Maelezo ya Kweli ya Kazi Katika Enzi ya Ukombozi

Mpango Wangu mzima wa usimamizi, mpango ambao una urefu wa miaka elfu sita, unashirikisha hatua tatu, au enzi tatu: Enzi ya Sheria mwanzoni; Enzi ya Neema (ambayo pia ni Enzi ya Ukombozi); na katika siku za mwisho, Enzi ya Ufalme. Kazi Yangu katika enzi hizi tatu hutofautiana katika maudhui kulingana na asili ya kila enzi, lakini katika kila hatua huambatana na mahitaji ya mwanadamu—au, kwa usahihi zaidi, inafanywa kulingana na ujanja ambao Shetani hutumia katika vita Vyangu dhidi yake. Madhumuni ya Kazi Yangu ni kumshinda Shetani, ili kudhihirisha hekima Yangu na kudura, kufichua ujanja wote wa Shetani na hivyo kuokoa wanadamu wote, wanaoishi chini ya miliki yake. Ni ili kuonyesha hekima Yangu na kudura na wakati uo huo kufichua ubovu wa Shetani usiovumilika. Aidha, ni ili kufundisha viumbe Wangu kubagua kati ya mema na mabaya, kutambua kwamba Mimi ndiye Mtawala wa vitu vyote, kuona wazi kwamba Shetani ni adui wa binadamu, wa chini kuliko wote, yule mwovu, na kujua, kwa uhakika kabisa tofauti kati ya mema na mabaya, ukweli na uwongo, utakatifu na uchafu, kilicho kikuu na kilicho cha aibu. Kwa njia hii, binadamu wasiofahamu wataweza kunishuhudia kwamba si Mimi Ninayewapotosha wanadamu, na kwamba ni Mimi tu—Bwana wa viumbe—Ninayeweza kumwokoa binadamu, Ninayeweza kumpa mwanadamu vitu kwa ajili ya raha yake; na atapata kujua kwamba Mimi Ndimi Mtawala wa vitu vyote na Shetani ni mmoja tu wa viumbe niliowaumba na ambaye baadaye alinigeuka. Mpango Wangu wa usimamizi wa miaka elfu sita umegawanywa katika hatua tatu ili kufikia matokeo yafuatayo: kuruhusu viumbe Wangu wawe mashahidi Wangu, kuelewa mapenzi Yangu, na wajue kwamba Mimi Ndimi ukweli. Hivyo, wakati wa awamu ya kwanza ya kazi ya katika Mpango Wangu wa usimamizi wa miaka elfu sita, Nilifanya kazi ya sheria, ambayo ilikuwa ndiyo kazi ambayo kwayo Yehova aliwaongoza watu Wake. Hatua ya pili ilianzisha kazi ya Enzi ya Neema katika vijiji vya Yudea. Yesu Anawakilisha kazi yote ya Enzi ya Neema; Alipata mwili na kusulubiwa, na pia Akazindua Enzi ya Neema. Alisulubiwa ili kukamilisha kazi ya ukombozi, ili kumaliza Enzi ya Sheria na kuanzisha Enzi ya Neema, na hivyo Yeye Aliitwa “Kamanda Mkuu”, “Sadaka ya Dhambi,” “Mkombozi.” Kwa hiyo kazi ya Yesu ilitofautiana katika maudhui na kazi ya Yehova, ingawa zilikuwa sawa katika kanuni. Yehova Alianzisha Enzi ya Sheria, Akaunda msingi wa nyumbani, yaani, mahali pa asili, pa kazi Yake hapa duniani, na Akatoa amri na sheria. Hizi ndizo sehemu mbili za kazi Aliyotekeleza, na zinawakilisha Enzi ya Sheria. Kazi ya Yesu katika Enzi ya Neema haikuwa kutoa sheria bali kuzitimiza, na hivyo kukaribisha Enzi ya Neema na kuhitimisha Enzi ya Sheria ambayo ilidumu kwa miaka elfu mbili. Alikuwa mwanzilishi, aliyekuja ili kuianzisha Enzi ya Neema, ilhali ukombozi ulibakia msingi wa kazi Yake. Na hivyo mafanikio Yake yalikuwa pia mara mbili: kufungua enzi mpya, na kukamilisha kazi ya ukombozi kupitia kusulubiwa Kwake, nakisha Akaondoka. Na hapo ndipo Enzi ya Sheria ilifikia mwisho wake na Enzi ya Neema ikaanza.

