa kutisha, “Leo umekuwa na bahati nzuri kweli, lakini subiri tu uone kile ambacho nimekuandalia kesho!” Nilijua kuwa Mungu alikuwa Amenilinda tena, na nilimshukuru mara nyingi moyoni mwangu. Wakati huo huo, maneno haya kutoka kwa Mungu yalinijia: “Ulimwengu na vitu vyote vimo mikononi Mwangu. Kama Nikisema, itakuwa. Kama Nikiliamua, ndivyo litakavyokuwa. Shetani yu chini ya miguu Yangu, yu katika kuzimu!(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 15). “Mimi ni msaada wenu na ni lazima muwe na roho ya mwana wa kiume! Shetani yuko katika hekaheka zake za kifo cha mwisho lakini bado hataweza kuhepa hukumu Yangu. Shetani yuko chini ya miguu Yangu na pia anakanyagwa chini ya miguu yenu—ni ukweli!(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Matamko ya Kristo Mwanzoni, Sura ya 17). Siku hiyo, mimi mwenyewe nilishuhudia ulinzi wa ajabu wa Mungu kwangu, na nilijionea mwenyewe kuwa kweli Mungu ni mweza na kwamba Anatawala kila kitu, kwamba kila kitu mbinguni na duniani kiko mikononi Mwake, na kwamba vitu vyote, kilicho hai au la, vinatawaliwa kabisa na Mungu. Niliona kwamba maafisa hao polisi waovu walikuwa chini ya mipango ya Mungu, na ingawa waliweza kuonekana wakatili kwa sura, bila idhini ya Mungu hawakuweza kunidhuru hata kidogo. Ilimradi ningeweka imani yangu kwa Mungu na kuwa tayari kuachana na maisha yangu ili kumridhisha, na nilikuwa tayari kuwa shahidi Kwake, pepo hao kwa hakika wangeaibishwa na kushindwa. Huu ulikuwa mfano wa uweza wa Mungu na ushindi Wake kamili!

Maafisa hao walinitesa katika jumba lile dogo la ghorofa mbili bila kukoma kuanzia saa 8 alasiri hadi saa 12 jioni kabla ya kunirudisha kwenye kituo cha polisi. Tuliporudi, waliniingiza katika tundu la chuma na hawakunipa chochote cha kula au kunywa. Nikihisi baridi, njaa, na dhaifu kimwili, niliegemea mapingo ya tundu na kukumbuka kila kitu kilichojiri siku hiyo. Baadhi ya maneno ya Mungu yaliibuka akilini mwangu: “Genge hili la washiriki jinai![1] Wanakuja miongoni mwa walio na mwili wa kufa na kuendeleza starehe na kuvuruga mpangilio. Usumbufu wao unaleta kigeugeu duniani na kusababisha hofu katika moyo wa mwanadamu, na wamemchezea mwanadamu sana kiasi kwamba mwonekano wake umekuwa ule wa mnyama wa mashambani, mbaya sana, na kutoka athari ya mwisho ya mwanadamu asilia imepotea. Aidha, wanatamani kuwa wa nguvu za ukuu duniani. Wanakwamisha kazi ya Mungu kiasi kwamba isiweze kusonga mbele kiasi kidogo na wanamfunga mwanadamu kwa mkazo kama wapo nyuma ya kuta za shaba na chuma cha pua. Baada ya kufanya dhambi mbaya sana na kusababisha majanga mengi sana, je, bado wanatarajia kitu tofauti na kuadibu?(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Kazi na Kuingia (7)). Kulinganisha maneno ya Mungu na ukweli, mwishowe niliona waziwazi kuwa maafisa wa polisi ambao nilikuwa nikiwaheshimu hapo zamani walikuwa kwa kweli wakatili na wakali sana. Wanaonekana wenye heshima sana na kila wakati wanapiga domo kuhusu wajibu na uadilifu, wakijivalia sura za ukarimu kama “watumishi wa watu,” lakini kwa kweli, wao ni kikundi cha wanyama wa kikatili na wasio na huruma, pepo ambao wanaweza kumuua mtu bila kujali. Je, nini kilikuwa kosa kwangu kuwa na imani? Je, nini kilikuwa kosa kwangu kumwabudu Mungu? Maafisa hao waovu waliniona kama adui mkubwa na walinitendea kwa ukatili wa kinyama kama huo, walinishinikiza hadi nikachungulia kaburi. Je, mwanadamu anawezaje kuwa na uwezo wa kutenda hayo? Je, sio mambo ambayo pepo tu ndiye awezaye kuyafanya? Ni hapo tu ndipo niligundua kuwa wale maafisa wa polisi walionekana wanadamu kwa sura, lakini ndani, nafsi yao ilikuwa ile ya pepo na roho waovu ambao wanachukia ukweli na wanamchukia Mungu, na ambao ni maadui wa asili wa Mungu. Wamekuja ulimwenguni hasa kama mazimwi walio hai ili kuwadhuru watu na kuwaangamiza watu. Nilijawa na chuki kwao na wakati huo huo nikawa na ufahamu wa kina wa fadhila na uzuri wa Mungu. Ingawa nilikuwa nimeanguka pangoni mwa ibilisi, Mungu alikuwa pamoja nami kila wakati na alikuwa akinilinda kisirisiri, akinitia moyo na kunifariji kwa maneno Yake, na akinipa imani na nguvu ili niweze kudumu tena na tena mapepo wao wakinitesa na kuniangamiza. Hata mara nyingi nilipokuwa nikichungulia kifo, Mungu alinilinda kwa nguvu Yake kubwa, akiniokoa kutoka kwa kifo changu. Upendo wa Mungu kwangu ni wa kweli sana! Nilijishawishi kimoyomoyo: Bila kujali pepo hawa watanitesa namna gani siku zijazo, nitakuwa shahidi na kumridhisha Mungu. Nuru na mwongozo wa maneno ya Mungu uliufariji moyo wangu na maumivu yangu ya mwili yalipunguzwa vikubwa. Kwa kuandamana na upendo wa Mungu, nilidumu hadi mwisho wa usiku.

