Kazi katika Enzi ya Sheria
Kazi ambayo Yehova alifanya juu ya Waisraeli ilianzisha miongoni mwa binadamu mahali pa asili pa Mungu duniani, ambapo pia palikuwa mahali patakatifu ambapo Yeye alikuwepo. Aliiwekea mipaka kazi Yake kwa watu wa Israeli. Mwanzoni, Hakufanya kazi nje ya Israeli, lakini badala yake, Alichagua watu Aliowapata kuwa wanaofaa ili kuwekea mipaka upeo wa kazi Yake. Israeli ni mahali ambapo Mungu aliwaumba Adamu na Hawa, na kutoka kwa mavumbi ya mahali hapo Yehova alimfanya mwanadamu; mahali hapa pakawa kituo cha kazi Yake duniani. Waisraeli, ambao walikuwa dhuria ya Nuhu na pia dhuria ya Adamu, walikuwa msingi wa kibinadamu wa kazi ya Yehova duniani.
Wakati huu, umuhimu, kusudi, na hatua za kazi ya Yehova katika Israeli zilikuwa kutekeleza kazi Yake katika dunia nzima, ambayo, ikichukua Israeli kama kitovu chake, ilienea polepole katika Mataifa. Hii ndiyo kanuni ambayo kwayo Yeye hufanya kazi ndani ya ulimwengu—kuanzia mahali fulani ili kuendesha yote, na kisha kupanua kazi Yake hadi watu wote katika ulimwengu wawe wameipokea injili Yake. Waisraeli wa kwanza walikuwa dhuria ya Nuhu. Watu hawa walijaliwa tu pumzi ya Yehova, na walijua jinsi ya kushughulikia mahitaji ya lazima ya msingi ya maisha, lakini hawakujua Yehova alikuwa Mungu wa aina gani, au nia Zake kwa mwanadamu, sembuse jinsi walivyopaswa kumcha Muumba. Kuhusu iwapo kulikuwa na kanuni na sheria za kutiiwa,[a] au iwapo kulikuwa na wajibu ambao viumbe walioumbwa walipaswa kumfanyia Muumba, dhuria ya Adamu haikujua chochote kuhusu mambo haya. Kile tu walichojua kilikuwa kwamba mume alipaswa kutokwa na jasho na kufanya kazi ili kuikimu familia yake, na kwamba mke alipaswa kumtii mumewe na kuendeleza kizazi cha binadamu ambacho Yehova alikuwa amekiumba. Kwa maneno mengine, watu kama hao, ambao walikuwa tu na pumzi ya Yehova na uzima Wake, hawakujua chochote kuhusu jinsi ya kufuata sheria za Mungu au jinsi ya kumridhisha Muumba. Walielewa machache mno. Kwa hivyo ingawa hakukuwa na chochote kilicho potovu au kidanganyifu mioyoni mwao, na wivu na mzozo viliibuka mara chache miongoni mwao, hata hivyo hawakuwa na maarifa au ufahamu wa Yehova, Muumba. Mababu hawa wa mwanadamu walijua tu kula vitu vya Yehova, na kufurahia vitu vya Yehova, lakini hawakujua kumcha Yehova; hawakujua kwamba Yehova ndiye Yule waliyepaswa kumwabudu kwa kupiga magoti. Kwa hivyo wangewezaje kuitwa viumbe Wake walioumbwa? Hili lingekuwa hivi, je, maneno, “Yehova ni Muumba” na “Alimuumba mwanadamu ili mwanadamu aweze kumdhihirisha, kumtukuza, na kumwakilisha” hayangekuwa yamesemwa bure? Watu waliokosa mioyo ya kumcha Yehova wangewezaje kuwa ushuhuda kwa utukufu Wake? Wangewezaje kuwa udhihirisho wa utukufu Wake? Je, maneno ya Yehova “Nilimuumba mwanadamu kwa mfano Wangu” basi hayangetumiwa kama kisingizio na Shetani, yule mwovu? Je, maneno haya basi hayangekuwa alama ya aibu kwa uumbaji wa Yehova wa mwanadamu? Ili kukamilisha hatua hiyo ya kazi, Yehova, baada ya kumuumba binadamu, hakuwaelekeza au kuwaongoza kutoka kwa Adamu hadi Nuhu. Badala yake, haikuwa mpaka baada ya gharika kuiharibu dunia ndipo Alipoanza rasmi kuwaongoza Waisraeli, ambao walikuwa