Kazi ambayo Yesu alifanyika ililingana na mahitaji ya mwanadamu katika enzi hiyo. Kazi Yake ilikuwa ni kuwakomboa wanadamu, kuwasamehe dhambi zao, na kwa hivyo tabia Yake yote ilikuwa ya unyenyekevu, uvumilivu, upendo, ucha Mungu, ustahamilivu, huruma na wema. Aliwabariki wanadamu kwa wingi na kuwaletea neema nyingi, na mambo yote ambayo wangeweza kufurahia, Aliwapa kwa ajili ya furaha yao: amani na furaha, uvumilivu Wake na upendo, huruma Yake na wema. Katika siku hizo, chote alichokutana nacho mwanadamu kilikuwa wingi wa vitu vya kufurahia tu: Moyo wake ulikuwa na amani na uhakikisho, roho yake ilifarijika, na alikuwa anaruzukiwa na Mwokozi Yesu. Sababu iliyomfanya mwanadamu aweze kufaidi mambo haya ni matokeo ya enzi alimoishi. Katika Enzi ya Neema mwanadamu alikuwa amepotoshwa tayari na Shetani, na hivyo kazi ya ukombozi wa wanadamu wote ulihitaji neema nyingi, ustahimili na uvumilivu usio na mwisho, na hata zaidi, sadaka ya kutosha kulipia dhambi za wanadamu, ili kufikia athari yake. Kile wanadamu walichoona katika Enzi ya Neema kilikuwa tu sadaka Yangu ya kulipia dhambi za binadamu, yaani, Yesu. Yote waliyojua ni kwamba Mungu angeweza kuwa mwenye huruma na uvumilivu, na yote waliyoona ni huruma ya Yesu na wema Wake. Hii yote ilikuwa ni kwa sababu wao walizaliwa katika Enzi ya Neema. Na hivyo, kabla ya kuweza kukombolewa, walilazimika kufurahia neema za aina nyingi ambazo Yesu aliwapa; hili pekee ndilo lilikuwa la manufaa kwao. Kwa njia hii, wangeweza kusamehewa dhambi zao kupitia kufurahia kwao neema, na pia wangeweza kuwa na nafasi ya kukombolewa kupitia kufurahia ustahimili wa Yesu na uvumilivu. Ni kwa njia ya ustahimili wa Yesu na uvumilivu pekee ndio walipata haki ya wa kupokea msamaha na kufurahia neema nyingi kutoka kwa Yesu—kama vile Yesu alivyosema: Sijakuja kuwakomboa wenye haki, ila wenye dhambi, kukubali dhambi zao zisamehewe. Kama Yesu angepata mwili wa tabia ya hukumu, laana, na kutovumilia makosa ya mwanadamu, basi mwanadamu kamwe hangeweza kupata nafasi ya kukombolewa, na daima yeye angebaki mwenye dhambi. Hali ingekuwa hivi, mpango wa usimamizi wa miaka elfu sita ungekoma katika Enzi ya Sheria na Enzi ya Sheria ingeendelea kwa miaka elfu sita. Dhambi za mwanadamu zingeongezeka zaidi na kuwa mbaya zaidi tu, na uumbaji wa binadamu ungekuwa wa bure. Wanadamu wangeweza tu kumtumikia Yehova chini ya sheria, bali dhambi zao zingezidi za wanadamu wa kwanza kuumbwa. Jinsi Yesu alivyowapenda wanadamu zaidi, Akisamehe dhambi zao na kuwapa huruma na wema wa kutosha, ndivyo wanadamu walizidi kuwa na uwezo wa kuokolewa, wa kuitwa wanakondoo waliopotea ambao Yesu Aliwanunua tena kwa gharama kubwa. Shetani hakuweza kuingilia katika kazi hii, kwa sababu Yesu Aliwatunza wafuasi Wake kama mama mwenye upendo anavyotunza mtoto mchanga aliye kifuani pake. Yeye hakuwa na hasira nao au kuwadharau, bali Alikuwa Amejaa faraja; Yeye kamwe hakuwa na ghadhabu miongoni mwao, lakini alistahimili dhambi zao na Akapuuza upumbavu wao na kutofahamu, hata kusema, “Uwasamehe wengine mara sabini mara saba.” Kwa hiyo moyo Wake ulirekebisha mioyo ya wengine. Ilikuwa ni kwa njia hii ndiyo watu walipokea msamaha wa dhambi kupitia uvumilivu Wake.