Siku iliyofuata, maafisa wawili kati yao walikuja kusimama mbele ya tundu baada ya kupata kifungua kinywa. Mmoja wao alitabasamu kwa hila na kusema, “Unaendeleaje? Je, ulikuwa na wakati wa kutafakari mambo usiku uliopita? Kwa hivyo, utazungumza au la?” Nilimtazama lakini sikujibu. Alipoona hivyo alibadilisha mwenendo wake mara moja—aliingiza mkono mmoja ndani ya tundu, akashika nywele zangu kadhaa, na kunivuta kwa nguvu mbele ya uso wake. Kisha akachoma pua yangu kwa ncha ya sigara yake na, akinitazama kikatili, akasema, “Ninakwambia, wahalifu wengi hupitia hapa na hata mtu anayekaidi zaidi kuzungumza hawezi kukimbia mfumbato wangu. Hata kama hutakufa hapa, bado nitakuadhibu vikali!” Maafisa wengine wawili walikuja kabla ya muda mrefu; walilifungua tundu na kunitoa nje. Kufikia wakati huo miguu yangu ilisikika kuwa migumu na dhaifu na sikuweza kusimama. Nilianguka chini. Mmoja wa maafisa alidhani kuwa nilikuwa nikijisingizia, kwa hivyo akaja kwangu na kunipiga mateke kikatili mara kadhaa, akasema kwa sauti kubwa, “Unadhani kuwa utajifanya aliyekufa?” Maafisa wengine wawili waliniinua na kubembeza ngumi zao kwangu, wakinipiga makonde usoni mwangu na sehemu ya juu ya mwili wangu. Baada ya kufanya hivyo kwa muda, waliona kuwa mwili wangu ulikuwa unalegea kama maiti, kulikuwa na damu iliyokuwa ikitoka puani na mdomoni mwangu, na uso wangu ulipigwa hadi kuwa shapo lenye damu na usiosikia. Mmoja wao alisema, “Haidhuru, hebu tuache. Inaonekana kama hatadumu kwa muda mrefu na ikiwa atakufa mikononi mwetu basi hiyo itatusababishia shida nyingi.” Ni hapo tu ndipo walipokomesha shambulio lao la nguvu kwangu na kunirusha kando. Niliweza kuwasikia wakizungumza kati yao kimya kimya, na mmoja wao alisema, “Sijawahi kuona mtu shupavu kama yeye wakati wote nimekuwa afisa wa polisi. Hajasema hata neno moja wakati wote—ni jambo la ajabu!” Nilihisi ningeweza kusikia sauti ya Shetani akiaibika, akishusha pumzi kwa huzuni kwa ajili ya maneno yao, na ningeweza kumwona akikimbia akiwa na hofu kwa kukabiliwa na ushinde. Niliweza pia kumwona Mungu akitabasamu kutokana na kupata utukufu na nilihisi furaha isiyoelezeka. Nilimshukuru Mungu kimoyomoyo na sikuweza kujizuia kuimba wimbo wa kanisa, Ufalme, moyoni mwangu. “Mungu ni msaada wangu, kuna nini cha kuhofu? Ninaahidi maisha yangu kupigana na Shetani mpaka mwisho. Mungu anatuinua, tunapaswa kuacha kila kitu nyuma na kupigana kuwa na ushuhuda kwa Kristo. Mungu atatekeleza mapenzi Yake duniani. Nitaandaa upendo wangu na uaminifu na kuvitoa kwa Mungu. Nitakaribisha kurudi kwa Mungu kwa shangwe atakaposhuka katika utukufu, na kukutana na Yeye tena ufalme wa Kristo utakapofanyika. … Kutokana na shida kunatokea askari wengi wenye ushindi mzuri. Sisi ni washindi na Mungu na tunakuwa ushahidi wa Mungu. Watu wote wanatiririka kwenye mlima huu, wakitembea katika nuru ya Mungu. Itazame siku ambayo Mungu anapata utukufu, inakuja na nguvu isiyoweza kushindwa. Utukufu wa ufalme usio na kifani lazima uwe wazi duniani kote” (“Ufalme” katika Mfuateni Mwanakondoo na Kuimba Nyimbo Mpya). Kadiri nilipoimba zaidi, ndivyo nilivyojawa na nguvu zaidi. Nilihisi kwamba kwa kumfuata Mungu, kuweza kupitia aina hii ya mateso na dhiki ilikuwa kweli heshima kwangu. Imani yangu iliongezeka kwa kasi, na niliapa kupigana na Shetani hadi mwisho. Hivi ndivyo nilivyodumu hadi siku nyingine.