dhuria ya Nuhu na pia ya Adamu. Kazi na matamko Yake katika Israeli yaliwapa mwongozo watu wote wa Israeli walipoishi maisha yao kote katika nchi ya Israeli, na hivyo kumwonyesha mwanadamu kwamba Yehova si tu kwamba aliweza kumpulizia mwanadamu pumzi, ili aweze kuwa na uzima kutoka Kwake na kuinuka kutoka mavumbini kuwa binadamu aliyeumbwa, bali kwamba Angeweza pia kumteketeza mwanadamu, na kumlaani mwanadamu, na kutumia fimbo Yake kumtawala mwanadamu. Hivyo, pia, waliona kwamba Yehova angeweza kuongoza maisha ya mwanadamu duniani, na kuzungumza na kufanya kazi miongoni mwa binadamu kulingana na saa za mchana na za usiku. Kazi Aliyofanya ilikuwa tu ili viumbe Wake walioumbwa wapate kujua kwamba mwanadamu alitokana na mavumbi yaliyochukuliwa na Yeye, na zaidi ya hayo kwamba mwanadamu alikuwa amefanywa na Yeye. Sio hili tu, bali Alifanya kazi Yake kwanza katika Israeli ili watu na mataifa mengine (ambao kwa kweli hawakuwa wametengana na Israeli, bali walikuwa wametokana na Waisraeli, lakini bado walikuwa dhuria ya Adamu na Hawa) waweze kuipokea injili ya Yehova kutoka Israeli, ili viumbe wote walioumbwa katika ulimwengu waweze kumcha Yehova na kumtukuza kama mkuu. Kama Yehova asingeanza kazi Yake katika Israeli, lakini badala yake, baada ya kuwaumba wanadamu, angewaacha tu waishi maisha yasiyo na wasiwasi duniani, basi katika hali hiyo, kwa kuzingatia asili ya kimwili ya mwanadamu (asili inamaanisha kwamba mwanadamu hawezi kamwe kujua vitu asivyoweza kuona, ambayo ni kusema kwamba asingejua kwamba ni Yehova aliyemuumba mwanadamu, sembuse kwa nini Alifanya hivyo), asingejua kamwe kwamba ni Yehova aliyemuumba mwanadamu au kwamba Yeye ni Bwana wa vitu vyote. Ikiwa Yehova angemuumba mwanadamu na kumweka duniani, na kupangusa tu mikono Yake na kuondoka, badala ya kubaki miongoni mwa wanadamu ili kuwapa mwongozo kwa kipindi cha muda, basi binadamu wote wangegeuzwa kuwa si kitu; hata mbingu na ardhi na vitu vyote, ambavyo Aliviumba, vingegeuzwa kuwa si kitu, na binadamu wote pia wangegeuzwa kuwa si kitu na zaidi ya hayo kukanyagwa na Shetani. Katika hali hiyo, matamanio ya Yehova kwamba “Duniani, yaani, katikati ya uumbaji Wake, Aweze kuwa na mahali pa kusimama, mahali patakatifu” yangesambaratika. Na hivyo, baada ya kuwaumba binadamu, Alibaki miongoni mwao ili kuwaongoza katika maisha yao, na kuzungumza nao kutoka miongoni mwao—haya yote yalikuwa ili kutimiza matamanio Yake, na kutimiza mpango Wake. Kazi Aliyofanya katika Israeli ilikusudiwa tu kutimiza mpango Aliokuwa ameufanya kabla ya uumbaji Wake wa vitu vyote, na kwa hivyo kufanya Kwake kazi kwanza miongoni mwa Waisraeli na uumbaji Wake wa vitu vyote havikupingana, bali vyote vilifanywa kwa ajili ya usimamizi Wake, kazi Yake, na utukufu Wake, na vilifanywa ili kuongeza kina cha maana ya uumbaji Wake wa binadamu. Alielekeza maisha ya binadamu duniani kwa miaka elfu mbili baada ya Nuhu, akiwasaidia watu kuelewa jinsi ya kumcha Yehova, Bwana wa vitu vyote, jinsi ya kuendesha maisha yao, na jinsi ya kuishi, na zaidi ya yote, jinsi ya kuwa na ushuhuda kwa Yehova, kumtii, na kumcha, hata kumsifu kwa muziki kama alivyofanya Daudi na makasisi wake.