Ingawa Yesu katika mwili Wake hakuwa na hisia kabisa, Yeye daima Aliwafariji wanafunzi Wake, Aliwapa mahitaji yao, Akawasaidia, na Akawaruzuku. Bila kujali kiwango cha kazi Alichofanya au kiasi gani cha mateso Alivumilia, Yeye kamwe hakuwa na matarajio ya kupita kiasi kwa mwanadamu, lakini kila mara Alikuwa mwenye subira na kuvumilia dhambi zao, kiasi kwamba katika Enzi ya Neema kwa upendo watu walimwita “Mwokozi Yesu anayependeka.” Kwa watu wa wakati huo—kwa watu wote—kile Yesu Alikuwa nacho na kile Alichokuwa, kilikuwa huruma na wema. Yeye kamwe hakukumbuka dhambi za, na hakuwatendea kulingana na dhambi zao. Kwa sababu hiyo ilikuwa enzi tofauti, mara nyingi Alitoa chakula na vinywaji kwa watu ili waweze kula hadi washibe. Yeye Aliwatendea wafuasi Wake wote kwa ukarimu, akaponya wagonjwa, kufukuza mapepo na kufufua wafu. Ili kwamba watu waweze kumwamini na kuona kwamba yote Aliyofanya yalifanyika kwa bidii na kwa dhati, Yeye Alifika kiwango cha kufufua maiti iliyooza, kuwaonyesha kwamba mikononi Mwake hata wafu wanaweza kuwa hai tena. Kwa njia hii Alivumilia kwa kimya na kufanya kazi Yake ya ukombozi kati yao. Hata kabla Asulubiwe, Yesu Alikuwa tayari Amebeba dhambi za binadamu na kuwa sadaka ya dhambi kwa ajili ya wanadamu. Hata kabla Asulubiwe, Alikuwa tayari Amefungua njia ya msalaba ili kuwakomboa wanadamu. Mwishowe Aligongwa misumari msalabani, Alijitoa sadaka Yeye Mwenyewe kwa ajili ya msalaba, na Alitoa huruma Yake yote, wema Wake, na utakatifu kwa wanadamu. Kwa wanadamu daima alikuwa mvumilivu, kamwe Hakutafuta kulipiza kisasi, lakini Aliwasamehe dhambi zao, Akiwasihi watubu, na kuwafundisha kuwa na subira, uvumilivu na upendo, kufuata nyayo Zake na kujitoa wenyewe kwa ajili ya msalaba. Upendo Wake kwa ndugu ulizidi upendo Wake kwa Maria. Kanuni ya kazi Aliyofanya ilikuwa kuwaponya watu na kutoa mapepo, yote kwa ajili ya ukombozi Wake. Haijalishi Alikoenda, Yeye Aliwatendea wote waliomfuata kwa neema. Aliwafanya maskini kuwa tajiri, viwete watembee, vipofu waone na viziwi wasikie; Yeye hata Aliwaalika watu wa hadhi ya chini kabisa, maskini zaidi, wenye dhambi, kula pamoja naye, Akikosa kuwaepuka kamwe ila daima Alikuwa na subira, hata kusema: Wakati mchungaji anampoteza kondoo mmoja kati ya mia, yeye ataondoka na kuwaacha nyuma wale tisini na tisa ili amtafute kondoo mmoja aliyepotea, na anapompata yeye atafurahia sana. Yeye Aliwapenda wafuasi Wake kama kondoo anavyopenda wanakondoo wake. Ingawa walikuwa wajinga na wasio na ufahamu, na walikuwa wenye dhambi katika macho Yake, na zaidi walikuwa washirika wa chini zaidi katika jamii, Aliona hawa wenye dhambi—waliodharauliwa na wengine—kama vipenzi Vyake. Kwa kuwa Aliwapendelea, Alitoa uhai Wake kwa ajili yao, kama mwana kondoo alitolewa madhabahuni. Alitembea kati yao kama mtumishi wao, Akiwaruhusu kumtumia na kumchinja, Alijinyenyekeza kwao bila masharti. Kwa wafuasi Wake Alikuwa Mwokozi Yesu aliyependeka, lakini kwa Mafarisayo, ambao waliwahubiria watu kutoka viweko virefu vya mnara, Hakuonyesha huruma na wema, bali chuki na maudhi. Hakufanya kazi nyingi miongoni mwa Mafarisayo, Akiwahubiria na kuwakemea mara chache tu; Yeye hakutembea miongoni mwao akifanya kazi ya ukombozi, au kufanya ishara na maajabu. Alitoa huruma Yake na wema Wake wote kwa wafuasi Wake, akivumilia kwa ajili ya hawa wenye dhambi mpaka mwisho kabisa, wakati Alipigwa misumari msalabani na akastahimili kila udhalilishaji mpaka Alivyowakomboa wanadamu wote kikamilifu. Hii ndiyo ilikuwa kazi Yake yote.