Afisa wa polisi alifika takribani saa tatu asubuhi siku ya tatu. Wakati alipoingia alijitambulisha kwangu na kusema kuwa alikuwa mkuu wa polisi katika kituo hicho. Alisimama mbele yangu na, kwa kusingizia upole, alisema, “Umeteseka kweli. Nimekuwa kwenye kaunti katika mikutano kwa muda wa siku kadhaa zilizopita; nimerudi tu na nikasikia kuhusu kilichokukufanyikia. Niliwakemea sana kwa ukali—wangewezaje kumpiga mtu kiholela bila kwanza kuelewa hali? Hilo halikufaa hata kidogo.” Sikuweza kujizuia kufadhaika nilipokabiliwa na “wema” huu usiotarajiwa kutoka kwa afisa wa polisi mwovu, lakini wakati huo nilipata kumbusho kutoka kwa maneno mengine ya Mungu: “Nyakati zote, watu Wangu wanapaswa kujihadhari dhidi ya hila danganyifu za Shetani(Neno, Vol. 1. Kuonekana na Kazi ya Mungu. Maneno ya Mungu kwa Ulimwengu Mzima, Sura ya 3). Niligundua kuwa hii ilikuwa mojawapo ya hila za Shetani—anapoona kwamba fimbo haifanyi kazi, yeye hujaribu karoti katika jaribio la kunifanya nimsaliti Mungu na kulisaliti kanisa. Moyo wangu ulichangamka na nilihisi hali ya ujasiri wa kiroho. Niliwaza, “Hekima ya Mungu hutekelezwa kulingana na hila ya Shetani. Kwa hivyo bila kujali wewe Shetani mzee ni mjanja au mdanganyifu kiasi gani, nina maneno ya Mungu ya kuniongoza. Unaota ikiwa unafikiri hila zako zitafanikiwa!” Bila kujali alisema “vitu” vingapi “vizuri” ili kunishawishi, sikusikiliza alichokisema. Alipoona yote hayakufanikiwa, mwishowe hakuwa na lingine la kufanya ila kuondoka. Baada ya hayo, maafisa wengine wawili walikuja na kusema kwa sauti kubwa, wakiwa wamekasirika, “Wewe baradhuli mchanga, subiri tu. Ikiwa hutazungumza kamwe hutatoka hapa! Tunaweza kukufanya uhukumiwe bila ushahidi wowote. Subiri tu uone!” Nilitulia sana nilipokabiliwa na vitisho vyao, nikijiwazia, “Ninaamini kuwa kila kitu kiko mikononi mwa Mungu, na ikiwa nitapata hukumu au la pia iko mikononi Mwake. Pepo hawa hawana uamuzi, Mungu ana uamuzi. Bila kujali litakalotokea, ninaamini kuwa pana maana katika kila kitu ambacho Mungu hufanya na niko tayari kutii hadi mwisho kabisa.”