Kabla ya miaka elfu mbili ambayo kwayo Yehova alifanya kazi Yake, mwanadamu hakujua chochote, na karibu binadamu wote walikuwa wametumbukia katika upotovu, hadi, kabla ya maangamizo ya dunia kwa gharika, walikuwa wamefikia kina cha uasherati na upotovu, na hawakuwa na Yehova mioyoni mwao hata kidogo, sembuse njia Yake. Hawakuwahi kuelewa kazi ambayo Yehova alikuwa akienda kufanya; hawakuwa na busara, sembuse maarifa, na, kama mashine zilizopumua, walikuwa wajinga kabisa kuhusu mwanadamu, Mungu, vitu vyote, uzima, na kadhalika. Duniani, walijihusisha katika ushawishi mwingi, kama nyoka, na kusema mambo mengi yaliyomkosea Yehova, lakini kwa sababu walikuwa wajinga, Yehova hakuwaadibu wala kuwatia adabu. Ni baada tu ya gharika, Nuhu alipokuwa na umri wa miaka 601, ndipo Yehova alimtokea Nuhu rasmi na kumwelekeza yeye na familia yake, akiwaongoza ndege na wanyama ambao walikuwa wamenusurika gharika pamoja na Nuhu na dhuria yake, hadi mwisho wa Enzi ya Sheria, iliyodumu kwa jumla ya miaka 2,500. Alikuwa akifanya kazi katika Israeli, yaani, akifanya kazi rasmi, kwa jumla ya miaka 2,000, na akifanya kazi kwa wakati mmoja ndani ya Israeli na nje yake kwa miaka 500, kwa pamoja ikijumlisha miaka 2,500. Katika kipindi hiki, Aliwaagiza Waisraeli kwamba ili kumtumikia Yehova, walipaswa kujenga hekalu, kuvaa kanzu za ukuhani, na kutembea pekupeku kuingia hekaluni wakati wa mapambazuko, isije ikawa viatu vyao vinalichafua hekalu la Yehova na moto ukashushwa juu yao kutoka kwenye kilele cha hekalu na kuwateketeza hadi kufa. Walitekeleza wajibu wao na kutii mipango ya Yehova. Walimwomba Yehova hekaluni, na baada ya kupokea ufunuo wa Yehova, yaani, baada ya Yehova kuzungumza, waliuongoza umati na kuufundisha kwamba walipaswa kumcha Yehova—Mungu wao. Na Yehova aliwaambia kwamba walipaswa kujenga hekalu na madhabahu, na wakati wa Yehova, yaani, siku ya Pasaka, walipaswa kuandaa ndama na wanakondoo wazaliwa wa kwanza kuwaweka kwenye madhabahu kama dhabihu za kumtumikia Yehova, ili kuwazuia na kuweka hofu kwa Yehova mioyoni mwao. Iwapo walitii sheria hii ikawa kipimo cha uaminifu wao kwa Yehova. Yehova pia aliiamrisha siku ya Sabato, siku ya saba ya uumbaji Wake. Siku iliyofuata baada ya Sabato, Aliifanya siku ya kwanza, siku kwao ya kumsifu Yehova, kumtolea dhabihu, na kumfanyia muziki. Kwenye siku hii, Yehova aliwaita pamoja makasisi wote kugawanya dhabihu kwenye madhabahu ili watu wale, ili waweze kufurahia dhabihu kwenye madhabahu ya Yehova. Na Yehova alisema kwamba walikuwa wamebarikiwa, kwamba walishiriki sehemu pamoja na Yeye, na kwamba walikuwa watu Wake wateule (ambalo lilikuwa agano la Yehova na Waisraeli). Hii ndiyo sababu, hadi leo hii, watu wa Israeli bado wanasema kwamba Yehova ni Mungu wao pekee, na si Mungu wa watu wa mataifa.