Bila ukombozi wa Yesu, wanadamu wangeishi milele katika dhambi, na kuwa watoto wa dhambi, kizazi cha mapepo. Kama ingeendelea hivyo, dunia yote ingekuwa mahali pa kulala pa Shetani, maskani yake. Lakini kazi ya ukombozi ilihitaji kuonyesha huruma na wema kwa wanadamu; kupitia kwa njia hiyo tu ndio wanadamu wangeweza kupokea msamaha na mwishowe kupata haki ya kukamilishwa na kumilikiwa kikamilifu. Bila hatua hii ya kazi, mpango wa usimamizi wa miaka elfu sita haungeweza kuendelea mbele. Kama Yesu hangesulubiwa, kama Yeye Angewaponya tu watu na kufukuza mapepo, basi watu hawangesamehewa dhambi zao kikamilifu. Katika miaka mitatu na nusu ambayo Yesu Alitumia kufanya kazi Yake hapa duniani alikamilisha tu nusu ya kazi Yake ya ukombozi; kisha, kwa kupigiliwa misumari msalabani na kuwa mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kukabidhiwa kwa yule mwovu, Yeye Alikamilisha kazi ya kusulubiwa na Akaendesha majaaliwa ya wanadamu. Baada ya Yeye kukabidhiwa mikononi mwa Shetani tu, ndipo alipowakomboa wanadamu. Kwa miaka thelathini na mitatu na nusu Aliteseka duniani, Akidhihakiwa, kukashifiwa, na kuachwa, kiasi cha Yeye kukosa mahali pa kulaza kichwa chake, mahali pa kupumzika; kisha Akasulubiwa, huku nafsi Yake yote—mwili mtakatifu na usio na hatia—kupigiliwa misumari msalabani. Alivumilia kila namna ya mateso yaliyoko. Wale waliokuwa madarakani wakamdhihaki na kumcharaza mijeledi, na maaskari hata wakamtemea mate usoni; ilhali Alibaki kimya na kuvumilia mpaka mwisho, Akinyenyekea bila masharti mpaka wakati wa kifo, ambapo Yeye Alikomboa wanadamu wote. Hapo tu ndipo Aliruhusiwa kupumzika. Kazi ambayo Yesu alifanya inawakilisha tu Enzi ya Neema; haiwakilishi Enzi ya Sheria wala si mbadala wa kazi ya siku za mwisho. Hiki ndicho kiini cha kazi ya Yesu katika Enzi ya Neema, enzi ya pili ambayo wanadamu wamepitia—Enzi ya Ukombozi.

Iliyotangulia: Kazi katika Enzi ya Sheria

Inayofuata: Unapaswa Kujua Namna Ambavyo Binadamu Wote Wameendelea Hadi Siku ya Leo

Ulimwengu umezongwa na maangamizi katika siku za mwisho. Je, hili linatupa onyo lipi? Na tunawezaje kulindwa na Mungu katikati ya majanga?

Mipangilio

  • Matini
  • Mada

Rangi imara

Mada

Fonti

Ukubwa wa Fonti

Nafasi ya Mstari

Nafasi ya Mstari

Upana wa ukurasa

Yaliyomo

Tafuta

  • Tafuta Katika Maneno Haya
  • Tafuta Katika Kitabu Hiki

Wasiliana nasi kupitia WhatsApp