Polisi hawakuwa na ushahidi wowote wa kunitia hatiani, lakini bado hawakuwa tayari kuniruhusu niondoke. Walikuwa wameninyima chakula na maji kwa muda wa siku nyingi mfululizo. Jioni hiyo nilihisi njaa sana hadi sikuwa na nguvu ya mwili hata kidogo, na nilijiuliza ikiwa nitaishia kufa kama mambo yangeendelea hivyo. Wakati huo tu nikafikiria, “Majaliwa ya watu yamo mikononi mwa Mungu, kwa hivyo ikiwa Mungu hataki mtu afe, hatakufa. Ninachotakiwa tu kufanya ni kujisalimisha kwa utaratibu na mipangilio ya Mungu.” Muda si muda, polisi waliwaleta watu sita ambao walikuwa wamekamatwa wakicheza kamari. Hao sita waliwaambia maafisa wakawanunulie kila mmoja wao takribani ratili moja ya sambusa, na maafisa wakatela ratili saba. Waliishia kulipa faini yao na wakaachiliwa haraka; punde kabla hawajaondoka, walinipa masazo yao ya sambusa, bila polisi kujua. Niliona kwa mara nyingine kwamba watu, hafla, na vitu vyote vimepangwa mikononi mwa Mungu. Macho yangu yalidondokwa na machozi na niliguswa kwa njia ambayo siwezi kuelezea. Nilihisi tu jinsi Mungu anavyopendeza na wa ajabu! Hata ingawa nilikuwa nimeanguka kwenye pango la pepo, Mungu alikuwa pamoja nami wakati wote, akinitunza na kunilinda, akifanya kazi ya nguvu yangu ya nafsi, akinihimili kushinda kujaribiwa na Shetani tena na tena. Alionyesha pia huruma kwa udhaifu wangu, akanisaidia kuzishinda shida hizi. Mungu ni wa vitendo sana, na upendo Wake ni halisi mno!

Kufikia siku ya sita, polisi walikuwa wameshindwa kabisa kupata ushahidi wowote wa kunishtaki kwa kosa, kwa hivyo waliishia kunitoza faini ya yuani 200 na kuniruhusu niondoke. Nilifahamu kwa kina kuwa Mungu alikuwa akitawala yote haya, na kwamba Mungu alijua kwa hakika ni kiasi gani cha mateso nilipaswa kuvumilia na ni njia ngapi nilipaswa kutembea—Mungu hangeniruhusu niteseke siku hata moja ambayo sikuhitaji kuteseka. Nilijua kwamba polisi hawakutaka kuniacha niondoke siku hiyo kwani, kwa sababu ya asili zao za kishetani, mbaya, kamwe hawangeweza kuniruhusu niondoke kwa urahisi sana. Lakini Mungu hangeliruhusu hilo tena, kwa hivyo hawakuwa na usemi katika jambo hilo. Hili pia liliniruhusu kuona kwamba Shetani na pepo zake waovu wanamtumikia Mungu anapowakamilisha watu Wake waliochaguliwa, na ingawa wanaweza kuonekana kuwa wakatili, Mungu anatawala kila kitu. Ilimradi tumtegemee Mungu kwa dhati na kujisalimisha Kwake, Atatulinda ili tuweze kushinda vikosi vyote vya shetani, na kupitia kwenye hatari hadi kwenye usalama.