Wakati wa Enzi ya Sheria, Yehova alimpa Musa amri nyingi ili awapitishie Waisraeli waliomfuata kutoka Misri. Amri hizi zilitolewa na Yehova kwa Waisraeli na hazikuwa na uhusiano wowote na Wamisri; zilikusudiwa kuwazuia Waisraeli, na Alitumia amri hizo kuweka matakwa kwao. Iwapo walishika Sabato, iwapo waliwaheshimu wazazi wao, iwapo waliabudu sanamu, na kadhalika—hizi zilikuwa kanuni ambazo kwazo walihukumiwa kuwa wenye dhambi au wenye haki. Miongoni mwao, kulikuwa na baadhi ambao walipigwa na moto wa Yehova, baadhi ambao walipigwa mawe hadi kufa, na baadhi ambao walipokea baraka ya Yehova, na hili liliamuliwa kulingana na iwapo walitii amri hizi au la. Wale ambao hawakushika Sabato walipigwa mawe hadi kufa. Wale makasisi ambao hawakushika Sabato walipigwa na moto wa Yehova. Wale ambao hawakuwaheshimu wazazi wao pia walipigwa mawe hadi kufa. Haya yote yalikubaliwa na Yehova. Yehova alianzisha amri na sheria Zake ili kwamba, Alipowaongoza katika maisha yao, watu wangesikiliza na kutii neno Lake na kutomwasi Yeye. Alitumia sheria hizi kuidhibiti jamii changa ya wanadamu, ili kuweka msingi kwa ajili ya kazi Yake ya baadaye. Na hivyo, kulingana na kazi ambayo Yehova alifanya, enzi ya kwanza iliitwa Enzi ya Sheria. Ingawa Yehova alitoa matamko mengi na kufanya kazi nyingi, Aliwaongoza tu watu kwa njia chanya, akiwafundisha watu hawa wajinga jinsi ya kujiendesha, jinsi ya kuishi, na jinsi ya kuelewa njia ya Yehova. Kwa sehemu kubwa, kazi Aliyofanya ilikuwa kuwafanya watu washike njia Yake na kufuata sheria Zake. Kazi ilifanywa kwa watu ambao walikuwa wamepotoshwa kwa kijuujuu; haikuenea hadi kufikia kubadilisha tabia au maendeleo yao katika uzima. Aliwazuia tu na kuwadhibiti watu kwa kuwafanya watii sheria. Kwa Waisraeli wakati huo, Yehova alikuwa tu Mungu hekaluni, Mungu mbinguni. Alikuwa nguzo ya wingu, nguzo ya moto. Kile ambacho Yehova aliwataka wafanye kilikuwa kutii kile ambacho watu leo wanakijua kama sheria na amri—mtu angeweza hata kusema kanuni—kwa sababu kile ambacho Yehova alifanya hakikukusudiwa kuwabadilisha, bali kuwapa vitu zaidi ambavyo mwanadamu alipaswa kuwa navyo, na kuwaambia vitu hivi Yeye binafsi, kwa sababu baada ya kuumbwa mwanadamu hakuwa na chochote alichopaswa kumiliki. Na hivyo, Yehova aliwapa watu vitu walivyopaswa kumiliki kwa ajili ya maisha yao duniani, akiwafanya watu Aliowaongoza kuwapita mababu zao, Adamu na Hawa, kwa sababu kile ambacho Yehova aliwapa kilipita kile Alichokuwa amewapa Adamu na Hawa hapo mwanzo. Bila kujali, kazi ambayo Yehova alifanya katika Israeli ilikuwa tu kuwaongoza wanadamu na kuwafanya wanadamu wamtambue Muumba. Hakuwashinda au kuwabadilisha, bali Aliwaongoza tu. Huu ndio ukamilifu wa kazi ya Yehova katika Enzi ya Sheria. Ni usuli, hadithi halisi, kiini cha kazi Yake katika nchi nzima ya Israeli, na mwanzo wa kazi Yake ya miaka elfu sita—kuwaweka wanadamu chini ya udhibiti wa mkono wa Yehova. Kutokana na hili ilizaliwa kazi zaidi katika mpango Wake wa usimamizi wa miaka elfu sita.
Tanbihi:
a. Nakala ya asili haina fungu la maneno “za kutiiwa.”