Niliteswa kwa muda wa siku sita kamili kwenye kituo cha polisi, na tukio hilo la pekee la siku hizo sita lilinisaidia kuona sura mbaya ya serikali ya CCP na kiini na asili yake ya kupinga maendeleo. Niliona kuwa ni pepo ambaye ni adui wa Mungu, na kwamba imeundwa kwa genge la walaghai. Pia liliniruhusu kuelewa uweza, mamlaka, ustaajabishaji, na hekima ya Mungu, na kujionea mwenyewe upendo na wokovu wa Mungu; Nilikuja kufahamu kuwa Mungu ni mwweza, mwaminifu, mkuu, na Mungu mzuri, na kuwa Yeye ndiye Anayestahili milele imani na ibada ya wanadamu. Hata zaidi, Yeye ndiye anayestahili upendo wa wanadamu. Tukio hilo likawa kipindi muhimu katika maisha yangu ya imani kwa sababu, bila hilo, singesitawisha chuki ya kweli kwa Shetani, wala nisingepata ufahamu wa kweli wa Mungu. Kisha imani yangu katika Mungu ingekuwa haina maana na singeweza kupata wokovu kamili. Ni kwa kupitia tu mateso ya kikatili na kukandamizwa na CCP ndipo nilikuja kufahamu Shetani na ibilisi wake waovu ni nani, jehanamu duniani ni nini, na nguvu za giza, za uovu ni gani. Na ni kupitia tu tukio hilo ndipo ningeweza kutambua ni neema gani kubwa na huruma ambayo Mungu alikuwa akinionyesha kuwa mimi—mzaliwa wa China, katika nchi kama hii ya uovu, mbaya, najisi—ningeweza kutoroka kutoka kwenye kucha za Shetani na kuja kutembea njia ya imani na kutafuta nuru katika maisha! Nilishuhudia pia uweza na utawala wa Mungu na nikaona mamlaka na uwezo wa maneno Yake. Maneno Yake kwa kweli yanaweza kuwa maisha ya mtu, na yanaweza kuwaokoa watu kutoka katika ushawishi wa Shetani na kuwasaidia kushinda vizuizi vya kifo. Pia nilipata kuona kwa kweli kuwa ni Mungu tu ndiye ana uwezo wa kuwa na upendo wa kweli watu, na wokovu wa kweli kwa watu, ilhali yote Shetani na pepo wake wanayoweza kuyafanya ni kuwadanganya watu, kuwadhuru, na kuwaangamiza tu. Ninamshukuru Mungu kwa kutumia ukandamizaji wa CCP kuniruhusu kutofautisha kati ya mema na mabaya, kuona waziwazi uzuri na uovu. Kuanzia leo hii na kuendelea, ningependa kutafuta kufahamu na kupata ukweli zaidi ili kupata ufahamu wa kweli ya Mungu, na kueneza injili ya Mungu kwa bidii na kuwa na ushuhuda kwa jina Lake ili watu wengi zaidi waje mbele za Mungu na kumwabudu!

Tanbihi:

1. “Washiriki jinai” ni wa namna moja na “kundi la majambazi.”

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Maudhui Yanayohusiana

Imani Isiyoweza Kuvujika

Meng Yong, China Mimi kwa asili ni mtu mwaminifu, ikiwa ndiyo maana nimekuwa nikidhulumiwa daima na watu wengine. Kwa sababu hiyo, nimeonja...

Leave a Reply

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp